Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 45

Jinsi Roho Takatifu Inavyotusaidia

Jinsi Roho Takatifu Inavyotusaidia

“Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”​—FLP. 4:13.

WIMBO 104 Roho Takatifu—Zawadi Kutoka kwa Mungu

MUHTASARI *

1-2. (a) Ni nini kinachotusaidia tuendelee kusonga mbele siku baada ya siku? Eleza. (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

“NINAPOFIKIRIA kuhusu majaribu ambayo nimepitia, ninajua kwamba nisingeweza kukabiliana nayo kwa uwezo wangu mwenyewe.” Je, umewahi kusema jambo kama hilo? Wengi wetu tumewahi kusema hivyo. Labda ulisema hivyo ulipokumbuka jinsi ulivyofanikiwa kukabiliana na ugonjwa fulani mbaya au kifo cha mpendwa wako. Unapofikiria jambo hilo, unahisi kwamba ulifaulu kusonga mbele siku baada ya siku kwa sababu roho takatifu ya Yehova ilikupa “nguvu zinazopita zile za kawaida.”—2 Kor. 4:7-9.

2 Pia, tunategemea roho takatifu ili tupinge vishawishi vya ulimwengu huu mwovu. (1 Yoh. 5:19) Isitoshe, tunapambana na “majeshi ya roho waovu.” (Efe. 6:12) Tukiwa na changamoto hizo zote akilini, tutazungumzia njia mbili ambazo roho takatifu hutusaidia. Kisha tutazungumzia mambo tunayoweza kufanya ili roho takatifu itunufaishe kikamili.

ROHO TAKATIFU HUTUPATIA NGUVU

3. Taja njia moja ambayo Yehova anatumia ili kutusaidia kuvumilia majaribu.

3 Roho takatifu ya Yehova hutusaidia kwa kutupatia nguvu au uwezo ili tutimize majukumu yetu licha ya majaribu. Mtume Paulo alihisi kwamba alifanikiwa kuendelea kumtumikia Yehova licha ya majaribu kwa sababu alitegemea “nguvu za Kristo.” (2 Kor. 12:9) Alipokuwa katika safari yake ya pili ya umishonari, Paulo hakujitahidi tu kuhubiri habari njema bali pia alijitegemeza mwenyewe kifedha. Alikaa katika jiji la Korintho kwenye nyumba ya Akila na Prisila. Walifanya kazi ya kutengeneza mahema. Kwa kuwa Paulo pia alitengeneza mahema, alifanya kazi ya muda pamoja nao. (Mdo. 18:1-4) Roho takatifu ilimpa Paulo nguvu za kufanya kazi ya kimwili na nguvu za kutimiza huduma yake.

4. Kulingana na 2 Wakorintho 12:7b-9, Paulo alipambana na nini?

4 Soma 2 Wakorintho 12:7b-9. Katika andiko hili, Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba alipambana na “mwiba katika mwili”? Ikiwa una mwiba mwilini, ungehisi maumivu makali sana. Hivyo, Paulo alimaanisha kwamba alikabiliana na jaribu fulani lenye maumivu makali. Aliliita jaribu hilo “malaika wa Shetani” ambaye aliendelea ‘kumpiga kofi.’ Huenda Shetani au roho wake waovu hawakusababisha moja kwa moja majaribu ya Paulo, kana kwamba walikuwa wakiuingiza mwiba huo kwenye mwili wake. Lakini roho hao waovu walipouona “mwiba” huo, huenda walitamani sana kuusukuma hata zaidi ili kumwongezea Paulo maumivu. Paulo alifanyaje?

5. Yehova alijibuje sala ya Paulo?

5 Mwanzoni, Paulo alitaka “mwiba” huo uondolewe. Anakiri hivi: “Mara tatu nilimwomba Bwana [Yehova] . . . kwamba aniondolee.” Hata hivyo, licha ya ombi lake, aliendelea kubaki na mwiba huo mwilini mwake. Je, hilo linamaanisha kwamba Yehova hakujibu sala ya Paulo? Hapana. Yehova aliijibu. Yehova hakuondoa tatizo hilo, lakini alimpatia Paulo nguvu za kulivumilia. Yehova alisema: “Nguvu zangu zinakamilika katika udhaifu.” (2 Kor. 12:8, 9) Na kwa msaada wa Mungu, Paulo alifanikiwa kudumisha shangwe yake na amani ya moyoni!—Flp. 4:4-7.

6. (a) Yehova anaweza kujibu sala zetu jinsi gani? (b) Maandiko yaliyo kwenye fungu yanataja uhakikisho gani unaokupa nguvu?

6 Kama Paulo, je, umewahi kumwomba Yehova akuondolee jaribu fulani? Ikiwa licha ya kumsihi kwa bidii sana tatizo hilo liliendelea—au lilizidi kuwa baya hata zaidi—je, ulihisi kwamba huenda Yehova hafurahishwi nawe? Ikiwa ndivyo, mkumbuke Paulo. Kama tu Yehova alivyojibu sala za Paulo, ndivyo kwa hakika atakavyojibu sala zako pia! Huenda Yehova asiondoe tatizo lako. Lakini kupitia roho takatifu, atakupatia nguvu unazohitaji ili kuvumilia jaribu. (Zab. 61:3, 4) Huenda ‘ukaangushwa chini,’ lakini Yehova hatakuacha kamwe.—2 Kor. 4:8, 9; Flp. 4:13.

ROHO TAKATIFU INATUSAIDIA TUSONGE MBELE

7-8. (a) Roho takatifu ni kama upepo jinsi gani? (b) Petro alifafanuaje jinsi roho takatifu inavyofanya kazi?

7 Roho takatifu inatusaidia kwa njia gani nyingine? Kama upepo mzuri kwenye bahari iliyochafuka, roho takatifu hutusaidia tusonge mbele tunapoendelea kukabiliana na majaribu yaliyo kama dhoruba ili tuingie katika ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu.

8 Akiwa mvuvi, mtume Petro alijua mambo mengi kuhusu ubaharia. Hivyo, si ajabu kwamba alipokuwa akifafanua kuhusu jinsi roho takatifu inavyofanya kazi, alitumia maneno yanayohusiana na mambo ya ubaharia . Aliandika hivi: “Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ongozwa” kihalisi linamaanisha “kuchukuliwa.”—2 Pet. 1:21; maelezo ya chini.

9. Petro alimaanisha nini alipotumia neno ‘kuchukuliwa’?

9 Petro alimaanisha nini alipotumia neno ‘kuchukuliwa’? Neno kama hilo lilitumiwa na Luka katika Kigiriki, kufafanua meli ‘inayosukumwa’ na upepo. (Mdo. 27:15) Hivyo, Petro aliposema kwamba waandikaji wa Biblia ‘walichukuliwa,’ alitumia “ulinganifu wenye kusisimua wa safari za baharini,” kama msomi mmoja wa Biblia anavyoeleza. Kwa maneno mengine Petro anasema kwamba, kama tu ambavyo meli huchukuliwa au kusukumwa na upepo ili ifike inakoenda, ndivyo manabii na waandikaji wa Biblia walivyochukuliwa au kusukumwa na roho takatifu ili waweze kutimiza kazi yao. Msomi huyo alisema hivi: “Ni kana kwamba manabii waliinua juu matanga yao.” Yehova alitimiza sehemu yake kwa kuandaa “upepo,” au roho takatifu. Nao waandikaji wa Biblia wakatimiza sehemu yao. Walitenda kulingana na mwongozo wa roho hiyo.

HATUA YA 1: Shiriki kwa ukawaida katika utendaji wa kiroho

HATUA YA 2: Timiza kikamili utendaji huo wa kiroho kwa uwezo wako wote (Tazama fungu la 11) *

10-11. Ni hatua gani mbili tunazohitaji kuchukua ili kuhakikisha kwamba tunaongozwa na roho takatifu? Toa mfano.

10 Bila shaka leo, Yehova hawaongozi watu kuandika maandishi matakatifu. Hata hivyo, roho takatifu bado inawapa nguvu watu wa Mungu. Yehova anaendelea kutimiza sehemu yake. Roho takatifu ya Mungu inaweza kutunufaishaje? Tunapaswa kuhakikisha kwamba tunaendelea kutimiza sehemu yetu. Tunafanyaje hivyo?

11 Fikiria mfano huu. Ili upepo uweze kumsaidia baharia, ni lazima afanye mambo mawili. Kwanza, anapaswa kuiweka mashua yake mahali upepo unapovuma. Ikiwa baharia ataiweka mashua yake bandarini, mbali na mahali ambapo upepo unavuma, mashua yake haitasonga. Pili, anahitaji kupandisha na kukunjua kabisa tanga. Ni wazi kwamba hata kama pepo zinavuma, mashua yake itasonga mbele ikiwa tu tanga zimejaa upepo. Vivyo hivyo, tutaendelea na utumishi wetu kwa Yehova ikiwa tu Yehova anatupatia roho yake takatifu. Ili tunufaike na roho hiyo, ni lazima tuchukue hatua mbili muhimu. Kwanza, ni lazima tujiweke kabisa mahali palipo na roho ya Mungu kwa kushiriki katika utendaji utakaotuleta chini ya mwongozo wa roho hiyo. Pili, tunapaswa “kupandisha tanga zetu” juu kabisa kwa kufanya yote tuwezayo katika utendaji huo. (Zab. 119:32) Tunapochukua hatua hizo, roho takatifu itatusukuma mbele ili tupambane na mawimbi ya upinzani na majaribu na itatusaidia tuvumilie kwa uaminifu hadi tutakapofika katika ulimwengu mpya wa Mungu.

12. Tutazungumzia nini sasa?

12 Kufikia sasa tumezungumzia njia mbili ambazo roho takatifu inaweza kutusaidia. Roho takatifu hutupatia nguvu na kutusaidia tuendelee kuwa waaminifu tunapokabili majaribu. Pia, inatuchochea tusonge mbele na kutusaidia tubaki katika njia inayoelekea kwenye uzima wa milele. Sasa tutazungumzia mambo manne ambayo ni lazima tufanye ili roho takatifu itunufaishe kikamili.

JINSI YA KUNUFAIKA NA ROHO TAKATIFU

13. Kulingana na 2 Timotheo 3:16, 17, Maandiko yanaweza kutunufaishaje, lakini ni lazima tufanye nini?

13 Kwanza, jifunze Neno la Mungu. (Soma 2 Timotheo 3:16, 17.) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘limeongozwa na roho ya Mungu’ kihalisi linamaanisha ‘lililotiwa pumzi ya Mungu.’ Mungu alitumia roho yake “kutia” mawazo yake katika akili za waandikaji wa Biblia. Tunaposoma Biblia na kutafakari mambo tunayosoma, mafundisho ya Mungu huingia katika akili na mioyo yetu. Mawazo hayo yaliyoongozwa na Mungu hutuchochea kupatanisha maisha yetu na mapenzi ya Mungu. (Ebr. 4:12) Lakini ili roho takatifu itunufaishe kikamili ni lazima tutenge wakati wa kujifunza Biblia kwa ukawaida na kutafakari kwa kina mambo tunayojifunza. Kisha Neno la Mungu litaongoza mambo yote tunayosema na kutenda.

14. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba “upepo huvuma” katika mikutano yetu ya Kikristo? (b) Tunaweza kufanya nini ili tuhudhurie mikutano tukiwa na “tanga zilizokunjuliwa kabisa”?

14 Pili, mwabudu Mungu pamoja na wengine. (Zab. 22:22) Kwa njia fulani, mikutano ya Kikristo ni mahali ambapo “upepo huvuma.” Katika mikutano yetu kuna roho ya Yehova. (Ufu. 2:29) Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Kwa sababu tunapokutana pamoja na Wakristo wenzetu kwa ajili ya ibada, tunasali ili tupate roho takatifu, tunaimba nyimbo za Ufalme zinazotegemea Neno la Mungu, na tunasikiliza mafundisho yanayotegemea Biblia yanayowasilishwa na akina ndugu waliowekwa rasmi na roho takatifu. Na roho hiyohiyo takatifu huwasaidia akina dada kutayarisha na kutoa migawo yao. Hata hivyo, ili roho takatifu itunufaishe kikamili, tunapaswa kuhudhuria mikutano tukiwa tumejitayarisha ili tuweze kushiriki. Kwa njia hiyo, tunahudhuria mikutano, tukiwa na “tanga zilizokunjuliwa kabisa.”

15. Roho takatifu hutusaidiaje katika kazi yetu ya kuhubiri?

15 Tatu, hubiri. Tunapotumia Biblia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha, tunaruhusu roho takatifu itusaidie katika huduma yetu. (Rom. 15:18, 19) Hata hivyo, ili roho takatifu ya Mungu itunufaishe kikamili, ni lazima tushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri na tutumie Biblia kadiri inavyowezekana. Njia moja ya kuboresha zaidi huduma yako ni kwa kutumia mapendekezo ya kuanzisha mazungumzo yaliyo katika Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha.

16. Taja njia ya moja kwa moja ya kupata roho takatifu.

16 Nne, sali kwa Yehova. (Mt. 7:7-11; Luka 11:13) Njia ya moja kwa moja ya kupata roho takatifu ni kwa kumwomba Yehova kupitia sala. Hakuna chochote kinachoweza kufanya sala zetu zisimfikie Yehova au kuzuia zawadi nzuri ya roho takatifu ya Mungu kutufikia—iwe ni kuta za gereza au hata Shetani mwenyewe. (Yak. 1:17) Tunapaswa kusali jinsi gani ili roho takatifu itunufaishe kikamili? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze kwa undani zaidi mambo fulani kuhusu sala kwa kuchunguza mfano unaopatikana katika Injili ya Luka pekee. *

SALI BILA KUACHA

17. Tunajifunza somo gani kuhusu sala kutokana na mfano wa Yesu kwenye Luka 11:5-9, 13?

17 Soma Luka 11:5-9, 13. Mfano huo wa Yesu unaonyesha jinsi tunavyopaswa kusali ili tupate roho takatifu. Mwanamume anayetajwa katika mfano huo alipata kitu alichohitaji ‘kwa sababu aliendelea kuomba’ kwa ujasiri. Hakuogopa kumwomba rafiki yake msaada hata ingawa ilikuwa usiku sana. (Tazama habari za utafiti kuhusu Luka 11:8 kwenye mwb 18 Julai 16-22.) Yesu alitumiaje mfano huo kufundisha kuhusu sala? Alisema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.” Tunajifunza nini? Ili tupate msaada wa roho takatifu, ni lazima tuendelee kumwomba Yehova bila kuacha.

18. Kulingana na mfano wa Yesu, kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatupatia roho takatifu?

18 Pia, mfano wa Yesu unatusaidia kuelewa kwa nini Yehova atatupatia roho yake takatifu. Mwanamume anayetajwa katika mfano huo alitaka kumtunza mgeni wake vizuri. Alihisi kwamba ni lazima amwandalie chakula mgeni huyo aliyefika usiku sana lakini hakuwa na chochote cha kumpa. Yesu alisema kwamba jirani yake alifungua mlango kwa sababu aliendelea kumwomba mkate kwa ujasiri. Yesu alikuwa akifundisha nini? Ikiwa mwanadamu asiye mkamilifu alikuwa tayari kumsaidia jirani yake aliyeendelea kumwomba mkate, je, Baba yetu wa mbinguni mwenye fadhili hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaoendelea kumwomba? Hivyo, tunaweza kusali tukiwa na uhakika kwamba Yehova atajibu sala yetu ya kumwomba roho takatifu tunapoihitaji.—Zab. 10:17; 66:19.

19. Kwa nini tuna hakika kwamba tutaibuka tukiwa washindi?

19 Tuna hakika kwamba licha ya jitihada zisizokoma za Shetani za kutushambulia, tutaibuka tukiwa washindi. Kwa nini? Kwa sababu roho takatifu hutusaidia katika njia mbili. Kwanza, inatupatia nguvu tunazohitaji ili tushinde majaribu. Pili, ndiyo nguvu au kani “inayojaza tanga zetu,” ikitusaidia kusonga mbele katika utumishi wetu kwa Yehova huku tukitazamia kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu. Acheni tuazimie kunufaika kikamili kutokana na msaada wa roho takatifu!

WIMBO 41 Tafadhali Sikiliza Sala Yangu

^ fu. 5 Makala hii inaeleza jinsi roho takatifu ya Mungu inavyoweza kutusaidia kuvumilia. Pia, inazungumzia jinsi roho takatifu inavyoweza kutunufaisha kikamili.

^ fu. 16 Luka, kuliko mwandikaji mwingine yeyote wa Injili, anakazia kwamba sala ilikuwa sehemu muhimu ya maisha ya Yesu.—Luka 3:21; 5:16; 6:12; 9:18, 28, 29; 18:1; 22:41, 44.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: HATUA YA 1: Ndugu na dada wakiwasili kwenye Jumba la Ufalme. Wanapokutanika pamoja na waamini wenzao, wanashirikiana pamoja nao mahali ambapo kuna roho takatifu. HATUA YA 2: Wamejitayarisha ili washiriki kwenye mikutano. Hatua hizo mbili zinahusika pia katika utendaji mwingine tuliozungumzia kwenye makala hii, yaani, kujifunza Neno la Mungu, kushiriki katika kazi ya kuhubiri, na kusali kwa Yehova.