Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 48

‘Malizeni Kile Mlichoanza Kufanya’

‘Malizeni Kile Mlichoanza Kufanya’

‘Malizeni kile mlichoanza kufanya.’—2 KOR. 8:11.

WIMBO 35 “Mhakikishe Mambo Muhimu Zaidi”

MUHTASARI *

1. Yehova anaturuhusu tufanye nini?

YEHOVA anaturuhusu tuchague njia tutakayofuata maishani. Anatufundisha jinsi ya kufanya maamuzi mazuri, na anatusaidia tufanikiwe tunapofanya maamuzi yanayomfurahisha. (Zab. 119:173) Kadiri tunavyotumia hekima inayopatikana katika Neno la Mungu, ndivyo tutakavyofanya maamuzi mazuri zaidi.—Ebr. 5:14.

2. Huenda tukakabili changamoto gani baada ya kufanya maamuzi?

2 Hata ingawa huenda tukafanya maamuzi ya hekima, bado inaweza kuwa vigumu kumaliza kile tulichoanza. Fikiria mifano ifuatayo: Ndugu kijana anaamua kusoma Biblia nzima. Anashikamana na ratiba yake kwa majuma kadhaa kisha anaiacha kwa sababu fulani. Dada anaamua kuwa painia wa kawaida lakini anaahirisha-ahirisha tarehe ya kuanza utumishi huo. Baraza la wazee linakubaliana kwa pamoja kufanya ziara nyingi zaidi za uchungaji, lakini baada ya miezi mingi bado hawajaanza. Hali hizo zinatofautiana lakini zinafanana kwa njia fulani. Maamuzi hayo yote hayakutekelezwa kikamili. Wakristo wa karne ya kwanza katika jiji la Korintho walikabili changamoto hiyo. Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwao.

3. Wakorintho walifanya uamuzi gani, lakini ni nini kilichotokea?

3 Katika mwaka wa 55 W.K., Wakorintho walifanya uamuzi fulani muhimu. Walipata habari kwamba ndugu zao huko Yerusalemu na Yudea walikuwa wakikabili hali ngumu na umaskini na kwamba makutaniko yalikuwa yakikusanya pesa ili kuwasaidia. Wakichochewa na moyo wenye fadhili na ukarimu, Wakorintho waliazimia kuwachangia ndugu zao wenye uhitaji na wakamuuliza mtume Paulo jinsi ya kufanya hivyo. Alituma mwongozo kwa kutaniko hilo na kumweka rasmi Tito ili asaidie kukusanya michango hiyo. (1 Kor. 16:1; 2 Kor. 8:6) Hata hivyo, miezi michache baadaye mtume Paulo alipata habari kwamba Wakorintho bado hawakuwa wametoa michango hiyo. Na kwa sababu hiyo, zawadi yao haingekuwa tayari ili kupelekwa Yerusalemu pamoja na michango ya makutaniko mengine.—2 Kor. 9:4, 5.

4. Kama inavyotajwa kwenye 2 Wakorintho 8:7, 10, 11, Paulo aliwatia moyo Wakorintho wafanye nini?

4 Wakorintho walikuwa wamefanya uamuzi mzuri na Paulo aliwapongeza kwa imani yao ya pekee na tamaa yao ya kuonyesha ukarimu kutoka moyoni. Lakini pia aliwatia moyo wamalize kile walichoanza. (Soma 2 Wakorintho 8:7, 10, 11.) Jambo hilo linatufundisha kwamba inaweza kuwa vigumu hata kwa Wakristo waaminifu kutekeleza uamuzi wao mzuri.

5. Tutajibu maswali gani?

5 Kama ilivyokuwa kwa Wakorintho, huenda ikawa vigumu kwetu kutekeleza maamuzi tuliyofanya. Kwa nini? Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, huenda tukawa na zoea la kuahirisha mambo. Au hali zisizotazamiwa zinaweza kufanya iwe vigumu kwetu kutimiza jambo tulilokuwa tumeamua kufanya. (Mhu. 9:11; Rom. 7:18) Tunaweza kuchunguza upya jinsi gani uamuzi tuliofanya na kuona ikiwa tunahitaji kuubadilisha? Na tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tunafanikiwa kumaliza kile tunachoanza?

KABLA YA KUFANYA UAMUZI

6. Kwa nini huenda tukahitaji kubadili uamuzi wetu?

6 Kuna baadhi ya maamuzi muhimu ambayo hatuwezi kuyabadili. Kwa mfano, tunashikamana na uamuzi wetu wa kumtumikia Yehova na tumeazimia kuwa waaminifu kwa mwenzi wetu wa ndoa. (Mt. 16:24; 19:6) Hata hivyo, kuna maamuzi mengine ambayo huenda tukahitaji kuyabadili. Kwa nini? Kwa sababu hali hubadilika. Ni hatua zipi zinazoweza kutusaidia tufanye maamuzi bora zaidi?

7. Tunapaswa kusali kuhusu nini, na kwa nini?

7 Sali ili upate hekima. Yehova alimwongoza Yakobo kuandika hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu.” (Yak. 1:5) Kwa njia fulani, sisi sote ‘tunakosa hekima.’ Hivyo, mtegemee Yehova unapofanya au kuchunguza upya uamuzi fulani. Kisha Yehova atakusaidia kufanya maamuzi ya hekima.

8. Ni utafiti gani tunaopaswa kufanya kabla ya kufanya uamuzi?

8 Fanya utafiti wa kina. Chunguza Neno la Mungu, soma machapisho ya tengenezo la Yehova, na uzungumze na watu unaowaamini. (Met. 20:18) Utafiti kama huo ni muhimu kabla ya kufanya uamuzi wa kubadili kazi, kuhama, au wa kuchagua elimu itakayokusaidia kutimiza huduma yako.

9. Tutanufaikaje ikiwa tutachunguza nia yetu tunapofanya uamuzi fulani?

9 Chunguza nia yako. Nia yetu ni jambo muhimu machoni pa Yehova. (Met. 16:2) Anataka tuwe wanyoofu katika mambo yote. Hivyo, tunapofanya maamuzi, tunapaswa kuchunguza nia yetu na kuwa wanyoofu kwa wengine. Ikiwa hatutakuwa wanyoofu kabisa kuhusu nia yetu, huenda tukashindwa kushikamana na uamuzi wetu. Kwa mfano, huenda ndugu kijana akaamua kuwa painia wa kawaida. Hata hivyo, baada ya muda fulani, anashindwa kutimiza takwa la saa na anapoteza shangwe katika huduma. Huenda alifikiri kwamba nia yake kuu ya kufanya upainia ilikuwa tamaa yake ya kumpendeza Yehova. Hata hivyo, huenda jambo kuu lililomchochea lilikuwa tamaa ya kuwapendeza wazazi wake au mtu fulani anayemheshimu.

10. Ni nini kinachohitajika ili mtu afanye mabadiliko?

10 Mfikirie mwanafunzi wa Biblia anayeamua kuacha kuvuta sigara. Mwanzoni anapambana na anafanikiwa kwa juma moja au mawili, kisha anashindwa na kuanza tena kuvuta sigara. Mwishowe, anafanikiwa kushinda zoea hilo! Upendo wake kwa Yehova na tamaa yake ya kumpendeza imemsaidia kushinda zoea hilo.—Kol. 1:10; 3:23.

11. Kwa nini tunapaswa kuwa na malengo hususa?

11 Uwe na malengo hususa. Ukiwa na malengo hususa itakuwa rahisi zaidi kwako kuyafikia. Kwa mfano, huenda uliamua kusoma Biblia mara nyingi zaidi. Hata hivyo, ikiwa huna ratiba hususa, huenda usifikie lengo lako. * Au huenda wazee kutanikoni wakaamua kufanya ziara za uchungaji mara nyingi zaidi, lakini baada ya muda wakashindwa kutimiza malengo yao. Ili wafanikiwe, wanaweza kujiuliza maswali yafuatayo: “Je, tumetambua ni ndugu na dada gani watakaonufaika hasa na ziara za uchungaji? Je, tumetenga wakati hususa wa kuwatembelea?”

12. Huenda tukahitaji kufanya nini, na kwa nini?

12 Ona mambo kihalisi. Hakuna yeyote kati yetu aliye na wakati, rasilimali, au nguvu za kufanya kila kitu ambacho angependa kufanya. Hivyo, ona mambo kihalisi na uwe na usawaziko. Hali ikikulazimu, huenda ukahitaji kubadili uamuzi ambao ulizidi uwezo wako wa kuutekeleza. (Mhu. 3:6) Hata hivyo, tuseme kwamba umeuchunguza tena uamuzi wako, ukaubadili kadiri inavyohitajika, na kuhisi kwamba sasa unaweza kuutekeleza. Fikiria hatua tano zinazoweza kukusaidia umalize kile ulichoanza kufanya.

HATUA ZITAKAZOKUSAIDIA UTEKELEZE UAMUZI WAKO

13. Unaweza kupataje nguvu unazohitaji ili kutekeleza uamuzi wako?

13 Sali upate nguvu za kutenda. Mungu anaweza kukupa “nguvu za kutenda” na kutekeleza uamuzi wako. (Flp. 2:13) Hivyo, mwombe Yehova akupatie roho yake takatifu ili uwe na nguvu unazohitaji. Endelea kusali hata ikiwa unahisi kwamba sala yako haijibiwi kwa wakati. Yesu alisema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa [roho takatifu].”—Luka 11:9, 13.

14. Kanuni inayotajwa kwenye Methali 21:5 inaweza kukusaidiaje kutekeleza uamuzi wako?

14 Weka mipango hususa. (Soma Methali 21:5.) Ili kukamilisha mradi wowote unaoanzisha, unahitaji kuwa na mpango hususa. Kisha unahitaji kushikamana kabisa na mpango huo. Vivyo hivyo, unapofanya uamuzi fulani, orodhesha hatua zote unazokusudia kufuata ili kutekeleza uamuzi huo. Ikiwa jambo ulilokusudia kufanya ni kubwa unaweza kuligawanya katika vipengele vidogovidogo ili uweze kufuatilia maendeleo yako kwa urahisi zaidi. Paulo aliwatia moyo Wakorintho waweke kando kitu fulani kama mchango “siku ya kwanza ya kila juma” badala ya kusubiri na kujaribu kukusanya michango hiyo wakati alipofika. (1 Kor. 16:2) Kugawanya kazi kubwa katika vipengele vidogovidogo kunaweza kukusaidia usihisi umelemewa.

15. Unaweza kufanya nini baada ya kuweka mipango hususa?

15 Ikiwa utaandika jambo hususa ulilopanga kufanya, itakuwa rahisi zaidi kulitekeleza. (1 Kor. 14:40) Kwa mfano, baraza la wazee limepewa mwongozo kwamba wanapaswa kumpa mzee mmoja mgawo wa kuandika kila uamuzi uliofanywa na baraza la wazee, kutia ndani wale waliopewa mgawo fulani hususa na tarehe ya kuukamilisha. Itakuwa rahisi zaidi kwa wazee wanaofuata mwongozo huo kutekeleza maamuzi yao. (1 Kor. 9:26) Unaweza kujaribu kufanya hivyo inapohusu mambo yako ya kibinafsi. Kwa mfano, unaweza kutayarisha orodha ya mambo unayotaka kufanya kila siku na kuyaorodhesha kulingana na jinsi utakavyoyatimiza. Jambo hilo litakusaidia umalize yale uliyoanza kufanya na utimize mengi zaidi ndani ya muda mfupi.

16. Unahitaji kufanya nini ili kutimiza uamuzi wako, na andiko la Waroma 12:11 linaungaje mkono jambo hilo?

16 Tia bidii. Unahitaji kujikakamua ili kutekeleza na kumaliza mambo uliyoanza kufanya. (Soma Waroma 12:11.) Paulo alimwambia Timotheo ‘aendelee kujitahidi’ na ‘aendelee’ kuwa mwalimu mzuri. Ushauri huo unahusu pia malengo mengine ya kiroho.—1 Tim. 4:13, 16.

17. Andiko la Waefeso 5:15, 16 linaweza kutusaidiaje kutekeleza uamuzi wetu?

17 Tumia wakati wako kwa hekima. (Soma Waefeso 5:15, 16.) Tenga wakati wa kutekeleza uamuzi wako na ushikamane nao. Epuka kusubiri mpaka hali zitakapokuwa nzuri kabisa ndipo uanze kutekeleza uamuzi wako; huenda wakati huo usifike kamwe. (Mhu. 11:4) Uwe mwangalifu ili mambo yasiyo muhimu sana yasimalize wakati na nguvu unazohitaji ili kutimiza mambo muhimu zaidi. (Flp. 1:10) Ikiwezekana, tenga wakati wa kufanya mambo hayo wakati ambapo wengine hawatakukengeusha. Wajulishe wengine kwamba unahitaji wakati wa kukazia fikira jambo unalofanya. Pia, unaweza kuamua kuzima simu na kusoma barua pepe au jumbe kwenye mitandao ya kijamii baadaye. *

18-19. Ni nini kinachoweza kukusaidia usife moyo unapokabili mambo yanayokuzuia kutekeleza uamuzi wako?

18 Kazia fikira matokeo mazuri utakayopata. Matokeo ya uamuzi wako ni kama mwisho wa safari yako. Hata ikiwa barabara imefungwa, ikiwa kwa kweli unatamani kufika mwisho wa safari yako, utaendelea kusafiri hata ikiwa utalazimika kutafuta barabara nyingine ili kufika huko. Kwa njia hiyohiyo, ikiwa tutakazia fikira matokeo mazuri ya maamuzi yetu, hatutakufa moyo kwa urahisi tunapokabili vizuizi au tunapohitaji kutafuta njia nyingine.—Gal. 6:9.

19 Si rahisi kufanya maamuzi mazuri, na inaweza kuwa changamoto kuyatekeleza. Lakini kwa msaada wa Yehova, unaweza kupata hekima na nguvu unazohitaji ili kumaliza kile ulichoanza kufanya.

WIMBO 65 Songa Mbele!

^ fu. 5 Je, unajutia baadhi ya maamuzi uliyofanya? Au je, nyakati nyingine inakuwa vigumu kwako kufanya maamuzi mazuri na kuyatekeleza? Makala hii itakusaidia kupambana na changamoto hizo na kumaliza kile ulichoanza kufanya.

^ fu. 11 Ili kupata msaada wa kupanga ratiba ya usomaji wako wa Biblia, unaweza kutumia “Ratiba ya Usomaji wa Biblia” inayopatikana katika tovuti ya jw.org®.

^ fu. 17 Ili upate habari zaidi kuhusu jinsi ya kutumia vizuri wakati wako, tazama makala “Mbinu 20 za Kutafuta Wakati Zaidi” kwenye toleo la Aprili 2010 la gazeti Amkeni!