Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 46

Uwe Jasiri​—Yehova Ni Msaidizi Wako

Uwe Jasiri​—Yehova Ni Msaidizi Wako

“Sitakuacha wala kukutupa kamwe.” —EBR. 13:5.

WIMBO 55 Msiwaogope!

MUHTASARI *

1. Ni nini kitakachotufariji tunapohisi kwamba tuko peke yetu au tumelemewa na matatizo? (Zaburi 118:5-7)

JE, UMEWAHI kuhisi kwamba uko peke yako, na kwamba hakuna mtu wa kukusaidia kukabiliana na matatizo unayopitia? Watu wengi wamewahi kuhisi hivyo, kutia ndani watumishi waaminifu wa Yehova. (1 Fal. 19:14) Ikiwa utapitia hali kama hiyo, kumbuka ahadi hii ya Yehova: “Sitakuacha wala kukutupa kamwe.” Hivyo tunaweza kusema hivi kwa uhakika: “Yehova ni msaidizi wangu, sitaogopa.” (Ebr. 13:5, 6) Mtume Paulo aliwaandikia maneno hayo waamini wenzake huko Yudea karibu mwaka wa 61 W.K. Maneno yake yanatukumbusha mambo ambayo mtunga zaburi aliandika kwenye Zaburi 118:5-7.​—Soma.

2. Tutachunguza nini katika makala hii, na kwa nini?

2 Kama ilivyokuwa kwa mtunga zaburi, Paulo alijua kwamba Yehova alikuwa Msaidizi wake kwa sababu ya mambo aliyojionea maishani. Kwa mfano, miaka miwili kabla ya kuandika barua yake kwa Waebrania, Paulo aliokoka dhoruba kali alipokuwa akisafiri baharini. (Mdo. 27:4, 15, 20) Katika safari hiyo yote na kipindi kilichotangulia safari hiyo, Yehova alithibitika kuwa Msaidizi wa Paulo katika njia mbalimbali. Tutachunguza njia tatu kati ya hizo. Yehova alimsaidia Paulo kupitia Yesu na malaika, watu wenye mamlaka, na waabudu wenzake. Kuchunguza matukio hayo katika maisha ya Paulo, kutaimarisha tumaini letu katika ahadi ya Mungu kwamba atajibu sala zetu za kuomba msaada.

MSAADA KUTOKA KWA YESU NA MALAIKA

3. Huenda Paulo alijiuliza swali gani, na kwa nini?

3 Paulo alihitaji msaada. Karibu mwaka wa 56 W.K., umati ulimkokota nje ya hekalu huko Yerusalemu na kujaribu kumuua. Siku iliyofuata maadui wa Paulo walikuwa karibu kumrarua-rarua alipokuwa mbele ya Sanhedrini. (Mdo. 21:30-32; 22:30; 23:6-10) Wakati huo, huenda Paulo alijiuliza, ‘Nitaweza kuvumilia hali hii hadi lini?’

4. Yehova alimtumiaje Yesu kumsaidia Paulo?

4 Paulo alipata msaada gani? Usiku uliofuata, “Bwana,” yaani, Yesu, alisimama kando yake na kumwambia: “Jipe moyo! Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili kunihusu katika Yerusalemu, ndivyo utakavyotoa ushahidi huko Roma pia.” (Mdo. 23:11) Alitiwa moyo kwa wakati unaofaa! Yesu alimpongeza Paulo kwa ushahidi ambao alikuwa ametoa huko Yerusalemu. Na aliahidi kwamba Paulo atafika salama Roma, ambako pia angetoa ushahidi. Baada ya kupata uhakikisho huo, lazima Paulo alihisi akiwa salama kama mtoto aliyebebwa mikononi mwa baba yake.

Wakati wa dhoruba kali baharini, malaika anamhakikishia Paulo kwamba kila mtu kwenye meli ataokoka safiri hiyo yenye hatari (Tazama la fungu la 5)

5. Yehova alimsaidiaje Paulo kupitia malaika? (Tazama picha kwenye jalada.)

5 Paulo alikabili changamoto gani nyingine? Miaka miwili hivi baada ya matukio hayo huko Yerusalemu, Paulo alikuwa amepanda meli iliyokuwa ikielekea Italia wakati meli hiyo ilipopigwa na dhoruba kali hivi kwamba mabaharia na abiria walifikiri kwamba wangekufa. Hata hivyo, Paulo hakuogopa. Kwa nini? Aliwaambia hivi wale waliokuwa ndani ya meli: “Usiku huu malaika wa Mungu ambaye mimi ni mali yake na ambaye ninamtolea utumishi mtakatifu, alisimama kando yangu akasema: ‘Usiogope Paulo. Utasimama mbele ya Kaisari, na tazama! Mungu amekupa wale wote wanaosafiri pamoja nawe.’” Yehova alikuwa amemtumia malaika kurudia ahadi ambayo hapo awali alikuwa amempa Paulo kupitia Yesu. Na kwa kweli, Paulo alifika Roma.​—Mdo. 27:20-25; 28:16.

6. Ni ahadi gani ya Yesu inayoweza kutuimarisha, na kwa nini?

6 Sisi tunapata msaada gani? Yesu atatutegemeza kama alivyofanya kwa Paulo. Kwa mfano, Yesu anawaahidi hivi wale wote wanaomfuata: “Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Maneno ya Yesu yanaweza kutuimarisha. Kwa nini? Kwa sababu nyakati nyingine ni vigumu kwetu kuvumilia. Kwa mfano, tunapofiwa na mpendwa wetu, ni lazima tuvumilie maumivu hayo si kwa siku chache tu, bali huenda tutahitaji kuvumilia maumivu hayo kwa miaka mingi. Wengine wanalazimika kukabiliana na matatizo yanayotokana na uzee. Na bado kuna siku ambazo wengine wanalemewa na hisia za kushuka moyo. Hata hivyo, tunapata nguvu za kuendelea kuvumilia kwa sababu tunajua kwamba Yesu yupo pamoja nasi sikuzote,”  hata zile siku ngumu zaidi maishani mwetu.​—Mt. 11:28-30.

Malaika wanatutegemeza na kutuongoza tunaposhiriki katika kazi ya kuhubiri (Tazama fungu la 7)

7. Kulingana na Ufunuo 14:6, Yehova anatusaidiaje leo?

7 Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova anatusaidia kupitia malaika wake. (Ebr. 1:7, 14) Kwa mfano, malaika wanatutegemeza na kutuongoza tunapowahubiria “habari njema ya Ufalme” watu wa “kila taifa na kabila na lugha.”​—Mt. 24:13, 14; soma Ufunuo 14:6.

MSAADA KUTOKA KWA WENYE MAMLAKA

8. Yehova alimsaidiaje Paulo kupitia kamanda wa jeshi?

8 Paulo alipata msaada gani? Katika mwaka wa 56 W.K., Yesu alimhakikishia Paulo kwamba angefika Roma. Hata hivyo, baadhi ya Wayahudi huko Yerusalemu walipanga njama ya kumshambulia Paulo na kumuua. Klaudio Lisia, kamanda wa jeshi la Roma, alipoambiwa kuhusu njama hiyo, alimsaidia Paulo. Bila kukawia, Klaudio alimpeleka Paulo Kaisaria huku akiwa analindwa na wanajeshi wengi, wakipitia barabara yenye urefu wa kilomita 105 hivi kutoka Yerusalemu. Akiwa huko Kaisaria, Gavana Feliksi aliamuru kwamba Paulo “awekwe chini ya ulinzi katika jumba la kifalme la Herode.” Wayahudi waliotaka kumuua Paulo wasingeweza kumuua akiwa huko.​—Mdo. 23:12-35.

9. Gavana Festo alimsaidiaje Paulo?

9 Miaka miwili baadaye, bado Paulo alikuwa chini ya ulinzi huko Kaisaria. Festo alikuwa amechukua mahali pa Feliksi akiwa gavana mpya. Wayahudi walimsihi Festo ampeleke Paulo Yerusalemu ili akahukumiwe, lakini Festo alikataa. Huenda gavana huyo alijua kwamba Wayahudi walikuwa “wanapanga kumvizia Paulo na kumuua barabarani.”​—Mdo. 24:27-25:5.

10. Gavana Festo alifanya nini Paulo alipomwomba akahukumiwe na Kaisari?

10 Baadaye, kesi ya Paulo iliendeshwa akiwa Kaisaria. Kwa kuwa Festo alitaka kukubaliwa na Wayahudi, alimuuliza Paulo hivi: “Je, ungependa kupanda kwenda Yerusalemu ukahukumiwe huko mbele yangu?” Paulo alijua kwamba huenda angeuawa Yerusalemu, na pia alijua jambo la kufanya ili aokoe uhai wake, afike Roma, na kutimiza huduma yake. Alisema hivi: “Ninakata rufaa kwa Kaisari.” Baada ya kuzumgumza na baraza la washauri, Festo alimwambia hivi Paulo: “Umekata rufaa kwa Kaisari, nawe utaenda kwa Kaisari.” Uamuzi wa Festo wa kumpeleka Paulo Roma, ulimwokoa Paulo kutoka kwa maadui wake. Baada ya muda mfupi, Paulo angekuwa Roma, mbali kabisa na Wayahudi ambao walikuwa wanataka kumuua.​—Mdo. 25:6-12.

11. Huenda Paulo alitafakari maneno gani yenye kutia moyo yaliyosemwa na nabii Isaya?

11 Paulo alipokuwa akisubiri kuanza safari yake ya kwenda Italia, huenda alitafakari kwa makini onyo ambalo nabii Isaya aliongozwa na roho kuwapa wale waliompinga Yehova: “Fanyeni mpango, lakini utavunjwa! Semeni mnachotaka, lakini hakitafanikiwa, kwa maana Mungu yuko pamoja nasi!” (Isa. 8:10) Paulo alijua kwamba Mungu angemsaidia, na jambo hilo lazima lilimwimarisha sana alipokabili majaribu yaliyokuwa mbele yake.

Kama alivyofanya wakati uliopita, leo Yehova anaweza kuwachochea wenye mamlaka wawalinde watumishi wake (Tazama fungu la 12)

12. Yulio alimtendeaje Paulo, na huenda hilo lilimfanya Paulo atambue nini?

12 Katika mwaka wa 58 W.K., Paulo alianza safari yake ya kuelekea Roma. Kwa sababu alikuwa mfungwa, aliwekwa chini ya uangalizi wa ofisa wa jeshi Mroma aliyeitwa Yulio. Kuanzia wakati huo na kuendelea, Yulio alikuwa na mamlaka ya kufanya maisha ya Paulo yawe magumu au yawe rahisi. Yulio angetumiaje mamlaka yake? Siku iliyofuata, walipofika kituo chao cha kwanza, “Yulio [alimtendea] Paulo kwa fadhili na kumruhusu aende kwa rafiki zake.” Baadaye, Yulio hata aliokoa uhai wa Paulo. Jinsi gani? Wanajeshi walitaka kuwaua wafungwa wote waliokuwa kwenye meli, lakini Yulio aliwazuia. Kwa nini? Alikuwa “ameazimia kumfikisha Paulo salama.” Inaelekea Paulo alitambua kwamba Yehova alikuwa anamtumia ofisa huyo mwenye fadhili ili kumsaidia na kumlinda.​—Mdo. 27:1-3, 42-44.

Tazama fungu la 13

13. Yehova anaweza kuwatumiaje watu wenye mamlaka?

13 Sisi tunapata msaada gani? Yehova anaweza kuitumia roho yake takatifu yenye nguvu kuwafanya watu wenye mamlaka watende kulingana na mapenzi yake, ikiwa hilo linapatana na kusudi lake. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Moyo wa mfalme ni kama vijito vya maji mkononi kwa Yehova. Yeye huuelekeza mahali popote anapopenda.” (Met. 21:1) Methali hiyo inamaanisha nini? Wanadamu wanaweza kuchimba mfereji ili kuyafanya maji ya kijito yaelekee mahali wanakotaka. Vivyo hivyo, Yehova anaweza kuitumia roho yake kuelekeza mawazo ya watawala yapatane na kusudi lake. Jambo hilo linapotokea, watu wenye mamlaka huchochewa kufanya maamuzi yatakayowanufaisha watu wa Mungu.​—Linganisha Ezra 7:21, 25, 26.

14. Kulingana na Matendo 12:5, tunaweza kusali kwa ajili ya akina nani?

14 Tunaweza kufanya nini? Tunaweza kusali “kwa ajili ya . . . wafalme na wote wenye mamlaka” pindi wanapohitaji kufanya maamuzi ambayo yanaweza kuathiri maisha na huduma yetu ya Kikristo. (1 Tim. 2:1, 2, maelezo ya chini; Neh. 1:11) Kama Wakristo wa karne ya kwanza walivyofanya, sisi pia tunasali kwa bidii kwa Mungu kwa ajili ya ndugu na dada zetu ambao wako gerezani. (Soma Matendo 12:5; Ebr. 13:3) Zaidi ya hilo, tunaweza kusali kwa ajili ya walinzi wa gereza wanaowasimamia ndugu na dada zetu. Tunaweza kumsihi Yehova aelekeze mawazo ya watu kama hao, ili wachochewe kutenda kama Yulio na kuwatendea waamini wenzetu waliofungwa gerezani “kwa fadhili za kibinadamu.”​—Mdo. 27:3, maelezo ya chini.

MSAADA KUTOKA KWA WAAMINI WENZETU

15-16. Yehova alimsaidiaje Paulo kupitia Aristarko na Luka?

15 Paulo alipata msaada gani? Wakati wa safari yake kuelekea Roma, Paulo alipokea tena na tena msaada ambao Yehova aliandaa kupitia waabudu wenzake. Acheni tuchunguze baadhi ya mifano hiyo.

16 Marafiki wawili wa Paulo walio waaminifu, Aristarko na Luka, waliamua kusafiri pamoja naye kwenda Roma. * Walihatarisha uhai wao kwa hiari ili wawe na Paulo, ingawa inaelekea hakuna hata mmoja wao aliyehakikishiwa kibinafsi na Yesu kwamba angefika Roma. Walikuja kutambua baadaye, wakati wa safari yao yenye msukosuko, kwamba wangefika salama. Hivyo, Aristarko na Luka walipopanda meli huko Kaisaria, ni lazima Paulo alisali kutoka moyoni kwa Yehova akimshukuru kwa msaada alioandaa kupitia waabudu hao wenzake wenye ujasiri.​—Mdo. 27:1, 2, 20-25.

17. Yehova alimsaidiaje Paulo kupitia waamini wenzake?

17 Wakati wa safari yake, Paulo alisaidiwa na waabudu wenzake mara kadhaa. Kwa mfano, katika bandari ya jiji la Sidoni, Yulio alimruhusu Paulo “aende kwa rafiki zake akatunzwe nao.” Na baadaye, katika jiji la Puteoli, Paulo na wenzake ‘walikutana na akina ndugu, wakawasihi wakae pamoja nao kwa siku saba.’ Akina ndugu katika maeneo hayo walipokuwa wakishughulikia mahitaji ya Paulo na rafiki zake, bila shaka aliwafanya wenyeji wake washangilie sana kwa kuwasimulia mambo yenye kujenga. (Linganisha Matendo 15:2, 3.) Baada ya ziara hiyo yenye kutia moyo, Paulo na waandamani wake waliendelea na safari.—Mdo. 27:3; 28:13, 14.

Kama Paulo, tunapokea msaada kutoka kwa Yehova kupitia waamini wenzetu (Tazama fungu la 18)

18. Ni nini kilichomchochea Paulo amshukuru Mungu na kujipa moyo?

18 Kadiri Paulo alivyokaribia kufika Roma, ni lazima alitafakari kuhusu maneno haya aliyoliandikia kutaniko lililokuwa katika jiji hilo, miaka mitatu iliyopita: “Kwa miaka mingi nimetamani kuja kwenu.” (Rom. 15:23) Hata hivyo, hakutarajia kwamba angeenda huko akiwa mfungwa. Wazia jinsi alivyotiwa moyo alipowaona akina ndugu kutoka Roma wakiwa wanamsubiri barabarani ili kumsalimu! “Paulo alipowaona akamshukuru Mungu na kujipa moyo.” (Mdo. 28:15) Ona kwamba Paulo alimshukuru Mungu alipowaona akina ndugu. Kwa nini? Kwa sababu kwa mara nyingine tena, Paulo aliona Yehova akimsaidia kupitia waamini wenzake.

Tazama fungu la 19

19. Kama inavyotajwa kwenye 1 Petro 4:10, Yehova anaweza kututumiaje ili kuwasaidia wale walio na uhitaji?

19 Tunaweza kufanya nini? Je, unamfahamu ndugu au dada katika kutaniko lako ambaye anateseka kwa sababu ya ugonjwa au kwa sababu anapitia hali nyingine ngumu maishani? Au huenda wamepoteza mpendwa wao katika kifo. Tukifahamu kwamba kuna mtu fulani anayehitaji msaada, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie kusema au kufanya jambo fulani la fadhili na upendo. Huenda maneno na matendo yetu yakawa ndiyo kitia moyo ambacho ndugu au dada yetu anahitaji. (Soma 1 Petro 4:10.) * Wale tunaowasaidia wanaweza kuamini kwa mara nyingine tena kwamba ahadi ya Yehova, inayosema “Sitakuacha wala kukutupa kamwe,” inawahusu wao pia. Je, hilo halingekufanya uwe mwenye shangwe?

20. Kwa nini tunaweza kusema kwa uhakika: “Yehova ni msaidizi wangu”?

20 Kama ilivyokuwa katika kisa cha Paulo na waandamani wake, sisi pia tunakumbana na dhoruba kali katika safari yetu ya maisha. Wakati huohuo, tunajua kwamba tunaweza kuwa na ujasiri kwa sababu Yehova yuko pamoja nasi. Anatusaidia kupitia Yesu na malaika. Pia, ikiwa inapatana na kusudi lake Yehova anaweza kutusaidia kupitia watu wenye mamlaka. Na kama ambavyo wengi wetu tumejionea kibinafsi, Yehova huitumia roho yake takatifu kuichochea mioyo ya ndugu na dada zetu ili watusaidie. Hivyo, kama Paulo tuna sababu nzuri ya kusema hivi kwa uhakika: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?”​—Ebr. 13:6.

WIMBO 38 Atakupa Nguvu

^ fu. 5 Katika makala hii tutazungumzia njia tatu ambazo Yehova alimsaidia mtume Paulo kuvumilia matatizo. Kuchunguza jinsi ambavyo Yehova alithibitika kuwa Msaidizi wakati uliopita, kutaimarisha uhakika wetu kwamba atatusaidia leo tunapokabili matatizo.

^ fu. 16 Awali, Aristarko na Luka walikuwa wameandamana na Paulo kwenye safari zake. Pia, wanaume hao washikamanifu walibaki pamoja na Paulo alipokuwa mfungwa huko Roma.—Mdo. 16:10-12; 20:4; Kol. 4:10, 14.