Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onésime na Géraldine

Yehova Huwabariki Wale Wanaorudi Katika Nchi Walizozaliwa

Yehova Huwabariki Wale Wanaorudi Katika Nchi Walizozaliwa

IDADI kubwa ya ndugu na dada ambao awali walihama kutoka katika nchi walizozaliwa na kwenda nchi za Magharibi wamerudi katika nchi zao. Wakichochewa na upendo wao kwa Yehova na kwa wanadamu wenzao, wamehamia kwenye maeneo yaliyo na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. (Mt. 22:37-39) Wamedhabihu mambo gani, na wamepata baraka gani? Ili kupata jibu acheni tukazie fikira nchi ya Kamerun huko Afrika Magharibi.

“MAHALI SAHIHI KWA AJILI YA KUVUA”

Mwaka wa 1998 ndugu anayeitwa Onésime alihama kutoka nchi aliyozaliwa ya Kamerun. Kwa miaka 14 ameishi katika nchi ya kigeni. Siku moja akiwa kwenye mkutano wa kutaniko alisikia mfano kuhusu kazi ya kuhubiri. Msemaji alisema hivi: “Ikiwa marafiki wawili walikuwa wanavua kwenye maeneo tofauti na mmoja wao alikuwa akivua samaki wengi zaidi kuliko mwingine, je, yule ambaye alikuwa anavua samaki wachache hatahamia eneo ambalo samaki wengi wanapatikana?”

Mfano huo ulimchochea Onésime afikirie kurudi kwenye eneo la uvuvi wa kiroho lenye matokeo zaidi nchini Kamerun ili awasaidie wahubiri wenyeji. Lakini alikuwa na wasiwasi. Je, angeweza kuzoea kuishi tena Kamerun baada ya kuishi nchi za nje kwa miaka yote hiyo? Ili kuona kama atafaulu Onésime alitembelea Kamerun kwa miezi sita. Kisha mwaka wa 2012, aliamua kuishi moja kwa moja nchini Kamerun.

Onésime anasimulia hivi: “Nilihitaji kuzoea hali ya hewa ya joto na hali mpya ya maisha. Kwenye Jumba la Ufalme nilihitaji kuzoea tena kuketi kwenye mabenchi.” Kisha anasema hivi huku akitabasamu: “Lakini kadiri nilivyokazia zaidi programu ndivyo kumbukumbu ya viti vyenye kustarehesha ilivyopotea.”

Mwaka wa 2013, Onésime alimwoa Géraldine ambaye alikuwa amerudi Kamerun baada ya kuishi Ufaransa kwa miaka tisa. Wenzi hao wa ndoa walipata baraka gani kwa kutanguliza utendaji wa kitheokrasi maishani? Onésime anasema hivi: “Tulihudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme tukiwa wenzi na tulitumikia Betheli. Mwaka uliopita wanafunzi 20 wa Biblia katika kutaniko letu walibatizwa. Sasa ninahisi kwamba niko mahali sahihi kwa ajili ya kuvua. (Marko 1:17, 18) Géraldine anaongezea hivi: “Nimepata baraka nyingi zaidi kuliko nilivyotarajia.”

SHANGWE YA KUPATA WATOTO WA KIROHO

Judith na Sam-Castel

Judith alikuwa amehamia Marekani lakini alitamani sana kupanua huduma yake. Anasema hivi: “Muda wa kuondoka ulipofika baada ya kuitembelea familia yangu nchini Kamerun, nililia kwa sababu nilihitaji kuwaacha watu ambao nilikuwa nimeanza kujifunza Biblia pamoja nao. Hata hivyo, Judith alisita kuhamia Kamerun. Alikuwa na kazi yenye mshahara mnono ambayo ilimwezesha kulipia gharama za matibabu ya baba yake ambaye alikuwa anaishi Kamerun. Hata hivyo, kwa kumtumaini Yehova alihamia Kamerun. Anakiri kwamba anakosa baadhi ya vitu alivyokuwa anafurahia alipokuwa akiishi Marekani. Alisali kwa Yehova ili amsaidie kuzoea hali mpya na aliimarishwa na kitia moyo alichopata kutoka kwa mwangalizi wa mzunguko na mke wake.

Akikumbuka wakati huo, Judith anasema hivi: “Katika kipindi cha miaka mitatu nilifurahia kupata watoto wanne wa kiroho.” Judith alianza kutumikia akiwa painia wa pekee. Leo anaandamana na mume wake, Sam-Castel, katika kazi ya kuzungukia makutaniko. Lakini ilikuwaje kwa baba ya Judith? Judith na familia yake walifaulu kupata hospitali nje ya nchi iliyokuwa tayari kufadhili matibabu ya upasuaji wa baba yake. Inapendeza kwamba upasuaji ulifanikiwa.

WANAJIONEA UTEGEMEZO WA YEHOVA

Caroline na Victor

Ndugu anayeitwa Victor alihamia Kanada. Baada ya kusoma makala katika gazeti la Mnara wa Mlinzi iliyozungumzia elimu ya juu, alitafakari kuhusu masomo yake. Aliacha kusoma chuo kikuu, naye akaanza kusoma masomo ya ufundi ya muda mfupi. Anaeleza hivi: “Hilo lilinisaidia kupata kazi haraka na kufanya kazi ambayo nilitamani kuifanya kwa muda mrefu, yaani upainia. Baadaye Victor alimwoa Caroline, na wakatembelea Kamerun. Wakiwa huko walitembelea ofisi ya tawi na wakatiwa moyo kufikiria uwezekano wa kutumikia nchini Kamerun. Victor anasema hivi: “Hatukuwa na sababu yoyote ya kukataa, na kwa kuwa tulikuwa tumerahisisha maisha yetu tulikubali mwaliko huo. Ingawa Caroline alikuwa na matatizo fulani ya kiafya, waliamua kuendelea na mipango ya kuhama.

Victor na Caroline walianza kutumikia wakiwa mapainia wa kawaida ili kuwasaidia watu waliopendezwa waliopatikana katika huduma ya shambani. Kwa muda fulani, walijitegemeza kupitia pesa walizokuwa wametunza. Baadaye, walirudi Kanada ili kufanya kazi kwa miezi michache, jambo linalowawezesha kurudi tena Kamerun na kuendelea na upainia. Walipata baraka gani? Walihudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, wakatumikia wakiwa mapainia wa pekee, na sasa wanatumikia wakiwa watumishi wa ujenzi. Victor anasema hivi: “Kuacha maisha tuliyoyazoea kulituruhusu tujionee utegemezo wa Yehova.”

SHANGWE YA KUWASAIDIA WATU WAJIWEKE WAKFU KWA YEHOVA

Stéphanie na Alain

Mwaka wa 2002, Alain, mwanafunzi wa chuo kikuu nchini Ujerumani alisoma trakti yenye kichwa, “Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu?” Habari alizosoma zilimchochea kujiwekea malengo mapya. Mwaka wa 2006, alihudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma na kupewa mgawo wa kwenda nchini Kamerun, nchi aliyozaliwa.

Nchini Kamerun alipata kazi aliyokuwa akifanya kwa saa chache. Baadaye, alipata kazi yenye mshahara mzuri, lakini alikuwa na wasiwasi kwamba ingemfanya atumie muda mchache zaidi katika huduma. Hivyo, alipoalikwa atumikie akiwa painia wa pekee, alikubali bila kusita. Mwajiri wake alimwambia angemwongezea mshahara, lakini Alain alishikamana na uamuzi wake. Baadaye Alain alimwoa Stéphanie aliyekuwa ameishi kwa miaka mingi nchini Ufaransa. Stéphanie alikabili changamoto gani alipohamia Kamerun?

Stéphanie anaeleza hivi: “Nilikuwa na mizio pamoja na matatizo mengine madogo-madogo ya afya, lakini nilifanikiwa kupata matibabu kwa ukawaida na nikapata nafuu.” Wenzi hao wa ndoa walithawabishwa kwa uvumilivu wao. Alain anasimulia hivi: “Tulipoenda kuhubiri kwenye kijiji fulani cha mbali kinachoitwa Katé, tulikutana na watu kadhaa waliotaka kujifunza Biblia. Baadaye, tuliweza kujifunza nao Biblia kwa kutumia simu. Wawili kati ya wanafunzi hao walibatizwa na kikundi cha wahubiri kikaanzishwa.” Stéphanie anaongezea hivi: “Hakuna shangwe kubwa inayoweza kulinganishwa na shangwe ya kuwasaidia watu wajiweke wakfu kwa Yehova. Kwa kutumikia hapa tumejionea shangwe hiyo mara nyingi. Leo, Alain na Stéphanie wanazungukia makutaniko.

“TULIFANYA KILE TULICHOPASWA KUFANYA”

Léonce na Gisèle

Gisèle alibatizwa alipokuwa anasomea udaktari nchini Italia. Alivutiwa na maisha rahisi ambayo wenzi wa ndoa mapainia waliomfundisha Biblia walikuwa wakiishi, na alitaka kufanya mengi zaidi katika huduma. Hivyo, Gisèle alianza kutumikia akiwa painia wa kawaida huku akimalizia masomo yake.

Gisèle alikuwa anatamani kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova nchini Kamerun, lakini alikuwa na wasiwasi. Anasema hivi: “Nilihitaji kukubali kupoteza kibali cha kuishi nchini Italia na kutenganishwa na marafiki na watu wa familia waliokuwa wakiishi nchini humo.” Licha ya hayo, mwezi wa Mei 2016 Gisèle alirudi kuishi Kamerun. Baadaye aliolewa na Léonce, na ofisi ya tawi nchini Kamerun ikapendekeza kwamba wahamie Ayos, mji uliokuwa na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme.

Maisha yalikuwaje huko Ayos? Gisèle anaeleza hivi: “Mara nyingi hakukuwa na umeme kwa majuma mengi na tusingeweza kuchaji simu zetu. Muda mwingi hatungeweza kutumia simu zetu. Nilijifunza kupikia jiko la kuni, na tulienda kuchota maji kwa toroli na tochi usiku wakati hakukuwa na watu wengi kwenye chemchemi ya maji. Wenzi hao walikabilianaje na hali hiyo? Gisèle anasema hivi: “Roho takatifu ya Yehova, mwenzi wa ndoa anayejali, kitia moyo na pindi kwa pindi utegemezo wa kifedha kutoka kwa watu wa familia na marafiki ni mambo yaliyotusaidia wakati huo.”

Je, Gisèle anafurahi kwamba alirudi nchini kwao? Anasema hivi: “Ndiyo! Bila shaka yoyote! Mwanzoni kulikuwa na hali ngumu na tulivunjika moyo, lakini tuliposhinda mambo hayo yote, mimi na mume wangu tuliona kwamba tumefanya kile tulichopaswa kufanya. Tunamtumaini Yehova na tunahisi tuko karibu naye zaidi.” Léonce na Gisèle walihudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, na sasa wanatumikia wakiwa mapainia wa pekee wa muda.

Kama wavuvi wanaokabiliana na hali mbalimbali kwa ujasiri ili wavue samaki wengi, wale wanaorudi kwenye nchi walizozaliwa wanajidhabihu kwa hiari ili wawasaidie watu wenye mioyo minyoofu wanaokubali ujumbe wa Ufalme. Bila shaka, Yehova atawakumbuka wahubiri hao wenye bidii kwa upendo walioonyesha kwa ajili ya jina lake. (Neh. 5:19; Ebr. 6:10) Ikiwa unaishi katika nchi ya kigeni na kuna uhitaji wa wahubiri katika nchi uliyozaliwa, je unaweza kurudi? Ukifanya hivyo Yehova atakubariki.​—Met. 10:22.