Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

1918​—Miaka Mia Moja Iliyopita

1918​—Miaka Mia Moja Iliyopita

Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1918, lilianza kwa maneno haya: “Mwaka wa 1918 utaleta nini?” Vile Vita Vikuu vilikuwa vikiendelea barani Ulaya, lakini matukio fulani yaliyotendeka mwanzoni mwa mwaka huo yaliashiria mambo mema kwa Wanafunzi wa Biblia na ulimwengu kwa ujumla.

ULIMWENGU UNAZUNGUMZIA AMANI

Katika hotuba yake aliyotoa kwenye Bunge la Marekani mwezi wa Januari 8, 1918, Rais Woodrow Wilson, alitaja mambo 14 ambayo alihisi yalikuwa muhimu ili kuwe na “amani isiyo na upendeleo na ya kudumu.” Alipendekeza mataifa mbalimbali yafanye mazungumzo ya wazi ya kidiplomasia, na yapunguze silaha walizo nazo, na vilevile kuanzishwa kwa “shirika la muungano wa mataifa,” ambalo lingenufaisha “nchi kubwa na ndogo pia.” Hatimaye, ‘mapendekezo yake 14’ yalitumiwa kuunda Ushirika wa Mataifa na kusaidia katika kuandaa Mkataba wa Versailles, na hivyo kukomesha vile Vita Vikuu.

WAPINZANI WASHINDWA

Licha ya msukosuko wa mwaka uliotangulia, * Wanafunzi wa Biblia walitarajia pia kipindi chenye amani kwa sababu ya mambo yaliyotukia kwenye mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society.

Katika mkutano huo uliofanyika mwezi wa Januari 5, 1918, wanaume kadhaa waliokuwa na mamlaka katika tengenezo na ambao walikuwa wameachishwa mgawo wao wa Betheli, walitaka kuliongoza tengenezo. Richard H. Barber, ndugu mwaminifu aliyetumikia akiwa mwangalizi anayesafiri, alifungua mkutano huo kwa sala. Baada ya ripoti ya kazi ya kuhubiri ya mwaka uliotangulia kusomwa, uchaguzi wa kila mwaka wa baraza la waelekezi ulifanywa. Ndugu Barber alimchagua ndugu Joseph Rutherford na ndugu wengine sita. Kisha mwanasheria aliyewaunga mkono wapinzani aliwachagua wanaume wengine saba, kutia ndani wale waliokuwa wameachishwa utumishi wa Betheli. Hata hivyo, hawakushinda. Idadi kubwa sana ya wanahisa walimchagua Ndugu Rutherford na ndugu wengine waaminifu sita, wawe waelekezi wa Shirika la Watch Tower.

Ndugu wengi waliohudhuria mkutano huo waliuita “kusanyiko lililobarikiwa zaidi walilowahi kuhudhuria.” Lakini furaha yao ilikuwa ya muda mfupi.

KITABU THE FINISHED MYSTERY CHAIBUA HISIA MBALIMBALI

Kwa miezi kadhaa Wanafunzi wa Biblia walikuwa wakisambaza kitabu The Finished Mystery. Wasomaji wenye moyo mnyoofu walifurahia kusoma kweli za Biblia zilizokuwemo.

E. F. Crist, aliyetumikia akiwa mwangalizi anayesafiri nchini Kanada, alisimulia kuhusu wenzi fulani wa ndoa ambao, baada ya kusoma kitabu The Finished Mystery, waliikubali kweli ndani ya kipindi cha majuma matano tu! Alisema hivi: “Wote pamoja, mume na mke wake wamejitenga kabisa na mafundisho ya uwongo na wameanza kufanya maendeleo mazuri.”

Baada ya kupokea kitabu hicho, bila kukawia mwanamume mmoja alianza kukisoma pamoja na rafiki zake. “Aligongwa” na ujumbe wake. Anaeleza hivi: “Nilikuwa nikitembea kwenye mtaa wa Third Avenue nilipogongwa na kitu fulani kwenye bega ambacho nilifikiri ni tofali, lakini kumbe kilikuwa kitabu ‘The Finished Mystery.’ Nilienda nacho nyumbani na kukisoma chote. . . . Baadaye niligundua kwamba kasisi fulani . . . ndiye aliyekuwa amekitupa kwa hasira kupitia dirishani . . . Kupitia tendo hilo moja, ninasadiki kwamba aliwasaidia watu wengi sana kubadili mambo waliyoamini na kupata tumaini la kweli kuliko tendo lingine lolote alilowahi kufanya maishani mwake. . . . Kupitia ghadhabu ya kasisi huyo sasa tunamsifu Mungu.”

Si kasisi huyo peke yake aliyekuwa na hisia kama hizo. Wenye mamlaka nchini Kanada walikipiga marufuku mwezi wa Februari 12, 1918, wakidai kwamba kilikuwa na habari zenye uchochezi na zilizowakataza watu kwenda vitani. Muda mfupi baadaye, wenye mamlaka nchini Marekani walifanya vivyo hivyo. Maofisa wa serikali walienda Betheli na ofisi zilizokuwa New York, Pennsylvania, na California, na kuanza kupekua ili kutafuta ushahidi watakaotumia kuwashtaki ndugu waliokuwa wakiongoza katika tengenezo. Katika mwezi wa Machi 14, 1918, Wizara ya Sheria ya Marekani ilipiga marufuku kitabu The Finished Mystery, ikidai kwamba kuchapishwa na kusambazwa kwa kitabu hicho kulizorotesha jitihada za vita, jambo linalokiuka Sheria ya Ujasusi.

WAFUNGWA GEREZANI!

Katika mwezi wa Mei 7, 1918, Wizara ya Sheria ilipata idhini ya kuwakamata Giovanni DeCecca, George Fisher, Alexander Macmillan, Robert Martin, Frederick Robison, Joseph Rutherford, William Van Amburgh, na Clayton Woodworth. Walishtakiwa kwamba walikuwa “wamevunja sheria, wametenda kwa uhalifu, na kuwachochea watu kimakusudi wasijitiishe chini ya mamlaka, wasiwe wazalendo na wakatae kutumikia kwenye jeshi la nchi kavu na la majini la Marekani.” Kesi hiyo ilianza kusikilizwa mwezi wa Juni 3, 1918, lakini ilikuwa wazi kwamba wangepatikana na hatia. Kwa nini?

Mkuu wa Sheria wa Marekani alisema kwamba Sheria ya Ujasusi waliyokuwa wameshtakiwa kwamba wameivunja, ni “silaha madhubuti dhidi ya propaganda.” Mwezi wa Mei 16, 1918, Bunge la Marekani lilipinga mswada wa kurekebisha Sheria ya Ujasusi ambayo ingewalinda wale waliochapisha habari “za kweli, wakiwa na nia nzuri, na malengo halali.” Kitabu The Finished Mystery kilijadiliwa sana. Likizungumzia kuhusu kitabu hicho, Bunge la Marekani lilisema hivi: “Mojawapo ya mifano ya propaganda hatari zaidi ni kitabu kinachoitwa ‘The Finished Mystery’ . . . Kusudi kuu la kitabu hicho ni kuwachochea wanajeshi wadharau jitihada zetu na kuwachochea . . . watu wasijiandikishe jeshini.”

Katika mwezi wa Juni 20, 1918, jopo la mahakimu liliwapata ndugu wote nane na hatia katika mashtaka yote. Siku iliyofuata, hakimu alitamka hukumu yake. Alisema hivi: “Propaganda ya kidini ambayo washtakiwa hawa wamekuwa wakiitetea na kuieneza kwa hali na mali . . . ni hatari zaidi kuliko kikosi cha Jeshi la Ujerumani. . . . Wanapaswa kuadhibiwa vikali.” Majuma mawili baadaye, ndugu hao nane walitupwa katika Gereza Kuu huko Atlanta, Georgia, wakiwa wamehukumiwa vifungo vya miaka 10 hadi 20.

KAZI YA KUHUBIRI YASONGA MBELE

Katika kipindi hicho chote Wanafunzi wa Biblia walikabili upinzani mkali sana. Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) lilifanya upelelezi wa kina kuhusu utendaji wao, na kukawa na maelfu ya nyaraka zilizotokana na uchunguzi wao. Rekodi hizo zinaonyesha kwamba ndugu zetu walikuwa wameazimia kuendelea kuhubiri.

Kwenye barua aliyoandikia shirika la FBI, msimamizi mkuu wa ofisi ya posta ya Orlando, Florida, alisema hivi: “[Wanafunzi wa Biblia] wanaenda nyumba kwa nyumba katika mji huu na mara nyingi wanafanya hivyo usiku. . . . Inaonekana kwamba wanaendelea kuongeza kuni kwenye moto ili usizimike.”

Kanali mmoja katika Wizara ya Vita aliliandikia shirika la FBI akiripoti kuhusu shughuli za Frederick W. Franz, ambaye baadaye alitumikia kwenye Baraza Linaloongoza. Kanali huyo aliandika hivi: “F. W. Franz . . . amekuwa akihusika sana katika shughuli za kuuza maelfu ya mabuku ya ‘Finished Mystery’.”

Charles Fekel, ambaye baadaye alitumikia katika Baraza Linaloongoza, alikabili mateso makali sana. Wenye mamlaka walimkamata kwa kusambaza kitabu The Finished Mystery na kufuatilia mawasiliano yake kwa ukaribu alipokuwa gerezani. Alifungwa gerezani kwa mwezi mmoja huko Baltimore, Maryland, na alijulikana kama “adui wa kigeni kutoka Austria.” Alipokuwa akiwatolea ushahidi kwa ujasiri maofisa waliokuwa wakimhoji, alikumbuka maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 9:16, yanayosema: “Ole wangu nisipotangaza habari njema!” *

Mbali na jitihada zao za kuhubiri kwa bidii, Wanafunzi wa Biblia walieneza kwa bidii waraka wa kuomba ndugu hao nane waliokuwa wamefungwa gerezani huko Atlanta wawekwe huru. Anna K. Gardner alisema hivi: “Tulijaribu kuwasaidia katika njia mbalimbali. Ndugu hao walipokuwa gerezani, kazi yetu ilikuwa kutafuta sahihi za watu. Tulienda nyumba kwa nyumba. Tulipata maelfu ya sahihi! Tuliwaambia watu tuliozungumza nao kwamba wanaume hao walikuwa Wakristo wa kweli na kwamba walikuwa wamefungwa gerezani isivyo haki.”

MAKUSANYIKO

Wakati wa kipindi hicho kigumu, makusanyiko yalifanywa mara nyingi ili kuwaimarisha kiroho akina ndugu. Gazeti la Mnara wa Mlinzi lilieleza hivi: “Zaidi ya makusanyiko 40 . . . yamefanywa mwaka huu . . . Tumepokea ripoti zenye kusisimua kutoka kwenye makusanyiko hayo yote. Mwanzoni makusanyiko yote yalifanywa mwishoni mwa msimu wa kiangazi au mwanzoni mwa majira ya kupukutika kwa majani; lakini sasa makusanyiko yanafanywa kila mwezi kwa mwaka mzima.”

Watu wenye moyo mnyoofu walikuwa bado wakisikiliza habari njema. Katika kusanyiko moja lililofanywa huko Cleveland, Ohio, watu 1,200 hivi walihudhuria na 42 wakabatizwa kutia ndani mvulana mdogo “aliyempenda Mungu na ambaye alikuwa tayari kujitoa kwake kikamili, kitu ambacho kingewaaibisha watu wengi wenye umri mkubwa wasiomjua Mungu.”

NI NINI KILICHOFUATA?

Mwaka wa 1918 ulipokaribia kwisha, Wanafunzi wa Biblia hawakujua hali ingekuwaje. Baadhi ya majengo huko Brooklyn yaliuzwa na makao makuu yakahamishiwa Pittsburgh, Pennsylvania. Ndugu waliokuwa wakiongoza walipoendelea kutumikia kifungo chao gerezani, mkutano mwingine wa kila mwaka wa wanahisa wa Shirika la Watch Tower ulipangwa kufanywa Januari 4, 1919. Hali ingekuwaje?

Ndugu zetu walisonga mbele na kazi yao. Walikuwa na uhakika mkubwa kwamba hali ingekuwa nzuri hivi kwamba wakachagua andiko la mwaka wa 1919 kuwa: “Hakuna silaha yoyote itakayotokezwa dhidi yako itakayofanikiwa.” (Isa. 54:17) Hatimaye, msingi ulikuwa umewekwa kwa ajili ya mabadiliko makubwa ambayo yangewatia nguvu na kuimarisha imani yao ili watimize kazi kubwa iliyokuwa mbele yao.

^ fu. 6 Tazama sehemu yenye kichwa “Miaka Mia Moja Iliyopita—1917” kwenye Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2017, uku. 172-176.

^ fu. 22 Tazama simulizi la maisha la Charles Fekel, “Nimepata Shangwe Nyingi kwa Kudumu Katika Kazi Njema,” kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi toleo la Kiingereza la Machi 1, 1969.