Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Amani ya Akili Licha ya Mabadiliko

Dumisha Amani ya Akili Licha ya Mabadiliko

“Nimeituliza na kuinyamazisha nafsi yangu.”—ZAB. 131:2.

NYIMBO: 128, 129

1, 2. (a) Maisha ya Mkristo yanaweza kuathiriwaje na mabadiliko yasiyotarajiwa? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Kulingana na andiko la Zaburi 131, ni mtazamo gani unaoweza kutusaidia kudumisha amani ya akili?

MWANZONI Lloyd na Alexandra walipoambiwa kwamba hawataendelea kutumikia wakiwa Wanabetheli, walihuzunika. Walikuwa wametumikia wakiwa Wanabetheli kwa zaidi ya miaka 25. Lloyd anasema hivi: “Nilihisi kwamba mgawo wa Betheli na kazi niliyofanya vilikuwa sehemu ya maisha yangu. Nilielewa sababu ya badiliko hilo, lakini kwa majuma na miezi kadhaa iliyofuata, nilihisi sina thamani yoyote. Hisia zangu zilibadilika-badilika. Nyakati fulani nilikuwa na maoni mazuri kuhusu badiliko hilo, lakini nyakati nyingine nilivunjika moyo sana.”

2 Maisha yanapobadilika bila kutarajia, changamoto tutakazolazimika kukabili zinaweza kusababisha tupatwe na wasiwasi na mkazo wa kihisia. (Met. 12:25) Hata inaweza kuwa vigumu kukubali mabadiliko hayo. Chini ya hali kama hizo, tunaweza ‘kuitulizaje na kuinyamazisha’ nafsi yetu? (Soma Zaburi 131:1-3.) Acheni tuchunguze jinsi baadhi ya watumishi wa Mungu katika nyakati za Biblia na nyakati zetu walivyofanikiwa kudumisha amani ya akili licha ya mabadiliko.

PATA “AMANI YA MUNGU”

3. Yosefu alijipata katika hali gani?

3 Yosefu alikuwa na umri wa miaka 17 hivi ndugu zake walipomuuza utumwani kwa sababu ya wivu. Kabla ya kuuzwa, Yosefu ndiye aliyekuwa mwana aliyependwa zaidi na baba yake. (Mwa. 37:2-4, 23-28) Kwa takriban miaka 13, Yosefu alilazimika kuvumilia akiwa mtumwa na mfungwa gerezani nchini Misri, mbali na Yakobo, baba yake mpendwa. Ni nini kilichomsaidia Yosefu asikate tamaa na asilemewe na uchungu wa hisia?

4. (a) Yosefu alikazia nini alipokuwa gerezani? (b) Yehova alijibuje sala za Yosefu?

4 Alipokuwa akiteseka gerezani, ni wazi kwamba Yosefu alikazia mambo yaliyoonyesha kuwa Yehova alikuwa akimbariki. (Mwa. 39:21; Zab. 105:17-19) Inaonekana pia kwamba ndoto za kinabii alizoota alipokuwa kijana mdogo zilimpa uhakika wa kwamba alikuwa na kibali cha Yehova. (Mwa. 37:5-11) Ni wazi kwamba alimmiminia Yehova mahangaiko yake zaidi ya mara moja. (Zab. 145:18) Yehova alijibu sala za kutoka moyoni za Yosefu kwa kumpa uhakikisho wenye nguvu kwamba angekuwa “pamoja naye” katika majaribu yake yote.—Mdo. 7:9, 10. *

5. “Amani ya Mungu” inaweza kutusaidiaje tuendelee kufuatia malengo yetu ya kiroho?

5 Licha ya hali ngumu tunazokabili leo, sisi pia tunaweza kujionea moja kwa moja jinsi “amani ya Mungu” inayolinda nguvu zetu za akili ilivyo na nguvu za kututuliza. (Soma Wafilipi 4:6, 7.) Hivyo, tunapomtegemea Yehova wakati ambapo tunahisi kwamba tumelemewa na mahangaiko, amani ya Mungu inaweza kutusaidia tuimarishe azimio letu la kufikia malengo ya kiroho na kutulinda ili tusikate tamaa. Acheni tuchunguze baadhi ya mifano ya nyakati zetu inayothibitisha ukweli wa jambo hilo.

MTEGEMEE YEHOVA ILI UPATE TENA AMANI YA AKILI

6, 7. Kutaja mambo kihususa katika sala kunaweza kutusaidiaje kupata amani ya akili? Toa mfano.

6 Ryan na Juliette walipoambiwa kwamba hawangeendelea kutumikia wakiwa mapainia wa pekee wa muda, walivunjika moyo sana. Ryan anasema hivi: “Mara moja tulimweleza Yehova jambo hilo katika sala. Tulitambua kwamba hiyo ilikuwa fursa ya pekee ya kuonyesha kwamba tunamtumaini. Ndugu na dada wengi kutanikoni walikuwa wapya katika kweli, hivyo tulisali kwa Yehova atusaidie tuwe kielelezo bora cha imani.”

7 Yehova alijibuje sala yao? Ryan anasema hivi: “Punde tu baada ya kusali, hisia zisizofaa na wasiwasi tuliokuwa nao mwanzoni ulitoweka. Amani ya Mungu ilikuwa ikilinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili. Tulitambua kwamba Yehova angeendelea kututumia ikiwa tungedumisha mtazamo unaofaa.”

8-10. (a) Roho ya Mungu inaweza kutusaidiaje kukabiliana na wasiwasi? (b) Yehova anaweza kutumia njia zipi kutusaidia tunapojitahidi kudumisha mtazamo wa kiroho?

8 Zaidi ya kututuliza, roho ya Mungu inaweza kuvuta uangalifu wetu kwenye Maandiko hususa yatakayotusaidia tuendelee kutanguliza mambo ya maana zaidi maishani. (Soma Yohana 14:26, 27.) Fikiria mfano wa Philip na Mary, wenzi wa ndoa waliokuwa wametumikia Betheli kwa karibu miaka 25. Katika kipindi cha miezi minne tu baada ya kutoka Betheli, wote wawili waliwapoteza mama zao katika kifo na pia mtu mwingine wa ukoo, na wakaanza kumtunza baba ya Mary aliyekuwa na ugonjwa wa kupoteza kumbukumbu.

9 Philip anasema hivi: “Nilifikiri nilikuwa nikikabiliana na hali hiyo vizuri, lakini jambo fulani lilikosekana. Nilipata andiko la Wakolosai 1:11 katika makala ya funzo ya gazeti la Mnara wa Mlinzi. Ni kweli kwamba nilikuwa nikivumilia, lakini sikuwa nikifanya hivyo kikamili. Nilihitaji ‘kuvumilia kikamili kwa subira na shangwe.’ Mstari huo ulinikumbusha kwamba shangwe yangu maishani haikutegemea hali nilizokabili, bali jinsi roho ya Mungu ilivyokuwa ikifanya kazi maishani mwangu.”

10 Kwa kuwa Philip na Mary walijitahidi kudumisha mtazamo wa kiroho kuhusu hali walizokabili, Yehova aliwabariki katika njia mbalimbali. Muda mfupi baada ya kutoka Betheli, wote wawili walipata watu waliotaka kujifunza Biblia zaidi ya mara moja kwa juma na ambao walitamani kufanya maendeleo ya kiroho. Akikumbuka wakati huo, Mary anasema hivi: “Walikuwa chanzo cha shangwe yetu na njia ya Yehova ya kutuambia kwamba kila kitu kitakuwa sawa.”

MPE YEHOVA SABABU YA KUKUBARIKI

Tunaweza kuigaje mfano wa Yosefu licha ya hali tunazopitia? (Tazama fungu la 11 hadi 13)

11, 12. (a) Yosefu alifanya jambo gani lililomfanya Yehova ambariki? (b) Yosefu alithawabishwaje kwa sababu ya uvumilivu wake?

11 Tunapokabili mabadiliko yasiyotarajiwa, ni rahisi kwetu kuruhusu mahangaiko kuhusu wakati ujao yadhoofishe nguvu zetu. Huenda Yosefu angepatwa na jambo kama hilo. Badala yake, alijitahidi kadiri alivyoweza kushughulika na hali yake kwa njia nzuri, na hivyo akampa Yehova sababu ya kumbariki. Ingawa alikuwa gerezani, Yosefu alitimiza kwa bidii kazi yoyote aliyopewa na ofisa mkuu wa gereza, kama alivyokuwa akifanya alipokuwa mfanyakazi wa Potifa.—Mwa. 39:21-23.

12 Siku moja, Yosefu alipewa jukumu la kuwasimamia wanaume wawili ambao hapo awali walitumikia katika vyeo vikubwa kwenye makao ya Farao. Kwa kuwa Yosefu alikuwa mwenye fadhili, wanaume hao walijihisi huru kumweleza mahangaiko yao na ndoto zao zenye kutatanisha walizokuwa wameota usiku uliotangulia. (Mwa. 40:5-8) Yosefu hakutambua kwamba mazungumzo yake pamoja na wanaume hao mwishowe yangemfanya aachiliwe huru. Ingawa aliendelea kubaki gerezani kwa miaka miwili zaidi, hatimaye Yosefu aliachiliwa huru, na siku hiyohiyo akateuliwa kuwa mtawala wa pili baada ya Farao.—Mwa. 41:1, 14-16, 39-41.

13. Ni katika njia gani tunaweza kumpa Yehova sababu za kutubariki licha ya hali zozote tunazokabili?

13 Kama Yosefu, sisi pia tunaweza kukabili hali inayopita uwezo wetu. Hata hivyo, tukiendelea kuwa na subira na kujitahidi kadiri tuwezavyo kushughulika na hali yetu kwa njia nzuri, tutampa Yehova sababu ya kutubariki. (Zab. 37:5) Ni kweli kwamba nyakati nyingine huenda ‘tukafadhaishwa,’ lakini kama mtume Paulo alivyotaja, hatutaachwa kamwe katika hali ya ‘kukata tamaa.’ (2 Kor. 4:8; maelezo ya chini) Tutajionea ukweli wa maneno hayo ya Paulo, hasa ikiwa tutaendelea kukazia fikira huduma yetu.

ENDELEA KUKAZIA FIKIRA HUDUMA YAKO

14-16. Ni nini kilichomsaidia Filipo mweneza-injili aendelee kukazia fikira huduma yake licha ya mabadiliko maishani mwake?

14 Filipo mweneza-injili ni mfano wa mtu aliyeendelea kukazia fikira huduma yake licha ya mabadiliko mbalimbali katika maisha yake. Wimbi la mateso lilizuka jijini Yerusalemu baada ya Stefano kuuawa. * Wakati huo, Filipo alikuwa akifurahia pendeleo fulani jipya la utumishi. (Mdo. 6:1-6) Lakini wafuasi wa Kristo walipolazimika kutawanyika katika maeneo mengine, Filipo hangeketi kitako tu bila kufanya lolote. Alienda kuhubiri Samaria, jiji ambalo kufikia wakati huo, halikuwa limefikiwa kikamili na ujumbe wa habari njema.—Mt. 10:5; Mdo. 8:1, 5.

15 Filipo alikuwa tayari kwenda popote ambapo roho ya Mungu ingemwongoza, hivyo Yehova alimtumia kwenda kuhubiri katika maeneo ambayo hayakuwa yamewahi kuhubiriwa. Inaonekana kwamba mtazamo wake wa kutowabagua wengine uliwaburudisha Wasamaria, ambao walidharauliwa sana na Wayahudi. Hivyo, haishangazi kwamba umati ulimsikiliza “wote kwa pamoja”!—Mdo. 8:6-8.

16 Kisha Filipo aliongozwa na roho ya Mungu kwenda Ashdodi na Kaisaria, majiji mawili yaliyokuwa na idadi kubwa ya watu wasio Wayahudi. (Mdo. 8:39, 40) Baada ya miaka 20 hivi tangu alipohubiri Samaria mara ya kwanza, inaonekana hali za Filipo zilikuwa zimebadilika. Sasa alikuwa mwanamume mwenye familia na alihubiri katika eneo aliloishi. Licha ya mabadiliko hayo, Filipo aliendelea kukazia fikira huduma yake, na kwa sababu hiyo yeye pamoja na familia yake walibarikiwa sana na Yehova.—Mdo. 21:8, 9.

17, 18. Kukazia fikira huduma yetu kunaweza kutusaidiaje kuendelea kuwa na usawaziko hali zetu zinapobadilika?

17 Watumishi wengi wa wakati wote wamejionea kwamba kukazia fikira huduma kuliwasaidia waendelee kuwa na usawaziko licha ya mabadiliko. Osborne na Polite, wenzi wa ndoa kutoka Afrika Kusini walipoombwa waondoke Betheli, walifikiri kwamba wangepata mara moja kazi ya muda na mahali pa kuishi. Osborne anaendelea kusema hivi: “Kwa kusikitisha, hatukupata kazi haraka kama tulivyotarajia.” Polite, mke wake, anasema: “Hatukupata kazi yoyote kwa miezi mitatu na hatukuwa na akiba ya pesa. Ilikuwa changamoto kubwa sana.”

18 Ni nini kilichowasaidia wakabiliane na hali hiyo yenye mkazo? Osborne anaeleza kilichowasaidia: “Kuhubiri pamoja na kutaniko kulitusaidia sana tusikengeuke na tuwe na mtazamo mzuri. Tuliamua kuzama katika kazi ya kuhubiri badala ya kuketi na kusongwa na mawazo, na hilo lilituletea shangwe nyingi sana. Tulitafuta kazi kila mahali, na mwishowe tukapata.”

MNGOJEE YEHOVA KWA SUBIRA

19-21. (a) Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kuwa na amani ya akili? (b) Tunaweza kupata manufaa gani tunapojitahidi kuzoea hali yetu mpya?

19 Kama mifano tuliyozungumzia inavyoonyesha, tukijitahidi kadiri tuwezavyo kushughulika na hali zetu kwa njia nzuri na kumngojea Yehova tukiwa na uhakika, tutadumisha amani yetu ya akili. (Soma Mika 7:7.) Huenda hata tukagundua kwamba tumepata manufaa mengi ya kiroho kwa kujitahidi kuzoea hali yetu mpya. Akizungumzia mambo aliyojionea, Polite, dada aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Badiliko la mgawo limenifundisha maana hasa ya kumtegemea Yehova hata hali ziwe ngumu kadiri gani. Uhusiano wangu naye umeimarika sana.”

20 Mary, dada aliyetajwa awali, anaendelea na upainia huku akimtunza baba yake ambaye amezeeka. Anakiri hivi: “Nimejifunza kwamba ninaposhikwa na wasiwasi, ninahitaji kutua, nisali, kisha niache kuhangaika. Somo kubwa zaidi ambalo nimejifunza ni kuacha mambo mikononi mwa Yehova, na sote tutahitaji kufanya hivyo hata zaidi wakati ujao.”

21 Lloyd na Alexandra, wenzi wa ndoa waliotajwa mwanzoni mwa makala hii, wanakiri kwamba mabadiliko waliyopitia yalijaribu imani yao kwa njia ambazo hawakutarajia. Lakini wanasema hivi: “Majaribu ya imani hufunua ikiwa imani yetu ni ya kweli na ikiwa ina nguvu za kututegemeza na kutufariji katika nyakati ngumu. Majaribu hayo huboresha utu wetu.”

Mabadiliko yasiyotarajiwa yanaweza kuleta baraka zisizotazamiwa! (Tazama fungu la 19 hadi 21)

22. Tunahakikishiwa nini ikiwa tutajitahidi kadiri tuwezavyo kushughulika kwa njia nzuri na hali tunazopitia?

22 Maisha yako yanapobadilika bila kutarajia, iwe ni kwa sababu mgawo wako umebadilika, matatizo ya afya, au majukumu mapya ya familia, uwe na hakika kwamba Yehova anakujali naye atakusaidia kwa wakati unaofaa. (Ebr. 4:16; 1 Pet. 5:6, 7) Kwa sasa, jitahidi kadiri uwezavyo kushughulika kwa njia nzuri na hali unayopitia. Mkaribie Baba yako wa mbinguni kupitia sala, na ujifunze kujiacha katika mikono yake yenye upendo. Kwa njia hiyo, wewe pia utaendelea kuwa na amani ya akili hata upatwe na mabadiliko gani maishani.

^ fu. 4 Wakati fulani baada ya kuachiliwa huru kutoka gerezani, Yosefu alitambua kwamba Yehova alikuwa ametuliza maumivu yake ya wakati uliopita kwa kumpa mwana. Alimpa mwana wake wa kwanza jina Manase kwa sababu, kama alivyosema: “Mungu amenifanya nisahau taabu yangu yote.”—Mwa. 41:51, maelezo ya chini.

^ fu. 14 Tazama makala, “Je, Wajua?” katika toleo hili.