Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumaini Kiongozi Wetu​—Kristo

Mtumaini Kiongozi Wetu​—Kristo

“Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”—MT. 23:10.

NYIMBO: 16, 14

1, 2. Yoshua alikabili changamoto gani baada ya Musa kufa?

MANENO ya Yehova yalikuwa bado akilini mwa Yoshua: “Musa mtumishi wangu amekufa. Sasa jitayarishe, vuka Mto Yordani pamoja na watu hawa wote, mwingie katika nchi ambayo ninawapa.” (Yos. 1:1, 2) Hilo lilikuwa badiliko la ghafla kwa Yoshua ambaye alikuwa ametumikia akiwa mtumishi wa Musa kwa karibu miaka 40!

2 Kwa kuwa Musa alikuwa ametumikia akiwa kiongozi wa Waisraeli kwa muda mrefu sana, huenda Yoshua alijiuliza watu wa Mungu wangeitikiaje atakapokuwa kiongozi wao. (Kum. 34:8, 10-12) Kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema hivi kuhusu andiko la Yoshua 1:1, 2: “Katika nyakati za kale na za kisasa, kipindi cha kubadilisha uongozi kutoka kwa kiongozi mmoja kwenda kwa mwingine ndicho kipindi ambacho usalama wa nchi huwa hatarini zaidi kuliko wakati mwingine wowote.”

3, 4. Tunajuaje kwamba Yoshua hakukosea alipoweka tumaini lake kwa Mungu, na huenda tukajiuliza swali gani?

3 Yoshua alikuwa na sababu ya kuwa na wasiwasi, lakini baada ya siku chache alichukua hatua. (Yos. 1:9-11) Yoshua hakukosea kwa kuweka tumaini lake kwa Mungu. Kama simulizi la Biblia linavyoonyesha, Yehova alimtumia malaika kama mwakilishi wake kumwongoza Yoshua na watu Wake, Israeli. Kuna uwezekano mkubwa kwamba malaika huyo alikuwa Neno, Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu.—Kut. 23:20-23; Yoh. 1:1.

4 Kwa msaada wa Yehova, Waisraeli walifanikiwa kukabiliana na mabadiliko chini ya uongozi mpya wa Yoshua. Sisi pia tunaishi katika kipindi cha mabadiliko makubwa sana, na huenda tukajiuliza, ‘Tengenezo la Mungu linapozidi kusonga mbele kwa kasi, je, tuna sababu nzuri za kumtumaini Yesu, Kiongozi wetu aliyewekwa rasmi?’ (Soma Mathayo 23:10.) Fikiria jinsi Yehova alivyoandaa uongozi wenye kutumainika katika nyakati za kale kulipokuwa na mabadiliko.

WATU WA MUNGU WAONGOZWA KUINGIA KANAANI

5. Yoshua alijionea nini alipokuwa akikaribia Yeriko? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

5 Muda mfupi baada ya Waisraeli kuvuka Mto Yordani, Yoshua alijionea jambo fulani ambalo hakutazamia. Alipokuwa akikaribia Yeriko, alikutana na mwanamume aliyekuwa ameshika upanga uliochomolewa. Kwa kuwa hakujua mwanamume huyo alikuwa nani, Yoshua alimuuliza hivi: “Uko upande wetu au wa maadui wetu?” Yoshua alishangaa shujaa huyo alipojitambulisha. Shujaa huyo alikuwa “kiongozi wa jeshi la Yehova,” na alikuwa tayari kuwalinda watu wa Mungu. (Soma Yoshua 5:13-15 na maelezo ya chini.) Ingawa kwingineko simulizi hilo linamrejelea Yehova akizungumza moja kwa moja na Yoshua, hapana shaka kwamba Mungu alikuwa akimtumia malaika kama mwakilishi wake, kama alivyofanya katika nyakati zilizotangulia.—Kut. 3:2-4; Yos. 4:1, 15; 5:2, 9; Mdo. 7:38; Gal. 3:19.

6-8. (a) Kwa nini huenda baadhi ya maagizo ya Yehova yangeonekana kuwa yasiyo ya kawaida kwa maoni ya kibinadamu? (b) Tunajuaje kwamba maagizo hayo yalikuwa ya hekima na yalitolewa kwa wakati unaofaa? (Tazama pia maelezo ya chini.)

6 Yoshua alipokea maagizo yaliyo wazi kutoka kwa Kiongozi huyo kuhusu jinsi ya kuliteka jiji la Yeriko. Mwanzoni, baadhi ya maagizo aliyopewa hayakuonekana kama yangewasaidia kufanikiwa. Kwa mfano, Yehova aliamuru wanaume wote watahiriwe, jambo ambalo lingewafanya washindwe kwenda vitani kwa siku kadhaa. Je, kweli huo ulikuwa wakati unaofaa wa kuwatahiri wanaume hao?—Mwa. 34:24, 25; Yos. 5:2, 8.

7 Wakiwa katika hali hiyo, inawezekana kwamba wanajeshi hao Waisraeli walijiuliza wangefaulu vipi kulinda familia zao ikiwa majeshi ya maadui yangevamia kambi yao. Lakini punde si punde, wakapokea habari kwamba “malango ya jiji la Yeriko yalikuwa yamefungwa kabisa kwa sababu ya Waisraeli.” (Yos. 6:1) Je, si kweli kwamba matukio hayo yasiyotazamiwa yaliwachochea waendelee kutumaini mwongozo wa Mungu hata zaidi?

8 Isitoshe, Waisraeli waliamriwa wasilishambulie jiji la Yeriko, bali walizunguke mara moja kila siku kwa siku sita, na katika siku ya saba walizunguke mara saba. Labda baadhi ya wanajeshi walifikiri hivi: ‘Kufanya hivyo ni kupoteza wakati na nguvu!’ Lakini Kiongozi asiyeonekana wa Waisraeli alijua vizuri alichokuwa akifanya. Mbinu hiyo haikuimarisha tu imani ya Waisraeli, bali pia iliwaepusha na mashambulizi ya moja kwa moja kutoka kwa mashujaa wenye nguvu wa Yeriko.—Yos. 6:2-5; Ebr. 11:30. *

9. Kwa nini tunapaswa kufuata maagizo tunayopata katika tengenezo la Mungu? Toa mfano.

9 Tunajifunza nini kutokana na simulizi hilo? Nyakati nyingine, huenda tusielewe kikamili kwa nini tengenezo limefanya mabadiliko fulani. Kwa mfano, labda mwanzoni tulijiuliza ikiwa ni wazo linalofaa kutumia vifaa vya kielektroni katika funzo letu la kibinafsi, katika huduma, na katika mikutano. Lakini sasa tunaelewa manufaa ya kuvitumia inapowezekana. Tunapoona matokeo mazuri ya mabadiliko hayo licha ya shaka zozote ambazo huenda tulikuwa nazo, imani na umoja wetu huimarika.

UONGOZI WA KRISTO KATIKA KARNE YA KWANZA

10. Ni nani aliyeongoza mambo ili baraza linaloongoza lifanye mkutano muhimu huko Yerusalemu?

10 Miaka 13 hivi baada ya Kornelio kuwa Mkristo, baadhi ya waamini Wayahudi walikuwa bado wakiendeleza desturi ya kutahiriwa. (Mdo. 15:1, 2) Mgawanyiko ulipotokea huko Antiokia, mipango ilifanywa ili Paulo awasilishe suala hilo kwa baraza linaloongoza huko Yerusalemu. Lakini ni nani aliyekuwa akiongoza mambo? Paulo alisema hivi: “Nilienda kutokana na ufunuo.” Ni wazi kwamba Kristo aliongoza mambo ili baraza linaloongoza lisuluhishe suala hilo.—Gal. 2:1-3.

Uongozi wa Kristo ulikuwa dhahiri katika karne ya kwanza (Tazama fungu la 10 na 11)

11. (a) Waamini Wayahudi waliendelea kushikilia maoni gani kuhusu suala la tohara? (b) Utayari wa Paulo wa kuwaunga mkono wazee wa Yerusalemu ulijaribiwaje? (Tazama pia maelezo ya chini.)

11 Chini ya mwongozo wa Kristo, baraza linaloongoza lilionyesha wazi kwamba Wakristo wasio Wayahudi hawakuhitaji kutahiriwa. (Mdo. 15:19, 20) Hata hivyo, miaka mingi baada ya uamuzi huo kufanywa, waamini wengi Wayahudi bado walikuwa wakiwatahiri watoto wao. Wazee huko Yerusalemu waliposikia uvumi ulioenezwa kumhusu Paulo kwamba hakuwa akishika Sheria ya Musa, walimpa maagizo fulani yasiyotarajiwa. * (Mdo. 21:20-26) Walimwambia aende na wanaume wanne hekaluni ili watu waone kwamba Paulo ‘alishika Sheria.’ Paulo angeweza kutilia shaka ikiwa kufanya hivyo kulikuwa jambo la hekima, na kusisitiza kwamba Wakristo Wayahudi ndio waliokuwa na tatizo kwa sababu hawakuelewa vizuri suala la tohara. Hata hivyo, kwa unyenyekevu Paulo alitii maagizo aliyopewa, na hivyo kuonyesha kwamba aliunga mkono jitihada za wazee hao za kuendeleza umoja miongoni mwa Wakristo. Ingawa hivyo, huenda tukajiuliza, ‘Kwa nini Yesu aliruhusu suala hilo liendelee kwa muda mrefu bila kutatuliwa ilhali kifo chake kilikuwa kimefuta Sheria ya Musa?’—Kol. 2:13, 14.

12. Kwa nini huenda Kristo aliruhusu muda upite kabla ya kutatua suala la tohara?

12 Huenda ikachukua muda kwa baadhi ya watu wa Mungu kuunga mkono uelewaji fulani mpya. Wakristo Wayahudi walihitaji muda wa kutosha ili kubadili maoni yao. (Yoh. 16:12) Ilikuwa vigumu kwa baadhi yao kukubali kwamba desturi ya kutahiriwa haikuwa tena ishara iliyoonyesha kwamba walikuwa katika uhusiano wa pekee pamoja na Mungu. (Mwa. 17:9-12) Wengine waliogopa kuonekana kuwa tofauti na Wayahudi wenzao kwa sababu walihofia kuteswa. (Gal. 6:12) Hata hivyo, baada ya muda, Kristo alitoa mwongozo zaidi kupitia barua zilizoongozwa na roho ambazo ziliandikwa na Paulo.—Rom. 2:28, 29; Gal. 3:23-25.

KRISTO ANGALI ANALIONGOZA KUTANIKO LAKE

13. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuendelee kumuunga mkono Kristo akiwa kiongozi wetu leo?

13 Tunapokosa kuelewa kikamili sababu zilizofanya mabadiliko fulani yafanywe katika tengenezo, ni vizuri kutafakari jinsi Kristo alivyowaongoza watu wa Mungu katika nyakati zilizopita. Tangu siku za Yoshua au katika karne ya kwanza, sikuzote Kristo amekuwa akitoa mwongozo wenye hekima ili kuwalinda watu wa Mungu wakiwa kikundi, kuimarisha imani yao, na kuwasaidia wadumishe umoja miongoni mwao.—Ebr. 13:8.

14-16. Uthibitisho wa kwamba Kristo anajali sana hali yetu ya kiroho unaonekanaje wazi kupitia mwongozo tunaopata kutoka kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”?

14 Uthibitisho wa jinsi Yesu anavyotujali kwa upendo unaonekana waziwazi kupitia mwongozo tunaopokea kwa wakati unaofaa kutoka kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Marc, baba aliye na watoto wanne, anasema hivi: “Shetani anajitahidi kuyadhoofisha makutaniko kwa kushambulia familia. Sasa kwa kuwa vichwa vya familia wametiwa moyo kuongoza ibada ya familia kila juma, basi ujumbe ni dhahiri kwao—lindeni familia zenu!”

15 Tunapoona jinsi Kristo anavyotuongoza, tunatambua kwamba anahangaikia sana hali yetu ya kiroho. Patrick, ambaye ni mzee wa kutaniko, anasema hivi: “Mwanzoni, baadhi ya ndugu na dada hawakupendezwa sana na mpango wa kukutana katika vikundi vidogo kwa ajili ya utumishi wa shambani wakati wa miisho juma. Lakini kupitia mpango huo, tunajionea wazi mojawapo ya sifa kuu za Yesu, yaani, jinsi anavyopendezwa na watu wa hali ya chini. Akina ndugu na dada wenye haya au ambao hawashiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani, sasa wanahisi kwamba wanathaminiwa na wanatimiza fungu fulani, na kwa sababu hiyo hali yao ya kiroho imeimarika.”

16 Mbali na kwamba Kristo anahangaikia sana mahitaji yetu ya kiroho, anatusaidia pia kukazia fikira kazi ya maana zaidi inayofanywa duniani leo. (Soma Marko 13:10.) André, ndugu aliyewekwa rasmi kuwa mzee hivi karibuni, sikuzote amekuwa makini sana kuhusiana na mabadiliko yanayofanywa ndani ya tengenezo la Mungu. Anasema hivi: “Kupunguzwa kwa idadi ya Wanabetheli kunatukumbusha kwamba wakati uliobaki umepungua sana na kwamba tunahitaji kuelekeza nguvu zetu katika kazi ya kuhubiri.”

KUUNGA MKONO KWA USHIKAMANIFU MWONGOZO WA KRISTO

17, 18. Kwa nini ni vizuri kutafakari faida tunazopata tunapoenda sambamba na mabadiliko yaliyofanywa hivi karibuni?

17 Bila shaka, Yesu Kristo, Mfalme wetu anayetawala, anazingatia hali yetu ya wakati ujao, kama tunavyoona kupitia mwongozo anaotoa. Hivyo, acheni tushangilie kwa sababu ya manufaa tunayopata tunapoenda sambamba na mabadiliko yaliyofanywa hivi karibuni. Wakati wa ibada yenu ya familia, mtatiwa moyo sana iwapo mtazungumzia jinsi mlivyofaidika na mabadiliko yaliyofanywa katika mikutano ya kila juma au katika huduma yetu.

Je, unaisaidia familia yako na waabudu wenzako kwenda sambamba na tengenezo la Yehova? (Tazama fungu la 17 na 18)

18 Tunapoelewa kwa nini tengenezo la Yehova linatoa maagizo fulani na manufaa tunayopata kwa kuyafuata, itakuwa rahisi zaidi kwetu kufuata miongozo hiyo kwa shangwe. Tunafurahi kuona kwamba tangu idadi ya machapisho ipunguzwe tengenezo limeokoa pesa nyingi; kutumia teknolojia mpya kumetuwezesha kuendeleza kazi ya Ufalme duniani kote. Tukiwa na hilo akilini, sasa tunaweza kutumia machapisho ya kielektroni, video, na rekodi za sauti kwa ukamili zaidi kadiri iwezekanavyo. Kwa njia hiyo, tutaonyesha kwamba tunamuunga mkono Kristo kwa kutumia mali ya tengenezo kwa hekima.

19. Kwa nini tunapaswa kuunga mkono mwongozo wa Kristo?

19 Tunapounga mkono kwa bidii mwongozo wa Kristo, tunaimarisha imani ya ndugu na dada zetu na kuchangia umoja wetu. Anapotafakari kuhusu mpango wa kupunguza idadi ya Wanabetheli ulimwenguni pote, André anasema hivi: “Mtazamo mzuri unaoonyeshwa na ndugu na dada ambao awali walikuwa Wanabetheli na ambao wameunga mkono mabadiliko hayo, hunichochea niwaheshimu sana na nimtumaini kiongozi wetu, Kristo. Wanaenda sambamba na gari la kimbingu la Yehova kwa kutimiza kwa shangwe mgawo wowote wanaopokea.”

KWA MACHO YA IMANI, MTUMAINI KIONGOZI WETU

20, 21. (a) Kwa nini tunaweza kumtumaini Kristo, Kiongozi wetu? (b) Tutazungumzia swali gani katika makala inayofuata?

20 Hivi karibuni, Yesu Kristo, Kiongozi wetu aliyewekwa rasmi ‘atakamilisha ushindi wake’ na “[kutimiza] mambo yanayoogopesha.” (Ufu. 6:2; Zab. 45:4) Kwa sasa, anawatayarisha watu wa Mungu kwa ajili ya maisha ya wakati ujao baada ya mfumo huu wa mambo kuondolewa, ambapo kila mmoja wetu atashiriki katika kazi kubwa ya ujenzi na ya kufundisha itakayofanywa wakati wa ufufuo.

21 Mfalme wetu aliyetiwa mafuta atatuongoza kuingia katika ulimwengu mpya, maadamu tunaendelea kumtumaini kikamili licha ya hali zinazobadilika. (Soma Zaburi 46:1-3.) Nyakati nyingine, huenda ikawa vigumu kwenda sambamba na mabadiliko yanayofanywa, hasa ikiwa mabadiliko hayo yanagusa maisha yetu kwa njia ambayo hatukutazamia. Hivyo basi, tunaweza kudumishaje amani ya akili na kuendelea kumtumaini Yehova kikamili? Tutazungumzia swali hilo katika makala inayofuata.

^ fu. 8 Wachimbuaji wa vitu vya kale walikuta nafaka nyingi katika magofu ya jiji la Yeriko, jambo linaloonyesha kwamba jiji hilo halikuzingirwa kwa muda mrefu kwa kuwa hifadhi ya chakula haikuwa imekwisha. Kwa kuwa Waisraeli hawakuruhusiwa kujichukulia nyara, ni wazi kwamba kipindi walichovamia jiji la Yeriko kilikuwa kipindi mwafaka kabisa kwa sababu ulikuwa wakati wa mavuno na chakula kilikuwa tele mashambani.—Yos. 5:10-12.

^ fu. 11 Tazama sanduku, “Paulo Akabili Jaribu kwa Unyenyekevu” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Machi 15, 2003, uku. 24.