Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Semeni Ukweli

Semeni Ukweli

“Kila mtu amwambie mwenzake ukweli.”—ZEK. 8:16.

NYIMBO: 56, 124

1, 2. Ni kitu gani ambacho kimewasababishia wanadamu matatizo makubwa sana, na ni nani aliyekianzisha?

KUVUMBULIWA kwa vitu kama vile simu, balbu, magari, na friji kumeboresha kwa kadiri fulani maisha ya kila siku. Hata hivyo, vitu vingine vilivyovumbuliwa vimezidi kuhatarisha maisha ya watu. Baadhi ya vitu hivyo ni baruti, mabomu ya kutegwa ardhini, sigara, na mabomu ya atomu. Ingawa hivyo, kuna kitu fulani ambacho kimekuwapo kabla ya vitu hivyo vyote, nacho kimewasababishia wanadamu matatizo makubwa sana. Ni kitu gani hicho? Ni uwongo, yaani, kusema jambo ambalo unajua kwamba si kweli ukiwa na kusudi la kumpotosha mtu. Na ni nani aliyetunga uwongo wa kwanza? Yesu Kristo alimtambulisha “Ibilisi” kuwa “baba ya uwongo.” (Soma Yohana 8:44.) Ibilisi alitamka lini uwongo wa kwanza?

2 Hilo lilitendeka maelfu ya miaka iliyopita katika bustani ya Edeni. Wenzi wa ndoa wa kwanza, Adamu na Hawa, walikuwa wakifurahia maisha katika Paradiso ambayo Muumba wao alikuwa amewaandalia. Kisha Ibilisi akatokea. Alijua kwamba Mungu alikuwa amewaamuru wenzi hao wasile matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya,” ili wasije wakafa kwa sababu ya kutotii. Licha ya hilo, Shetani, akimtumia nyoka alimwambia Hawa hivi: “Hakika hamtakufa [uwongo wa kwanza kuwahi kusemwa]. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”—Mwa. 2:15-17; 3:1-5.

3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Shetani alikuwa na nia yenye uovu aliposema uwongo, na matokeo yamekuwa nini?

3 Shetani alisema uwongo akiwa na nia yenye uovu kwa sababu alijua vizuri kabisa kwamba ikiwa Hawa angekula tunda hilo, angekufa. Adamu na Hawa walikufa kwa sababu hawakutii amri ya Yehova. (Mwa. 3:6; 5:5) Zaidi ya hilo, kupitia dhambi hiyo, “kifo kikaenea kwa watu wote.” Isitoshe, “kifo kilitawala kama mfalme . . . , hata juu ya wale ambao hawakuwa wamefanya dhambi kama vile Adamu alivyofanya kosa.” (Rom. 5:12, 14) Sasa badala ya kufurahia maisha makamilifu yasiyo na mwisho kama Mungu alivyokuwa amekusudia awali, wanadamu huishi “miaka 70, au miaka 80 ikiwa mtu ana nguvu za pekee.” Pamoja na hilo, maisha hayo “[yamejaa] taabu na huzuni.” (Zab. 90:10) Ni msiba ulioje—yote hayo kwa sababu ya uwongo wa Shetani!

4. (a) Tunapaswa kujua majibu ya maswali gani? (b) Kulingana na Zaburi 15:1, 2, ni nani pekee wanaoweza kuwa rafiki za Yehova?

4 Yesu alipokuwa akifafanua matendo ya Ibilisi alisema hivi: “Hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haimo ndani yake.” Hata sasa bado kweli haimo ndani yake, kwa sababu anaendelea “[kuipotosha] dunia nzima inayokaliwa” kwa uwongo wake. (Ufu. 12:9) Hatungependa kupotoshwa na Ibilisi. Hivyo, acheni tuchunguze maswali matatu: Shetani anawapotoshaje wanadamu? Kwa nini watu husema uwongo? Na ili tusipoteze uhusiano wetu mzuri pamoja na Yehova kama Adamu na Hawa walivyofanya, tunaweza kuonyeshaje kwamba sisi ni watu ‘wanaosema ukweli’ nyakati zote?—Soma Zaburi 15:1, 2.

JINSI SHETANI ANAVYOWAPOTOSHA WANADAMU

5. Shetani anawapotoshaje wanadamu leo?

5 Mtume Paulo alijua kwamba tunaweza kuepuka ‘kudanganywa na Shetani, kwa maana hatukosi kujua nia yake.’ (2 Kor. 2:11; maelezo ya chini) Tunajua kwamba ulimwengu mzima—kutia ndani dini ya uwongo, mifumo ya kisiasa yenye ufisadi, na mifumo ya kibiashara yenye pupa—uko chini ya mamlaka ya Ibilisi. (1 Yoh. 5:19) Hivyo, hatushangai kuona kwamba Shetani na roho wake waovu huwashawishi watu wenye mamlaka ‘waseme uwongo.’ (1 Tim. 4:1, 2) Ukweli wa jambo hilo huonekana wakati wafanyabiashara maarufu wanapowashawishi watu kupitia matangazo ya biashara wanunue bidhaa zinazodhuru na wajiingize kwenye miradi iliyokusudiwa kuwalaghai.

6, 7. (a) Kwa nini viongozi wa kidini wanaofundisha uwongo wana hatia kubwa? (b) Ni mafundisho gani ya uwongo ambayo umewahi kusikia viongozi wa kidini wakifundisha?

6 Viongozi wa kidini wanaofundisha uwongo wana hatia kubwa kwa sababu wanawafanya wale wanaoamini uwongo wao wapoteze fursa ya kuishi milele. Mtu akikubali fundisho fulani la uwongo na kutenda jambo ambalo Mungu amekataza, anaweza kukosa uzima wa milele. (Hos. 4:9) Yesu alijua kwamba viongozi wa kidini wa siku zake walikuwa na hatia kwa sababu waliwadanganya watu. Aliwaambia hivi waziwazi: “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo wanafiki! kwa sababu mnasafiri baharini na kwenye nchi kavu ili kumgeuza imani mtu mmoja, na anapogeuka, mnamfanya astahili Gehena [adhabu ya milele] mara mbili zaidi yenu.” (Mt. 23:15; maelezo ya chini) Yesu aliwashutumu vikali viongozi hao wa kidini waliofundisha uwongo. Kwa kweli walikuwa ‘wametoka kwa baba yao Ibilisi, muuaji.’—Yoh. 8:44.

7 Iwe wanajulikana kwa majina ya cheo kama vile mchungaji, pasta, kasisi, rabi, swami, au jina lingine la cheo, viongozi wa kidini wameenea kote ulimwenguni. Kama ilivyokuwa kwa viongozi wa kidini katika karne ya kwanza, wao pia “wanaikandamiza kweli” ya Neno la Mungu na “[kuibadili] kweli ya Mungu kwa ajili ya uwongo.” (Rom. 1:18, 25) Wanafundisha mafundisho ya uwongo kama vile “ukiokolewa, umeokolewa milele,” kutokufa kwa nafsi, kuzaliwa upya katika mwili mwingine, na wazo la kipumbavu kwamba Mungu hukubali ndoa za watu wa jinsia moja au njia yao ya maisha.

8. Ni uwongo gani tunaotarajia wanasiasa watangaze hivi karibuni, lakini tunapaswa kuitikiaje?

8 Wanasiasa hutumia mbinu ya kusema uwongo ili kuwapotosha wanadamu. Hivi karibuni watu watatangaza uwongo mkubwa zaidi kuwahi kusikika kwamba wamepata “amani na usalama!” Lakini “ndipo uharibifu wa ghafla utakapowapata mara moja.” Tusipumbazwe kamwe na jitihada zao za kujaribu kutupotosha kwamba ulimwengu huu haupo hatarini! Ukweli ni kwamba “[tunajua] vema kwamba siku ya Yehova inakuja kama vile mwizi anavyokuja usiku.”—1 The. 5:1-4.

KWA NINI WATU HUSEMA UWONGO

9, 10. (a) Kwa nini watu husema uwongo, na zoea hilo huwa na matokeo gani? (b) Tunapaswa kukumbuka nini kumhusu Yehova?

9 Watu wanapovumbua au kubuni kitu fulani kinachopendwa na watu wengi, hatimaye kitu hicho hutengenezwa kwa wingi. Na ndivyo ilivyo na uwongo. Kueneza habari za uwongo ni jambo la kawaida leo, na si watu mashuhuri tu wanaowadanganya wengine. Makala yenye kichwa “Kwa Nini Tunasema Uwongo” iliyoandikwa na Y. Bhattacharjee, inasema hivi: “Leo, kusema uwongo ni tabia ya wanadamu ambayo imekita mizizi sana.” Mara nyingi watu huamua kusema uwongo ili kujilinda au ili wasifiwe na watu. Watu husema uwongo ili kufunika makosa au kasoro zao au kujinufaisha kiuchumi na kibinafsi. Kama makala hiyo ilivyotaja, baadhi ya watu “huliona kuwa jambo rahisi sana kuwadanganya watu wasiowafahamu, wafanyakazi wenzao, marafiki, na wapendwa wao, iwe ni kuhusu mambo madogo au makubwa.”

10 Matokeo ya zoea hilo la kusema uwongo yamekuwa nini? Watu huacha kutumainiana na mahusiano yanaweza kuvunjika. Kwa mfano, wazia jinsi mume aliye mwaminifu kwa mke wake anavyoweza kuvunjika moyo anapogundua kwamba mke wake amefanya uzinzi na ameficha jambo hilo kwa kusema uwongo. Au wazia mwanamume anayemtendea mke au watoto wake kwa jeuri faraghani, lakini anapokuwa mbele ya watu anajifanya kuwa mume bora anayestahili kuigwa na wengine. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba watu kama hao wadanganyifu hawawezi kumficha Yehova jambo lolote kwa sababu “vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi” mbele zake.—Ebr. 4:13.

11. Mfano mbaya wa Anania na Safira unatufundisha nini? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

11 Kwa mfano, Biblia inatuambia jinsi ‘Shetani alivyowapa ujasiri’ wenzi fulani wa ndoa Wakristo katika karne ya kwanza ili waseme uwongo. Anania na Safira walitunga hila moyoni mwao ili wawadanganye mitume. Waliuza mali fulani lakini wakawaletea mitume kiasi fulani tu cha pesa walizopata. Wenzi hao walitaka kutaniko liwaone kuwa watu wema, kana kwamba walikuwa wakarimu sana walipotoa mchango wao ilhali haikuwa hivyo kihalisi. Ingawa hivyo, Yehova aliona jambo walilofanya, naye akawapa adhabu waliyostahili.—Mdo. 5:1-10.

12. Mwisho wa waongo wote wasiotubu utakuwaje, na kwa nini?

12 Yehova anahisije kuhusu kusema uwongo? Shetani na watu wote wasiotubu wanaomwiga, ambao wamezoea kusema uwongo ili kuwadhuru wengine, mwisho wao ni katika lile “ziwa la moto.” (Ufu. 20:10; 21:8; Zab. 5:6) Kwa nini? Kwa sababu machoni pa Yehova waongo hao wako katika kundi moja na “wale ambao matendo yao yanamchukiza Mungu.”—Ufu. 22:15, maelezo ya chini.

13. Tunajua nini kumhusu Yehova, na kujua hilo hutuchochea kufanya nini?

13 Tunajua kwamba Yehova “si mwanadamu anayesema uwongo.” Isitoshe, “Mungu hawezi kamwe kusema uwongo.” (Hes. 23:19; Ebr. 6:18) “Yehova anachukia . . . ulimi wa uwongo.” (Met. 6:16, 17) Ili tupate kibali chake, ni lazima tuishi kulingana na kiwango chake cha kusema ukweli. Hiyo ndiyo sababu ‘hatuambiani uwongo.’—Kol. 3:9.

SISI ‘HUAMBIANA UKWELI’

14. (a) Kuna tofauti gani kati yetu na washiriki wa dini ya uwongo? (b) Fafanua kanuni iliyo kwenye Luka 6:45.

14 Wakristo wa kweli ni tofauti na washiriki wa dini ya uwongo katika njia gani? Sisi ‘huambiana ukweli.’ (Soma Zekaria 8:16, 17.) Paulo anaeleza hivi: “Tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu, . . . kwa kusema maneno ya kweli.” (2 Kor. 6:4, 7) Yesu alisema hivi: “Kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni” mwa mtu. (Luka 6:45) Hivyo, mtu mwema anaposema ukweli moyoni mwake, maneno ya ukweli yatatoka kinywani mwake. Atawaambia watu wote ukweli—watu asiowafahamu, wafanyakazi wenzake, marafiki, na wapendwa wake, iwe ni kuhusu mambo madogo au makubwa. Acheni tuchunguze baadhi ya mambo tunayoweza kufanya yanayoonyesha kwamba tunajitahidi kuwa wanyoofu katika mambo yote.

Je, unatambua tatizo katika maisha ya dada huyu? (Tazama fungu la 15 na 16)

15. (a) Kwa nini si jambo la hekima kamwe kuishi maisha maradufu? (b) Ni nini kitakachowasaidia vijana kuepuka kushinikizwa na vijana wenzao? (Tazama maelezo ya chini.)

15 Vipi ikiwa wewe ni kijana na hungependa kuonekana kuwa tofauti na vijana wenzako? Usiruhusu kamwe tamaa hiyo ikufanye uishi maisha maradufu kama ambavyo vijana wengine wamefanya. Wao huonekana kuwa wenye maadili mazuri wanapokuwa pamoja na watu wa familia zao au kutanikoni, lakini huwa tofauti kabisa wakiwa na vijana wengine wasiomjua Yehova au wanapotumia mitandao ya kijamii. Huenda wanatumia lugha chafu, wanavalia isivyofaa, wanasikiliza miziki michafu, wanakunywa pombe kupita kiasi au kutumia dawa za kulevya, wanaendeleza kisiri urafiki wa kimapenzi, au kufanya mambo mengine mabaya zaidi. Wanaishi maisha ya udanganyifu mbele ya wazazi wao, waabudu wenzao, na mbele za Mungu. (Zab. 26:4, 5) Yehova anajua wakati ‘tunapomheshimu kwa midomo yetu, lakini mioyo yetu iko mbali naye.’ (Marko 7:6) Ni bora zaidi kufanya kama methali hii inavyosema: “Moyo wako usiwaonee wivu watenda dhambi, bali mwogope Yehova mchana kutwa.”—Met. 23:17. *

16. Kusema ukweli huhusikaje tunapojaza ombi la utumishi fulani wa pekee?

16 Huenda ungependa kutumikia ukiwa painia wa kawaida au kuingia katika utumishi wa wakati wote wa pekee, kama vile utumishi wa Betheli. Unapojaza fomu ya ombi lako, ni muhimu uwe mnyoofu na useme ukweli unapojibu maswali yote yanayoulizwa kuhusu afya yako, burudani unazopenda, na maadili. (Ebr. 13:18) Vipi ikiwa umejihusisha katika mwenendo fulani usio safi kiadili au unaotiliwa shaka na bado hujawajulisha wazee wa kutaniko? Wajulishe ili upate msaada utakaokusaidia kutumikia ukiwa na dhamiri safi.—Rom. 9:1; Gal. 6:1.

17. Tunapaswa kufanya nini tunapozungumza na wapinzani kuhusu ndugu zetu?

17 Unapaswa kufanya nini ikiwa wenye mamlaka katika nchi unayoishi wameiwekea vizuizi kazi ya Ufalme, nawe umeitwa ili uhojiwe kuhusu utendaji wa ndugu zako? Je, ni lazima uwaambie mambo yote unayojua? Yesu alifanya nini alipohojiwa na gavana Mroma? Nyakati nyingine Yesu alitumia kanuni ya Maandiko inayosema kuna “wakati wa kunyamaza na wakati wa kuongea,” hivyo alinyamaza! (Mhu. 3:1, 7; Mt. 27:11-14) Katika hali kama hiyo, litakuwa jambo bora kutenda kwa busara ili tusiwahatarishe ndugu zetu.—Met. 10:19; 11:12.

Ni nini kitakachokusaidia kuamua wakati wa kunyamaza au wakati wa kusema ukweli kamili? (Tazama fungu la 17 na 18)

18. Ni wajibu gani tulio nao tunapozungumza na wazee wa kutaniko kuhusu ndugu zetu?

18 Vipi ikiwa ndugu au dada kutanikoni ametenda dhambi nzito nawe unajua jambo hilo? Huenda wazee, ambao ndio walio na jukumu la kuhakikisha kwamba kutaniko linaendelea kuwa safi kiadili, wakakuuliza mambo unayojua kuhusu jambo lililotendeka. Utafanya nini hasa ikiwa yule aliyetenda dhambi hiyo ni rafiki wa karibu au mtu wa familia? Biblia inasema hivi: “Anayetoa ushahidi kwa uaminifu atasema ukweli.” (Met. 12:17; 21:28) Hivyo, una wajibu wa kuwaambia wazee ukweli kamili, si ukweli nusu-nusu, na ni lazima uepuke kupotosha ukweli. Wazee wana haki ya kujua habari kamili ili wajue njia bora zaidi watakayotumia kumsaidia mtenda dhambi awe tena na uhusiano mzuri pamoja na Yehova.—Yak. 5:14, 15.

19. Tunatazamia kujifunza nini katika makala inayofuata?

19 Mtunga zaburi Daudi, alisali hivi kwa Yehova: “Unapendezwa na ukweli katika utu wa ndani.” (Zab. 51:6) Daudi alijua kwamba kusema ukweli ni jambo linalotoka ndani yetu, ndani ya moyo wetu. Katika nyanja zote za maisha, Wakristo wa kweli hutii agizo hili: “Kila mtu amwambie mwenzake ukweli.” Njia nyingine tunayoweza kuonyesha kwamba sisi ni tofauti tukiwa wahudumu wa Mungu ni kuwafundisha wengine kweli zake tunapokuwa katika huduma. Tutachunguza jinsi ya kufanya hivyo katika makala inayofuata.

^ fu. 15 Tazama sura ya 15, “Nitashindaje Mkazo Kutoka kwa Vijana Wenzangu?,” na sura ya 16, “Kuwa na Nyuso Mbili​—Kuna Ubaya Gani?,” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2.