Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Alibariki Sana Uamuzi Wangu

Yehova Alibariki Sana Uamuzi Wangu

Mapambazuko yalikuwa yakikaribia tulipomaliza kuweka trakti chini ya milango ya nyumba chache zilizokuwa zimesalia katika eneo tulilokuwa tumegawiwa. Ulikuwa mwaka wa 1939, na tulikuwa tumeamka katikati ya usiku ili kusafiri kwa muda wa zaidi ya saa moja hadi kwenye jiji dogo linaloitwa Joplin kusini magharibi mwa jimbo la Missouri, nchini Marekani. Mara tu tulipomaliza kimyakimya kazi iliyokuwa imetupeleka huko, tulirudi kwenye gari letu na kusafiri hadi mahali tulipokuwa tumepanga kukutana na vikundi vingine vya wahubiri waliokuwa katika magari mengine. Huenda unashangaa kwa nini tulienda kuhubiri asubuhi sana kabla ya mapambazuko na kisha kuondoka upesi katika eneo hilo. Nitawaeleza baadaye.

NINASHUKURU kwamba nililelewa na wazazi Wakristo, Fred na Edna Molohan, ambao walinifundisha kumpenda Mungu. Tayari walikuwa Wanafunzi wa Biblia (Mashahidi wa Yehova) wenye bidii kwa miaka 20 kufikia wakati nilipozaliwa, mwaka wa 1934. Familia yetu iliishi katika mji mdogo ulioitwa Parsons, kusini mashariki mwa jimbo la Kansas. Tulishirikiana na kutaniko ambalo idadi kubwa ya wahubiri walikuwa watiwa-mafuta. Familia yetu ilikuwa na ratiba nzuri ya kuhudhuria mikutano na kuwahubiria wengine kweli ya Neno la Mungu. Kila Jumamosi alasiri tulikuwa tukishiriki katika mahubiri ya barabarani, kama mahubiri ya hadharani yalivyojulikana siku hizo. Nyakati nyingine tulichoka, lakini sikuzote baba alituburudisha kwa kutupeleka mahali fulani tukale aiskrimu baada ya kumaliza.

Kutaniko letu dogo lilikuwa na eneo kubwa lililotia ndani miji fulani midogo na vilevile mashamba mengi yaliyokuwa katika maeneo jirani. Tulipowatembelea wakulima, kwa kawaida tungewapa machapisho yetu nao wangetupatia mboga walizokuwa wamepanda mashambani mwao, mayai yaliyotoka tu kutagwa, au hata kuku walio hai. Kwa kuwa tayari Baba alikuwa ametoa mchango kwa ajili ya machapisho hayo, vyakula hivyo vilisaidia familia yetu kuwa na chakula cha kutosha.

KAMPENI ZA KUHUBIRI

Wazazi wangu walinunua gramafoni ambayo waliitumia kwenye kazi ya kuhubiri. Kwa kuwa nilikuwa na umri mdogo sikuweza kuitumia, hata hivyo Baba na Mama walipofanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia, nilifurahi kuwasaidia kucheza hotuba zilizorekodiwa za Ndugu Rutherford.

Nikiwa pamoja na Baba na Mama mbele ya gari letu lenye kipaza-sauti

Baba alibadili gari letu aina ya Ford la muundo wa mwaka wa 1936 na kuwa gari lenye kipaza-sauti kilichokuwa kimefungwa kwenye paa lake. Gari hilo lilisaidia sana kueneza ujumbe wa Ufalme. Kwa kawaida, muziki uliorekodiwa ulichezwa kwanza ili kunasa usikivu wa watu, na kisha hotuba ya Biblia iliyorekodiwa ilichezwa. Baada ya hotuba, tungewapa machapisho watu waliopendezwa.

Katika mji mdogo wa Cherryvale, Kansas, polisi walimwambia Baba kwamba hakuruhusiwa kutumia gari lake lenye kipaza-sauti kwenye bustani ya mji huo, ambapo watu wengi walikuwa wakipumzika siku za Jumapili, lakini angeweza kulitumia nje ya bustani hiyo. Baba hakubishana nao, badala yake alilihamisha gari hadi kwenye barabara iliyokuwa kando ya bustani ambapo watu waliokuwa ndani ya bustani wangeweza kusikia ujumbe. Nilifurahia sana kuwa pamoja na Baba na kaka yangu, Jerry, katika pindi kama hizo.

Mwishoni mwa miaka ya 1930, tulishiriki katika kampeni za pekee za kukamilisha kuhubiri maeneo yenye upinzani mkali kwa muda mfupi. Tulikuwa tukiamka kabla ya mapambazuko (kama tulivyofanya huko Joplin, Missouri) na kuweka kimyakimya trakti au vijitabu chini ya milango ya nyumba za watu. Baadaye, tungekutana nje ya jiji ili kuhakikisha kwamba hakuna yeyote aliyekamatwa na polisi.

Siku hizo, mbinu nyingine yenye kusisimua ya huduma yetu ilijulikana kama maandamano ya kutangaza habari. Ili kutangaza Ufalme, tulivaa mabango na kupita katikati ya jiji tukiwa tumepanga mstari. Ninakumbuka siku moja maandamano hayo yalifanywa katika mji wetu na baadhi ya ndugu zetu walikuwa wamevaa mabango yaliyoandikwa “Dini Ni Mtego na Hila.” Walitembea kwa mwendo wa kilomita 1.6 katikati ya mji na kisha wakarudi nyumbani kwetu. Jambo la kufurahisha ni kwamba hawakukabili upinzani walipokuwa wakifanya maandamano hayo, badala yake walikutana na watazamaji wengi wenye kupendezwa.

MAKUSANYIKO YA ZAMANI

Mara nyingi familia yetu ingesafiri kutoka Kansas hadi Texas ili kuhudhuria makusanyiko. Baba alifanya kazi kwenye shirika la reli la Missouri-Kansas-Texas (ambalo pia liliitwa M-K-T, au Katy, Railroad), hivyo tungesafiri kwa treni kwa kutumia kibali cha Baba cha kazi, na kwa njia hiyo tungeweza kuwatembelea watu wetu wa ukoo na kuhudhuria makusanyiko tukiwa pamoja. Kaka ya mama, Fred Wismar, na mke wake, Eulalie, waliishi Temple, Texas. Mjomba wangu Fred alijifunza kweli akiwa kijana mwanzoni mwa miaka ya 1900, akabatizwa, na kuwahubiria wadogo zake, kutia ndani mama yangu. Alijulikana sana na akina ndugu kotekote katika eneo la kati la jimbo la Texas, ambapo alikuwa ametumikia akiwa mtumishi wa kanda (sasa anaitwa mwangalizi wa mzunguko). Alikuwa mwanamume mwenye fadhili na mwenye furaha na ambaye ungefurahia kuwa pamoja naye wakati wote. Alikuwa mwenye bidii kwa ajili ya kweli, na kwa hakika alinisaidia sana nilipokuwa kijana.

Katika mwaka wa 1941 familia yetu ilisafiri kwa treni hadi St. Louis, Missouri, ili kuhudhuria kusanyiko kubwa. Vijana wote walialikwa waketi pamoja kwenye eneo maalumu lililotengwa kwenye uwanja huo ili kusikiliza hotuba ya Ndugu Rutherford yenye kichwa “Watoto wa Mfalme.” Mwishoni mwa hotuba yake, kila kijana alifurahi kupokea zawadi ya kitabu kipya Children, kilichogawanywa na Ndugu Rutherford na wasaidizi wake. Kulikuwa na vijana zaidi ya 15,000 waliofurahia kupata baraka hiyo ya kiroho.

Katika mwezi wa Aprili, mwaka wa 1943 tulifurahia kusanyiko dogo lakini muhimu lenye kichwa “Mwito wa Utendaji” huko Coffeyville, Kansas. Shule mpya iliyoitwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ambayo ingekuwa ikifanywa katika makutaniko yote ilianzishwa, na kijitabu chenye masomo 52, ambacho kingetumiwa kwenye shule hiyo, kilitolewa. Baadaye mwaka huo, nilitoa hotuba yangu ya kwanza kwenye shule hiyo. Kusanyiko hilo pia lilikuwa la pekee kwangu kwa sababu mimi pamoja na wengine wachache, tulibatizwa kwenye kidimbwi chenye maji baridi kwenye shamba lililokuwa jirani.

KAZI NILIYOTAMANI—UTUMISHI WA BETHELI

Nilimaliza shule mwaka wa 1951, na nilihitaji kufanya maamuzi kuhusu wakati wangu ujao. Nilitamani sana kuingia katika utumishi wa Betheli ambako kaka yangu, Jerry, alikuwa ametumikia awali. Basi mimi pia nilituma ombi langu bila kukawia kwenye ofisi ya Brooklyn. Uamuzi huo ulininufaisha sana kiroho. Baada ya muda mfupi, ombi langu lilikubaliwa, nami nikaalikwa nianze utumishi wa Betheli mwezi wa Machi 10, 1952.

Nilitamani kufanya kazi kwenye kiwanda cha uchapishaji ili nishiriki kwenye kazi ya kuchapisha magazeti na machapisho mengine. Hata hivyo, nilipewa kazi ya kuwa mhudumu wa vyakula na baadaye nilifanya kazi jikoni, ambako nilifurahia kujifunza mambo mengi kwelikweli. Hivyo, sikuwahi kupata pendeleo la kufanya kazi kwenye kiwanda cha uchapishaji. Hata hivyo, ratiba ya kazi ya jikoni ilinisaidia sana kwa sababu nilipata wakati wa kujifunza kibinafsi wakati wa kipindi cha mchana nikitumia maktaba ya Betheli iliyokuwa na machapisho mengi sana. Jambo hilo lilinisaidia nikue kiroho na liliimarisha imani yangu. Pia, lilifanya niazimie hata zaidi kumtumikia Yehova nikiwa Mwanabetheli kwa muda mrefu kadiri nilivyoweza. Jerry alikuwa ametoka Betheli mwaka wa 1949 na kumwoa Patricia, lakini waliishi Brooklyn karibu na Betheli. Sikuzote walikuwa msaada mkubwa kwangu na walinitia moyo katika miaka yangu ya kwanza nikiwa Mwanabetheli.

Muda mfupi baada ya kuwasili Betheli, kulikuwa na majaribio yaliyopangwa ili kuongeza akina ndugu zaidi kwenye orodha ya wasemaji wa Betheli. Akina ndugu waliokuwa kwenye orodha hiyo walipewa mgawo wa kutembelea makutaniko yaliyokuwa umbali usiozidi kilomita 322 kutoka Brooklyn, ili watoe hotuba za watu wote na kushirikiana na makutaniko hayo kwenye utumishi wa shambani. Nilikuwa na pendeleo la kuwekwa kwenye orodha hiyo. Nikiwa na wasiwasi, nilitoa hotuba yangu ya kwanza ya watu wote, ambayo wakati huo ilikuwa na urefu wa saa moja hivi. Kwa kawaida, nilisafiri kwa treni ili kufika kwenye makutaniko hayo. Ninakumbuka vizuri Jumapili moja alasiri wakati wa majira ya baridi kali, mwaka wa 1954. Nilipanda treni iliyokuwa ikielekea New York ambayo ingeniwezesha kurudi Betheli jioni. Hata hivyo, dhoruba kali yenye upepo ulioambatana na baridi kali na theluji ilitokea. Injini za treni zilizokuwa zikiendeshwa kwa umeme zilizima. Hatimaye, treni hiyo ikafanikiwa kufika jiji la New York City alfajiri saa 11 Jumatatu. Kisha nikaingia kwenye treni ya chini ya ardhi kuelekea Brooklyn, na nilipofika nikaelekea moja kwa moja kwenye mgawo wangu jikoni, nikiwa nimechelewa kidogo na nimechoka baada ya kuketi usiku kucha kwenye treni mbovu. Lakini niliziona changamoto hizo kuwa si kitu ikilinganishwa na shangwe niliyopata kwa kuwatumikia akina ndugu na kupata marafiki wengi wapya nilipokuwa nikiwatembelea wakati wa miisho juma hiyo.

Tukijitayarisha kwa ajili ya kipindi kwenye studio ya WBBR

Katika miaka yangu ya mapema Betheli, nilipewa mgawo wa kushiriki katika vipindi vya redio kwenye stesheni ya WBBR. Wakati huo studio zilikuwa kwenye ghorofa ya kwanza ya jengo la 124 Columbia Heights. Nilipewa mgawo wa kushiriki kwenye programu ya funzo la Biblia iliyokuwa ikipeperushwa kila juma. Ndugu A. H. Macmillan, mshiriki wa muda mrefu wa familia ya Betheli, alishiriki kwa ukawaida kwenye programu hiyo. Tulizoea kumwita Ndugu Mac, naye alituwekea mfano mzuri wa uvumilivu katika utumishi wa Yehova tukiwa Wanabetheli vijana.

Tulichochea upendezi kwa kuwapa watu mwaliko huu wa kusikiliza WBBR

Katika mwaka wa 1958 nilipewa mgawo wa kufanya kazi kwa ukaribu na Shule ya Gileadi. Kazi yangu ilikuwa kuwasaidia wahitimu kupata viza na kushughulikia usafiri wa ndugu na dada hao wenye bidii. Usafiri wa anga ulikuwa ghali sana siku hizo, hivyo ni wahitimu wachache tu walioutumia. Wengi waliosafiri kwenda Afrika na Mashariki ya Mbali walisafiri kwa meli za mizigo. Huduma za ndege za biashara zilipoanza, gharama za nauli za ndege zikawa nafuu zaidi na hivyo baada ya muda mfupi wamishonari wengi walisafiri kwa ndege ili kufika kwenye migawo yao.

Nikikusanya diploma za wanafunzi wa Gileadi kabla ya programu ya kuhitimu

SAFARI ZA MAKUSANYIKO

Majukumu yangu yaliongezeka katika mwaka wa 1960, nilipopewa kazi ya kushughulikia usafiri wa kutumia ndege za kukodi kutoka Marekani kwenda Ulaya, kwa ajili ya makusanyiko ya kimataifa yaliyofanywa mwaka wa 1961. Nilipanda ndege ya kukodi iliyokuwa ikisafiri kutoka New York kwenda Hamburg, Ujerumani, ili kuhudhuria kusanyiko hilo. Baada ya kusanyiko, mimi pamoja na ndugu wengine watatu kutoka Betheli tulikodi gari na kuliendesha hadi Italia ili kutembelea ofisi ya tawi jijini Rome. Kisha safari yetu ilitufikisha Ufaransa, tukasafiri hadi kwenye Milima ya Pyrenees, halafu tukaingia nchi ya Hispania, ambako kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku. Tulifanikiwa kuingiza machapisho kadhaa yaliyokuwa yamefungwa kama zawadi, na kuwapatia ndugu zetu jijini Barcelona. Tulisisimka sana kukutana nao! Baada ya hapo tuliendesha gari hadi Amsterdam, ambako tulipanda ndege kurudi New York.

Mwaka mmoja hivi baadaye, mgawo wangu Betheli ulihusisha kufanya mipango ya usafiri kwa ajili ya wajumbe waliochaguliwa kuhudhuria mfululizo wa makusanyiko ya pekee ya kimataifa ulimwenguni kote. Kusanyiko hilo la mwaka wa 1963 lilikuwa na kichwa, “Habari Njema za Milele.” Mipango ilifanywa ili wajumbe 583 wasafiri kotekote duniani ili kuhudhuria makusanyiko huko Ulaya, Asia, na Kusini mwa Pasifiki, na kisha kukamilisha ziara yao huko Honolulu, Hawaii, na kisha Pasadena, California. Pia, walifanya ziara ya pekee huko Lebanoni na Jordan ili wajifunze kuhusu maeneo yanayotajwa katika Biblia. Mbali na kufanya mipango kwa ajili ya safari za ndege na malazi yao hotelini, idara yetu Betheli ilifanya mipango ili wapate viza za nchi zote walizohitaji kutembelea.

MWANDAMANI MPYA WA KUSAFIRI NAYE

Mwaka wa 1963 ulikuwa mwaka muhimu kwangu kwa sababu nyingine ya pekee. Mwezi wa Juni 29, nilimwoa dada Lila Rogers kutoka Missouri, ambaye alikuwa ameanza utumishi wa betheli miaka mitatu mapema. Juma moja baada ya kufunga ndoa, mimi pamoja na Lila tulijiunga na wajumbe hao waliokuwa wakiuzunguka ulimwengu nasi tukatembelea Ugiriki, Misri, na Lebanoni. Tulisafiri kwa ndege kutoka Beirut hadi kwenye uwanja mdogo wa ndege uliopo Jordan. Kwa kuwa kazi yetu ilikuwa imewekewa vizuizi huko Jordan na tulikuwa tumeambiwa kwamba Mashahidi wa Yehova hawakuwa wakipewa viza za kuingia nchini humo, tulijiuliza hali ingekuwaje baada ya kuwasili huko. Wazia jinsi tulivyostaajabu kwa furaha tulipowasili kwenye uwanja wa ndege na kuona umati wa watu walioshika bango lililosema “Karibuni Mashahidi wa Yehova”! Na tulisisimka kwelikweli kujionea kwa macho yetu wenyewe maeneo mbalimbali yanayotajwa kwenye Biblia! Tulitembelea maeneo ambayo wazee wa kale wa ukoo waliishi, maeneo ambayo Yesu na mitume wake walihubiri, na mahali ambapo Ukristo ulianzia na kuenea katika miisho ya dunia.—Mdo. 13:47.

Kwa miaka 55, Lila amekuwa mwandamani wangu mshikamanifu katika migawo yetu yote ya utumishi. Tulifanikiwa kutembelea mara kadhaa nchi ya Hispania na ya Ureno kazi yetu ilipokuwa imepigwa marufuku katika nchi hizo. Tuliwatia moyo ndugu zetu katika nchi hizo na kuwaletea machapisho na vitu vingine walivyohitaji. Pia, tulifanikiwa kuwatembelea baadhi ya ndugu zetu waliofungwa kwenye ngome ya kale ya kijeshi huko Cádiz, Hispania. Moyo wangu ulijawa na shangwe nilipofanikiwa kuwatia moyo kupitia hotuba ya Biblia.

Tukiwa na Patricia na Jerry Molohan tukielekea kwenye Kusanyiko lenye kichwa “Amani Duniani” la mwaka wa 1969

Kwa miaka mingi tangu mwaka wa 1963, nimefurahia sana pendeleo la kushughulikia mipango ya usafiri kwa ajili ya wajumbe wa makusanyiko ya kimataifa huko Afrika, Australia, Amerika ya Kati na ya Kusini, Ulaya, Mashariki ya Mbali, Hawaii, New Zealand, na Puerto Riko. Mimi pamoja na Lila tumefurahia makusanyiko mengi ambayo kamwe hatutasahau, kutia ndani kusanyiko la Warsaw, Poland, la mwaka 1989. Ndugu wengi kutoka Urusi walihudhuria kusanyiko hilo kubwa—na ndilo lililokuwa kusanyiko lao la kwanza kuhudhuria! Akina ndugu na dada kadhaa tuliokutana nao walikuwa wamefungwa kwa miaka mingi gerezani kwa sababu ya imani yao kwenye nchi zilizokuwa katika Muungano wa Sovieti.

Nimefurahia sana pendeleo la kutembelea ofisi za tawi kote duniani ili kuwajenga na kuwatia moyo Wanabetheli na wamishonari. Mara ya mwisho tulipotembelea ofisi ya tawi ya Korea Kusini, tulifanikiwa kutembelea ndugu 50 waliofungwa gerezani huko Suwon. Ndugu hao wote walikuwa na mtazamo mzuri na walitazamia kwa hamu kuendelea na huduma yao bila vizuizi vyovyote. Kukutana nao kulitutia moyo sana!—Rom. 1:11, 12.

ONGEZEKO LANIPA SHANGWE

Kwa miaka mingi nimejionea jinsi Yehova anavyowabariki watu wake kwa kuwapa ongezeko. Nilipobatizwa mwaka wa 1943 kulikuwa na wahubiri 100,000 hivi, lakini sasa kuna zaidi ya wahubiri 8,000,000 wanaomtumikia Yehova katika nchi 240. Asilimia kubwa ya ongezeko hilo limechangiwa na kazi ya kuhubiri ambayo imekuwa ikifanywa kwa bidii na wahitimu wa Shule ya Gileadi. Imekuwa shangwe iliyoje kufanya kazi kwa ukaribu na wengi wa wamishonari hao na kuwasaidia wafike kwenye migawo yao!

Ninafurahi kwamba nilifanya uamuzi wa kupanua huduma yangu nikiwa kijana kwa kujaza ombi la kuingia kwenye utumishi wa Betheli. Yehova amenibariki sana katika kila hatua ya maisha yangu. Mbali na shangwe tunayopata kwa kutumikia Betheli, kwa miaka mingi mimi pamoja na Lila tulifurahia pendeleo la kushiriki katika huduma pamoja na makutaniko yaliyopo Brooklyn, ambapo tulipata marafiki wengi wa kudumu.

Kwa utegemezo wa Lila, ninazidi kusonga mbele siku baada ya siku katika utumishi wangu wa Betheli. Hata ingawa nina umri wa zaidi ya miaka 84, bado ninaweza kutimiza mgawo wangu wa kushughulikia barua za ofisi ya tawi.

Leo, nikiwa pamoja na Lila

Tumefurahia sana kuwa sehemu ya tengenezo zuri ajabu la Yehova, na kujionea tofauti kubwa iliyopo kati ya wale wanaomtumikia Yehova na wasiomtumikia. Tunaelewa vizuri andiko la Malaki 3:18: “Mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.” Kadiri siku zinavyozidi kupita, tunajionea mfumo wa Shetani ukizidi kuporomoka, mfumo uliojaa watu wasio na tumaini na ambao hawana shangwe. Lakini wale wanaompenda na kumtumikia Yehova wana maisha yenye furaha, hata katika nyakati hizi ngumu, na pia wana tumaini hakika la wakati ujao. Tuna pendeleo kubwa sana la kueneza habari njema ya Ufalme! (Mt. 24:14) Tunatazamia kwa hamu wakati ambapo hivi karibuni, Ufalme wa Mungu utakomesha ulimwengu huu wa kale na kuleta ulimwengu mpya pamoja na baraka zote zilizoahidiwa, kutia ndani afya njema na maisha yasiyo na mwisho. Wakati huo, watumishi waaminifu wa Yehova duniani watafurahia maisha milele.