Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndugu Rutherford akitoa hotuba kusanyikoni huko Cedar Point, Ohio, 1919

1919​—Miaka Mia Moja Iliyopita

1919​—Miaka Mia Moja Iliyopita

KUFIKIA mwaka wa 1919 vile Vita Vikuu (ambavyo baadaye viliitwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu), vilivyopiganwa kwa zaidi ya miaka minne, vilikuwa vimekwisha. Mwishoni mwa mwaka wa 1918, mataifa yaliacha kupigana, na Januari 18, 1919, Mkutano wa Amani wa Paris ulianza. Mojawapo ya mambo yaliyotimizwa na mkutano huo ni kuanzishwa kwa Mkataba wa Versailles, ambao ulikomesha rasmi vita kati ya Majeshi ya Muungano na Ujerumani. Mkataba huo ulitiwa sahihi Juni 28, 1919.

Pia, mkataba huo ulianzisha shirika jipya lililoitwa Ushirika wa Mataifa. Lengo la shirika hilo lilikuwa “kuendeleza ushirikiano wa kimataifa na kupata amani na usalama miongoni mwa mataifa.” Dini zinazodai kuwa za Kikristo ziliunga mkono shirika hilo. Baraza la Muungano wa Makanisa ya Kristo Nchini Marekani lilisifu shirika hilo likilifafanua kuwa “shirika la kisiasa linalowakilisha Ufalme wa Mungu duniani.” Baraza hilo liliunga mkono shirika hilo kwa kuwatuma wajumbe kwenye Mkutano wa Amani wa Paris. Mmojawapo wa wajumbe hao alisema kwamba mkutano huo “ulikuwa mwanzo wa kipindi kipya katika historia ya ulimwengu.”

Kipindi kipya kilianza, lakini hakikuletwa na wanaume waliokuwepo kwenye mkutano huo wa amani. Katika mwaka wa 1919, kipindi kipya katika kazi ya kuhubiri kilianza Yehova alipowatia nguvu watu wake ili wahubiri kwa bidii kuliko wakati mwingine wowote uliopita. Lakini kwanza, Wanafunzi wa Biblia walihitaji kupitia mabadiliko makubwa sana.

UAMUZI MGUMU

Joseph F. Rutherford

Uchaguzi wa kila mwaka wa baraza la waelekezi wa Shirika la Watch Tower Bible and Tract Society ulipangwa kufanywa Jumamosi, Januari 4, 1919. Wakati huo, Joseph F. Rutherford, aliyekuwa akiongoza miongoni mwa watu wa Yehova alikuwa amefungwa gerezani isivyo haki pamoja na ndugu wengine saba huko Atlanta, Georgia, Marekani. Swali lilizuka, Je, akina ndugu waelekezi waliokuwa gerezani walipaswa kuchaguliwa tena, au wengine wangechukua nafasi zao?

Evander J. Coward

Akiwa kwenye chumba chake gerezani, Ndugu Rutherford alikuwa na wasiwasi kuhusu hali ya wakati ujao ya tengenezo. Alijua kwamba baadhi ya akina ndugu walihisi kwamba ingefaa zaidi kumchagua ndugu mwingine ili awe msimamizi. Hivyo, aliwaandikia barua akina ndugu waliokuwa kwenye mkutano huo, akipendekeza kwamba Evander J. Coward achaguliwe kuwa msimamizi. Rutherford alimfafanua ndugu Coward kuwa mtu “mtulivu,” “mwenye busara,” na “mshikamanifu kwa Bwana.” Hata hivyo, ndugu wengi walipendelea suluhisho tofauti, yaani, kuahirisha uchaguzi huo kwa miezi sita. Jopo la wanasheria lililokuwa limewatetea akina ndugu walio gerezani lilikubaliana na wazo hilo. Mazungumzo yalipokuwa yakiendelea, baadhi ya akina ndugu walipandwa na hasira.

Richard H. Barber

Kisha jambo fulani likatokea ambalo baadaye ndugu Richard H. Barber alilifafanua kuwa ‘kumimina mafuta kwenye maji yenye msukosuko.’ Ndugu mmoja aliyekuwa kwenye mkutano huo alisema hivi waziwazi: “Mimi si mwanasheria, lakini inapohusu uhalali wa jambo hili, ninajua jambo fulani kuhusu sheria ya washikamanifu. Mungu anataka tuwe washikamanifu. Njia bora zaidi ya kuonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kwa Mungu ni kufanya uchaguzi na kumchagua tena Ndugu Rutherford kuwa msimamizi.”—Zab. 18:25.

Alexander H. Macmillan

Ndugu A. H. Macmillan aliyekuwa amefungwa gerezani, anakumbuka kwamba siku iliyofuata Ndugu Rutherford aligonga kwenye ukuta wa gereza alilokuwa na kusema, “Toa mkono wako nje.” Kisha Ndugu Rutherford akampa ujumbe wa telegramu. Macmillan alipouona ujumbe huo mfupi, alijua mara moja ulimaanisha nini. Ujumbe huo ulisema: “RUTHERFORD WISE VAN BARBER ANDERSON BULLY NA SPILL MSIMAMIZI MAOFISA WA KWANZA WATATU TUNAWAPENDA NYOTE.” Hiyo ilimaanisha kwamba waelekezi wote walikuwa wamechaguliwa tena, na kwamba Joseph Rutherford alikuwa ndiye msimamizi na William Van Amburgh, mwandishi mweka-hazina. Hivyo, Ndugu Rutherford angeendelea kuwa msimamizi.

WAACHILIWA HURU!

Ndugu hao wanane walipokuwa gerezani, Wanafunzi waaminifu wa Biblia walieneza waraka wa kuomba ndugu hao waachiliwe huru. Ndugu na dada hao jasiri walikusanya zaidi ya sahihi 700,000. Siku ya Jumatano, Machi 26, 1919, kabla ya kuwasilisha waraka huo, Ndugu Rutherford na ndugu wale wengine wenye majukumu waliachiliwa huru.

Ndugu Rutherford aliwaambia hivi wale waliomkaribisha baada ya kutoka gerezani: “Ninasadiki kwamba mambo haya ambayo sisi sote tumepitia yanatutayarisha kwa ajili ya nyakati ngumu zaidi zilizo mbele yetu. . . . Hamkupambana ili tu kuwatoa ndugu zenu gerezani. Hilo halikuwa jambo kuu. . . . Kusudi kuu la pambano ambalo mmefanya ni kutoa ushahidi kwa ajili ya Kweli, na wale ambao wameshiriki katika pambano hilo wamebarikiwa sana.”

Hali zilizojitokeza wakati wa kesi ya ndugu zetu zinaonyesha kwamba huenda Yehova ndiye aliyekuwa akiongoza mambo. Mei 14, 1919, mahakama ya rufaa ilitoa uamuzi huu: “Washtakiwa katika kesi hii hawakupewa hukumu waliyostahili . . . isiyopendelea upande wowote, na kwa sababu hiyo kesi yao ya awali imefutwa.” Ndugu hao walikuwa wameshtakiwa kwa makosa mazito, na ikiwa wangesamehewa au ikiwa wangepunguziwa tu kifungo chao, rekodi zingeonyesha kwamba bado wana hatia. Hawakufunguliwa mashtaka yoyote mengine. Hivyo, Jaji Rutherford alistahili kuendelea kuwatetea kisheria watu wa Yehova mbele ya Mahakama Kuu ya Marekani, jambo ambalo alifanya mara nyingi baada ya kuachiliwa huru.

WALIAZIMIA KUHUBIRI

Ndugu Macmillan alieleza hivi: “Tuliazimia kwamba hatungekaa tu kitako tukichezea vidole vyetu huku tukisubiri Bwana atuchukue kwenda mbinguni. Tulitambua kwamba tulipaswa kufanya jambo fulani ili tuweze kujua mapenzi ya Bwana wetu yalikuwa nini hasa.”

Lakini akina ndugu waliokuwa makao makuu hawangeweza kuendelea na kazi waliyokuwa wamefanya kwa miaka mingi. Kwa nini? Kwa sababu walipokuwa gerezani mabamba ya uchapishaji yaliyotumiwa kuchapisha machapisho yalikuwa yameharibiwa. Hilo lilikuwa jambo lenye kuvunja moyo, na baadhi ya akina ndugu walijiuliza ikiwa kazi ya kuhubiri ilikuwa imefikia mwisho.

Je, bado kulikuwa na watu waliopendezwa na ujumbe wa Ufalme uliokuwa ukihubiriwa na Wanafunzi wa Biblia? Ili kupata jibu, Ndugu Rutherford aliamua kutoa hotuba. Watu wote wangealikwa. Ndugu Macmillan alisema hivi: “Ikiwa hakuna yeyote ambaye angehudhuria mkutano huo basi tungejua kwamba kazi ya kuhubiri ilikuwa imefikia mwisho wake.”

Gazeti likitangaza hotuba ya Ndugu Rutherford, “Tumaini kwa Wanadamu Wanaoteseka,” huko Los Angeles, California, 1919

Hivyo, siku ya Jumapili, Mei 4, 1919, licha ya tatizo kubwa la kiafya alilokuwa nalo, Ndugu Rutherford alitoa hotuba yenye kichwa “Tumaini kwa Wanadamu Wanaoteseka” huko Los Angeles, California. Watu 3,500 hivi walihudhuria hotuba hiyo, na ilibidi mamia ya watu wasiruhusiwe kuingia ukumbini kwa kuwa nafasi haikutosha. Siku iliyofuata, watu wengine 1,500 walihudhuria. Akina ndugu walipata jibu walilotaka—bado watu walikuwa wanapendezwa!

Jambo ambalo akina ndugu walifanya baada ya hapo, liliweka msingi wa jinsi kazi ya kuhubiri inavyofanywa na Mashahidi wa Yehova hadi leo.

TAYARI KWA AJILI YA UKUZI WA WAKATI UJAO

Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1919, lilitangaza kwamba kungekuwa na kusanyiko mwanzoni mwa mwezi wa Septemba huko Cedar Point, Ohio. Clarence B. Beaty, ndugu kijana aliyekuwa Mwanafunzi wa Biblia kutoka Missouri alieleza hivi: “Kila mtu alihisi kwamba anapaswa kuhudhuria.” Zaidi ya ndugu na dada 6,000 walihudhuria kusanyiko hilo; idadi ambayo ilizidi sana ile iliyotarajiwa. Jambo lililosisimua hata zaidi ni kwamba zaidi ya watu 200 walibatizwa kwenye Ziwa Erie lililokuwa karibu.

Jalada la toleo la kwanza la The Golden Age la Oktoba 1, 1919

Katika siku ya tano ya kusanyiko hilo, yaani, Septemba 5, 1919, Ndugu Rutherford alipokuwa akitoa hotuba yenye kichwa “Hotuba kwa Wafanyakazi Wenzi,” alitangaza kuchapishwa kwa gazeti jipya lenye kichwa The Golden Age. * Gazeti hilo ‘lingezungumzia habari za karibuni za ulimwengu zilizo muhimu na kutoa ufafanuzi wa Kimaandiko unaoeleza kwa nini matukio hayo makubwa yalikuwa yakitokea.’

Wanafunzi wote wa Biblia walitiwa moyo wahubiri kwa ujasiri wakitumia chapisho hilo jipya. Barua iliyotoa mwongozo kuhusu jinsi ambavyo kazi hiyo ilipaswa kufanywa ilitaja hivi: “Acha kila mtu aliyebatizwa akumbuke kwamba ni pendeleo kubwa kutumikia, na atumie fursa hiyo sasa na hivyo kufanya mengi kadiri awezavyo kutoa ushahidi kwa ulimwengu.” Wengi waliitikia mwaliko huo! Kufikia mwezi wa Desemba, wahubiri wa Ufalme wenye bidii walikuwa wamepokea maandikisho 50,000 ya gazeti hilo jipya.

Akina ndugu huko Brooklyn, New York, wakiwa kando ya gari lililojaa magazeti ya The Golden Age

Mwishoni mwa mwaka wa 1919, watu wa Yehova walikuwa na nguvu mpya na walikuwa tayari kwa ajili ya kazi. Isitoshe, tayari unabii mbalimbali kuhusu siku za mwisho ulikuwa umetimizwa. Kipindi cha kujaribiwa na kutakaswa kwa watu wa Mungu kilichotabiriwa kwenye Malaki 3:1-4, kilikuwa kimekamilika. Watu wa Yehova walikuwa wamewekwa huru kutoka katika utekwa wa “Babiloni Mkubwa,” na Yesu alikuwa amemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” * (Ufu. 18:2, 4; Mt. 24:45) Sasa Wanafunzi wa Biblia walikuwa tayari kwa ajili ya kazi ambayo Yehova alitaka wafanye.

^ fu. 22 Mwaka wa 1937, gazeti The Golden Age lilibadilishwa jina na kuitwa Consolation na mwaka wa 1946 likaitwa Amkeni!