Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 41

Endelea Kuwa Mwaminifu Wakati wa “Dhiki Kuu”

Endelea Kuwa Mwaminifu Wakati wa “Dhiki Kuu”

“Mpendeni Yehova, enyi nyote mlio washikamanifu kwake! Yehova huwalinda waaminifu.”—ZAB. 31:23.

WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia

MUHTASARI *

1-2. (a) Viongozi wa ulimwengu watatangaza nini hivi karibuni? (b) Tunahitaji kupata majibu ya maswali gani?

WAZIA kwamba viongozi wa ulimwengu wametoka tu kutangaza tangazo la “amani na usalama” tulilokuwa tukisubiri kwa muda mrefu. Huenda wakajigamba kwamba sasa, kuliko wakati mwingine wowote, ulimwengu umekuwa mahali salama zaidi. Viongozi hao watataka tufikiri kwamba sasa wana uwezo wa kusuluhisha matatizo yote ya ulimwengu. Lakini kwa kweli hawatakuwa na uwezo wa kuzuia kitakachofuata! Kwa nini? Kulingana na unabii wa Biblia, “uharibifu wa ghafla [utawapata] mara moja, . . . nao hawataponyoka kamwe.”—1 The. 5:3.

2 Tunahitaji kupata majibu ya maswali haya muhimu: Ni nini kitakachotukia wakati wa “dhiki kuu”? Yehova anatarajia tufanye nini wakati huo? Na tunaweza kujitayarishaje sasa ili tudumu tukiwa waaminifu katika kipindi chote cha dhiki kuu?—Mt. 24:21.

NI NINI KITAKACHOTUKIA WAKATI WA “DHIKI KUU”?

3. Kulingana na Ufunuo 17:5, 15-18, Mungu atamwangamizaje “Babiloni Mkubwa”?

3 Soma Ufunuo 17:5, 15-18. “Babiloni Mkubwa” ataangamizwa! Kama ilivyotajwa awali, viongozi wa ulimwengu hawataweza kuzuia mambo yatakayotendeka wakati huo. Kwa nini? Kwa sababu “Mungu [atatia] hilo ndani ya mioyo yao ili kute-keleza wazo lake.” Wazo gani hilo? Wazo la kuangamiza milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo, kutia ndani dini zinazodai kuwa za Kikristo. * Mungu atatia wazo lake katika mioyo ya zile “pembe kumi” za “mnyama wa mwituni mwenye rangi nyekundu.” Pembe hizo zinafananisha serikali zote za kisiasa zinazomuunga mkono “yule mnyama wa mwituni,” yaani, Umoja wa Mataifa. (Ufu. 17:3, 11-13; 18:8) Serikali hizo za kisiasa zitakaposhambulia dini ya uwongo, jambo hilo litakuwa ishara ya kwamba dhiki kuu imeanza. Litakuwa tukio la ghafla na lenye kutisha sana litakalotokea ulimwenguni pote.

4. (a) Huenda mataifa yakasema nini ili kutetea au kuhalalisha shambulizi lao dhidi ya dini ya uwongo? (b) Inaelekea washiriki wa dini hizo watafanya nini?

4 Hatujui ni sababu zipi zitakazotolewa na mataifa ili kutetea au kuhalalisha shambulizi lao dhidi ya Babiloni Mkubwa. Huenda yakasema kwamba dini za ulimwengu zinazuia amani na kwamba sikuzote zinajiingiza katika mambo ya kisiasa. Au huenda yakasema kwamba mashirika ya kidini yamejikusanyia utajiri na mali nyingi sana. (Ufu. 18:3, 7) Inapatana na akili kwamba shambulizi hilo halimaanishi kwamba washiriki wote wa dini hizo wataangamizwa. Badala yake, inaelekea kwamba mataifa yatafutilia mbali mashirika ya kidini. Baada ya mashirika hayo kuondolewa, washiriki wa dini hizo watatambua kwamba viongozi wao wa kidini waliwadanganya na inaelekea kwamba watajaribu kujitenga kabisa na dini hizo.

5. Yehova ameahidi nini kuhusu dhiki kuu, na kwa nini?

5 Biblia haisemi kuhusu kipindi cha wakati kitakachohusika kumwangamiza Babiloni Mkubwa, lakini tunajua kwamba haitachukua muda mrefu sana. (Ufu. 18:10, 21) Yehova ameahidi kwamba ‘atazifupisha siku hizo’ za dhiki ili wale “waliochaguliwa” waokolewe na dini ya kweli isiangamizwe. (Marko 13:19, 20) Lakini Yehova anatarajia tufanye nini wakati dhiki kuu itakapoanza hadi wakati Har–Magedoni itakapofika?

ENDELEA KUTETEA IBADA SAFI YA YEHOVA

6. Ni jambo gani lingine ambalo ni lazima tufanye ili tujitenge kabisa na dini ya uwongo?

6 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, Yehova anatarajia waabudu wake wajitenge kabisa na Babiloni Mkubwa. Hata hivyo, kufanya hivyo kunahusisha mengi zaidi ya kuacha tu kushirikiana na dini ya uwongo. Ni lazima tuazimie kutetea dini ya kweli, yaani, ibada safi ya Yehova. Fikiria njia mbili zitakazotusaidia kufanya hivyo.

Tusiache kamwe kukutanika pamoja, hata katika nyakati ngumu (Tazama fungu la 7) *

7. (a) Tunaweza kudumishaje msimamo thabiti inapohusu viwango vya uadilifu vya Yehova vya maadili? (b) Andiko la Waebrania 10:24, 25 linakaziaje umuhimu wa kukutanika pamoja, na hasa nyakati zetu?

7 Kwanza, ni lazima tudumishe msimamo thabiti inapohusu viwango vya uadilifu vya Yehova vya maadili. Hatupaswi kamwe kukubali kanuni na viwango vya ulimwengu huu. Kwa mfano, hatuungi mkono upotovu wa maadili kingono wa aina yoyote, kutia ndani ndoa kati ya watu wa jinsia moja na tabia au njia ya maisha ya watu wanaofanya ngono na watu wa jinsia yao. (Mt. 19:4, 5; Rom. 1:26, 27) Pili, ni lazima tuendelee kushirikiana katika ibada na Wakristo wenzetu. Tunafanya hivyo mahali popote, iwe ni katika Majumba yetu ya Ufalme, au hali inapolazimu kwenye nyumba za watu binafsi au hata kwenye maeneo ya siri. Hata hali ziweje, hatuwezi kamwe kuacha desturi yetu ya kukutanika pamoja kwa ajili ya ibada. Ukweli ni kwamba, tunapaswa kukutanika pamoja na “kufanya hivyo zaidi kwa kadiri [tunavyoona] siku ile ikikaribia.”—Soma Waebrania 10:24, 25.

8. Huenda ujumbe wetu ukabadilika jinsi gani wakati ujao?

8 Inaelekea kwamba wakati wa dhiki kuu ujumbe tutakaotangaza utabadilika. Kwa sasa, tunahubiri habari njema ya Ufalme na tunajitahidi sana kufanya wanafunzi. Lakini wakati huo utakapofika, huenda tutatangaza ujumbe mzito kama mvua ya mawe. (Ufu. 16:21) Huenda tutatangaza kwamba ulimwengu wa Shetani umekaribia mwisho wake. Kwa wakati mwafaka, tutajua kikamili ujumbe tutakaotangaza na jinsi tutakavyouwasilisha. Je, tutatumia mbinu zilezile ambazo tumekuwa tukitumia kwa zaidi ya miaka mia moja ili kutimiza huduma yetu? Au tutatumia mbinu nyingine tofauti? Itabidi tusubiri ili tuone. Vyovyote vile, inaelekea kwamba tutakuwa na pendeleo la kutangaza kwa ujasiri ujumbe wa hukumu ya Yehova!—Eze. 2:3-5.

9. Huenda mataifa yataitikiaje ujumbe wetu, lakini tunaweza kuwa na uhakika gani?

9 Kuna uwezekano mkubwa kwamba ujumbe wetu utayachochea mataifa yajaribu kutunyamazisha milele. Kama tu ambavyo leo sisi humtegemea Yehova katika huduma yetu, ndivyo pia tutakavyohitaji utegemezo wake wakati huo. Tuna hakika kwamba Mungu wetu atatujaza nguvu ili tutimize mapenzi yake.—Mika 3:8.

JITAYARISHE KWA AJILI YA SHAMBULIZI DHIDI YA WATU WA MUNGU

10. Kama ilivyotabiriwa kwenye Luka 21:25-28, matukio ya wakati wa dhiki kuu yatawafanya watu wengi wahisije?

10 Soma Luka 21:25-28. Wakati wa dhiki kuu, watu watashtuka kuona jinsi ambavyo mambo yote waliyofikiri kwamba yangedumu milele, yanaanza kuporomoka. Watakuwa na “maumivu makali,” wakihofia sana maisha yao wakati wa kipindi hicho chenye giza zaidi katika historia ya wanadamu. (Sef. 1:14, 15) Wakati huo, inawezekana kwamba maisha yatakuwa magumu sana hata kwa watu wa Yehova. Kwa sababu sisi si sehemu ya ulimwengu, huenda tutapatwa na hali fulani ngumu. Huenda tutalazimika kuishi bila mahitaji fulani muhimu.

11. (a) Kwa nini mataifa yataelekeza fikira zao zote kwa Mashahidi wa Yehova? (b) Kwa nini hatuhitaji kuogopa dhiki kuu?

11 Katika kipindi cha dhiki kuu, utafika wakati ambapo huenda watu ambao dini zao ziliharibiwa watakasirika sana watakapowaona Mashahidi wa Yehova wakiendelea na ibada yao. Tunaweza kuwazia jinsi watu hao watakavyozungumzia jambo hilo kwa hasira, hata kwenye mitandao ya kijamii. Mataifa pamoja na mtawala wao, Shetani, yatatuchukia kwa sababu tutakuwa dini pekee ambayo haikuangamizwa. Mataifa hayatakuwa yametimiza lengo lao la kukomesha dini zote katika uso wa dunia. Hivyo, yataelekeza fikira zao zote kwetu. Siku hizo, mataifa hayo yatatenda yakiwa Gogu wa Magogu. * Yataungana pamoja ili kuwashambulia vikali watu wa Yehova. (Eze. 38:2, 14-16) Ni rahisi kuanza kuingiwa na wasiwasi kwa sababu hatujui kikamili hali zote zitakazokuwepo wakati huo. Hata hivyo, tuna uhakika kuhusu jambo hili: Hatuhitaji kuogopa dhiki kuu. Yehova atatupatia miongozo itakayotuokoa. (Zab. 34:19) ‘Tutasimama wima na kuinua vichwa vyetu’ kwa sababu tutajua kwamba ‘ukombozi wetu unakaribia.’ *

12. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amekuwa akitutayarisha jinsi gani kwa ajili ya mambo yatakayotokea wakati ujao?

12 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amekuwa akitutayarisha ili tuendelee kuwa waaminifu wakati wa kipindi chote cha dhiki kuu. (Mt. 24:45) Amefanya hivyo katika njia nyingi, lakini fikiria mfano mmoja: programu za makusanyiko ya eneo ya mwaka wa 2016 hadi 2018 zilizoandaliwa kwa wakati mwafaka. Kupitia programu hizo, tumetiwa moyo tuimarishe sifa tunazohitaji kuwa nazo kadiri siku ya Yehova inavyozidi kukaribia. Acheni tupitie kifupi sifa hizo.

ENDELEA KUIMARISHA USHIKAMANIFU, UVUMILIVU, NA UJASIRI WAKO

Jitayarishe sasa kuokoka “dhiki kuu” (Tazama fungu la 13-16) *

13. Tunaweza kuimarishaje ushikamanifu wetu kwa Yehova, na kwa nini ni lazima tufanye hivyo sasa?

13 Ushikamanifu: Kichwa cha kusanyiko la eneo la mwaka wa 2016 kilikuwa “Dumisha Ushikamanifu kwa Yehova!” Programu hiyo ilitufundisha kwamba ikiwa tuna uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova, tutakuwa washikamanifu kwake. Tulikumbushwa kwamba tunaweza kumkaribia Yehova kupitia sala za kutoka moyoni na kujifunza kwa bidii Neno lake. Tunapofanya hivyo, tunaimarishwa ili tuweze kushinda hata matatizo makubwa zaidi maishani. Kadiri mfumo wa Shetani unavyokaribia mwisho wake, tunatarajia kwamba tutakabili majaribu makali hata zaidi ya ushikamanifu wetu kwa Mungu na Ufalme wake. Inaelekea kwamba watu wataendelea kutudhihaki. (2 Pet. 3:3, 4) Na dhihaka hizo huenda zikaongezeka, hasa kadiri msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote utakavyozidi kujaribiwa. Ni lazima tuimarishe ushikamanifu wetu sasa ili tuendelee kuwa washikamanifu wakati wa dhiki kuu.

14. (a) Kutakuwa na mabadiliko gani kuhusu ndugu wanaoongoza walio duniani? (b) Kwa nini tutahitaji kuwa washikamanifu wakati huo?

14 Wakati wa dhiki kuu, kutakuwa na mabadiliko yatakayowahusu ndugu wanaoongoza walio duniani. Wakati utafika, ambapo watiwa-mafuta wote ambao bado wako duniani watakusanywa kwenda mbinguni ili washiriki katika vita vya Har–Magedoni. (Mt. 24:31; Ufu. 2:26, 27) Hilo linamaanisha kwamba Baraza Linaloongoza halitakuwa pamoja nasi hapa duniani. Hata hivyo, umati mkubwa utaendelea kuwa chini ya utaratibu fulani wa usimamizi. Ndugu wanaostahili ambao ni miongoni mwa kondoo wengine wataongoza mambo. Tutahitaji kuonyesha ushikamanifu kwa kuwaunga mkono ndugu hao na kwa kufuata miongozo kutoka kwa Mungu watakayotupatia. Wokovu wetu utategemea kufuata mwongozo wao!

15. Tunaweza kuimarishaje uvumilivu wetu, na kwa nini ni muhimu tufanye hivyo sasa?

15 Uvumilivu: Kichwa cha programu ya kusanyiko la eneo la mwaka wa 2017 kilikuwa “Usife Moyo!” Programu hiyo ilitusaidia kuimarisha uwezo wetu wa kuvumilia majaribu. Tulijifunza kwamba uvumilivu wetu hautegemei tu hali zinazofaa. Tunaweza kuimarisha uvumilivu wetu kwa kumtegemea Yehova. (Rom. 12:12) Tusisahau kamwe ahadi hii ya Yesu: “Yule anayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mt. 24:13, maelezo ya chini) Ahadi hiyo inamaanisha kwamba ni lazima tuendelee kuwa waaminifu licha ya changamoto zozote tunazokabili. Tunapovumilia majaribu yote sasa, tutakuwa na imani yenye nguvu zaidi kabla ya dhiki kuu kuanza.

16. Ni nini hasa kinachotufanya tuwe jasiri, na tunaweza kuimarishaje ujasiri wetu sasa?

16 Ujasiri: Kichwa cha programu ya kusanyiko la eneo la mwaka wa 2018 kilikuwa “Uwe Jasiri!” Programu hiyo ilitukumbusha kwamba kuwa jasiri hakutegemei uwezo tulio nao. Kama ilivyo na sifa ya uvumilivu, tunapata ujasiri wa kweli kwa kumtegemea Yehova. Tunaweza kufanya nini ili tumtegemee Yehova zaidi? Tunapaswa kusoma Neno lake kila siku na kutafakari kuhusu jinsi Yehova alivyowaokoa watu wake nyakati zilizopita. (Zab. 68:20; 2 Pet. 2:9) Mataifa yatakapotushambulia wakati wa dhiki kuu, tutahitaji kuwa jasiri na kumtumaini Yehova zaidi kuliko wakati mwingine wowote. (Zab. 112:7, 8; Ebr. 13:6) Ikiwa tutamtegemea Yehova sasa, tutakuwa na ujasiri unaohitajika ili kukabiliana na shambulizi la Gogu. *

TAZAMIA KWA HAMU WOKOVU WAKO

Hivi karibuni, Yesu pamoja na jeshi lake la mbinguni watawaangamiza maadui wa Mungu kwenye vita vya Har-Magedoni! (Tazama fungu la 17)

17. Kwa nini hatuna sababu ya kuogopa Har–Magedoni? (Tazama picha kwenye jalada.)

17 Kama tulivyoona katika makala iliyopita, wengi wetu tumezaliwa na kuishi maisha yetu yote katika siku za mwisho. Lakini pia tunatazamia kuokoka dhiki kuu. Vita vya Har–Magedoni ndivyo vitakavyokomesha kabisa mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, hatuna sababu ya kuogopa chochote. Kwa nini? Kwa sababu vita hivyo ni vya Mungu. (Met. 1:33; Eze. 38:18-20; Zek. 14:3) Kwa amri ya Yehova, Yesu Kristo ataliongoza jeshi la Yehova katika vita hivyo. Atashirikiana na watiwa-mafuta waliofufuliwa na pia makumi ya maelfu ya malaika. Wote kwa pamoja, watapigana vita dhidi ya Shetani, roho wake waovu, na majeshi yake yaliyo duniani.—Dan. 12:1; Ufu. 6:2; 17:14.

18. (a) Yehova ametuhakikishia nini? (b) Andiko la Ufunuo 7:9, 13-17 linakusaidiaje uwe na uhakika mwingi kuhusu wakati ujao?

18 Yehova ametuhakikishia hivi: “Hakuna silaha yoyote itakayotokezwa dhidi yako itakayofanikiwa.” (Isa. 54:17) “Umati mkubwa” wa waabudu waaminifu wa Yehova ‘watatoka katika ile dhiki kuu’ wakiwa hai! Kisha wataendelea kumtolea Yehova utumishi mtakatifu. (Soma Ufunuo 7:9, 13-17.) Kwa kweli, Biblia inatupatia uhakika mwingi sana kuhusu wakati wetu ujao! Tunajua kwamba “Yehova huwalinda waaminifu.” (Zab. 31:23) Wale wote wanaompenda na kumsifu Yehova watashangilia kumwona akilitetea jina lake takatifu.—Eze. 38:23.

19. Tunatazamia mambo gani mazuri hivi karibuni?

19 Fikiria jinsi maneno ya andiko la 2 Timotheo 3:2-5, yanavyoweza kusomeka ikiwa yangekuwa yanazungumzia watu katika ulimwengu mpya usio chini ya nguvu za Shetani. (Tazama sanduku “ Jinsi Watu Watakavyokuwa Wakati Huo.”) Ndugu George Gangas, * aliyekuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema hivi kuhusu jambo hilo: “Utakuwa ulimwengu mzuri ajabu wakati ambapo watu wote watakuwa ndugu au dada! Hivi karibuni, utapata pendeleo la kuishi katika mfumo mpya wa mambo. Utaishi sikuzote ambazo Yehova anaishi. Tutaishi milele.” Hilo ni tumaini zuri kwelikweli!

WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!

^ fu. 5 Tunajua kwamba hivi karibuni “dhiki kuu” itawakumba wanadamu. Hali itakuwaje kwa watumishi wa Yehova? Yehova anatarajia tufanye nini wakati huo? Ni sifa gani tunazohitaji kuimarisha sasa ili tuendelee kuwa waaminifu wakati huo? Tutajifunza mambo hayo katika makala hii.

^ fu. 3 UFAFANUZI WA MANENO: Dini zinazodai kuwa za Kikristo ni dini zinazosema kwamba zinamfuata Kristo lakini hazimwabudu Yehova kulingana na viwango vyake.

^ fu. 11 UFAFANUZI WA MANENO: Maneno Gogu wa Magogu (au kwa kifupi, Gogu) yanarejelea muungano wa mataifa yatakayoshambulia ibada safi wakati wa dhiki kuu.

^ fu. 11 Ili upate ufafanuzi zaidi kuhusu matukio yote yatakayotangulia vita vya Har–Magedoni, tazama sura ya 21 ya kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala! Kwa habari zaidi kuhusu shambulizi la Gogu wa Magogu na jinsi Yehova atakavyowalinda watu wake wakati wa Har–Magedoni, tazama sura ya 17 na ya 18 ya kitabu Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!

^ fu. 16 Programu ya kusanyiko la eneo la mwaka wa 2019 lenye kichwa “Upendo Haushindwi Kamwe!” inatuhakikishia kwamba tunaweza kuendelea kuwa salama sikuzote chini ya ulinzi wa Yehova wenye upendo.—1 Kor. 13:8.

^ fu. 19 Tazama makala “Matendo Yake Yamfuata” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1994.

^ fu. 65 MAELEZO YA PICHA: Wakati wa dhiki kuu, kikundi kidogo cha Mashahidi wanaonyesha ujasiri kwa kukutanika pamoja msituni kwa ajili ya mkutano wa kutaniko.

^ fu. 67 MAELEZO YA PICHA: Umati mkubwa wa waabudu waaminifu wa Yehova watatoka katika dhiki kuu wakiwa hai na wenye furaha!