Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu wanahitaji kusikia onyo kadiri “dhoruba” ya Mungu inavyozidi kukaribia!

Hukumu za Mungu​—Je, Sikuzote Anatoa Onyo Mapema vya Kutosha?

Hukumu za Mungu​—Je, Sikuzote Anatoa Onyo Mapema vya Kutosha?

MTABIRI wa hali ya hewa anachunguza rada inayoonyesha mabadiliko ya hali ya hewa. Anaona dhoruba kali ikikaribia haraka kwenye eneo lenye watu wengi. Kwa sababu anajali usalama wa watu, anawaonya bila kuchoka kabla haijawa kuchelewa mno.

Vivyo hivyo, Yehova anawaonya wakaaji wa dunia kuhusu “dhoruba” ambayo ni hatari zaidi kuliko dhoruba yoyote ambayo imewahi kutabiriwa. Anafanyaje hivyo? Na kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba anawapa watu wakati wa kutosha ili wachukue hatua? Ili tupate majibu, acheni kwanza tuchunguze maonyo fulani ambayo Yehova alitoa zamani.

MUNGU ALIPOTOA MAONYO KIMBELE

Katika nyakati za Biblia, Yehova alitoa maonyo kuhusu “dhoruba,” au matendo ya hukumu ambayo angeleta dhidi ya wale waliokosa kutii amri zake kimakusudi. (Met. 10:25; Yer. 30:23) Katika kila kisa, aliwajulisha mapema vya kutosha watu ambao wangepatwa na hukumu zake na kuwaagiza wafanye mabadiliko yaliyopatana na mapenzi yake. (2 Fal. 17:12-15; Neh. 9:29, 30) Ili kuwachochea wafanye mabadiliko yaliyohitajika, mara nyingi alitumia watumishi wake washikamanifu duniani ili kutangaza hukumu zake na kuwasaidia wachukue hatua bila kukawia.—Amo. 3:7.

Mfano mmoja wa watumishi hao waaminifu ni Noa. Kwa miaka mingi, Noa aliwaonya kwa ujasiri watu wa siku zake waliopotoka kimaadili na wakatili, kuhusu Gharika ambayo ingekuja ulimwenguni pote. (Mwa. 6:9-13, 17) Pia, aliwaambia kwa bidii mambo waliyohitaji kufanya ili waokolewe—hivi kwamba akaja kujulikana kuwa “mhubiri wa uadilifu.”—2 Pet. 2:5.

Licha ya jitihada za Noa, watu walioishi katika ulimwengu huo wa kabla ya Gharika walipuuza ujumbe wake kutoka kwa Mungu. Walionyesha ukosefu mkubwa wa imani. Na kwa sababu hiyo, walikufa Gharika ‘ilipokuja na kuwafagilia mbali wote.’ (Mt. 24:39; Ebr. 11:7) Walipokuwa wakiangamia hawangeweza kudai kwamba Mungu hakuwaonya.

Nyakati nyingine, Yehova aliwaonya watu muda mfupi kabla ya “dhoruba” ya hukumu yake kuanza. Ingawa hivyo, alihakikisha kwamba amewapa watu muda wa kutosha wa kufanya mabadiliko. Kwa mfano, alitoa maonyo mapema vya kutosha wakati wa yale Mapigo Kumi yaliyoikumba Misri ya kale. Mfano mmoja ni wakati ambapo Yehova alimtuma Musa na Haruni wakamwonye Farao na watumishi wake kuhusu pigo la saba, yaani, mvua ya mawe ambayo ingeleta uharibifu mkubwa. Kwa kuwa mvua hiyo ya mawe ingeanza siku iliyofuata, je, Mungu alikuwa amewapa wakati wa kutosha wa kutafuta mahali pa kujikinga na hivyo kuwa salama? Biblia inaeleza hivi: “Mtumishi yeyote wa Farao aliyeogopa neno la Yehova aliwaingiza haraka watumishi wake na mifugo yake ndani ya nyumba, lakini yeyote ambaye hakuzingatia moyoni mwake neno la Yehova aliwaacha watumishi wake na mifugo yake shambani.” (Kut. 9:18-21) Ni wazi kwamba Yehova alitoa onyo mapema vya kutosha, na hivyo wale waliochukua hatua haraka hawakupatwa na madhara makubwa ya pigo hilo.

Vilevile, Yehova aliwaonya Farao na watumishi wake kabla ya kuleta pigo la kumi. Hata hivyo, walipuuza kipumbavu onyo hilo. (Kut. 4:22, 23) Matokeo ni kwamba walijionea wana wao wazaliwa wa kwanza wakifa. Lilikuwa jambo lenye kusikitisha sana! (Kut. 11:4-10; 12:29) Je, walikuwa na muda wa kutosha wa kutii onyo walilopewa? Ndiyo! Bila kukawia, Musa aliwaonya Waisraeli kuhusu pigo la kumi ambalo Yehova angeleta na akawapa maagizo kuhusu jinsi ambavyo wangeokoa familia zao. (Kut. 12:21-28) Ni watu wangapi waliotii onyo hilo? Kulingana na makadirio fulani, zaidi ya watu milioni tatu, kutia ndani Waisraeli na “kundi kubwa lenye mchanganyiko wa watu” ambao hawakuwa Waisraeli, na pia Wamisri, waliokoka hukumu ya Mungu na kuondoka Misri.—Kut. 12:38; maelezo ya chini.

Kama mifano hiyo inavyoonyesha, sikuzote Yehova alihakikisha kwamba watu walikuwa na muda wa kutosha wa kutii maonyo yake. (Kum. 32:4) Kwa nini Mungu alifanya hivyo? Mtume Petro alieleza kwamba Yehova “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9) Naam, Yehova aliwajali watu. Alitaka watu watubu na kufanya mabadiliko yaliyohitajika kabla ya kuleta hukumu yake.—Isa. 48:17, 18; Rom. 2:4.

KUTII MAONYO YA MUNGU LEO

Leo pia, ni lazima watu wote watii onyo muhimu linaloendelea kutolewa duniani kote. Alipokuwa duniani, Yesu alionya kwamba hatimaye mfumo huu wa mambo utaangamizwa wakati wa “dhiki kuu.” (Mt. 24:21) Akieleza kuhusu hukumu hiyo ambayo ingekuja wakati ujao, Yesu alitoa unabii unaotaja mambo hususa ambayo wafuasi wake wangetarajia kuona na kukabili kadiri muda huo ulivyokaribia. Hivyo, Yesu alieleza kuhusu matukio makubwa muhimu tunayoona yakitendeka leo duniani kote.—Mt. 24:3-12; Luka 21:10-13.

Sambamba na unabii huo, leo Yehova anawahimiza watu wote wajitiishe chini ya utawala Wake wenye upendo. Anatamani watu watiifu wafurahie maisha mazuri sasa na pia baraka zitakazokuwepo wakati ujao kwenye ulimwengu wake mpya wenye uadilifu. (2 Pet. 3:13) Ili kuwatia moyo watu wasitawishe imani katika ahadi zake, Yehova ameandaa ujumbe wenye kuokoa uhai, yaani, “habari njema ya Ufalme,” ambayo Yesu alitabiri kwamba “itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Mungu amewapanga kitengenezo waabudu wake wa kweli ili watoe “ushahidi,” au wahubiri ujumbe huo kutoka kwa Mungu katika nchi 240 hivi. Yehova anataka watu wengi kadiri iwezekanavyo watii onyo hilo na kuokoka “dhoruba” ya hukumu yake ya uadilifu inayokuja.—Sef. 1:14, 15; 2:2, 3.

Hivyo basi, swali tunalopaswa kujiuliza si ikiwa Yehova anawapatia watu muda wa kutosha ili kutii maonyo yake, kwani uthibitisho unaonyesha kwamba sikuzote yeye hufanya hivyo. Badala yake, swali tunalopaswa kujiuliza ni: Je, watu watatii onyo la Mungu kabla haijawa kuchelewa mno? Tukiwa wajumbe wa Mungu, acheni tuendelee kuwasaidia watu wengi kadiri iwezekanavyo waokoke mwisho wa mfumo huu wa mambo.