Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 43

Mwabudu Yehova Peke Yake

Mwabudu Yehova Peke Yake

“Yehova ni Mungu anayetaka watu wamwabudu yeye peke yake.”—NAH. 1:2.

WIMBO 51 Tumejiweka Wakfu kwa Mungu!

MUHTASARI *

1. Kwa nini Yehova peke yake ndiye anayestahili kuabudiwa?

YEHOVA peke yake ndiye anayestahili kuabudiwa kwa sababu yeye ni Muumba na Mpaji-Uhai wetu. (Ufu. 4:11) Hata hivyo, tunakabili changamoto fulani. Ingawa tunampenda na kumheshimu Yehova, huenda mambo mengine maishani yakatuzuia kumpenda na kumwabudu Yehova peke yake kama anavyostahili. Tunahitaji kuelewa jinsi jambo hilo linavyoweza kutukia. Lakini kwanza, acheni tuchunguze kinachomaanishwa na kumwabudu Yehova peke yake.

2. Kulingana na Kutoka 34:14, tutafanya nini ikiwa tumejitoa kwa Yehova peke yake?

2 Katika Biblia, kujitoa kabisa kwa Mungu kunaonyesha kwamba tuna upendo wenye nguvu kumwelekea. Ikiwa tumejitoa kwa Yehova peke yake, ni yeye peke yake tutakayemwabudu. Hatutamruhusu yeyote au kitu chochote kichukue mahali pake moyoni mwetu.—Soma Kutoka 34:14.

3. Kwa nini tuna sababu nzuri za kujitoa kwa Yehova?

3 Tuna sababu nzuri za kujitoa kwa Yehova. Kwa nini tunasema hivyo? Kwa sababu tumejifunza mambo mengi kumhusu. Tunavutiwa na sifa zake maridadi. Tunajua mambo ambayo Yehova anapenda na kuchukia, na tunahisi kama anavyohisi kuyahusu. Tunaelewa na tunaunga mkono kusudi lake kutuelekea. Tunaliona kuwa pendeleo kubwa kwamba anatupatia fursa ya kuwa rafiki zake. (Zab. 25:14) Kila jambo tunalojifunza kumhusu Muumba wetu linatufanya tumkaribie zaidi na zaidi.—Yak. 4:8.

4. (a) Ibilisi hutumia nini ili kudhoofisha upendo wetu kwa Yehova? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Ibilisi ndiye anayeuongoza mfumo huu wa mambo, naye huutumia kupotosha tamaa zetu za asili tukiwa wanadamu na kufanya iwe vigumu kwetu kupinga tamaa za mwili zisizofaa. (Efe. 2:1-3; 1 Yoh. 5:19) Lengo lake ni kuugawanya upendo wetu ili tusimwabudu Yehova peke yake. Acheni tuchunguze njia mbili anazotumia kufanya hivyo. Kwanza, anatushawishi tufuatie utajiri, na pili, anajaribu kutushawishi tufanye uchaguzi usiofaa inapohusu burudani.

JIHADHARI NA MTEGO WA KUPENDA PESA

5. Kwa nini ni lazima tujihadhari ili tusisitawishe tamaa ya kupenda pesa?

5 Kiasili, tunapenda kuwa na chakula cha kutosha, nguo nzuri za kuvaa, na mahali pazuri pa kuishi. Hata hivyo, ni lazima tujihadhari ili tusisitawishe tamaa ya kupenda pesa. Watu wengi katika ulimwengu wa Shetani ‘wanapenda pesa’ na vitu vinavyoweza kununuliwa na pesa. (2 Tim. 3:2) Yesu alijua kwamba wafuasi wake wanaweza kushawishiwa kusitawisha upendo huo. Alisema hivi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” (Mt. 6:24) Mtu anayemwabudu Yehova na wakati uleule anatumia wakati na jitihada nyingi sana akijaribu kutafuta utajiri katika ulimwengu huu, kwa njia fulani, ni kama anajaribu kutumikia mabwana wawili. Kwa kufanya hivyo, hangekuwa akijitoa ili kumwabudu Yehova peke yake.

6. Tunajifunza somo gani kutokana na maneno ya Yesu kwa kutaniko la Laodikia?

6 Karibu na mwisho wa karne ya kwanza W.K., washiriki wa kutaniko katika jiji la Laodikia walijigamba hivi: “Mimi ni tajiri, nimejipatia utajiri na sihitaji kitu chochote.” Lakini machoni pa Yehova na Yesu, walikuwa ‘wenye taabu na wa kusikitikiwa na maskini na vipofu na uchi.’ Yesu aliwashauri, si kwa sababu walikuwa matajiri, lakini kwa sababu kupenda kwao utajiri kulikuwa kukiharibu uhusiano wao pamoja na Yehova. (Ufu. 3:14-17) Tukigundua kwamba tamaa ya kufuatia utajiri inasitawi moyoni mwetu, ni lazima tuchukue hatua haraka ili kurekebisha njia yetu ya kufikiri. (1 Tim. 6:7, 8) Tusipofanya hivyo, moyo wetu utagawanyika na Yehova hatakubali ibada yetu. Anataka “watu wamwabudu yeye peke yake.” (Kum. 4:24) Lakini mtu anaweza kupotezaje usawaziko inapohusu mtazamo wake kuhusu pesa?

Jinsi Walaodikia fulani walivyojiona . . . na jinsi Yehova na Yesu walivyowaona (Tazama fungu la 6)

7-9. Umejifunza nini kutokana na kisa cha mzee wa kutaniko anayeitwa David?

7 Mfikirie David, mzee wa kutaniko mwenye bidii anayeishi Marekani. Anasema kwamba alikuwa mfanyakazi mwenye bidii sana. Alipandishwa cheo katika kampuni aliyofanyia kazi na hata alitambuliwa kitaifa kwa ubora wa kazi yake. David anaeleza hivi: “Wakati huo, nilifikiri kwamba mambo hayo niliyotunukiwa yalikuwa uthibitisho wa kwamba Yehova alikuwa akinibariki.” Lakini je, kweli mafanikio yake yalitoka kwa Yehova?

8 David alianza kuona dalili zilizoonyesha kwamba kazi yake ilikuwa ikiathiri urafiki wake pamoja na Yehova. Anasema hivi: “Nilipokuwa kutanikoni na katika huduma, nilijikuta nikifikiria kuhusu matatizo kazini. Nilikuwa nikipata pesa nyingi, lakini nilizidi kuwa na mkazo mwingi na uhusiano wangu pamoja na mke wangu ukaanza kuathiriwa.”

9 David alitambua kwamba alihitaji kuchunguza upya mambo aliyotanguliza. Anaeleza hivi: “Nilifanya uamuzi thabiti wa kurekebisha hali yangu.” David alitaka kubadili ratiba yake ya kazi, hivyo akamjulisha mwajiri wake kuhusu uamuzi wake. Ikawaje? David alipoteza kazi yake! Akafanyaje? Anasema hivi: “Siku iliyofuata, nilijaza ombi la kutumikia nikiwa painia msaidizi wa kuendelea.” Ili kujiruzuku, David na mke wake walianza kufanya kazi za usafi katika majengo makubwa. Baada ya muda, alianza upainia wa kawaida, na hatimaye mke wake pia akamuunga mkono na kuwa painia wa kawaida. Wenzi hao waliamua kufanya kazi ya kimwili ambayo inaonekana kuwa duni machoni pa wengi. Lakini jambo muhimu zaidi kwao si aina ya kazi ya kimwili wanayofanya. Ingawa kipato chao kimepungua hadi kufikia asilimia 10 ya kipato chao cha awali, kila mwezi wana kiasi cha pesa wanachohitaji ili kutosheleza mahitaji yao. Wanataka kumtanguliza Yehova maishani mwao, na wamejionea moja kwa moja jinsi anavyowatunza wale wanaotanguliza masilahi ya Ufalme.—Mt. 6:31-33.

10. Tunaweza kuulindaje moyo wetu?

10 Iwe tuna vitu vingi au vitu vichache vya kimwili, tunapaswa kuulinda moyo wetu. Jinsi gani? Usisitawishe tamaa ya kupenda utajiri. Na usiruhusu kazi yako ya kimwili iwe jambo kuu zaidi maishani mwako kuliko utumishi wako kwa Yehova. Unaweza kujuaje ikiwa umeathiriwa na mtazamo huo? Unaweza kujiuliza maswali kama haya: ‘Je, mara kwa mara mimi hufikiria kuhusu kazi yangu ya kimwili ninapokuwa mikutanoni au katika huduma? Je, nyakati zote mimi huwa na wasiwasi kwamba huenda sitakuwa na pesa za kutosha kwa ajili ya wakati ujao? Je, pesa na vitu vya kimwili ni chanzo cha matatizo kati yangu na mwenzi wangu wa ndoa? Je, niko tayari kufanya kazi ya kimwili inayodharauliwa na watu ikiwa kazi hiyo itaniruhusu kutumia muda mwingi zaidi kumtumikia Yehova?’ (1 Tim. 6:9-12) Tunapofikiria maswali hayo, acheni tukumbuke kwamba Yehova anatupenda na anawaahidi hivi wale wanaojitoa kwake: “Sitakuacha wala kukutupa kamwe.” Ndiyo sababu mtume Paulo aliandika hivi: “Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa.”—Ebr. 13:5, 6.

CHAGUA BURUDANI YAKO KWA MAKINI

11. Burudani inaweza kumwathirije mtu?

11 Yehova anataka tufurahie maisha, na burudani inaweza kutusaidia kufurahia maisha. Isitoshe, Neno la Mungu linasema “hakuna jambo bora analoweza kufanya mtu kuliko kula na kunywa na kufurahia kazi yake ngumu.” (Mhu. 2:24) Hata hivyo, burudani nyingi zilizopo leo zinaweza kutuletea madhara. Zinafanya viwango vya watu vya maadili vizorote, zikiwachochea waanze kuyakubali au hata kuyapenda mambo ambayo yanakatazwa na Neno la Mungu.

Ni nani anayetayarisha burudani yako? (Tazama fungu la 11-14) *

12. Kulingana na 1 Wakorintho 10:21, 22, kwa nini tunapaswa kuchagua burudani yetu kwa makini?

12 Tunataka kumwabudu Yehova peke yake, kwa hiyo hatupaswi kula kwenye “meza ya Yehova” na wakati uleule kwenye “meza ya roho waovu.” (Soma 1 Wakorintho 10:21, 22.) Kwa kawaida, kula chakula pamoja na mtu ni ishara ya urafiki. Ikiwa tutachagua burudani inayounga mkono ukatili au jeuri, kuwasiliana na roho, upotovu wa maadili kingono, au tamaa na mitazamo mingine ya kimwili, tutakuwa tukila chakula kilichotayarishwa na maadui wa Mungu. Matokeo ni kwamba tutajidhuru sisi wenyewe, na pia tutaharibu urafiki wetu mzuri pamoja na Yehova.

13-14. Kulingana na Yakobo 1:14, 15, kwa nini ni lazima tujihadhari inapohusu burudani tunazochagua? Toa mfano.

13 Fikiria baadhi ya njia hususa ambazo burudani ni kama chakula halisi. Tunapokula tunaweza kuchagua kitu tunachoingiza mdomoni. Lakini mara tu tunapomeza chakula hicho, mfumo wa asili wa umeng’enyaji unaanza kufanya kazi na mwishowe virutubisho vinafyonzwa na kuwa sehemu ya mwili wetu. Chakula chenye lishe kitaboresha afya yetu; chakula kibaya kitadhoofisha afya yetu. Matokeo hayataonekana papo hapo, lakini baada ya muda yataonekana waziwazi.

14 Vivyo hivyo, inapohusu burudani, tunachagua mambo tunayotaka kuingiza akilini. Baada ya hatua hiyo, kiasili burudani tuliyochagua inaanza kufanya kazi katika akili na moyo wetu. Burudani nzuri inaweza kutuburudisha; burudani mbaya itatudhuru. (Soma Yakobo 1:14, 15.) Athari za burudani mbaya huenda zisionekane papo hapo, lakini mwishowe zitaonekana waziwazi. Hiyo ndiyo sababu Biblia inatuonya hivi: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia; kwa sababu yule anayepanda kwa mwili wake atavuna uharibifu kutokana na mwili wake.” (Gal. 6:7, 8) Ni jambo la muhimu sana kwetu kukataa burudani zote zinazoendeleza mambo ambayo Yehova anachukia!—Zab. 97:10.

15. Yehova ametuandalia zawadi gani tunayoweza kufurahia?

15 Mashahidi wengi wa Yehova wanafurahia kutazama JW Broadcasting®, kituo chetu cha televisheni kinachotegemea intaneti. Dada anayeitwa Marilyn alisema hivi: “JW Broadcasting imenisaidia kuwa na mtazamo mzuri, na sihitaji kudhibiti vipindi vinavyopatikana kwa sababu vyote ni vizuri. Ninapojihisi mpweke au nimevunjika moyo, ninatafuta hotuba au programu ya Ibada ya Asubuhi yenye kutia moyo. Jambo hilo linanifanya nijihisi nikiwa karibu na Yehova na tengenezo lake. Programu ya JW Broadcasting imebadili kabisa maisha yangu.” Je, unafaidika na zawadi ya Yehova? Mbali na programu mpya za kila mwezi, JW Broadcasting ina video nyingi na rekodi za sauti na vilevile nyimbo zenye kujenga zinazopatikana wakati wowote.

16-17. Kwa nini ni lazima tudhibiti kiasi cha wakati tunachotumia kwenye burudani, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

16 Ni lazima tuchague kwa makini aina ya burudani tunayofurahia na vilevile kudhibiti kiasi cha wakati tunachotumia kuifurahia. Tusipofanya hivyo, huenda tukatumia muda mwingi zaidi kujiburudisha wenyewe kuliko tunaotumia kumtumikia Yehova. Watu wengi huona kuwa vigumu kudhibiti kiasi cha muda wanachotumia kwenye burudani. Abigail, dada mwenye umri wa miaka 18 anasema hivi: “Kutazama televisheni hunituliza baada ya siku yenye shughuli nyingi. Lakini nisipokuwa mwangalifu huenda nikatumia saa nyingi kutazama televisheni.” Ndugu kijana anayeitwa Samuel anasema hivi: “Mimi hujikuta nikitazama kwa mfululizo video fupi-fupi kwenye intaneti. Ninaanza na video moja na ghafla ninashtuka kwamba saa tatu au nne zimepita nikizitazama.”

17 Unaweza kudhibiti jinsi gani kiasi cha muda unachotumia kwenye burudani? Hatua ya kwanza ni kutambua hasa kiasi cha wakati unachotumia kwenye burudani. Kwa nini usiweke rekodi kwa juma moja, ya muda unaotumia kwenye burudani? Andika kwenye kalenda idadi ya saa unazotumia ukitazama televisheni, ukitumia intaneti, na ukicheza michezo ya kompyuta kwenye vifaa vya mkononi. Ukihisi kwamba unatumia muda mwingi kupita kiasi, jaribu kujiwekea ratiba. Tenga wakati wa kufanya mambo muhimu zaidi kwanza, kisha tenga wakati kwa ajili ya burudani. Halafu, mwombe Yehova akusaidie ushikamane na ratiba yako. Kwa njia hiyo utakuwa na wakati na nguvu unazohitaji kwa ajili ya kujifunza Biblia kibinafsi, ibada ya familia, mikutano ya kutaniko, na kumtumikia Yehova katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. Pia, hutahisi ukiwa na hatia kuhusu wakati unaotumia kwenye burudani.

ENDELEA KUMWABUDU YEHOVA PEKE YAKE

18-19. Tunaweza kuthibitishaje kwamba tunamwabudu Yehova peke yake?

18 Baada ya kuandika kuhusu mwisho wa ulimwengu wa Shetani na kuhusu ulimwengu mpya utakaokuja, mtume Petro alisema hivi: “Kwa hiyo, wapendwa, kwa kuwa mnangojea mambo hayo, fanyeni yote mnayoweza ili mwishowe awapate mkiwa bila doa wala dosari na mkiwa katika amani.” (2 Pet. 3:14) Tunapotii shauri hilo na kufanya yote tunayoweza ili kuendelea kuwa safi kiadili na kiroho, tunathibitisha kwamba tunamwabudu Yehova peke yake.

19 Shetani na ulimwengu wake utaendelea kutushawishi ili tubadili mambo tunayotanguliza maishani. (Luka 4:13) Lakini licha ya changamoto zozote, hatutamruhusu mtu yeyote au kitu chochote kichukue mahali pa Yehova katika mioyo yetu. Tumeazimia kumpa Yehova jambo ambalo ni yeye peke yake anastahili—kumwabudu yeye peke yake!

WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu

^ fu. 5 Tumejitoa ili kumtumikia Yehova. Lakini je, tumejitoa ili kumwabudu yeye peke yake? Maamuzi yetu maishani yanafunua ikiwa tunafanya hivyo. Acheni tuchunguze mambo mawili maishani mwetu yanayofunua ni kwa kadiri gani tumejitoa ili kumwabudu Yehova..

^ fu. 53 MAELEZO YA PICHA: Hatungependa kula chakula kisicho safi na kilichoandaliwa mahali pachafu. Hivyo, hatupaswi pia kutazama burudani iliyochafuliwa na ukatili au jeuri, yenye mambo ya kuwasiliana na roho, au upotovu wa maadili kingono.