Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 40

Uwe na Mengi ya Kufanya Katika Kipindi cha Mwisho cha “Siku za Mwisho”

Uwe na Mengi ya Kufanya Katika Kipindi cha Mwisho cha “Siku za Mwisho”

“Iweni imara, thabiti, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”—1 KOR. 15:58.

WIMBO 58 Kutafuta Marafiki wa Amani

MUHTASARI *

1. Ni nini kinachotusadikisha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho”?

JE, ULIZALIWA baada ya mwaka wa 1914? Ikiwa ndivyo, umekuwa ukiishi kipindi chote cha maisha yako katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. (2 Tim. 3:1) Sisi sote tumejionea matukio ambayo Yesu alitabiri kwamba yangetukia katika kipindi hiki. Matukio hayo yanatia ndani vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, magonjwa, ongezeko la uasi sheria, na mateso dhidi ya watu wa Yehova. (Mt. 24:3, 7-9, 12; Luka 21:10-12) Pia, tumejionea watu wakitenda kama mtume Paulo alivyotabiri. (Tazama sanduku “ Jinsi Watu Walivyo Leo.”) Tukiwa waabudu wa Yehova, tunasadiki kwamba tunaishi “katika kipindi cha mwisho cha zile siku.”—Mik. 4:1, maelezo ya chini.

2. Tunahitaji kupata majibu ya maswali gani?

2 Kwa sababu muda mrefu sana umepita tangu mwaka wa 1914, hapana shaka kwamba sasa tunaishi katika kipindi cha mwisho cha “siku za mwisho.” Kwa kuwa mwisho uko karibu sana, tunahitaji kupata majibu ya maswali fulani muhimu: Ni matukio gani yatakayotendeka mwishoni kabisa mwa “siku za mwisho”? Na Yehova anatarajia tufanye nini tunaposubiri matukio hayo?

NI NINI KITAKACHOTOKEA MWISHONI KABISA MWA “SIKU ZA MWISHO”?

3. Kulingana na unabii wa 1 Wathesalonike 5:1-3, mataifa yatatangaza nini?

3 Soma 1 Wathesalonike 5:1-3. Paulo anataja kuhusu “siku ya Yehova.” Katika andiko hili, siku ya Yehova inarejelea kipindi cha wakati kitakachoanza na shambulizi dhidi ya “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo, na ambacho kitaisha wakati wa Har–Magedoni. (Ufu. 16:14, 16; 17:5) Muda mfupi kabla ya siku hiyo kuanza, mataifa yatakuwa yakisema “Amani na Usalama!” Nyakati nyingine, viongozi wa ulimwengu wanatumia maneno kama hayo wanapozungumzia kuhusu kuimarisha uhusiano kati ya mataifa mbalimbali. * Hata hivyo, tangazo la “amani na usalama” linalotajwa na Biblia litakuwa tofauti. Kwa nini? Tangazo hilo litakapotolewa, watu wengi watafikiri kwamba viongozi wa ulimwengu wamefanikiwa kuufanya ulimwengu kuwa mahali salama zaidi pa kuishi. Lakini ukweli wa mambo ni kwamba “uharibifu wa ghafla” utatokea kwa sababu “dhiki kuu” itaanza.—Mt. 24:21.

Usipumbazwe na tangazo la “amani na usalama” litakalotolewa na viongozi wa ulimwengu (Tazama fungu la 3 hadi 6) *

4. (a) Ni mambo gani tusiyoyajua kuhusu tangazo la “amani na usalama”? (b) Tayari tunajua nini kuhusu tangazo hilo?

4 Tunajua mambo fulani kuhusu tangazo la “amani na usalama.” Lakini kuna mambo tusiyoyajua. Hatujui ni mambo gani yatakayosababisha tangazo hilo litolewe au jinsi litakavyotolewa. Na hatujui ikiwa litakuwa tangazo moja tu au mfululizo wa matangazo kadhaa ya amani na usalama. Vyovyote itakavyokuwa, tunajua jambo hili: Hatupaswi kupumbazwa kufikiri kwamba viongozi wa ulimwengu wanaweza kufanikiwa kuleta amani duniani. Badala yake, tangazo hilo ndilo ambalo Biblia inatuambia tulitarajie. Itakuwa ishara ya kwamba “siku ya Yehova” imekaribia kuanza!

5. Andiko la 1 Wathesalonike 5:4-6 linatusaidiaje kuwa tayari kwa ajili ya “siku ya Yehova”?

5 Soma 1 Wathesalonike 5:4-6. Himizo la Paulo linatusaidia kufahamu mambo tunayopaswa kufanya ili kuhakikisha kwamba tuko tayari kwa ajili ya “siku ya Yehova.” Hatupaswi “kulala usingizi kama wengine wanavyofanya.” Ni lazima “tukae macho” na kuendelea kuwa chonjo. Kwa mfano, tunapaswa kuwa chonjo ili tusijiingize katika hatari ya kulegeza msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote kwenye masuala ya kisiasa ya ulimwengu huu. Ikiwa tutajihusisha na mambo hayo, tutakuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 15:19) Tunajua kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la amani duniani.

6. Tungependa kuwasaidia watu kufanya nini, na kwa nini?

6 Mbali na sisi wenyewe kuendelea kuwa macho, tungependa pia kuwasaidia wengine wawe macho kwa kuwafundisha mambo ambayo Biblia ilitabiri kwamba yangetukia ulimwenguni. Tukumbuke kwamba mara tu dhiki kuu itakapoanza, itakuwa kuchelewa mno kwa watu kuanza kumtumikia Yehova. Hiyo ndiyo sababu kazi yetu inapaswa kufanywa kwa uharaka sana! *

UWE NA MENGI YA KUFANYA KATIKA KAZI YA KUHUBIRI

Leo tunapohubiri, tunawaonyesha watu kwamba Ufalme wa Mungu pekee ndio unaoweza kuleta amani na usalama wa kweli duniani (Tazama fungu la 7 hadi 9)

7. Yehova anatarajia tufanye nini leo?

7 Katika kipindi kifupi cha wakati kilichobaki kabla ya “siku” yake kuanza, Yehova anatarajia tuwe na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri. Tunapaswa kuhakikisha kwamba tuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58) Yesu alitabiri mambo ambayo tungefanya. Alipokuwa akizungumza kuhusu mambo yote muhimu ambayo yangetokea katika siku za mwisho, alisema hivi: “Pia, katika mataifa yote, lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:4, 8, 10; Mt. 24:14) Fikiria hili: Kila mara unapoenda katika huduma, unashiriki kutimiza unabii huo wa Biblia!

8. Tunajuaje kwamba kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme inaendelea kufanikiwa?

8 Kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme imefanikiwa jinsi gani? Mwaka baada ya mwaka, kazi hii inazidi kusonga mbele. Kwa mfano, fikiria kuhusu ongezeko la wahubiri wa Ufalme ulimwenguni pote katika siku za mwisho. Mwaka wa 1914, kulikuwa na wahubiri 5,155 katika nchi 43. Leo, kuna takriban wahubiri milioni nane na nusu katika nchi 240! Ingawa hivyo, kazi yetu bado haijaisha. Ni lazima tuendelee kutangaza kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee la matatizo yote ambayo wanadamu wanakabili.—Zab. 145:11-13.

9. Kwa nini ni lazima tuendelee kuhubiri ujumbe wa Ufalme?

9 Kazi yetu ya kuhubiri kuhusu Ufalme itaendelea hadi Yehova atakaposema imekamilika. Ni muda gani uliobaki kwa watu kumjua Yehova Mungu na Yesu Kristo? (Yoh. 17:3) Hatujui. Tunajua kwamba kabla ya dhiki kuu kuanza, mtu yeyote aliye na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” anaweza kukubali habari njema. (Mdo. 13:48) Tunaweza kuwasaidiaje watu hao kabla haijawa kuchelewa mno?

10. Yehova ametupatia nini ili kutusaidia kuwafundisha watu kweli?

10 Kupitia tengenezo lake, Yehova anatupatia kila kitu tunachohitaji ili kuwafundisha watu kweli. Kwa mfano, kila juma tunapokea mazoezi kwenye mkutano wa katikati ya juma. Mkutano huo hutusaidia kujua mambo tunayoweza kusema kwenye ziara ya kwanza na ziara za kurudia. Na unatufundisha jinsi ya kuongoza mafunzo ya Biblia. Pia, tengenezo la Yehova limetuandalia machapisho yaliyo katika Sanduku la Vifaa vya Kufundishia. Vifaa hivyo vinatusaidia . . .

  • kuanzisha mazungumzo,

  • kusitawisha upendezi,

  • kuwachochea watu watamani kujifunza zaidi,

  • kufundisha kweli tunapoongoza funzo la Biblia, na

  • kuwaalika wanaopendezwa watembelee tovuti yetu na Majumba yetu ya Ufalme.

Bila shaka, haitoshi tu kuwa na vifaa hivyo. Ni lazima tuvitumie. * Kwa mfano, ikiwa umemwachia mtu aliyependezwa trakti au gazeti baada ya mazungumzo mazuri pamoja naye, mtu huyo ataendelea kusoma chapisho hilo hadi mtakapowasiliana tena. Ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha kwamba ana mengi ya kufanya kila mwezi katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme.

11. Kwa nini Masomo ya Biblia Kwenye Mtandao yaliandaliwa?

11 Mfano mwingine wa jinsi Yehova anavyowasaidia watu wajifunze kweli ni kupitia Masomo ya Biblia Kwenye Mtandao yanayopatikana kwenye tovuti ya jw.org®. Kwa nini masomo hayo yaliandaliwa? Kila mwezi, makumi ya maelfu ya watu ulimwenguni pote hutafuta masomo ya Biblia kwenye mtandao. Masomo ya Biblia yaliyo katika tovuti yetu yanaweza kuwasaidia watu wajifunze kweli za Neno la Mungu. Huenda baadhi ya watu unaozungumza nao wakasita kukubali kujifunza Biblia pamoja nasi. Ikiwa ndivyo, waonyeshe masomo hayo kwenye tovuti yetu au watumie kiunganishi kitakachowaelekeza kwenye masomo hayo. *

12. Watu wanaweza kujifunza nini kupitia Masomo ya Biblia Kwenye Mtandao?

12 Masomo ya Biblia Kwenye Mtandao yanazungumzia habari kama vile: “Biblia na Mtungaji Wake,” “Wahusika Wakuu wa Biblia,” na “Ujumbe Wenye Tumaini wa Biblia.” Mtu anapochunguza habari hizo, atajifunza:

  • Jinsi Biblia inavyoweza kuwasaidia watu

  • Yehova, Yesu, na malaika ni nani

  • Kwa nini Mungu aliwaumba wanadamu

  • Kwa nini kuna mateso na uovu

Pia, masomo hayo yanazungumzia jinsi Yehova . . .

  • atakavyokomesha mateso na kifo,

  • atakavyowafufua wafu, na

  • atakavyoziondoa serikali za wanadamu na kusimamisha Ufalme wa Mungu.

13. Je, masomo ya Biblia mtandaoni yanachukua mahali pa mpango wa kujifunza Biblia pamoja na wenye nyumba? Eleza.

13 Masomo ya Biblia Kwenye Mtandao hayachukui mahali pa mpango wa kujifunza Biblia kibinafsi pamoja na wenye nyumba. Yesu ametupatia pendeleo la kufanya wanafunzi. Tunatumaini kwamba watu wanaopendezwa watachunguza masomo hayo mtandaoni, watathamini mambo wanayojifunza, na kutamani kujifunza mengi zaidi. Ikiwa ndivyo, huenda wakakubali tujifunze Biblia pamoja nao. Mwishoni mwa kila somo, msomaji anaalikwa awasilishe ombi la kufundishwa Biblia na mwalimu wake binafsi. Kwa wastani, kila siku kupitia tovuti yetu, tunapokea zaidi ya maombi 230 ya kujifunza Biblia! Kujifunza Biblia ana kwa ana pamoja na watu ni muhimu sana!

ENDELEA KUJITAHIDI KUFANYA WANAFUNZI

14. Kulingana na maagizo ya Yesu kwenye Mathayo 28:19, 20, tunajitahidi kadiri tuwezavyo kufanya nini, na kwa nini?

14 Soma Mathayo 28:19, 20. Tunapoongoza funzo la Biblia, tunapaswa kujitahidi kadiri tuwezavyo ‘kufanya wanafunzi na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo Yesu aliamuru.’ Tunahitaji kuwasaidia watu waelewe jinsi ilivyo muhimu sana kwao kuchukua msimamo upande wa Yehova na Ufalme wake. Hilo linamaanisha kuwachochea watu waifanye kweli kuwa mali yao kwa kutumia maishani mambo wanayojifunza, kuyaweka wakfu maisha yao kwa Yehova, na kubatizwa. Ikiwa watafanya hivyo, ndipo tu watakapookoka siku ya Yehova.—1 Pet. 3:21.

15. Hatuna muda wa kufanya nini, na kwa nini?

15 Kama ilivyotajwa awali, wakati uliobaki kabla ya mfumo huu wa mambo kuisha ni mfupi sana. Kwa sababu hiyo, hatuna muda wa kuendelea kujifunza Biblia pamoja na watu ambao hawana nia iliyo wazi ya kuwa wanafunzi wa Kristo. (1 Kor. 9:26) Kazi yetu ni ya uharaka! Bado kuna watu wengi ambao hawajasikia ujumbe wa Ufalme na wakati uliobaki ni mfupi sana.

JIEPUSHE KABISA NA DINI YA UWONGO

16. Kulingana na Ufunuo 18:2, 4, 5, 8, ni lazima sisi sote tufanye nini? (Tazama pia maelezo ya chini.)

16 Soma Ufunuo 18:2, 4, 5, 8Mistari hii inataja jambo lingine ambalo Yehova anatarajia kutoka kwa waabudu wake. Ni lazima Wakristo wote wa kweli wajitenge kabisa na Babiloni Mkubwa. Kabla ya kujifunza kweli, huenda mwanafunzi wa Biblia alikuwa akishirikiana na dini ya uwongo. Huenda alihudhuria ibada na kushiriki katika shughuli za kidini. Au huenda alitoa michango ya kifedha katika dini hiyo. Kabla ya mwanafunzi wa Biblia kuidhinishwa kuwa mhubiri ambaye bado hajabatizwa, ni lazima avunje kabisa uhusiano wowote na dini ya uwongo. Anapaswa kuwasilisha barua ya kufuta kabisa au kujiondoa kabisa kuwa mshiriki wa kanisa lake la awali na pia mashirika au vikundi vinavyohusiana na Babiloni Mkubwa. *

17. Ni lazima Mkristo aepuke kufanya kazi gani za kimwili, na kwa nini?

17 Ni lazima Mkristo wa kweli ahakikishe kwamba kazi yake ya kimwili haihusiani kwa vyovyote na Babiloni Mkubwa. (2 Kor. 6:14-17) Kwa mfano, hatakubali kuajiriwa na kanisa. Zaidi ya hilo, Mkristo ambaye ameajiriwa kwenye kampuni au biashara fulani, hawezi kukubali kufanya kazi inayohusisha mambo mengi kwenye jengo linalotumiwa kuendeleza ibada ya uwongo. Na ikiwa amejiajiri mwenyewe, bila shaka hatakubali kandarasi au mkataba wa kufanya kazi yoyote inayohusiana na Babiloni Mkubwa. Kwa nini tunachukua msimamo huo thabiti? Kwa sababu hatutaki kushiriki matendo au dhambi zozote za mashirika ya kidini ambayo si safi machoni pa Mungu.—Isa. 52:11. *

18. Ndugu mmoja alishikamana jinsi gani na kanuni za Biblia ilipohusu kazi ya kimwili?

18 Miaka mingi iliyopita, mzee mmoja wa kutaniko aliyekuwa amejiajiri mwenyewe aliombwa na mkandarasi fulani afanye kazi ndogo ya useremala kwenye kanisa moja katika mji aliokuwa akiishi. Mkandarasi huyo alijua wazi kwamba ndugu huyo hangekubali kufanya kazi kanisani. Lakini wakati huu, alihitaji haraka mtu wa kufanya kazi hiyo. Licha ya hilo, ndugu yetu alishikamana na kanuni za Biblia na kukataa kazi hiyo. Juma lililofuata, gazeti la habari katika eneo hilo lilikuwa na picha ya seremala mwingine akiweka msalaba kwenye kanisa hilo. Ikiwa ndugu yetu angelegeza msimamo wake, picha yake ndiyo ingekuwa kwenye gazeti hilo. Wazia jinsi ambavyo jambo hilo lingemharibia sifa miongoni mwa Wakristo wenzake! Pia, fikiria jinsi ambavyo Yehova angehisi!

TUMEJIFUNZA NINI?

19-20. (a) Tumejifunza mambo gani kufikia sasa? (b) Ni mambo gani zaidi tunayohitaji kujifunza?

19 Kulingana na unabii wa Biblia, tukio kubwa tunalotazamia hivi karibuni ni tangazo la “amani na usalama” litakalotolewa na viongozi wa ulimwengu. Kwa msingi wa mambo ambayo Yehova ametufundisha, tunajua kwamba mataifa hayawezi kupata amani ya kweli na inayodumu. Tunapaswa kufanya nini kabla ya tangazo hilo kutolewa na kabla ya uharibifu wa ghafla kutokea? Yehova anatarajia tuwe na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme na tujitahidi kufanya wanafunzi wengi zaidi. Wakati huohuo, tunahitaji kuendelea kujitenga na dini zote za uwongo. Hilo linatia ndani kuvunja ushirika wowote na Babiloni Mkubwa na kuepuka ajira yoyote inayohusiana naye.

20 Kuna matukio mengine yatakayotukia kwenye kipindi cha mwisho kabisa cha “siku za mwisho.” Pia, kuna mambo mengine ambayo Yehova anatarajia tufanye. Ni mambo gani hayo, na tunaweza kufanya nini ili tuwe tayari kwa ajili ya mambo yote yatakayotokea hivi karibuni? Tutajifunza mambo hayo katika makala inayofuata.

WIMBO 71 Sisi Ni Jeshi la Yehova!

^ fu. 5 Hivi karibuni, tunatarajia kusikia viongozi wa ulimwengu wakidai kwamba wamepata “amani na usalama!” Tangazo hilo litakuwa ishara ya kwamba dhiki kuu iko karibu kuanza. Yehova anatarajia tufanye nini tunaposubiri wakati huo? Makala hii itatusaidia kupata jibu.

^ fu. 3 Kwa mfano, kwenye tovuti yake, Umoja wa Mataifa hudai kwamba “unadumisha amani na usalama wa mataifa.”

^ fu. 10 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kutumia vifaa vilivyo katika Sanduku la Vifaa vya Kufundishia, tazama makala “Fundisha Kweli” katika toleo la Oktoba 2018 la gazeti Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 11 Kwa sasa masomo hayo yanapatikana katika Kiingereza na Kireno, na lugha nyingine zaidi zitafuata.

^ fu. 16 Pia, tunahitaji kuepuka mashirika au vikundi vya kidini kama vile kambi za vijana au sehemu za michezo na mazoezi zinazohusianishwa na dini ya uwongo. Kwa mfano, kwa habari zaidi kuhusu kuwa mshiriki wa YMCA (Young Men’s Christian Association), tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1979, la Kiingereza. Tunapaswa kuchukua msimamo huohuo inapohusu kuwa mshiriki wa YWCA (Young Women’s Christian Association). Hata ingawa huenda vikundi au mashirika hayo yanaweza kudai kwamba utendaji wao hauhusishi mambo ya kidini, ukweli wa mambo ni kwamba chimbuko lao na malengo wanayoendeleza ni ya kidini.

^ fu. 17 Kwa habari za kina zaidi kuhusu maoni ya Biblia inapohusu kazi ya kuajiriwa katika mashirika ya kidini, tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji,” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1999.

^ fu. 83 MAELEZO YA PICHA Ukurasa wa 10: Wateja kwenye mkahawa wakifuatilia kwa makini “Habari za Hivi Punde” kwenye televisheni kuhusu tangazo la “amani na usalama.” Wakiwa wamepumzika kidogo baada ya kuhubiri, wenzi wa ndoa Mashahidi hawapumbazwi na tangazo hilo.