Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 42

Yehova Anaweza Kukutumiaje?

Yehova Anaweza Kukutumiaje?

“Mungu . . . anawachochea, na kuwapa hamu na nguvu za kutenda.”—FLP. 2:13.

WIMBO 104 Roho Takatifu—Zawadi Kutoka kwa Mungu

MUHTASARI *

1. Yehova anaweza kufanya nini ili kutimiza kusudi lake?

YEHOVA anaweza kuwa chochote kinachohitajika katika kila hali ili kutimiza kusudi lake. Kwa mfano, Yehova amekuwa Mwalimu, Mfariji, na Mweneza-Injili—miongoni mwa majukumu yake mengine mengi. (Isa. 48:17; 2 Kor. 7:6; Gal. 3:8) Licha ya hayo, yeye huwatumia wanadamu kutimiza makusudi yake. (Mt. 24:14; 28:19, 20; 2 Kor. 1:3, 4) Pia, Yehova anaweza kumpatia yeyote miongoni mwetu hekima na nguvu anazohitaji ili awe chochote kinachohitajika na kutimiza mapenzi yake. Yote hayo ni sehemu ya maana ya jina la Yehova, kama wasomi wengi wanavyosema.

2. (a) Kwa nini huenda nyakati nyingine tukahisi kwamba hatutumiwi na Yehova? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Sisi sote tunatamani Yehova atutumie ili kutimiza mapenzi yake, lakini huenda wengine wakawa na shaka ikiwa kweli Yehova anawatumia. Kwa nini? Wanahisi kwamba hawawezi kutimiza mengi kwa sababu ya umri, hali, au uwezo wao. Kwa upande mwingine, huenda wengine wameridhika na mambo ambayo tayari wametimiza na hawaoni uhitaji wa kuendelea kufanya mengi zaidi. Katika makala hii, tutachunguza jinsi Yehova anavyoweza kumpa yeyote miongoni mwetu kile anachohitaji ili kutimiza kusudi lake. Kisha tutachunguza masimulizi ya Biblia yanayoonyesha jinsi Yehova alivyowapa watumishi wake—wanaume kwa wanawake—hamu na nguvu ya kutenda. Mwishowe, tutachunguza jinsi tunavyoweza kumruhusu Yehova atutumie.

JINSI YEHOVA ANAVYOTUPATIA KILE TUNACHOHITAJI

3. Kama inavyotajwa kwenye Wafilipi 2:13, Yehova anaweza kutupatiaje hamu ya kutenda?

3 Soma Wafilipi 2:13. * Yehova anaweza kutupatia hamu ya kutenda. Anafanyaje hivyo? Kwa mfano, huenda tukasikia kuhusu uhitaji fulani kutanikoni. Au wazee kutanikoni wanasoma barua kutoka kwenye ofisi ya tawi inayotaja kuhusu uhitaji uliotokea mahali pengine. Kisha tunajiuliza, ‘Tunaweza kufanya nini ili kusaidia?’ Au labda tumepewa mgawo fulani mgumu, na tunajiuliza ikiwa kweli tunaweza kuutimiza kwa njia inayostahili. Au baada ya kusoma mistari fulani ya Neno la Mungu, tunajiuliza, ‘Ninaweza kuitumiaje mistari hii kuwasaidia wengine?’ Yehova hatatulazimisha kufanya jambo lolote. Lakini anapoona kwamba tuna nia ya kujichunguza, Yehova anaweza kutupatia hamu ya kutimiza jambo tulilokusudia.

4. Yehova anaweza kutupatiaje nguvu za kutenda?

4 Pia, Yehova anaweza kutupatia nguvu za kutenda. (Isa. 40:29) Anaweza kukuza uwezo wetu wa asili kupitia roho yake takatifu. (Kut. 35:30-35) Kupitia tengenezo lake, Yehova anaweza kutufundisha jinsi ya kutimiza kazi fulani. Wakati wowote ule unapohisi kwamba huna uhakika kuhusu jinsi ya kutimiza mgawo fulani, omba msaada. Pia, jihisi huru kumwomba Baba yetu wa mbinguni aliye mkarimu “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7; Luka 11:13) Biblia ina mifano mingi ya jinsi Yehova alivyowasaidia wanaume na wanawake kwa kuwapatia hamu na nguvu za kutenda. Tunapochunguza baadhi ya masimulizi hayo, jaribu kufikiria njia mbalimbali ambazo Yehova anaweza kukutumia kama alivyowatumia wanaume na wanawake hao.

MAMBO AMBAYO YEHOVA ALIWASAIDIA WANAUME KUTIMIZA

5. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyomtumia Musa na wakati aliochagua kumtumia ili kuwakomboa watu Wake?

5 Yehova alimsaidia Musa kuwa mkombozi wa Waisraeli. Lakini Yehova alimtumia wakati gani? Je, alimtumia baada ya Musa kuhisi kwamba sasa anastahili kwa kuwa ‘amefundishwa hekima yote ya Wamisri’? (Mdo. 7:22-25) Hapana, Yehova alimtumia Musa baada tu ya kumfinyanga kuwa mwanamume mnyenyekevu na mpole. (Mdo. 7:30, 34-36) Yehova alimpatia Musa ujasiri wa kusimama mbele ya mtawala mwenye nguvu kuliko wote nchini Misri. (Kut. 9:13-19) Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyomtumia Musa na wakati aliochagua kumtumia? Yehova huwatumia wale wanaojitahidi kuiga sifa zake na wanaomtegemea yeye ili wapate nguvu.—Flp. 4:13.

6. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyomtumia Barzilai kumsaidia Mfalme Daudi?

6 Karne nyingi baadaye, Yehova alimtumia Barzilai ili kumsaidia Mfalme Daudi. Daudi na watu wake walikuwa na ‘njaa, uchovu, na kiu’ na walikuwa wakimkimbia Absalomu, mwana wa Daudi. Barzilai, ambaye alikuwa mzee wakati huo, alihatarisha maisha yake pamoja na ya watu wengine ili kumsaidia Daudi na watu wake. Barzilai hakuhisi kwamba hangeweza kutumiwa na Yehova eti kwa sababu alikuwa na umri mkubwa. Badala yake, alitoa kwa ukarimu vitu alivyokuwa navyo ili kuwasaidia watumishi wa Yehova wenye uhitaji. (2 Sam. 17:27-29) Tunajifunza somo gani? Hata iwe tuna umri gani, Yehova anaweza kututumia kuwasaidia waamini wenzetu wanaokosa mahitaji yao ya msingi, iwe ni katika eneo letu au katika nchi nyingine. (Met. 3:27, 28; 19:17) Hata ikiwa hatuwezi kuwasaidia moja kwa moja, tunaweza kutoa michango kwa ajili ya kazi ya uli-mwenguni pote ili pesa hizo zitumiwe kuwasaidia ndugu na dada zetu wanapokuwa na uhitaji.—2 Kor. 8:14, 15; 9:11.

7. Yehova alimtumiaje Simeoni, na kwa nini jambo hilo linatutia moyo?

7 Yehova alimwahidi Simeoni, mwanamume mzee mshikamanifu katika jiji la Yerusalemu kwamba hataona kifo kabla ya kumwona Masihi. Hapana shaka kwamba ahadi hiyo ilimtia moyo sana Simeoni, kwa sababu alikuwa amemsubiri Masihi kwa miaka mingi. Alithawabishwa kwa sababu ya imani na uvumilivu wake. Siku moja, “akiongozwa na roho” alifika hekaluni. Akiwa huko, alimwona mtoto Yesu, na Yehova akamtumia Simeoni kutoa unabii kuhusu mtoto huyo ambaye angekuja kuwa Kristo. (Luka 2:25-35) Ingawa huenda Simeoni hakuishi muda mrefu kiasi cha kumwona Yesu akitimiza huduma yake duniani, alishukuru sana kwa pendeleo alilopewa, na atajionea mambo mazuri hata zaidi wakati ujao! Katika ulimwengu mpya, mwanamume huyo mwaminifu atajionea jinsi utawala wa Yesu utakavyothibitika kuwa baraka kwa familia zote duniani. (Mwa. 22:18) Sisi pia tunaweza kushukuru sana kwa pendeleo lolote ambalo Yehova anatupatia katika utumishi wake.

8. Kama ilivyokuwa kwa Barnaba, Yehova anaweza kututumiaje?

8 Katika karne ya kwanza W.K., mwanamume mkarimu aliyeitwa Yosefu alijitoa kwa hiari ili atumiwe na Yehova. (Mdo. 4:36, 37) Mitume walimwita Yosefu jina Barnaba, linalomaanisha “Mwana wa Faraja,” inaelekea kwa sababu Yosefu alikuwa mfano mzuri wa kuwafariji wengine. Kwa mfano, baada ya Sauli kuwa mwamini, akina ndugu wengi waliogopa kumfikia kwa sababu ya sifa aliyokuwa nayo ya kuyatesa makutaniko. Lakini Barnaba, mwanamume mwenye shauku, alikuwa tayari kumsaidia Sauli, na hapana shaka kwamba Sauli alithamini sana fadhili alizoonyeshwa. (Mdo. 9:21, 26-28) Baadaye, wanaume wazee katika jiji la Yerusalemu waliona uhitaji wa kuwatia moyo akina ndugu waliokuwa wakiishi mbali huko Antiokia ya Siria. Walimtuma nani? Barnaba! Walimchagua mtu aliyefaa kabisa. Tunasoma kwamba Barnaba alianza “kuwatia moyo wote waendelee kukaa katika Bwana wakiwa wameazimia moyoni.” (Mdo. 11:22-24) Vivyo hivyo leo, Yehova anaweza kutusaidia tuwe ‘wana wa faraja’ kwa Wakristo wenzetu. Kwa mfano, anaweza kututumia kuwafariji wale waliowapoteza wapendwa wao katika kifo. Au anaweza kutuchochea tuwatembelee au kuwapigia simu wagonjwa na waliovunjika moyo ili tuwafariji kupitia maneno yenye fadhili. Je, utamruhusu Yehova akutumie kama alivyomtumia Barnaba?—1 The. 5:14.

9. Tunajifunza nini kutokana na jinsi ambavyo Yehova alimsaidia Ndugu Vasily kuwa mchungaji wa kiroho mwenye uwezo?

9 Yehova alimsaidia ndugu anayeitwa Vasily awe mchungaji wa kiroho mwenye uwezo. Vasily alipowekwa rasmi kuwa mzee wa kutaniko akiwa na umri wa miaka 26, alikuwa na wasiwasi kwamba hakustahili kuwasaidia akina ndugu na dada kiroho, hasa wale waliokuwa wakipitia hali ngumu. Hata hivyo, alipata mazoezi mazuri kutoka kwa wazee wenye uzoefu na kwa kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme. Vasily alitia bidii sana ili kuboresha hali yake. Kwa mfano, aliandika orodha ya miradi midogomidogo ambayo alitaka kutimiza. Kadiri alivyokuwa akitimiza mradi mmoja baada ya mwingine, ndivyo alivyofanikiwa kushinda wasiwasi wake. Leo anasema hivi: “Mambo yaliyonipa wasiwasi wakati huo, sasa yananipa shangwe nyingi. Yehova anaponisaidia kupata andiko linalofaa la kumfariji ndugu au dada kutanikoni, ninafurahi na kuridhika sana.” Akina ndugu, ikiwa mtakuwa tayari ku-tumiwa na Yehova kama Vasily, Yehova atawapa uwezo wa kushughulikia majukumu makubwa zaidi kutanikoni.

MAMBO AMBAYO YEHOVA ALIWASAIDIA WANAWAKE KUTIMIZA

10. Abigaili alifanya nini, na tunajifunza somo gani kutokana na mfano wake?

10 Daudi na watu walioshikamana naye walikuwa wakiwindwa na Mfalme Sauli, na walihitaji msaada. Wanaume wa Daudi walimwomba Mwisraeli tajiri aliyeitwa Nabali chakula chochote kidogo alichokuwa nacho. Walijihisi huru kumwomba kwa sababu walikuwa wakilinda kondoo wa Nabali nyikani. Lakini Nabali, mwanamume mwenye ubinafsi, alikataa kuwapa chochote. Daudi alikasirika sana na alikusudia kumuua Nabali na kila mwanamume katika nyumba yake. (1 Sam. 25:3-13, 22) Hata hivyo, Abigaili, mke mrembo wa Nabali, alikuwa mwanamke mwenye busara. Alionyesha ujasiri mkubwa alipoanguka miguuni pa Daudi akimsihi asijiletee hatia ya damu kwa kulipiza kisasi. Alimshauri kwa busara aache mambo mikononi mwa Yehova. Maneno ya Abigaili yenye unyenyekevu na matendo yake ya busara yaligusa moyo wa Daudi. Daudi alitambua kwamba Abigaili alitumwa na Yehova. (1 Sam. 25:23-28, 32-34) Abigaili alikuwa amesitawisha sifa zilizomfanya atumiwe na Yehova. Vivyo hivyo, akina dada Wakristo wanaositawisha sifa ya utambuzi na busara wanaweza kutumiwa na Yehova kuimarisha familia zao na wengine kutanikoni.—Met. 24:3; Tito 2:3-5.

11. Binti za Shalumu walifanya nini, na ni nani leo wanaowaiga?

11 Karne nyingi baadaye, binti za Shalumu walikuwa miongoni mwa watu waliotumiwa na Yehova kurekebisha kuta za Yerusalemu. (Neh. 2:20; 3:12) Ingawa baba yao alikuwa mkuu, binti za Shalumu walikuwa tayari kujitoa ili kufanya kazi hiyo ngumu na hatari. (Neh. 4:15-18) Walikuwa tofauti sana na wanaume mashuhuri Watekoa ambao “hawakutaka kujishusha ili kushiriki” katika kazi hiyo! (Neh. 3:5) Wazia shangwe ambayo binti za Shalumu walikuwa nayo mradi huo ulipokamilika ndani ya siku 52 tu! (Neh. 6:15) Katika siku zetu, akina dada wanaojitoa kwa hiari hufurahia kufanya aina fulani ya utumishi mtakatifu wa pekee, yaani, kujenga na kudumisha majengo yaliyowekwa wakfu kwa Yehova. Ustadi, uchangamfu, na ushikamanifu wao ni mambo muhimu yanayohitajika ili kufanikisha kazi hiyo.

12. Kama ilivyokuwa kwa Tabitha, Yehova anaweza kututumiaje?

12 Yehova alimchochea Tabitha azidi katika ‘matendo mema na zawadi za rehema,’ hasa kwa ajili ya wajane. (Mdo. 9:36) Kwa sababu ya fadhili na ukarimu wake wa pekee, watu wengi walilia sana alipokufa. Lakini walijawa na shangwe mtume Petro alipomfufua. (Mdo. 9:39-41) Mfano wa Tabitha unatufundisha nini? Iwe sisi ni vijana au wazee, wanaume au wanawake, sisi sote tunaweza kuwafanyia ndugu na dada zetu mambo mema ili kuwasaidia.—Ebr. 13:16.

13. Yehova alimtumiaje dada mwenye haya anayeitwa Ruth, na dada huyo alisema nini?

13 Dada mwenye haya anayeitwa Ruth, alitaka kuwa mmishonari. Alipokuwa msichana mdogo, alikuwa na bidii ya kuwagawia watu trakti haraka-haraka kutoka nyumba moja hadi nyingine. Anaeleza hivi: “Nilifurahia sana kufanya hivyo.” Lakini ilikuwa vigumu kwake kuzungumza na wenye nyumba na kuwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu. Licha ya kuwa mwenye haya, Ruth alianza upainia wa kawaida akiwa na umri wa miaka 18. Katika mwaka wa 1946, alihudhuria Shule ya Gileadi na baadaye akatumikia nchini Hawaii na Japani. Yehova alimtumia kwa njia kubwa sana kueneza habari njema katika nchi hizo. Baada ya kushiriki katika huduma kwa karibu miaka 80, Ruth alisema hivi: “Yehova amekuwa msaada mkubwa sana kwangu. Amenisaidia kushinda haya niliyokuwa nayo. Ninaamini kabisa kwamba Yehova anaweza kumtumia mtu yeyote anayemtegemea.”

MRUHUSU YEHOVA AKUTUMIE

14. Kulingana na Wakolosai 1:29, ni lazima tufanye nini ikiwa tunataka Yehova atutumie?

14 Katika historia yote ya wanadamu, Yehova amekuwa akiwatumia watumishi wake ili kutimiza majukumu mengi mbalimbali. Yehova atakutumiaje wewe? Kwa kadiri kubwa, jambo hilo linategemea hasa utayari wako wa kujikakamua kwa bidii kabisa. (Soma Wakolosai 1:29.) Ikiwa utamruhusu Yehova akutumie, anaweza kukusaidia uwe mweneza-injili mwenye bidii, mwalimu stadi, mfariji mzuri, mfanyakazi stadi, rafiki mzuri, au chochote kingine anachohitaji ili kutimiza mapenzi yake.

15. Kama andiko la 1 Timotheo 4:12, 15 linavyosema, ndugu vijana wanapaswa kumsihi Yehova awasaidie kufanya nini?

15 Namna gani ninyi ndugu vijana mnaokaribia kuwa watu wazima? Kuna uhitaji mkubwa wa wanaume wenye nguvu wanaoweza kutumikia wakiwa watumishi wa huduma. Katika makutaniko mengi idadi ya wazee wa kutaniko inazidi ile ya watumishi wa huduma. Enyi ndugu vijana, je, mnaweza kusitawisha hamu ya kufanya mengi zaidi katika kutaniko? Nyakati nyingine ndugu wengine husema, “Ninaridhika tu kuwa mhubiri kutanikoni.” Ikiwa hivyo ndivyo unavyohisi, msihi Yehova akusaidie kusitawisha hamu ya kustahili kuwa mtumishi wa huduma na akupatie nguvu ya kufanya yote unayoweza ili umtumikie. (Mhu. 12:1) Tunahitaji msaada wako!—Soma 1 Timotheo 4:12, 15.

16. Tunapaswa kumwomba nini Yehova, na kwa nini?

16 Yehova anaweza kukusaidia uwe chochote anachohitaji ili kutimiza mapenzi yake. Basi mwombe akupe hamu ya kufanya kazi yake, na pia umwombe akupe nguvu unazohitaji. Iwe wewe ni kijana au mzee, tumia wakati, nguvu, na mali zako kumheshimu Yehova leo. (Mhu. 9:10) Usiruhusu kamwe wasiwasi au hisia za kujiona kwamba hufai zikufanye upoteze fursa zenye thamani za kufanya yote unayoweza katika utumishi wa Yehova. Ni pendeleo kubwa sana kufanya yote tuwezayo, hata ikiwa ni jambo dogo, kumletea Yehova, Baba yetu anayetupenda heshima anayostahili!

WIMBO 127 Napaswa Kuwa Mtu wa Namna Gani?

^ fu. 5 Je, wewe huhisi kwamba hutimizi mengi katika utumishi wa Yehova? Je, unajiuliza ikiwa bado Yehova anaweza kukutumia? Au je, unashindwa kutambua umuhimu wa kurekebisha hali zako ili umtumikie Yehova kwa njia yoyote anayotaka? Makala hii itazungumzia njia mbalimbali ambazo Yehova anaweza kukupatia hamu na nguvu za kuwa chochote kinachohitajika ili utimize kusudi lake.

^ fu. 3 Ingawa Paulo aliwaandikia Wakristo wa karne ya kwanza barua hiyo, maneno yake yanawahusu watumishi wote wa Yehova