Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 41

Jinsi ya Kumsaidia Mwanafunzi wa Biblia Afikie Hatua ya Ubatizo—Sehemu ya Kwanza

Jinsi ya Kumsaidia Mwanafunzi wa Biblia Afikie Hatua ya Ubatizo—Sehemu ya Kwanza

“Ninyi ni barua ya Kristo ambayo tuliandika tukiwa wahudumu.”​—2 KOR. 3:3.

WIMBO 78 ‘Kufundisha Neno la Mungu’

MUHTASARI *

Je, kuna jambo lolote lenye kusisimua zaidi kwa kutaniko zima kuliko kumwona mwanafunzi wa Biblia ambaye wanampenda akibatizwa? (Tazama fungu la 1)

1. Andiko la 2 Wakorintho 3:1-3 linatusaidiaje kuthamini pendeleo letu la kumsaidia mwanafunzi wa Biblia afikie hatua ya ubatizo? (Tazama picha kwenye jalada.)

UNAHISIJE unapomwona mwanafunzi wa Biblia kutoka katika eneo la kutaniko lenu akibatizwa? Bila shaka moyo wako unashangilia. (Mt. 28:19) Na ikiwa wewe ndiye uliyejifunza naye, unasisimka sana unapomwona akibatizwa! (1 The. 2:19, 20) Wanafunzi wapya waliobatizwa ni ‘barua nzuri zinazowapendekeza’ wale waliojifunza nao na pia kutaniko zima.​—Soma 2 Wakorintho 3:1-3.

2. (a) Tunapaswa kutafakari kuhusu swali gani muhimu, na kwa nini? (b) Funzo la Biblia ni nini? (Tazama maelezo ya chini.)

2 Inapendeza kuona kwamba kwa miaka minne iliyopita kwa wastani mafunzo ya Biblia * 10,000,000 hivi yameripotiwa kila mwezi ulimwenguni pote. Katika kipindi hichohicho, kwa wastani wanafunzi zaidi ya 280,000 walibatizwa kila mwaka na kuwa Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wapya wa Kristo. Tunaweza kuwasaidiaje wengi zaidi kati ya mamilioni hayo ya wanafunzi wa Biblia wafikie hatua ya ubatizo? Maadamu Yehova anaonyesha subira kwa kuwapa watu wakati na fursa ya kuwa wanafunzi wa Kristo, tungependa kufanya yote tunayoweza kuwasaidia wafanye maendeleo na kubatizwa haraka iwezekanavyo. Wakati uliobaki ni mfupi sana!—1 Kor. 7:29a; 1 Pet. 4:7.

3. Tutajifunza nini katika makala hii kuhusu kuongoza mafunzo ya Biblia?

3 Ili kutimiza kazi muhimu na yenye uharaka ya kufanya wanafunzi, Baraza Linaloongoza liliziomba ofisi za tawi zitathmini jinsi tunavyoweza kuwasaidia wanafunzi wengi zaidi wa Biblia wafanye maendeleo na kufikia hatua ya ubatizo. Katika makala hii na ile inayofuata, tutaona mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa mapainia, wamishonari, na waangalizi wa mzunguko wenye uzoefu. * (Met. 11:14; 15:22) Wanaeleza mambo ambayo walimu wa Biblia na wanafunzi wao wanaweza kufanya ili funzo la Biblia liwe lenye matokeo zaidi. Katika makala hii, tutachunguza mambo matano ambayo kila mwanafunzi wa Biblia anahitaji kufanya ili afanye maendeleo na kufikia hatua ya ubatizo.

JIFUNZENI KILA JUMA

Muulize mwanafunzi wako ikiwa mnaweza kuketi ili kujifunza Biblia (Tazama fungu la 4 hadi 6)

4. Tunapaswa kutambua nini kuhusu mafunzo ya Biblia yanayoongozwa mlangoni?

4 Ndugu na dada zetu wengi wanaongoza mafunzo ya Biblia wakiwa wamesimama kwenye mlango wa mwenye nyumba. Ingawa huo ni mwanzo mzuri tunapotaka kuwasaidia wasitawishe upendezi katika Biblia, kwa kawaida mazungumzo hayo ni mafupi na huenda yasifanywe kila juma. Ili kusitawisha upendezi zaidi, baadhi ya ndugu na dada humwomba mtu anayependezwa awapatie habari zitakazowasaidia kuwasiliana naye, na kisha hushiriki naye wazo la Kimaandiko kupitia simu au ujumbe mfupi kabla ya kumtembelea tena. Huenda mazungumzo hayo ya pindi kwa pindi yakaendelea kwa miezi kadhaa bila kuwa funzo la Biblia linalofanya maendeleo. Je, kweli mwanafunzi wa Biblia atafanya maendeleo na kufikia kujiweka wakfu na kubatizwa ikiwa hatumii muda na jitihada nyingi zaidi ili kujifunza Neno la Mungu? Hapana.

5. Kulingana na Luka 14:27-33, Yesu alikazia jambo gani linaloweza kutusaidia katika kazi ya kufanya wanafunzi?

5 Pindi moja, Yesu alitoa mfano ili kuonyesha gharama zinazohusika mtu anapotaka kuwa mwanafunzi wake. Alizungumza kuhusu mtu anayetaka kujenga mnara na kuhusu mfalme anayetaka kwenda kupigana vita. Yesu alisema kwamba yule anayetaka kujenga lazima ‘aketi kwanza na kuhesabu gharama’ ili akamilishe mnara huo na kwamba ni lazima mfalme ‘aketi kwanza na kufikiri’ ili kuona ikiwa wanajeshi wake wanaweza kutimiza kile wanachokusudia kufanya. (Soma Luka 14:27-33.) Vivyo hivyo, Yesu alijua kwamba mtu aliyetaka kuwa mwanafunzi wake, alipaswa kuchanganua kwa uangalifu sana kile kinachomaanishwa na kuwa mfuasi wake. Kwa sababu hiyo, tunahitaji kuwatia moyo wanafunzi wetu wa Biblia wajifunze nasi kila juma. Tunaweza kufanyaje hivyo?

6. Huenda tukahitaji kufanya nini ili tuongoze mafunzo ya Biblia yenye matokeo?

6 Anza kwa kutumia muda mrefu zaidi unapoongoza mafunzo ya Biblia ya mlangoni. Badala ya kuzungumzia andiko moja tu kila unapomtembelea, labda unaweza kuzungumzia maandiko mawili. Mwenye nyumba atakapohisi yuko tayari kwa ajili ya mazungumzo marefu zaidi, mwulize ikiwa kuna mahali ambapo mnaweza kuketi pamoja na kuendeleza mazungumzo. Jibu la mwenye nyumba litafunua jinsi anavyothamini funzo hilo la Biblia. Ili kumsaidia afanye maendeleo haraka, unaweza kumuuliza ikiwa anaweza kuwa tayari kujifunza mara mbili kwa juma. Hata hivyo, unahitaji kufanya mengi zaidi ya kujifunza mara moja au mara mbili kila juma.

JITAYARISHE KWA AJILI YA KILA KIPINDI CHA FUNZO

Jitayarishe vizuri kwa ajili ya funzo la Biblia, na mwonyeshe mwanafunzi wako jinsi ya kujitayarisha (Tazama fungu la 7 hadi 9)

7. Mwalimu anaweza kujitayarishaje vizuri kwa ajili ya kila kipindi cha funzo?

7 Ukiwa mwalimu unahitaji kujitayarisha vizuri kwa ajili ya kila kipindi cha funzo. Unaweza kuanza kwa kusoma habari mtakayojifunza na maandiko yaliyopo. Elewa vizuri mambo makuu. Fikiria kichwa kikuu cha somo, vichwa vidogo, maswali, maandiko yaliyoandikwa “soma,” picha, na video zozote ambazo huenda zikakusaidia kufafanua habari mtakayozungumzia. Kisha, huku ukimfikiria mwanafunzi wako, tafakari mapema jinsi utakavyofafanua habari hiyo kwa njia rahisi na iliyo wazi ili mwanafunzi wako aweze kuielewa na kuitumia kwa urahisi.—Neh. 8:8; Met. 15:28a.

8. Maneno ya mtume Paulo kwenye Wakolosai 1:9, 10, yanatufundisha nini kuhusu kusali kwa ajili ya wanafunzi wetu wa Biblia?

8 Unapojitayarisha, sali kwa Yehova kuhusu mwanafunzi wako na mahitaji yake. Mwombe Yehova akusaidie umfundishe mwanafunzi wako Biblia kwa njia itakayoufikia moyo wake. (Soma Wakolosai 1:9, 10.) Fikiria mapema mambo ambayo huenda ikawa vigumu kwa mwanafunzi wako kuyaelewa au kuyakubali. Kumbuka kwamba lengo lako ni kumsaidia afikie hatua ya ubatizo.

9. Mwalimu anaweza kumsaidiaje mwanafunzi wake ajitayarishe kwa ajili ya funzo? Eleza.

9 Tunatumaini kwamba kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida, mwanafunzi atathamini mambo ambayo Yehova na Yesu wamefanya na atataka kujifunza mengi zaidi. (Mt. 5:3, 6) Ili anufaike kikamili kutokana na funzo, mwanafunzi anahitaji kukazia fikira mambo anayojifunza. Ili kumsaidia afanye hivyo, mweleze jinsi ilivyo muhimu kwake kujitayarisha kwa ajili ya kila kipindi cha funzo, kwa kupitia mapema somo mtakalojifunza na kutafakari jinsi habari hiyo inavyomhusu. Unaweza kumsaidiaje? Kwa kujitayarisha pamoja na mwanafunzi ili kumwonyesha jinsi anavyoweza kujitayarisha kwa ajili ya funzo. * Mweleze jinsi anavyoweza kupata majibu ya moja kwa moja ya maswali, na mwonyeshe jinsi ambavyo kuweka alama kwenye maneno makuu kunaweza kumsaidia kukumbuka majibu. Kisha mwombe ajibu kwa maneno yake mwenyewe. Anapofanya hivyo, utaweza kutambua anaelewa kwa kadiri gani mambo mnayojifunza. Hata hivyo, kuna jambo lingine ambalo unaweza kumtia moyo mwanafunzi wako afanye.

MFUNDISHE KUWASILIANA NA YEHOVA KILA SIKU

Mfundishe mwanafunzi wako jinsi ya kuwasiliana na Yehova (Tazama fungu la 10 na 11)

10. Kwa nini ni muhimu kusoma Biblia kila siku, na tunahitaji kufanya nini ili tufaidike kikamili na usomaji wa Biblia?

10 Zaidi ya kujifunza na mwalimu wake kila juma, mwanafunzi atafaidika kwa kufanya mambo fulani yeye mwenyewe kila siku. Anahitaji kuwasiliana na Yehova. Jinsi gani? Kwa kumsikiliza Yehova na kuzungumza naye. Anaweza kumsikiliza Mungu kwa kusoma Biblia kila siku. (Yos. 1:8; Zab. 1:1-3) Mwonyeshe jinsi ya kutumia “Ratiba ya Kusoma Biblia” inayoweza kuchapishwa, iliyo kwenye jw.org/sw. * Na bila shaka, ili kumsaidia afaidike zaidi na usomaji wake wa Biblia, mtie moyo atafakari kuhusu mambo ambayo Biblia inamfundisha kuhusu Yehova na jinsi anavyoweza kutumia mambo anayojifunza maishani mwake.—Mdo. 17:11; Yak. 1:25.

11. Mwanafunzi anaweza kujifunza jinsi gani kusali kwa njia sahihi, na kwa nini ni muhimu kwake kusali kwa Yehova kwa ukawaida?

11 Mtie moyo mwanafunzi wako azungumze na Yehova kwa kusali kila siku. Sali kutoka moyoni mwanzoni na mwishoni mwa kila kipindi cha funzo, na umtaje mwanafunzi wako katika sala hizo. Anaposikiliza sala hizo, atajifunza kusali kutoka moyoni na kwa unyoofu akielekeza sala zake kwa Yehova Mungu kupitia jina la Yesu Kristo. (Mt. 6:9; Yoh. 15:16) Wazia jinsi ambavyo kusoma Biblia kila siku (kumsikiliza Yehova) na kusali (kuzungumza na Yehova) kutavyomsaidia mwanafunzi wako amkaribie Mungu hata zaidi! (Yak. 4:8) Kusitawisha mazoea hayo kutamsaidia mwanafunzi wako afanye maendeleo na ajiweke wakfu na kubatizwa. Ni jambo gani lingine litakalomsaidia?

MSAIDIE ASITAWISHE UHUSIANO WA KIBINAFSI PAMOJA NA YEHOVA

12. Mwalimu anaweza kumsaidiaje mwanafunzi asitawishe uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova?

12 Mambo ambayo mwanafunzi wa Biblia anajifunza katika funzo lake la Biblia hayapaswi kuingia akilini tu, bali yanapaswa kumgusa moyo pia. Kwa nini? Kwa sababu moyo wetu, unaotia ndani tamaa na hisia zetu, hutuchochea kuchukua hatua. Yesu alitoa hoja zilizopatana na akili na ambazo ziliwavutia watu. Lakini pia, watu walimfuata kwa sababu aligusa mioyo yao. (Luka 24:15, 27, 32) Mwanafunzi wako anahitaji kumwona Yehova akiwa Mtu halisi, ambaye anaweza kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye, na kumwona akiwa Baba yake, Mungu wake, na Rafiki yake. (Zab. 25:4, 5) Wakati wa funzo, msaidie mwanafunzi wako akazie uangalifu sifa nzuri za Mungu wetu. (Kut. 34:5, 6; 1 Pet. 5:6, 7) Haidhuru habari mnayozungumzia, kazia sifa za utu wa Yehova. Msaidie mwanafunzi wako athamini sifa nzuri za Yehova, kama vile upendo, fadhili, na huruma yake. Yesu alisema kwamba “amri ya kwanza na iliyo kuu zaidi” ni ‘mpende Yehova Mungu wako.’ (Mt. 22:37, 38) Jitahidi kuwasaidia wanafunzi wako wasitawishe moyoni mwao upendo wenye kina kumwelekea Mungu.

13. Toa mfano wa jinsi ya kumsaidia mwanafunzi wa Biblia ajifunze kuhusu sifa nzuri za utu wa Yehova.

13 Unapozungumza na mwanafunzi wako, mweleze hisia zako za ndani kabisa kumwelekea Yehova. Kwa kufanya hivyo, huenda ukamsaidia mwanafunzi wako atambue kwamba yeye pia anahitaji kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu, na kujifunza kumpenda. (Zab. 73:28) Kwa mfano, je, kuna sentensi yoyote kwenye chapisho la kujifunzia au kwenye andiko fulani inayofunua jambo fulani kumhusu Yehova—kama vile upendo, hekima, haki, au nguvu zake—ambayo inagusa moyo wako? Mtajie mwanafunzi wako jambo hilo, na umwambie kwamba hilo ni kati ya mambo mengi yanayokufanya umpende Baba yetu wa mbinguni. Kuna jambo lingine ambalo kila mwanafunzi wa Biblia anahitaji kufanya ili afikie hatua ya ubatizo.

MTIE MOYO AHUDHURIE MIKUTANO YA KUTANIKO

Mtie moyo mwanafunzi wako aanze kuhudhuria mikutano mapema iwezekanavyo! (Tazama fungu la 14 na 15)

14. Andiko la Waebrania 10:24, 25 linatuambia jambo gani kuhusu mikutano, ambalo litamsaidia mwanafunzi wa Biblia afanye maendeleo ya kiroho?

14 Sote tungependa wanafunzi wetu wa Biblia wafanye maendeleo na kubatizwa. Njia moja muhimu tunayoweza kuwasaidia ni kwa kuwatia moyo wahudhurie mikutano ya kutaniko. Walimu wenye uzoefu wanasema kwamba wanafunzi wanaoanza kuhudhuria mikutano mapema wanafanya maendeleo haraka zaidi. (Zab. 111:1) Baadhi ya walimu huwaambia wanafunzi wao kwamba watapata nusu ya elimu yao ya Biblia kutoka kwenye funzo lao, na nusu nyingine kwenye mikutano. Soma Waebrania 10:24, 25 pamoja na mwanafunzi wako na umweleze faida atakazopata ikiwa atahudhuria mikutano. Mwonyeshe video Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme? * Msaidie mwanafunzi wako aione mikutano kuwa sehemu muhimu ya maisha yake.

15. Tunaweza kufanya nini ili kumtia moyo mwanafunzi ahudhurie mikutano kwa ukawaida?

15 Unaweza kufanya nini ikiwa mwanafunzi wako hajahudhuria mkutano wowote au hahudhurii mikutano kwa ukawaida? Msimulie kwa shauku jambo fulani ulilojifunza kwenye mkutano wa hivi karibuni. Hilo litamchochea zaidi kuliko kumwalika tu kwenye mikutano. Mpe gazeti la Mnara wa Mlinzi au Daftari la Huduma na Maisha ambalo linatumiwa kwenye mikutano. Mwonyeshe habari itakayozungumziwa kwenye mkutano unaofuata na muulize ni sehemu gani inayomvutia zaidi. Mambo ambayo mwanafunzi wako atajionea katika mkutano wake wa kwanza, yatapita mambo yoyote ambayo amewahi kujionea kwenye mikusanyiko mingine ya kidini. (1 Kor. 14:24, 25) Atakutana na watu ambao anaweza kuiga mfano wao mzuri na ambao watamsaidia kufanya maendeleo.

16. Tunahitaji kufanya nini ili kuwasaidia wanafunzi wa Biblia kufikia hatua ya ubatizo, na tutajifunza nini katika makala inayofuata?

16 Tunaweza kuwasaidiaje wanafunzi wa Biblia wafikie hatua ya ubatizo? Tunaweza kumsaidia kila mwanafunzi achukue kwa uzito funzo lake kwa kumtia moyo ajifunze kila juma na kujitayarisha kwa ajili ya kila kipindi cha funzo. Pia, tungependa kumtia moyo awasiliane na Yehova kila siku, na kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja naye. Tungependa kumchochea mwanafunzi wetu ahudhurie mikutano ya kutaniko. (Tazama sanduku “ Mambo Ambayo Mwanafunzi Anahitaji Kufanya ili Afikie Hatua ya Ubatizo.”) Hata hivyo, kama makala inayofuata itakavyoeleza, kuna mambo mengine matano ambayo mwalimu wa Biblia anaweza kufanya ili kumsaidia mwanafunzi afikie hatua ya ubatizo.

WIMBO 76 Unahisije?

^ fu. 5 Kumfundisha mtu jambo fulani, kunamaanisha kumsaidia “afikiri, ahisi, au atende kwa njia mpya au kwa njia tofauti.” Andiko letu la mwaka wa 2020, Mathayo 28:19, limetukumbusha umuhimu wa kujifunza pamoja na watu na kuwafundisha jinsi ya kuwa wanafunzi waliobatizwa wa Yesu Kristo. Katika makala hii na ile inayofuata, tutaona jinsi tunavyoweza kuboresha uwezo wetu wa kufanya kazi hii muhimu sana.

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Ikiwa unazungumza na watu kuhusu Biblia kwa ukawaida na kwa mpangilio hususa, hilo linamaanisha kwamba unaongoza funzo la Biblia. Funzo hilo linaweza kuripotiwa wakati limeongozwa mara mbili baada ya kumwonyesha mwanafunzi jinsi ya kujifunza, na ikiwa kuna sababu ya kuamini kwamba mtu huyo ataendelea kujifunza.

^ fu. 3 Makala hizi zinatia ndani mapendekezo kutoka kwenye mfululizo: “Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo,” unaopatikana kwenye Huduma Yetu ya Ufalme ya Julai 2004 hadi Mei 2005.

^ fu. 9 Tazama video ya dakika nne yenye kichwa Kuwafundisha Wanafunzi Wetu Kujitayarisha. Kwenye JW Library®, nenda kwenye MIDIA > MIKUTANO NA HUDUMA YETU > KUBORESHA USTADI WETU.

^ fu. 10 Nenda kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > VIFAA VYA KUJIFUNZIA BIBLIA.

^ fu. 14 Kwenye JW Library®, nenda kwenye MIDIA > MIKUTANO NA HUDUMA YETU > VIFAA VYA HUDUMA.