Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 42

Jinsi ya Kumsaidia Mwanafunzi wa Biblia Afikie Hatua ya Ubatizo—Sehemu ya Pili

Jinsi ya Kumsaidia Mwanafunzi wa Biblia Afikie Hatua ya Ubatizo—Sehemu ya Pili

“Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako.”​—1 TIM. 4:16.

WIMBO 77 Nuru Katika Ulimwengu Wenye Giza

MUHTASARI *

1. Tunajuaje kwamba kazi ya kufanya wanafunzi inaokoa uhai?

KAZI ya kufanya wanafunzi inaokoa uhai! Tunajuaje? Yesu alipotoa amri inayopatikana kwenye Mathayo 28:19, 20, alisema hivi: “Nendeni, . . . mkafanye wanafunzi . . . , mkiwabatiza.” Tunajua nini kuhusu umuhimu wa kubatizwa? Ikiwa tunataka kuishi milele ni lazima tubatizwe. Yule anayetaka kubatizwa ni lazima aamini kwamba wokovu unawezekana tu kwa sababu Yesu alikufa kifo cha kidhabihu naye alifufuliwa. Hiyo ndiyo sababu mtume Petro aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Ubatizo unawaokoa ninyi sasa . . . kupitia ufufuo wa Yesu Kristo.” (1 Pet. 3:21) Hivyo, mwanafunzi mpya wa Kristo anapobatizwa, anajiweka kwenye njia itakayomwongoza kwenye uzima wa milele.

2. Andiko la 2 Timotheo 4:1, 2 linasema tunapaswa kuwa walimu wa aina gani?

2 Ili kufanya wanafunzi tunahitaji kusitawisha “ustadi wa kufundisha.” (Soma 2 Timotheo 4:1, 2.) Kwa nini? Kwa sababu Yesu alituamuru hivi: “Nendeni, . . . mkafanye wanafunzi . . . , mkiwafundisha.” Mtume Paulo alisema “endelea” kufanya kazi hiyo, “kwa maana ukifanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.” Hivyo, Paulo alikuwa na sababu nzuri aliposema: “Angalia daima . . . kufundisha kwako.” (1 Tim. 4:16) Kwa kuwa kufundisha kunahusiana moja kwa moja na kufanya wanafunzi, tungependa ufundishaji wetu uwe bora kabisa.

3. Katika makala hii, tutachunguza nini kuhusu kuongoza mafunzo ya Biblia?

3 Tunawafundisha kwa ukawaida mamilioni ya watu kweli zinazopatikana kwenye Biblia. Lakini kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, tunataka kujua jinsi tunavyoweza kuwasaidia wengi kati ya watu hao wawe wanafunzi wa Kristo waliobatizwa. Katika makala hii, tutachunguza mambo mengine matano ambayo kila mwalimu anahitaji kufanya ili kumsaidia mwanafunzi afanye maendeleo na kufikia hatua ya ubatizo.

TUMIA BIBLIA UNAPOFUNDISHA

Mwombe mwalimu mwenye uzoefu akusaidie kuboresha ustadi wako wa kutumia Biblia unapofundisha (Tazama fungu la 4 hadi 6) *

4. Kwa nini ni lazima mwalimu awe na sifa ya kujizuia anapoongoza funzo la Biblia? (Tazama pia maelezo ya chini.)

4 Tunapenda mambo tunayofundisha kutoka katika Neno la Mungu. Hivyo, huenda tukashawishika kuzungumza kwa kirefu kuhusu mambo tunayopenda. Hata hivyo, iwe tunaongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi, Funzo la Biblia la Kutaniko, au funzo la Biblia la nyumbani, yule anayeongoza hapaswi kuzungumza kupita kiasi. Ili atumie Biblia kwa njia nzuri anapofundisha, mwalimu anapaswa kuwa na sifa ya kujizuia ili asifafanue kila kitu anachojua kuhusu habari au mstari fulani wa Biblia. * (Yoh. 16:12) Linganisha ujuzi wa Biblia uliokuwa nao wakati ulipobatizwa na ujuzi ulio nao sasa. Inaelekea wakati huo ulijua tu mafundisho ya msingi. (Ebr. 6:1) Ilikuchukua miaka mingi kujifunza mambo unayojua sasa, kwa hiyo usijaribu kumfundisha mwanafunzi mpya kila kitu kwa wakati mmoja.

5. (a) Kulingana na 1 Wathesalonike 2:13, tunataka mwanafunzi wetu aelewe nini anapojifunza? (b) Tunaweza kumtiaje moyo mwanafunzi azungumzie mambo anayojifunza?

5 Tunataka mwanafunzi wetu aelewe kwamba mambo anayojifunza yanatoka katika Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho takatifu. (Soma 1 Wathesalonike 2:13.) Tunaweza kufanyaje hivyo? Mtie moyo mwanafunzi azungumzie mambo anayojifunza. Badala ya sikuzote kumfafanulia maana ya mistari ya Biblia, mwombe akueleze jinsi anavyoelewa baadhi ya mistari hiyo. Msaidie mwanafunzi aone jinsi Neno la Mungu linavyomhusu yeye binafsi. Muulize maswali ya maoni na maswali yatakayomsaidia kufikiri—ili aeleze jinsi anavyofikiri na kuhisi kuhusu maandiko anayosoma. (Luka 10:25-28) Kwa mfano, unaweza kumuuliza hivi: “Andiko hili limekusaidiaje kuona mojawapo ya sifa za Yehova?” “Mambo haya uliyojifunza kutoka katika Biblia yanaweza kukusaidiaje?” “Unahisije kuhusu mambo uliyojifunza?” (Met. 20:5) Jambo muhimu zaidi si wingi wa mambo ambayo mwanafunzi anajua, bali, ni kwa kiwango gani anapenda na kutumia mambo anayojua.

6. Kwa nini huenda ikafaa kuambatana na mwalimu mwenye uzoefu kwenye funzo letu la Biblia?

6 Unapoongoza funzo la Biblia, je, wewe huandamana na wahubiri ambao ni walimu wenye uzoefu? Ikiwa unafanya hivyo, unaweza kuwauliza maoni yao kuhusu jinsi unavyoongoza funzo hilo na ikiwa unatumia Biblia vizuri unapofundisha. Ni lazima uwe mnyenyekevu ikiwa unataka kuboresha ustadi wako wa kufundisha. (Linganisha Matendo 18:24-26.) Baada ya hapo, muulize mhubiri huyo ikiwa anafikiri kwamba mwanafunzi anaelewa kweli anazojifunza. Pia, unaweza kumwomba mhubiri huyohuyo aongoze funzo hilo ikiwa hautakuwepo kwa juma moja au zaidi. Jambo hilo litafanya mwanafunzi ajifunze kwa ukawaida na litamsaidia aone umuhimu wa funzo lake. Usihisi kamwe kwamba hilo ni funzo “lako tu” na hakuna mtu mwingine anayeweza kuliongoza. Isitoshe, ungependa mwanafunzi wako afaidike, na aendelee kujifunza mengi zaidi kuhusu kweli.

FUNDISHA KWA SHAUKU NA USADIKISHO

Msimulie mwanafunzi wako kuhusu mifano halisi ya watu ili kumsaidia aelewe jinsi ya kutumia kanuni za Biblia (Tazama fungu la 7 hadi 9) *

7. Ni nini kitakachomsaidia mwanafunzi afurahie mambo anayojifunza?

7 Mwanafunzi wako anahitaji kuona shauku na usadikisho wako kuhusu kweli zinazopatikana katika Biblia. (1 The. 1:5) Kisha inaelekea atafurahia zaidi mambo ambayo anajifunza. Ikifaa, mweleze jinsi ambavyo kuishi kulingana na kanuni za Biblia kumekusaidia wewe binafsi. Halafu atatambua kwamba Biblia ina miongozo hususa ambayo inaweza kumnufaisha yeye pia.

8. Unaweza kufanya jambo gani lingine ili kumsaidia mwanafunzi wako, na kwa nini ufanye hivyo?

8 Mnapojifunza Biblia mwambie mwanafunzi wako kuhusu mifano ya watu halisi ambao walikabili changamoto kama zake na wakafaulu kuzishinda. Unaweza kuandama na mtu fulani kutanikoni ambaye mfano wake unaweza kumnufaisha mwanafunzi wako. Au unaweza kutafuta simulizi lenye kutia moyo kwenye jw.org katika mfululizo, “Biblia Inabadili Maisha.” * Makala na video kama hizo zitamsaidia mwanafunzi wako aone hekima ya kutumia kanuni za Biblia maishani mwake.

9. Unaweza kumtiaje moyo mwanafunzi ashiriki mambo anayojifunza pamoja na watu wa familia na marafiki?

9 Ikiwa mwanafunzi wa Biblia amefunga ndoa, je, mwenzi wake pia anajifunza? Ikiwa sivyo, mkaribishe mwenzi wake kwenye funzo. Mtie moyo mwanafunzi wako ashiriki mambo anayojifunza na watu wa familia yake na marafiki. (Yoh. 1:40-45) Jinsi gani? Unaweza kumuuliza hivi: “Unaweza kuwafafanuliaje watu wa familia yako kweli hii?” au “Unaweza kutumia andiko gani ili kumthibitishia rafiki yako jambo hili?” Kwa kufanya hivyo, utakuwa ukimzoeza mwanafunzi wako kuwa mwalimu. Kisha, atakapostahili ataweza kuanza kushiriki katika huduma akiwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Unaweza kumuuliza mwanafunzi ikiwa anamjua mtu yeyote ambaye angependa kujifunza Biblia. Ikiwa kuna yeyote anayemjua, wasiliana na mtu huyo mara moja na kumpendekezea funzo la Biblia. Mwonyeshe video Ni Nini Hutendeka Kwenye Funzo la Biblia? *

MTIE MOYO MWANAFUNZI ATAFUTE MARAFIKI KUTANIKONI

Mtie moyo mwanafunzi atafute marafiki kutanikoni (Tazama fungu la 10 na 11) *

10. Kama inavyoonyesha kwenye 1 Wathesalonike 2:7, 8, mwalimu anaweza kuigaje mfano wa Paulo?

10 Ni lazima mwalimu apendezwe kibinafsi na mwanafunzi wake. Amwone kuwa ndugu au dada yake mtarajiwa wa kiroho. (Soma 1 Wathesalonike 2:7, 8.) Si rahisi kwao kuwaacha marafiki zao ulimwenguni na kufanya mabadiliko yanayohitajika ili kumtumikia Yehova. Tunahitaji kuwasaidia kupata marafiki wa kweli kutanikoni. Mfanye mwanafunzi wako awe rafiki yako kwa kutumia wakati pamoja naye, si wakati wa funzo tu bali pia katika pindi nyingine. Tunapompigia simu, kumwandikia ujumbe mfupi, au kumtembelea kifupi wakati ambao si wa funzo tutaonyesha kwamba tunamjali kikweli.

11. Tungependa wanafunzi wetu wapate nini kutanikoni, na kwa nini?

11 Kuna msemo usemao: “Kijiji chote kinahitajika ili kumlea mtoto vizuri.” Kwa maneno mengine tunaweza kusema: “Kutaniko lote linahusika ili kufanya mwanafunzi wa Kristo.” Hiyo ndiyo sababu walimu wa Biblia wenye matokeo huwatambulisha wanafunzi wao kwa wengine kutanikoni, wanaoweza kuwasaidia wamkaribie Yehova zaidi. Kisha, wanafunzi wanaweza kufurahia kushirikiana na watu wa Mungu ambao wanaweza kuwasaidia kiroho na kihisia. Tungependa kila mwanafunzi ahisi kwamba yeye ni sehemu ya kutaniko na ya familia yetu ya kiroho. Tunataka avutiwe na undugu wetu wa Kikristo wenye upendo mchangamfu. Kisha, itakuwa rahisi zaidi kwake kuacha kushirikiana kwa ukaribu na watu ambao hawamsaidii kumpenda Yehova. (Met. 13:20) Ikiwa rafiki zake wa awali wataacha kushirikiana naye, atajua kwamba anaweza kupata marafiki wa kweli katika tengenezo la Yehova.—Marko 10:29, 30; 1 Pet. 4:4.

KAZIA LENGO LA KUJIWEKA WAKFU NA KUBATIZWA

Hatua kwa hatua, mwanafunzi mnyoofu wa Biblia anaweza kufikia lengo la kubatizwa! (Tazama fungu la 12 na 13)

12. Kwa nini tunapaswa kuzungumza na mwanafunzi wetu kuhusu kujiweka wakfu na kubatizwa?

12 Uwe ukizungumza waziwazi na mwanafunzi wako kuhusu umuhimu wa kujiweka wakfu na kubatizwa. Tunapoongoza funzo la Biblia, lengo letu ni kumsaidia mtu awe mwanafunzi wa Kristo aliyebatizwa. Baada ya kujifunza naye kwa ukawaida kwa miezi michache, na hasa baada ya kuanza kuhudhuria mikutano, mwanafunzi anapaswa kuelewa kwamba kusudi la kujifunza Biblia ni kumsaidia aanze kumtumikia Yehova akiwa mmoja wa Mashahidi Wake.

13. Mwanafunzi anafanya hatua gani anapofanya maendeleo ili afikie hatua ya ubatizo?

13 Hatua kwa hatua, mwanafunzi mnyoofu wa Biblia anaweza kufikia lengo la kubatizwa! Kwanza, mwanafunzi anaanza kumjua na kumpenda Yehova na kujenga imani katika Yehova. (Yoh. 3:16; 17:3) Kisha, mwanafunzi anaanzisha uhusiano na Yehova na anaanza kushirikiana na kutaniko. (Ebr. 10:24, 25; Yak. 4:8) Halafu, mwanafunzi anaacha mazoea mabaya na kutubu dhambi zake. (Mdo. 3:19) Wakati huohuo, imani yake inamchochea awaambie wengine kweli anazojifunza. (2 Kor. 4:13) Kisha, anajiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa kubatizwa. (1 Pet. 3:21; 4:2) Na hiyo ni siku yenye shangwe sana kwa kila mtu! Kadiri mwanafunzi anavyochukua hatua moja baada ya nyingine kuelekea lengo lake, mpongeze kwa ukawaida na kumtia moyo aendelee kusonga mbele.

PINDI KWA PINDI TATHMINI MAENDELEO YA MWANAFUNZI

14. Mwalimu anaweza kutathmini maendeleo ya mwanafunzi jinsi gani?

14 Tunahitaji kuwa wenye subira tunapomsaidia mwanafunzi afanye maendeleo ili afikie hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Lakini wakati utafika ambapo tutahitaji kujua ikiwa ana tamaa ya kumtumikia Yehova Mungu. Je, unaona ishara zinazoonyesha kwamba mwanafunzi anajitahidi kutii amri za Yesu? Au anataka tu kujifunza mambo yanayopendeza kutoka katika Biblia?

15. Ni mambo gani yatakayomsaidia mwalimu kutambua kwamba mwanafunzi anafanya maendeleo?

15 Mara kwa mara, changanua maendeleo ambayo mwanafunzi wako anafanya. Kwa mfano, je, anaeleza hisia zake kumhusu Yehova? Je, anasali kwa Yehova? (Zab. 116:1, 2) Je, anafurahia kusoma Biblia? (Zab. 119:97) Je, anahudhuria mikutano kwa ukawaida? (Zab. 22:22) Je, amefanya mabadiliko yoyote katika mtindo wake wa maisha? (Zab. 119:112) Je, ameanza kuwaeleza watu wa familia na marafiki mambo anayojifunza? (Zab. 9:1) Jambo muhimu hata zaidi, je, anataka kuwa Shahidi wa Yehova? (Zab. 40:8) Ikiwa mwanafunzi wa Biblia hafanyi maendeleo katika lolote kati ya mambo hayo, kwa busara jaribu kujua sababu na kisha zungumzia jambo hilo pamoja naye kwa fadhili lakini waziwazi. *

16. Ni mambo gani yanayoweza kukusaidia kujua ikiwa unapaswa kusitisha funzo la Biblia?

16 Pindi kwa pindi, tathmini ikiwa unapaswa kuendelea kujifunza na mtu. Jiulize hivi: ‘Je, mwanafunzi hajitayarishi kwa ajili ya funzo? Je, hataki kuhudhuria mikutano? Je, bado ana mazoea mabaya? Je, bado ni mshiriki wa dini ya uwongo?’ Ikiwa jibu ni ndiyo, kuendelea kujifunza na mtu kama huyo ni kama kujaribu kumfundisha kuogelea mtu ambaye hataki hata kugusa maji! Ikiwa mwanafunzi hathamini kutoka moyoni mambo anayojifunza na hayuko tayari kufanya mabadiliko, kwa nini uendelee kujifunza naye?

17. Kulingana na 1 Timotheo 4:16, ni lazima walimu wote wa Biblia wafanye nini?

17 Tunachukua kwa uzito jukumu letu la kufanya wanafunzi, na tungependa kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia wafikie hatua ya ubatizo. Hiyo ndiyo sababu tutafundisha kwa kutumia Biblia na kwa usadikisho. Tutawatia moyo wanafunzi wetu watafute marafiki kutanikoni. Tutakazia lengo la kujiweka wakfu na kubatizwa, huku pindi kwa pindi tukitathmini maendeleo ya mwanafunzi. (Tazama sanduku “ Mambo Ambayo Mwalimu Anahitaji Kufanya ili Kumsaidia Mwanafunzi Afikie Hatua ya Ubatizo.” Tunafurahi kwamba tunaweza kushiriki katika kazi hii inayookoa uhai! Acheni tuazimie kufanya yote tuwezayo ili kuongoza mafunzo ya Biblia yanayofanya maendeleo na kufikia hatua ya ubatizo.

WIMBO 79 Wafundishe Kusimama Imara

^ fu. 5 Tunapoongoza mafunzo ya Biblia tuna pendeleo la kuwasaidia watu wajifunze jinsi Yehova anavyotaka wafikiri, wahisi, na kutenda. Makala hii itatufafanulia zaidi jinsi tunavyoweza kuboresha ustadi wetu wa kufundisha.

^ fu. 4 Tazama makala “Epuka Mitego Hii Unapoongoza Funzo la Biblia” kwenye Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha la Septemba 2016.

^ fu. 8 Nenda kwenye KUTUHUSU > MASIMULIZI.

^ fu. 9 Kwenye JW Library®, nenda kwenye MIDIA > MIKUTANO NA HUDUMA YETU > VIFAA VYA HUDUMA.

^ fu. 15 Tazama makala, “Upendo na Uthamini Wetu kwa Yehova Hutuchochea Kubatizwa” na “Je, Uko Tayari Kubatizwa?” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 2020.

^ fu. 77 MAELEZO YA PICHA: Muda fulani baada ya funzo, dada mwenye uzoefu anamsaidia dada aliyekuwa akiongoza funzo atambue jinsi anavyoweza kuepuka kuzungumza kupita kiasi wakati wa funzo.

^ fu. 79 MAELEZO YA PICHA: Wakati wa funzo, mwanafunzi anajifunza jinsi ya kuwa mke bora. Baadaye, anamwambia mume wake mambo ambayo amejifunza.

^ fu. 81 MAELEZO YA PICHA: Mwanafunzi na mume wake wanafurahia ushirika katika nyumba ya mmoja wa marafiki aliokutana nao Jumba la Ufalme.