Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

1921—Miaka Mia Moja Iliyopita

1921—Miaka Mia Moja Iliyopita

“KWA hiyo, ni kazi gani hususa ambayo tunatarajia kufanya mwaka huu?” Wanafunzi wa Biblia waliuliza swali hilo kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1921. Ili kujibu, lilinukuu andiko la Isaya 61:1, 2, lililowakumbusha kazi yao ya kuhubiri. “BWANA amenitia mafuta, niwahubiri wanyenyekevu habari njema . . . . Kutangaza mwaka wa BWANA uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu.”

WAHUBIRI WALIO JASIRI

Ili kutimiza kazi yao ya kuhubiri, Wanafunzi wa Biblia walipaswa kuwa jasiri. Wangehitaji kutangaza “habari njema” kwa wapole, na pia kutangaza “siku ya kisasi” kwa waovu.

Ndugu J. H. Hoskin, aliyeishi nchini Kanada alitoa ushahidi kwa ujasiri licha ya upinzani. Katika kipindi cha majani kuchipuka mwaka wa 1921, alikutana na kasisi wa kanisa la Methodisti. Ndugu Hoskin alianza mazungumzo yake kwa kusema: “Tunapaswa kuwa na mazungumzo mazuri kuhusu Maandiko, na hata ikiwa hatukubaliani katika baadhi ya mambo, tunaweza kumaliza mazungumzo yetu kwa amani na kuendelea kuwa marafiki.” Lakini hilo halikutukia. Ndugu Hoskin anakumbuka hivi: “Tulizungumza kwa dakika chache tu, [kasisi huyo] alipogonga mlango kwa nguvu sana hivi kwamba nilihisi kioo chake kikubwa kingevunjika na kuanguka sakafuni.”

Kasisi huyo alizungumza kwa sauti kubwa akisema: “Kwa nini usiende kwa watu wasio Wakristo na kuzungumza nao?” Ndugu Hoskin hakujibu, lakini alipokuwa akiondoka alijiambia, ‘Nilihisi nilikuwa nikizungumza na mmoja wao!’

Siku iliyofuata kwenye mahubiri yake, kasisi huyo aliendelea na mashambulizi. Ndugu Hoskin alikumbuka hivi: “Aliwaonya wafuasi wake kunihusu, akiwaambia watu kwamba nilikuwa tapeli mbaya sana kuwahi kutokea kwenye mji huo, na kwamba nilipaswa kupigwa risasi.” Lakini Ndugu Hoskin hakuyumbishwa hata kidogo, aliendelea kuhubiri na alipata matokeo mazuri. Ndugu Hoskin alisema hivi: “Nilifurahia sana kuhubiri hapo. Baadhi ya watu hata walipaza sauti wakisema hivi, ‘Ninajua wewe ni mtu wa Mungu!’ na waliuliza ikiwa wangeweza kunisaidia na kunipatia vitu ninavyohitaji.”

FUNZO LA KIBINAFSI NA LA FAMILIA

Ili kuwasaidia watu wafanye maendeleo, Wanafunzi wa Biblia walichapisha programu ya kujifunzia Biblia kwenye gazeti The Golden Age. * Programu ya vijana ya kujifunza Biblia ilikuwa na maswali kwa ajili ya wazazi ambayo wangejadili na watoto wao. Wazazi walihitaji “kuwauliza watoto wao maswali hayo na kuwasaidia kupata majibu katika Biblia.” Baadhi ya maswali kama vile, “Kuna vitabu vingapi katika Biblia?,” yaliwafundisha mambo ya msingi. Maswali mengine kama vile, “Je, kila Mkristo wa kweli anapaswa kutarajia mateso ya aina fulani?,” yaliwatayarisha vijana wawe wahubiri jasiri.

Programu ya kujifunza zaidi katika kitabu Divine Plan of The Ages iliwapatia Wanafunzi wa Biblia waliokomaa maswali yenye kuchochea fikira yaliyotegemea buku la kwanza la kitabu Studies in the Scriptures. Maelfu ya wasomaji walinufaika kutokana na programu hizo, lakini gazeti The Golden Age la Desemba 21, 1921, lilitangaza kwamba programu hizo zote zingesitishwa. Kwa nini kulikuwa na badiliko hilo la ghafla?

KITABU KIPYA!

Kitabu The Harp of God

Kadi ikiwa na mgawo wa usomaji

Kadi zenye maswali

Ndugu waliokuwa wakiongoza walitambua kwamba Wanafunzi wapya wa Biblia walihitaji kujifunza kweli za msingi kwa utaratibu mzuri. Hivyo, kitabu The Harp of God kilitolewa Novemba 1921. Watu waliopendezwa na kukubali kitabu hicho waliandikishwa kwa ajili ya mafunzo ya Biblia ya kitabu The Harp of God. Mafunzo hayo ambayo wasomaji walijiongoza wenyewe, yaliwasaidia kutambua “mpango wa Mungu wa kuwabariki wanadamu kwa uzima wa milele.” Mafunzo hayo yalifanyikaje?

Mtu alipokubali nakala ya kitabu hicho, alipewa mgawo wa kusoma uliochapishwa kwenye kadi ndogo. Juma lililofuata, alipokea kadi yenye maswali yaliyotegemea mgawo huo. Kadi hiyo ilimalizia kwa kutoa mgawo wa usomaji kwa ajili ya juma lililofuata.

Kila juma kwa majuma 12, mwanafunzi alipokea kadi mpya kutoka kwa kikundi au kutaniko lililo karibu. Mara nyingi kadi hizo zilitumwa na ndugu na dada wenye umri mkubwa au ambao hali zao hazikuwaruhusu kufanya mengi. Kwa mfano, Anna K. Gardner, kutoka Millvale, Pennysylvania, Marekani, anakumbuka hivi: “Kitabu The Harp of God kilipotoka, kilimpatia Thayle, dada yangu aliyekuwa na tatizo la kutembea, kazi zaidi ambayo angeweza kufanya, yaani, kutuma kila juma kadi za maswali.” Mafunzo yalipokamilika, mwanafunzi alitembelewa kibinafsi ili kumsaidia aendelee na elimu yake ya Biblia.

Thayle Gardner akiwa katika kigari chake cha magurudumu

KAZI ILIYOKUWA MBELE

Mwishoni mwa mwaka huo, Ndugu J. F. Rutherford alituma barua kwa vikundi vyote. Alisema kwamba “ushahidi kuhusu Ufalme uliotolewa mwaka huu umekuwa mkubwa zaidi na wenye matokeo zaidi kuliko uliotolewa katika mwaka mwingine wowote katika kipindi cha mavuno.” Kisha aliongezea hivi: “Bado kuna kazi kubwa ya kufanya. Watieni moyo wengine wajiunge katika utumishi huu uliobarikiwa.” Ni wazi kwamba Wanafunzi wa Biblia walitumia ushauri huo. Katika mwaka wa 1922, wangeutangaza Ufalme kwa ujasiri na kwa njia ya pekee sana.

^ fu. 9 Gazeti The Golden Age lilibadilishwa jina na kuwa Consolation mwaka wa 1937, na baadaye Amkeni! mwaka wa 1946.