Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujenga Upya Urafiki Wako Pamoja na Yehova

Kujenga Upya Urafiki Wako Pamoja na Yehova

KILA mwaka, kondoo wengi wenye thamani wanarudishwa katika kutaniko la Kikristo. Wazia ‘shangwe kubwa inayokuwa mbinguni’ wakati kila mmoja anaporudi! (Luka 15:7, 10) Ikiwa umerudishwa kutanikoni, uwe na hakika kwamba Yesu, malaika, na Yehova mwenyewe wanafurahi kuona ukichukua tena msimamo upande wa kweli. Hata hivyo, unapojenga upya urafiki wako pamoja na Yehova, huenda ukakabili changamoto. Baadhi ya changamoto hizo ni zipi, na ni nini kinachoweza kukusaidia?

UTAKABILI CHANGAMOTO GANI?

Baada ya kurudi kutanikoni, ndugu na dada wengi wanapambana na hisia zisizofaa. Huenda unaelewa jinsi Mfalme Daudi alivyohisi. Hata baada ya kusamehewa dhambi zake, alisema hivi: “Makosa yangu . . .  yananilemea.” (Zab. 40:12; 65:3) Baada ya mtu kumrudia Yehova, huenda akahisi hatia au kuaibika kwa miaka mingi. Isabelle, alitengwa na ushirika kwa zaidi ya miaka 20. * Alisema hivi: “Ilikuwa vigumu sana kwangu kuamini kwamba Yehova anaweza kunisamehe.” Ikiwa utavunjika moyo, unaweza kudhoofika kiroho tena. (Met. 24:10) Jitahidi kutoruhusu jambo hilo litukie.

Wengine wanahofu kwamba hawatafaulu kufanya yote yanayohusika katika kurudisha uhusiano wao pamoja na Yehova. Antoine, alisema hivi baada ya kurudishwa: “Nilihisi kwamba nimesahau kila kitu kuhusu maisha yangu ya awali nikiwa Mkristo.” Kwa sababu ya hisia kama hizo, huenda baadhi ya watu wakasita kujihusisha kikamili katika utendaji wa kiroho.

Kwa mfano, mtu ambaye nyumba yake anayoipenda inapoharibiwa sana na kimbunga, huenda akahisi kulemewa anapofikiria nguvu na jitihada zinazohitajika ili kuijenga upya. Vivyo hivyo, ikiwa uhusiano wako pamoja na Yehova uliharibika kwa sababu ya dhambi nzito, huenda ukahisi kwamba jitihada kubwa sana inahitajika ili uwe tena na hali nzuri ya kiroho. Hata hivyo, msaada unapatikana.

Yehova anatoa mwaliko huu: “Sasa, njooni, na tunyooshe mambo kati yetu.” (Isa. 1:18) Tayari umefanya jitihada kubwa ili ‘kunyoosha mambo.’ Yehova anakupenda kwa kufanya jitihada hizo. Hebu wazia: Umempa Yehova msingi wa kujibu kwa uthabiti shutuma za Shetani!​—Met. 27:11.

Kwa kufanya hivyo, tayari umemkaribia zaidi Yehova, naye anaahidi kufanya vivyo hivyo. (Yak. 4:8) Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika kuliko kutambuliwa tu na wengine kuwa wewe ni sehemu ya kutaniko tena. Unahitaji kuendelea kuimarisha upendo wako kwa Baba na Rafiki yako, Yehova. Unaweza kufanyaje hivyo?

JIWEKEE MALENGO UNAYOWEZA KUYAFIKIA

Jitahidi kujiwekea malengo unayoweza kufikia. Kumbuka kwamba msingi wako wa kiroho, yaani, ujuzi wako kumhusu Yehova na ahadi zake za wakati ujao, ulibaki kama ulivyo. Lakini jengo, yaani, maisha yako ya Kikristo, linahitaji kujengwa upya, na hilo linatia ndani kuhubiri habari njema na kushirikiana kwa ukawaida na ndugu na dada zako. Fikiria malengo yafuatayo.

Zungumza na Yehova kwa ukawaida. Baba yako anaelewa kwamba unapoendelea kuhisi hatia inaweza kuwa vigumu kwako kusali kwake. (Rom. 8:26) Hata hivyo, ‘dumu katika sala,’ ukimweleza Yehova ni kwa kadiri gani unataka kuwa rafiki yake. (Rom. 12:12) Andrej anakumbuka hivi: “Nilihisi hatia sana na kuaibika. Lakini baada ya kila sala niliyotoa, hisia hizo zilipungua. Nilipata utulivu mwingi zaidi wa akili.” Ikiwa hujui usali kuhusu nini, fikiria sala za Mfalme Daudi aliyetubu, zinazopatikana kwenye Zaburi ya 51 na 65.

Jifunze Biblia kwa ukawaida. Kufanya hivyo kutakuimarisha kiroho na kusaidia upendo wako kwa Yehova uongezeke. (Zab. 19:7-11) Felipe anasema hivi: “Kutokuwa na ratiba nzuri ya kiroho, ndiyo sababu iliyofanya nidhoofike na kumuumiza Yehova mara ya kwanza. Sikutaka kurudia kosa hilohilo mara ya pili, hivyo niliamua kulifanya funzo langu la kibinafsi liwe ulinzi wangu.” Wewe pia unaweza kufanya hivyo. Ikiwa unahitaji msaada ili uweze kupata habari zinazofaa kwa ajili ya funzo lako la kibinafsi, unaweza kumwomba rafiki yako aliye mkomavu kiroho akusaidie.

Jenga upya urafiki wako pamoja na ndugu na dada zako. Baadhi ya ndugu na dada wanaorudi kutanikoni wanahofu kwamba wengine watawaona kwa njia isiyofaa. Larissa anakiri hivi: “Niliaibika sana. Nilihisi kwamba nilikuwa nimelisaliti kutaniko. Na nilihisi hivyo kwa muda mrefu.” Uwe na hakika kwamba wazee wa kutaniko na ndugu na dada wengine wakomavu kiroho, wako tayari kukusaidia unapojenga upya hali yako ya kiroho. (Tazama sanduku “ Wazee wa Kutaniko Wanaweza Kufanya Nini?”) Wanafurahi kwamba umerudi kutanikoni, na wanataka ufanye vizuri!​—Met. 17:17.

Ni nini kitakachokusaidia kulikaribia zaidi kutaniko? Shiriki kikamili katika mambo ambayo ndugu na dada wanafanya—hudhuria mikutano na kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani. Kufanya hivyo kutakusaidiaje? Felix alisema hivi: “Kutaniko lilikuwa linatazamia kwa hamu nirudi. Nilihisi ninathaminiwa. Wote walinisaidia kuwa sehemu ya familia tena, nihisi nimesamehewa, na kusonga mbele.”—Tazama sanduku “ Wewe Unaweza Kufanya Nini?

USIFE MOYO!

Shetani ataendelea kukuletea “vimbunga” ili kujaribu kukudhoofisha unapokuwa ukijenga upya urafiki wako pamoja na Yehova. (Luka 4:13) Jitayarishe kwa kuimarisha nyumba yako ya kiroho sasa.

Kuhusu kondoo wake, Yehova anaahidi hivi: “Aliyepotea nitamtafuta, anayetangatanga nitamrudisha, aliyejeruhiwa nitamfunga, na aliye dhaifu nitamtia nguvu.” (Eze. 34:16) Yehova amewasaidia wengine wengi warudishe tena uhusiano wao mzuri pamoja naye. Uwe na hakika kwamba anataka kukusaidia wewe pia uendelee kuimarisha hata zaidi uhusiano wako pamoja naye.

^ fu. 4 Majina katika makala hii yamebadilishwa.