Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 40

Toba ya Kweli Ni Nini?

Toba ya Kweli Ni Nini?

‘Nimekuja kuwahimiza watenda dhambi watubu.’​—LUKA 5:32.

WIMBO 36 Tuulinde Moyo Wetu

MUHTASARI *

1-2. Ahabu na Manase walitofautianaje, na tutachunguza maswali gani?

 ACHENI tuwachunguze kwa ukaribu wafalme wawili walioishi nyakati za kale. Mmoja alitawala ufalme wa Israeli wa makabila kumi, na mwingine ufalme wa Yuda wa makabila mawili. Ingawa waliishi nyakati tofauti, walifanana kwa njia nyingi. Wafalme wote wawili walimwasi Yehova na kuwapotosha watu wake. Wote wawili waliabudu sanamu na walikuwa wauaji. Hata hivyo, kulikuwa na tofauti kati ya wanaume hao wawili. Mmoja aliendelea na njia yake ya uovu hadi mwisho wa maisha yake, lakini mwingine alitubu, naye akasamehewa matendo yake maovu. Wafalme hao ni nani?

2 Majina yao ni Ahabu, mfalme wa Israeli, na Manase, mfalme wa Yuda. Tofauti zilizopo kati ya wanaume hao zinaweza kutufundisha mambo mengi kuhusu somo muhimu sana—toba. (Mdo. 17:30; Rom. 3:23) Toba ni nini, nayo inaonyeshwaje? Tunahitaji kujua habari hizo kwa sababu tunataka Yehova atusamehe tunapotenda dhambi. Ili kupata majibu ya maswali hayo, tutachunguza maisha ya wafalme hao wawili na tutaona mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wao. Kisha, tutachunguza mambo ambayo Yesu alifundisha kuhusu toba.

MAMBO TUNAYOWEZA KUJIFUNZA KUTOKA KWA MFALME AHABU

3. Ahabu alikuwa mfalme wa aina gani?

3 Ahabu alikuwa mfalme wa saba wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Alimwoa Yezebeli, binti ya mfalme wa Sidoni, taifa tajiri lililokuwa upande wa kaskazini. Huenda ndoa hiyo ilileta utajiri mwingi katika taifa la Israeli. Lakini pia, iliharibu hata zaidi uhusiano wa taifa hilo pamoja na Yehova. Yezebeli alikuwa mwabudu wa Baali, na alimchochea Ahabu aendeleze dini hiyo yenye kuchukiza, iliyohusisha ukahaba wa hekaluni na hata kutoa dhabihu za watoto. Yezebeli alipokuwa malkia hakuna nabii wa Yehova aliyekuwa salama. Aliagiza manabii wengi wauawe. (1 Fal. 18:13) Na Ahabu mwenyewe “alikuwa mwovu sana machoni pa Yehova kuliko wote waliomtangulia.” (1 Fal. 16:30) Yehova aliyaona matendo ya Ahabu na Yezebeli. Hata hivyo, kwa rehema, Yehova alimtuma nabii Eliya ili awaonye watu Wake waache matendo yao mabaya kabla haijawa kuchelewa mno. Lakini Ahabu na Yezebeli hawakusikiliza.

4. Ahabu alipewa hukumu gani, naye aliitikiaje?

4 Mwishowe, subira ya Yehova ilifikia kikomo. Alimtuma Eliya akatoe hukumu dhidi ya Ahabu na Yezebeli. Nasaba yao yote ingefutiliwa mbali. Maneno ya Eliya yalimshtua sana Ahabu! Kwa kushangaza, mwanamume huyo mwenye kiburi ‘akajinyenyekeza.’​—1 Fal. 21:19-29.

Kwa sababu hakuwa ametubu kikweli, Mfalme Ahabu alimtupa gerezani nabii wa Mungu (Tazama fungu la 5 na 6) *

5-6. Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba Ahabu hakutubu kikweli?

5 Ingawa Ahabu alijinyenyekeza pindi hiyo, matendo yake yaliyofuata yalionyesha kwamba hakuwa ametubu kikweli. Hakujitahidi kuondoa ibada ya Baali katika ufalme wake. Na hakuendeleza ibada ya Yehova. Ahabu alionyesha kwamba hakuwa ametubu katika njia nyingine pia.

6 Baadaye, Ahabu alipomwalika mfalme mzuri Yehoshafati wa Yuda ajiunge naye katika vita dhidi ya Wasiria, Yehoshafati alipendekeza kwamba watafute kwanza ushauri wa nabii wa Yehova. Mwanzoni, Ahabu alikataa pendekezo lake, akisema: “Bado kuna mtu mmoja ambaye tunaweza kumwomba ushauri kutoka kwa Yehova; lakini ninamchukia, kwa maana hatabiri kamwe mambo mema kunihusu, ila mabaya tu.” Hata hivyo, walitafuta ushauri kwa nabii Mikaya. Kama tu Ahabu alivyosema, nabii wa Mungu alitabiri mambo mabaya kumhusu! Badala ya kutubu na kutafuta msamaha wa Yehova, mfalme mwovu Ahabu alimtupa nabii huyo gerezani. (1 Fal. 22:7-9, 23, 27) Ingawa mfalme huyo alifaulu kumtupa gerezani nabii wa Yehova, hangeweza kuzuia unabii huo kutimia. Katika pambano lililofuata, Ahabu aliuawa.​—1 Fal. 22:34-38.

7. Yehova alimfafanuaje Ahabu baada ya kifo chake?

7 Baada ya Ahabu kufa, Yehova alifunua jinsi alivyomwona mwanamume huyo. Mfalme mzuri Yehoshafati aliporudi nyumbani akiwa salama, Yehova alimtuma nabii Yehu akamkemee kwa sababu ya kushirikiana na Mfalme Ahabu. Nabii wa Yehova alisema hivi: “Je, unapaswa kuwasaidia waovu, na je, unapaswa kuwapenda wale wanaomchukia Yehova?” (2 Nya. 19:1, 2) Fikiria jambo hili: Ikiwa Ahabu alikuwa ametubu kikweli, ni wazi kwamba nabii huyo asingemwita Ahabu mwanamume mwovu aliyemchukia Yehova. Ni wazi kwamba ingawa Ahabu kwa kadiri fulani alionyesha kwamba amejutia kosa lake, hakuwa ametubu kikweli.

8. Kisa cha Ahabu kinatufundisha nini kuhusu toba?

8 Tunajifunza nini kutoka kwa Ahabu? Aliposikia ujumbe wa Eliya kuhusu msiba ambao ungeipata nasaba yake, mwanzoni Ahabu alijinyenyekeza. Huo ulikuwa mwanzo mzuri. Lakini matendo yake ya baadaye yalionyesha kwamba hakuwa ametubu kutoka moyoni. Hivyo, ni lazima toba ihusishe mengi zaidi ya kuonyesha sikitiko la muda mfupi. Acheni tuchunguze mfano mwingine utakaotusaidia kuelewa toba ya kweli inahusisha nini.

MAMBO TUNAYOWEZA KUJIFUNZA KUTOKA KWA MFALME MANASE

9. Manase alikuwa mfalme wa aina gani?

9 Karne mbili hivi baadaye, Manase alikuja kuwa mfalme wa Yuda. Huenda alikuwa mfalme mbaya hata zaidi kuliko Ahabu! Tunasoma hivi: “Alitenda kwa kiwango kikubwa sana mambo maovu machoni pa Yehova, na kumkasirisha.” (2 Nya. 33:1-9) Manase alijenga madhabahu kwa ajili ya miungu ya kipagani na hata kuweka sanamu ya kuchongwa ya mti mtakatifu—ambao huenda ni ishara ya ibada ya ngono—ndani kabisa ya hekalu takatifu la Yehova! Alifanya uchawi, uaguzi, na ulozi. Pia, “alimwaga damu nyingi sana isiyo na hatia.” Mauaji ya kikatili aliyofanya yalitia ndani ‘kuwateketeza motoni wanawe mwenyewe,’ wakiwa dhabihu kwa miungu ya uwongo.​—2 Fal. 21:6, 7, 10, 11, 16.

10. Yehova alimtiaje nidhamu Manase, na mfalme huyo aliitikiaje?

10 Kama Ahabu, Manase alipuuza kwa ukaidi maonyo ambayo Yehova alimpatia kupitia manabii Wake. Mwishowe, “Yehova akawaleta wakuu wa jeshi la mfalme wa Ashuru ili wawashambulie [Yuda], nao wakamkamata Manase kwa kulabu na kumfunga kwa pingu mbili za shaba na kumpeleka Babiloni.” Akiwa gerezani katika nchi ya kigeni, inaonekana Manase alitafakari mambo kwa uzito. Naye “akaendelea kujinyenyekeza sana mbele za Mungu wa mababu zake.” Na alifanya mengi hata zaidi. “Alimsihi Yehova Mungu wake amwonyeshe kibali.” Isitoshe, Manase “aliendelea kusali kwa Mungu.” Mwanamume huyo mwovu alikuwa akibadilika. Alianza kumwona Yehova kuwa “Mungu wake,” naye aliendelea kusali kwake kwa bidii.​—2 Nya. 33:10-13.

Kwa sababu alikuwa ametubu kikweli, Mfalme Manase alipinga ibada ya uwongo (Tazama fungu la 11) *

11. Kulingana na 2 Mambo ya Nyakati 33:15, 16, Manase alionyeshaje kwamba alikuwa ametubu kikweli?

11 Baada ya muda, Yehova alijibu sala za Manase. Aliona mabadiliko katika moyo wa mwanamume huyo, ambayo yanaonekana pia katika maneno aliyotaja katika sala zake. Yehova aliguswa na maombi ya Manase, naye akamrudishia kiti chake cha ufalme. Manase alitumia fursa hiyo kikamili ili kuonyesha kina cha toba yake. Alifanya jambo ambalo Ahabu hakufanya kamwe. Alibadili mwenendo wake. Alipinga kwa uthabiti ibada ya uwongo na kuendeleza ibada ya kweli. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 33:15, 16.) Kwa hakika, mabadiliko hayo yalihitaji ujasiri na imani, kwa kuwa Manase alikuwa ameathiri vibaya familia yake, wakuu wake, na watu wake kwa miaka mingi. Lakini sasa, katika miaka yake ya mwishoni, Manase alijitahidi kurekebisha baadhi ya matatizo aliyokuwa amesababisha. Inaelekea alimwekea mfano mzuri Yosia, mjukuu wake, ambaye baadaye alikuja kuwa mfalme mzuri sana.​—2 Fal. 22:1, 2.

12. Tunaweza kujifunza nini kuhusu toba kutokana na mfano wa Manase?

12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Manase? Alijinyenyekeza, lakini pia alifanya mengi zaidi. Alisali akisihi aonyeshwe rehema. Na alibadili mwenendo wake. Alijitahidi sana kuondoa madhara aliyokuwa amesababisha, na kufanya yote aliyoweza ili kumwabudu Yehova na kuwasaidia wengine wafanye hivyo pia. Kisa cha Manase kinawapa tumaini hata wale ambao wamefanya mambo maovu sana. Tunaona uthibitisho wenye nguvu kwamba Yehova Mungu “ni mwema na [yuko] tayari kusamehe.” (Zab. 86:5) Wale wanaotubu kikweli, wanaweza kusamehewa.

13. Toa mfano unaotusaidia kuelewa jambo muhimu kuhusu toba.

13 Manase alifanya mengi zaidi ya kusikitika tu kwa sababu ya dhambi zake. Jambo hilo linatufundisha somo muhimu kuhusu toba. Fikiria mfano huu: Unaenda dukani na kuagiza keki. Lakini badala ya muuzaji kukupatia keki anakupatia yai. Je, utaridhika? Bila shaka, la! Je, itasaidia ikiwa muuzaji anakwambia kwamba yai ni kiungo muhimu cha kutengeneza keki? Kwa mara nyingine tena, la! Vivyo hivyo, Yehova anawataka watenda dhambi watubu. Ikiwa mtenda dhambi atasikitika kwa sababu ya dhambi yake, ni jambo jema. Hisia hizo ni kiungo muhimu katika toba, lakini hazitoshi. Ni jambo gani lingine linalohitajika? Tunajifunza mengi zaidi kutokana na mfano wenye kugusa moyo ambao Yesu alifundisha.

JINSI YA KUTAMBUA TOBA YA KWELI

Aliporudiwa na fahamu, mwana mpotevu alifunga safari ndefu ya kurudi nyumbani (Tazama fungu la 14 na 15) *

14. Katika mfano wa Yesu, mwana mpotevu alionyeshaje dalili za kwanza za toba?

14 Yesu alizungumzia simulizi lenye kugusa moyo kuhusu mwana mpotevu, kwenye Luka 15:11-32. Mwanamume fulani kijana alimwasi baba yake, akaondoka nyumbani, na kusafiri “kwenda nchi ya mbali.” Akiwa huko, aliishi maisha yaliyopotoka na ya anasa. Hata hivyo, maisha yalipokuwa magumu, alitafakari kuhusu maisha yake kwa uzito. Alitambua jinsi maisha yalivyokuwa mazuri sana alipokuwa katika nyumba ya baba yake. Yesu alisema kwamba mwanamume huyo kijana ‘alirudiwa na fahamu.’ Akaazimia kurudi nyumbani na kuomba msamaha kwa baba yake. Lilikuwa jambo la muhimu kwa mwana huyo kutambua kwamba alikuwa amefanya maamuzi mengi mabaya. Lakini je, hilo lilitosha? Hapana. Alihitaji kuchukua hatua.

15. Mwana mpotevu katika mfano wa Yesu alionyeshaje toba yake?

15 Mwana mpotevu alionyesha toba ya kweli kwa mambo mabaya aliyokuwa amefanya. Alifunga safari ndefu ya kurudi nyumbani. Kisha, alipomkaribia baba yake alisema hivi: “Nimetenda dhambi dhidi ya mbingu na dhidi yako. Sistahili tena kuitwa mwanao.” (Luka 15:21) Kwa kukiri makosa yake kwa unyoofu, mwanamume huyo alionyesha kwamba alitaka kurudisha uhusiano wake pamoja na Yehova. Pia, alitambua kwamba matendo yake yalimuumiza baba yake. Na alikuwa tayari kufanya kazi kwa bidii ili kupata kibali cha baba yake, hata alikuwa tayari kutendewa kama mmoja wa wafanyakazi wa baba yake! (Luka 15:19) Mfano huo si tu simulizi lenye kugusa moyo. Kanuni zinazopatikana kwenye simulizi hilo, zinaweza kuwasaidia wazee wa kutaniko wanapojitahidi kutambua ikiwa mwamini mwenzao ametubu dhambi yake nzito.

16. Kwa nini huenda ikawa vigumu kwa wazee wa kutaniko kutambua ikiwa mtu ametubu kikweli?

16 Si kazi rahisi kwa wazee wa kutaniko kutambua ikiwa mtu fulani aliyetenda dhambi nzito ametubu kikweli. Kwa nini? Wazee wa kutaniko hawawezi kusoma mioyo, hivyo ni lazima wategemee uthibitisho unaoonekana kwa nje kwamba ndugu yao amebadili kabisa mtazamo wake kuelekea dhambi aliyofanya. Katika visa fulani, inawezekana mtu akawa ametenda dhambi mbaya kwa ufidhuli, bila aibu, hivi kwamba huenda wazee wa kutaniko waliokutana naye wasisadiki kwamba ametubu kikweli.

17. (a) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba kusikitika tu huenda kusitoshe kuonyesha toba ya kweli? (b) Kama inavyofafanuliwa kwenye 2 Wakorintho 7:11, mtu anayetubu kikweli anatarajiwa kufanya nini?

17 Fikiria mfano huu. Ndugu anafanya uzinzi kwa miaka mingi. Badala ya kutafuta msaada, anamficha mwenendo huo mpotovu mke wake, rafiki zake, na wazee wa kutaniko. Mwishowe anagunduliwa. Wazee wa kutaniko wanapomwambia kwamba wana uthibitisho unaoonyesha kwamba amefanya uzinzi, anakubali kosa lake na hata anaonekana kwamba amesikitika sana. Je, hilo linatosha? Kwa kweli, wazee wanaoshughulikia kisa hicho watahitaji kuona mengi zaidi ya kusikitika tu. Si kwamba mwanamume huyo alifanya dhambi mara moja kwa sababu ya uamuzi mbaya, bali alitenda dhambi nzito kwa miaka mingi. Mkosaji huyo hakukiri kosa lake kwa hiari, bali mtu mwingine alifunua dhambi yake. Hivyo, wazee wa kutaniko watahitaji kuona uthibitisho wa mabadiliko ya kweli katika njia ya kufikiri, hisia, na matendo ya mkosaji. (Soma 2 Wakorintho 7:11.) Huenda ikachukua muda mrefu kwa mwanamume huyo kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. Kuna uwezekano mkubwa kwamba ataondolewa katika kutaniko la Kikristo kwa kipindi fulani cha wakati.​—1 Kor. 5:11-13; 6:9, 10.

18. Mtu aliyetengwa na ushirika anaweza kuonyeshaje toba ya kweli, na matokeo yatakuwa nini?

18 Ili kuonyesha kwamba ametubu kikweli, mtu aliyetengwa na ushirika atahudhuria kwa ukawaida mikutano na kufuata shauri la wazee la kuwa na ratiba nzuri ya kusali na kujifunza. Pia, atajitahidi sana kuepuka hali zilizosababisha atende dhambi. Ikiwa atajitahidi kwa bidii kurudisha uhusiano wake pamoja na Yehova, anaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atamsamehe kikamili na kwamba wazee watamrudisha kutanikoni. Bila shaka, wazee wanaposhughulika na mkosaji, watachanganua kila kisa kulingana na hali zake za kipekee na wataepuka kuhukumu kwa ukali.

19. Toba ya kweli inahusisha nini? (Ezekieli 33:14-16)

19 Kama tulivyojifunza, toba ya kweli inahusisha mengi zaidi ya kusema tu kwamba tunasikitika kwa sababu ya dhambi nzito tuliyofanya. Inahusisha mabadiliko ya kweli katika akili na moyo, yanayotuongoza kwenye matendo yanayofaa. Hilo linahusisha kuacha mwenendo huo mbaya na kugeuka ili kutembea tena katika njia za Yehova. (Soma Ezekieli 33:14-16.) Jambo muhimu zaidi kwa mtenda dhambi linapaswa kuwa kurudisha uhusiano wake pamoja na Yehova.

WAHIMIZE WATENDA DHAMBI WATUBU

20-21. Tunaweza kumsaidiaje mtu aliyetenda dhambi nzito?

20 Yesu alifafanua sehemu muhimu ya huduma yake aliposema: ‘Nimekuja kuwahimiza watenda dhambi watubu.’ (Luka 5:32) Sisi pia tunapaswa kuwa na tamaa hiyo. Tuseme tumegundua kwamba rafiki yetu wa karibu ametenda dhambi nzito. Tunapaswa kufanya nini?

21 Ikiwa tutajaribu kuficha dhambi yake, tutakuwa tukimsababishia madhara rafiki yetu. Isitoshe, mara nyingi jitihada hizo hazifanikiwi kwa sababu Yehova anaona. (Met. 5:21, 22; 28:13) Unaweza kumsaidia rafiki yako kwa kumkumbusha kwamba wazee wanataka kumsaidia. Ikiwa rafiki yako atakataa kukiri kosa lake kwa wazee, unapaswa kuwaeleza wazee, kwa kufanya hivyo utaonyesha kwamba kwa kweli unataka kumsaidia. Uhusiano wake pamoja na Yehova uko hatarini!

22. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

22 Namna gani ikiwa mtenda dhambi amefanya dhambi nzito sana, na kwa muda mrefu sana hivi kwamba wazee wakaamua ni lazima atengwe na ushirika? Je, hilo litamaanisha kwamba wamemtendea bila rehema. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi Yehova anavyowatia nidhamu watenda dhambi kwa rehema, na jinsi tunavyoweza kumwiga.

WIMBO 103 Wachungaji​—Zawadi Katika Wanadamu

^ fu. 5 Toba ya kweli inahusisha mengi zaidi ya kusema tu tunasikitika kwa dhambi tuliyotenda. Makala hii itatusaidia kuelewa toba ya kweli inamaanisha nini, kupitia kisa cha Mfalme Ahabu, Mfalme Manase, na mwana mpotevu katika mfano wa Yesu. Pia, itazungumzia mambo ambayo ni lazima wazee wa kutaniko wafikirie wanapochanganua toba ya mwamini mwenzao aliyetenda dhambi nzito.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Kwa hasira, Mfalme Ahabu anawaamuru walinzi wake wakamfunge gerezani Mikaya, nabii wa Yehova.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Mfalme Manase anawaamuru wafanyakazi waharibu sanamu alizokuwa ameziweka hekaluni.

^ fu. 64 MAELEZO YA PICHA: Mwana mpotevu akiwa amechoka baada ya safari ndefu, anafarijika anapoiona nyumba yao kwa mbali..