Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kushindania Baraka za Yehova

Endelea Kushindania Baraka za Yehova

“Wewe umeshindana na Mungu na wanadamu hata ukashinda mwishowe.”​—MWA. 32:28.

NYIMBO: 60, 38

1, 2. Watumishi wa Yehova wanakabili changamoto gani?

TANGU kipindi cha mwanadamu mwaminifu wa kwanza, Abeli, mpaka leo, waabudu washikamanifu wamelazimika kupambana na hali ngumu. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania kwamba “[walivumilia] shindano kubwa chini ya mateso” walipokuwa wakitafuta kibali na baraka za Yehova. (Ebr. 10:32-34) Paulo alilinganisha mapambano ya Wakristo na jitihada za wanamichezo walioshiriki mashindano ya Wagiriki, kama vile mbio, mieleka, na michezo ya ngumi. (Ebr. 12:1, 4) Leo, tuko kwenye shindano la mbio za uzima, na tunakabili wapinzani ambao wanataka kutukengeusha, kututega, kutuangusha, na kunyakua shangwe na thawabu yetu ya wakati ujao.

2 Kwanza, tuna pambano kubwa na tunashindana mweleka na Shetani na ulimwengu wake mwovu. (Efe. 6:12) Ni muhimu tujitahidi ili tusiathiriwe na “ngome zenye nguvu” za ulimwengu huu. Ngome hizo zinahusisha mafundisho, falsafa, na mazoea mabaya, kama vile kujihusisha katika upotovu wa maadili katika ngono, kuvuta sigara, kunywa pombe kupita kiasi, na kutumia dawa za kulevya. Pia, tunapaswa kupambana kila wakati na udhaifu wetu wa kimwili na kuvunjika moyo.—2 Kor. 10:3-6; Kol. 3:5-9.

3. Mungu anatuzoeza jinsi gani kupigana na adui zetu?

3 Je, kweli inawezekana kushinda wapinzani hao na uvutano huo wenye nguvu? Ndiyo, lakini lazima tupambane. Akitumia mfano wa wapiganaji wa ngumi wa nyakati za zamani, Paulo alisema hivi kuhusu pambano lake: “Jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa.” (1 Kor. 9:26) Kama tu ambavyo bondia anapigana na mpinzani wake, sisi pia tunapaswa kuwazuia adui zetu wasitushinde. Yehova anatuzoeza na kutusaidia kwenye pigano letu. Katika Neno lake, ameandaa mwongozo unaoweza kuokoa uhai. Pia, anatusaidia kupitia machapisho yanayotegemea Biblia tunayopokea, mikutano ya Kikristo, na makusanyiko. Je, unatumia mambo unayojifunza? Ukishindwa kufanya hivyo, ni kana kwamba ‘unapiga hewa,’ yaani, hutakuwa ukimpinga adui yako kikamili.

4. Tunaweza kuepukaje kushindwa na uovu?

4 Adui zetu wanaweza kutushambulia wakati ambapo hatutarajii, na kutupiga tunapokuwa dhaifu, kwa hiyo ni lazima tuendelee kuwa macho. Biblia inatuonya hivi: “Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Rom. 12:21) Maneno “usiache ushindwe na uovu” yanaonyesha kwamba tunaweza kuushinda uovu. Tunaweza kushinda ikiwa tutaendelea kupambana. Kinyume cha hilo, tunaweza kushindwa na Shetani, ulimwengu wake mwovu, na kutokamilika kwetu ikiwa hatutakuwa waangalifu na hivyo kuacha kupambana. Usimruhusu kamwe Shetani akufanye ulegeze mikono yako na ukubali kushindwa!—1 Pet. 5:9.

5. (a) Ni nini kinachoweza kutusaidia tuendelee kupambana ili tupate baraka za Mungu? (b) Tutazungumzia mifano gani kutoka kwenye Biblia?

5 Ili wafanikiwe, wale wanaoshindana wanapaswa kukumbuka sababu zinazowafanya wapambane. Ili wapate kibali cha Mungu na baraka zake, wanapaswa kuzingatia uhakikisho tunaosoma katika Waebrania 11:6: “Yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” Kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa ‘kutafuta kwa bidii’ kinaleta wazo la kukaza fikira na kujitahidi sana. (Mdo. 15:17) Maandiko yana mifano mizuri ya wanaume na wanawake waliojitahidi sana ili wapate baraka za Yehova. Yakobo, Raheli, Yosefu, na Paulo walikabili hali zenye kuchosha kimwili na kihisia, lakini walithibitisha kwamba ustahimilivu huleta baraka nyingi. Tunaweza kuwaigaje wapiganaji hao wanne wenye kutokeza?

USTAHIMILIVU HULETA BARAKA

6. Ni nini kilichomsaidia Yakobo aonyeshe ustahimilivu, naye alithawabishwaje? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

6 Mzee wa ukoo Yakobo alipambana na alionyesha ustahimilivu kwa sababu alimpenda Yehova, alithamini mambo ya kiroho, na alikuwa na imani kamili katika ahadi ya Yehova ya kubariki uzao wake. (Mwa. 28:3, 4) Hilo linatusaidia kuelewa kwa nini Yakobo alipokuwa na umri wa miaka 100 hivi alifanya yote awezayo ili apate baraka za Mungu; hata alipigana mweleka na malaika aliyejivika mwili wa kibinadamu. (Soma Mwanzo 32:24-28.) Je, Yakobo alikuwa na nguvu na uvumilivu uliohitajiwa ili kushindana na malaika mwenye nguvu bila msaada wowote? Hapana! Lakini alikuwa mpiganaji aliyejitoa, na alithibitisha kwamba hakuwa tayari kushindwa! Alithawabishwa sana kutokana na ustahimilivu wake. Alipewa jina linalofaa, yaani, Israeli, (linalomaanisha “Anayeshindana na Mungu” au “Mungu Anashindana”). Yakobo alipata thawabu kubwa ambayo sisi pia tunatafuta, yaani, kibali na baraka za Yehova.

7. (a) Raheli alikabili hali gani yenye kufadhaisha? (b) Ni nini kilichomsaidia kuendelea kushindana na hatimaye kubarikiwa?

7 Raheli pia, mke mpendwa wa Yakobo, alikuwa na hamu ya kuona jinsi ambavyo Yehova angetimiza ahadi yake kwa mume wake. Lakini kulikuwa na tatizo ambalo lilionekana kana kwamba haliwezi kutatuliwa. Hakuwa na watoto. Katika siku hizo, hali hiyo ilionwa kuwa yenye kusikitisha sana. Raheli alipataje nguvu za kihisia na kimwili kuendelea kupambana na hali zenye kuvunja moyo na zilizopita kabisa uwezo wake? Alishikilia tumaini lake. Alisali kwa bidii hata zaidi na hivyo kuendelea kushindana. Yehova alisikiliza dua za kutoka moyoni za Raheli, na mwishowe akambariki kwa kumpa watoto. Hiyo ndiyo sababu pindi fulani Raheli alipaaza sauti hivi kwa shangwe: “Nimepigana miereka yenye nguvu . . . Nami nimekuwa mshindi!”—Mwa. 30:8, 20-24.

8. Yosefu alikabili hali gani ngumu kwa muda mrefu, na alituwekea mfano gani kutokana na jinsi alivyotenda?

8 Bila shaka, Yakobo na Raheli walimwekea Yosefu mfano wa kuwa mwaminifu uliomsaidia kukabiliana na majaribu ya imani aliyopata. Yosefu alipokuwa na umri wa miaka 17, maisha yake yalibadilika kabisa. Ndugu zake walimwuza utumwani kwa sababu walimwonea wivu. Baadaye, alilazimika kuvumilia kifungo kisicho cha haki kwa miaka mingi huko Misri. (Mwa. 37:23-28; 39:7-9, 20-21) Yosefu hakukata tamaa; wala hakufunga kinyongo ambacho kingemfanya alipize kisasi. Badala yake, moyoni na akilini alikazia fikira uhusiano wake mzuri na Yehova. (Law. 19:18; Rom. 12:17-21) Mfano wa Yosefu unapaswa kutusaidia. Kwa mfano, hata ikiwa tulilelewa chini ya hali ngumu au hali zetu ni mbaya hivi kwamba tunaelekea kukata tamaa, tunahitaji kuendelea kushindana na kuonyesha ustahimilivu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tukifanya hivyo, Yehova atatubariki.—Soma Mwanzo 39:21-23.

9. Tunapaswa kufanya nini ili tupate baraka za Yehova kama walivyofanya Yakobo, Raheli, na Yosefu?

9 Fikiria hali fulani unayokabili kwa sasa, na ambayo ni kama jaribu kwako. Huenda ni aina fulani ya ukosefu wa haki, ubaguzi, au dhihaka. Au labda jaribu unalokabili ni mashtaka ya uwongo kwa sababu ya kuonewa wivu. Badala ya kuvunjika moyo, kumbuka kilichowasaidia Yakobo, Raheli, na Yosefu waendelee kumtumikia Yehova kwa shangwe. Mungu aliwaimarisha na kuwabariki kwa sababu waliendelea kuonyesha uthamini wenye kina kuelekea mambo ya kiroho. Waliendelea kushindana na kutenda kulingana na sala zao za unyoofu. Tunaishi karibu na mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo; hivyo ni muhimu tuendelee kushika tumaini letu hakika! Je, uko tayari kujitahidi sana na kupambana ili upate kibali cha Yehova?

UWE TAYARI KUSHINDANA ILI UPATE BARAKA

10, 11. (a) Ni mambo gani tunayoweza kufanya ili kushindania baraka za Mungu? (b) Ni nini kitakachotusaidia kufanya maamuzi yanayofaa na kushinda pigano letu dhidi ya kuvunjika moyo na kukengeushwa?

10 Ni hali gani zinazoweza kutulazimu kushindania baraka za Mungu? Kushinda udhaifu fulani ni moja kati ya hali ambazo wengi wamekabili. Wengine wamelazimika kujitahidi sana ili kudumisha maoni yanayofaa kuhusu huduma. Au huenda unahitaji kuendelea kuvumilia licha ya hali mbaya ya afya au upweke. Pia, hatupaswi kupuuza jinsi ambavyo wengine wanapambana sana ili kumsamehe mtu ambaye amewakosea au amewatendea dhambi. Iwe tumemtumikia Yehova kwa muda mrefu au la, sote tunapaswa kupigana dhidi ya mambo ambayo huenda yakaathiri utumishi wetu kwa Mungu, ambaye huwathawabisha waaminifu.

Je, unashindania baraka za Mungu? (Tazama fungu la 10 na 11)

11 Kwa kweli, huenda tukahitaji kupambana sana ili tufanye maamuzi yanayofaa na kufuata mwenendo wa Kikristo. Inakuwa vigumu hata zaidi wakati ambapo moyo wetu wenye hila unatusukuma kuelekea mambo yasiyofaa. (Yer. 17:9) Ukitambua kwamba umeathiriwa kwa njia fulani, usikose kusali ili upate roho takatifu. Sala na roho takatifu zinaweza kukupatia nguvu za kutenda kwa njia inayofaa na hivyo upate baraka za Yehova. Tenda kulingana na sala zako. Jitahidi kusoma Biblia kila siku, kuwa na funzo la kibinafsi, na Ibada ya Familia ya kawaida.—Soma Zaburi 119:32.

12, 13. Wakristo wawili walipata msaada gani wa kudhibiti tamaa zisizofaa?

12 Kuna mifano mingi inayoonyesha jinsi ambavyo Neno la Mungu, roho yake, na machapisho ya Kikristo yamewasaidia Wakristo kushinda tamaa zisizofaa. Kijana mmoja alisoma makala yenye kichwa, “Unawezaje Kushinda Tamaa Mbaya?,” iliyochapishwa kwenye gazeti la Amkeni! la Desemba 8, 2003. Baada ya kusoma, alisema hivi: “Ninapigana kudhibiti mawazo yasiyofaa. Kwenye makala hiyo nilisoma kwamba ‘kwa watu wengi pambano hilo ni kali zaidi,’ na hilo lilifanya nijione kuwa sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote. Nilihisi kwamba sikuwa peke yangu.” Kijana huyo alinufaika pia na makala yenye kichwa: “Je, Mungu Anakubali Ngono Isiyo ya Asili?” kutoka kwenye toleo la Oktoba 8, 2003. Kwenye makala hiyo alisoma kwamba kwa wengine pambano hilo ni “mwiba katika mwili.” (2 Kor. 12:7) Wanapoendelea kupambana ili kudumisha mwenendo wa uadilifu, wanaweza kutazamia wakati ujao mzuri. Alisema hivi: “Kwa sababu hiyo, kila siku inapopita ninahisi kwamba ninaweza kubaki mwaminifu. Ninamshukuru sana Yehova kwa kutumia tengenezo lake kutusaidia kila siku kupambana na mfumo huu mwovu.”

13 Fikiria pia kisa cha dada mmoja kutoka Marekani. Aliandika hivi: “Ningependa kuwashukuru kwa kuendelea kutulisha kile hasa tunachohitaji na kwa wakati unaofaa. Mara nyingi ninahisi kwamba makala hizi ziliandikwa kwa ajili yangu. Kwa miaka mingi nimekuwa nikipambana na tamaa yenye nguvu kuelekea kitu ambacho Yehova anachukia. Nyakati nyingine, ninataka kukata tamaa na kuacha kupambana. Ninajua kwamba Yehova ana rehema na ni mwenye kusamehe, lakini kwa sababu nina tamaa hii mbaya ambayo hata siichukii, ninahisi kwamba sistahili kupokea msaada wake. Pambano hili la kila siku limeathiri sana maisha yangu. . . . Baada ya kusoma makala yenye kichwa: ‘Je, Una “Moyo wa Kumjua” Yehova?’ katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2013, kwa kweli nilihisi kwamba Yehova anataka kunisaidia.”

14. (a) Paulo alihisije kuhusu mapambano yake? (b) Tunaweza kushinda pambano dhidi ya udhaifu wetu wa kimwili jinsi gani?

14 Soma Waroma 7:21-25. Paulo alijua jinsi ilivyo vigumu kupambana dhidi ya tamaa zisizofaa na vilevile udhaifu wa kimwili. Hata hivyo, alikuwa na uhakika kabisa kwamba angeweza kushinda pambano lake kwa kumtegemea Yehova katika sala na kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Namna gani sisi? Tunapoendelea kupambana dhidi ya udhaifu wetu wa kimwili, sisi pia tunaweza kushinda. Jinsi gani? Kwa kumwiga Paulo, kuwa na imani katika fidia, na pia kwa kumtegemea Yehova kikamili badala ya kutegemea nguvu zetu wenyewe.

15. Sala inaweza kutusaidiaje kuendelea kuwa waaminifu na kuvumilia majaribu?

15 Nyakati nyingine, Mungu anaweza kuacha tuonyeshe jinsi ambavyo jambo fulani linatuhangaisha. Kwa mfano, namna gani ikiwa sisi, au mshiriki wa familia anapatwa na ugonjwa mbaya au kutendewa isivyo haki? Tutaonyesha kwamba tunamtegemea Yehova kabisa ikiwa tutamwomba atupe nguvu za kuendelea kuwa waaminifu na atusaidie kudumisha shangwe yetu na usawaziko wa kiroho. (Flp. 4:13) Visa vya watu wengi katika siku za Paulo na siku zetu pia, vinathibitisha kwamba sala inaweza kutusaidia kupata nguvu mpya na ujasiri wa kuendelea kuvumilia.

ENDELEA KUSHINDANIA BARAKA ZA YEHOVA

16, 17. Umeazimia kufanya nini ukiwa mshindanaji?

16 Ibilisi angependa kuona ukikata tamaa na kukubali kushindwa kwa kuacha mikono yako ilegee. Azimia “[kushika] sana yaliyo mazuri.” (1 The. 5:21) Uwe na uhakika kwamba unaweza kushinda pigano dhidi ya Shetani, ulimwengu wake mwovu, na mwelekeo wowote wenye dhambi. Unaweza kufanya hivyo ikiwa utategemea kikamili uwezo wa Mungu wa kukuimarisha.—2 Kor. 4:7-9; Gal. 6:9.

17 Basi, fanya yote uwezayo ili uendelee kupigana. Endelea kupambana. Endelea kushindania baraka za Yehova. Endelea kustahimili. Uwe na uhakika kabisa kwamba Yehova “[atakumwagia] baraka hata kusiwe na uhitaji tena.”—Mal. 3:10.