Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutetea Habari Njema Mbele ya Maofisa Wakuu

Kutetea Habari Njema Mbele ya Maofisa Wakuu

“MTU HUYU ni chombo kilichochaguliwa kwangu ili kupeleka jina langu kwa mataifa na vilevile kwa wafalme.” (Mdo. 9:15) Bwana Yesu alisema maneno hayo kumhusu mwanamume Myahudi aliyegeuka kuwa Mkristo, ambaye baadaye alifahamika kama mtume Paulo.

Mmoja wa “wafalme” hao alikuwa Nero, maliki Mroma. Ungehisije ikiwa ungelazimika kutetea imani yako mbele ya mtawala mwenye mamlaka kama huyo? Wakristo wanatiwa moyo wamwige Paulo. (1 Kor. 11:1) Njia moja ya kufanya hivyo ni kuchunguza jinsi ambavyo Paulo alishughulika na mfumo wa kisheria katika siku zake.

Sheria ya Musa ndiyo iliyoongoza nchi ya Israeli, na ilitoa mwongozo wa maadili kwa Wayahudi waaminifu popote walipokuwa. Baada ya Pentekoste 33 W.K., waabudu wa kweli hawakuhitaji kushika Sheria ya Musa. (Mdo. 15:28, 29; Gal. 4:9-11) Lakini Paulo na Wakristo wengine hawakuidharau Sheria, hivyo waliweza kutolea ushahidi jamii za Kiyahudi bila kizuizi chochote. (1 Kor. 9:20) Kwa kweli, mara nyingi Paulo alienda kwenye masinagogi ili awahubirie watu waliomjua Mungu wa Abrahamu na wale ambao angeweza kusababu nao kwa kutumia Maandiko ya Kiebrania.—Mdo. 9:19, 20; 13:5, 14-16; 14:1; 17:1, 2.

Mitume walichagua Yerusalemu kuwa kituo cha kwanza kilichotumiwa kuelekeza kazi ya kuhubiri. Walifundisha kwa ukawaida hekaluni. (Mdo. 1:4; 2:46; 5:20) Mara kwa mara, Paulo alisafiri kwenda Yerusalemu, na mwishowe alifungwa gerezani huko. Hatua hiyo ilianzisha mchakato wa kisheria uliomfikisha Roma.

PAULO NA SHERIA YA ROMA

Wenye mamlaka huko Roma wangekuwa na maoni gani kuhusu imani ambayo Paulo alihubiri? Ili tujibu swali hilo, ni muhimu tujue maoni ya Waroma kuhusu dini zote kwa ujumla. Hawakulazimisha makabila mbalimbali katika milki yao waache dini zao isipokuwa wakati dini hizo zilipohatarisha Taifa lao au maadili.

Roma iliwapa Wayahudi uhuru mkubwa ndani ya milki yake. Kitabu kimoja (Backgrounds of Early Christianity) kinasema hivi: “Wayahudi walifurahia pendeleo la pekee katika milki ya Roma. . . . Wayahudi walikuwa na uhuru wa ibada na hawakulazimishwa kuabudu miungu ya Waroma. Waliruhusiwa kuongoza maisha ndani ya jamii zao kulingana na sheria zao wenyewe.” Pia hawakuhitaji kujiunga na jeshi. * Paulo angeweza kutumia ulinzi ambao sheria ya Roma iliandaa kuelekea imani ya Kiyahudi alipotetea Ukristo mbele ya mamlaka za Roma.

Wapinzani wa Paulo walijaribu njia mbalimbali kuwafanya watu wa kawaida na wenye mamlaka wampinge mtume huyo. (Mdo. 13:50; 14:2, 19; 18:12, 13) Fikiria kisa kimoja. Wazee Wakristo wa kutaniko la Yerusalemu walisikia uvumi kati ya Wayahudi kwamba Paulo alikuwa akihubiri “uasi-imani wa kumwacha Musa.” Uvumi kama huo ungewafanya Wayahudi waliogeuka karibuni kuwa Wakristo wafikiri kwamba Paulo hakuheshimu mipango ya Mungu. Pia, Sanhedrini ingeweza kutangaza kwamba Ukristo ulikuwa uasi-imani kutoka kwenye imani ya Kiyahudi. Ikiwa hilo lingefanyika, Wayahudi walioshirikiana na Wakristo wangeadhibiwa. Wangetengwa na jamii na kuzuiwa wasihubiri hekaluni au kwenye masinagogi. Kwa sababu hiyo, wazee wa kutaniko walimshauri Paulo afanye jambo ambalo lingethibitisha kwamba uvumi huo si wa kweli kwa kwenda hekaluni na kufanya jambo ambalo halikuwa takwa la Mungu lakini ambalo halikuwa kosa pia.—Mdo. 21:18-27.

Paulo alifanya hivyo na akapata nafasi za “kutetea na kuithibitisha kisheria habari njema.” (Flp. 1:7) Akiwa hekaluni, Wayahudi walianzisha vurugu na kutaka kumwua. Kiongozi wa kijeshi wa Roma alimfunga Paulo gerezani. Paulo alipokuwa karibu kupigwa mijeledi, alisema kwamba yeye ni raia wa Roma. Hilo lilifanya apelekwe Kaisaria, mahali ambako Waroma walisimamia shughuli za Yudea. Akiwa huko angepata nafasi za pekee za kutoa ushahidi kwa ujasiri mbele ya wenye mamlaka. Huenda hilo liliwasaidia watu wajue mengi zaidi kuhusu Ukristo.

Kitabu cha Matendo sura ya 24 kinaeleza kesi ya Paulo mbele ya Feliksi, gavana Mroma wa Yudea, ambaye tayari alikuwa amesikia mambo machache kuhusu imani ya Wakristo. Wayahudi walimshtaki Paulo kwamba amevunja sheria ya Roma kwa kufanya mambo matatu. Walisema kwamba Paulo alichochea uasi kati ya Wayahudi katika milki nzima; alikuwa kiongozi wa madhehebu hatari; na alikuwa akijaribu kulichafua hekalu ambalo lilikuwa chini ya ulinzi wa Waroma. (Mdo. 24:5, 6) Mashtaka hayo yangeweza kufanya ahukumiwe kifo.

Wakristo leo wanapendezwa na jinsi Paulo alivyoshughulikia mashtaka hayo. Aliendelea kuonyesha heshima na alibaki mtulivu. Paulo alirejelea Sheria na Manabii, na alisema kwamba ana haki ya kumwabudu ‘Mungu wa mababu zake.’ Wayahudi wengine walikuwa na haki hiyohiyo chini ya sheria ya Roma. (Mdo. 24:14) Baadaye, Paulo alitetea na kutangaza imani yake mbele ya gavana aliyefuata, Porkio Festo, na vilevile mbele ya Mfalme Herode Agripa.

Mwishowe, ili kesi yake isikilizwe kwa haki, Paulo alisema hivi: “Ninakata rufani kwa Kaisari!”—ambaye alikuwa mtawala mkuu zaidi wakati huo.—Mdo. 25:11.

KESI YA PAULO KWENYE MAHAKAMA YA KAISARI

Baadaye malaika alimwambia Paulo hivi: “Utasimama mbele ya Kaisari.” (Mdo. 27:24) Mwanzoni mwa utawala wake, Maliki Mroma Nero alisema kwamba hangeshughulikia kesi zote mwenyewe. Katika miaka minane ya kwanza ya utawala wake, aliwaomba wengine washughulikie kesi kwa niaba yake. Kitabu fulani kinaripoti kwamba Nero alipokubali kusikiliza kesi fulani, alisikiliza kesi hizo kwenye kasri lake, ambako alisaidiwa na kikundi cha washauri waliokuwa na uzoefu na uvutano mkubwa kwenye maamuzi yake.—The Life and Epistles of Saint Paul.

Biblia haisemi ikiwa Nero mwenyewe alisikiliza kesi ya Paulo au alimpa mtu mwingine aisikilize na kutoa ripoti kwake. Vyovyote vile, inaelekea Paulo alieleza kwamba anamwabudu Mungu wa Wayahudi na aliwahimiza watu wote waipe serikali heshima inayostahili. (Rom. 13:1-7; Tito 3:1, 2) Inaonekana kwamba Paulo alifaulu kutetea habari njema mbele ya maofisa wakuu, kwa kuwa mahakama ya Kaisari ilimwachilia huru.—Flp. 2:24; Flm. 22.

JUKUMU LETU LA KUTETEA HABARI NJEMA

Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtakokotwa na kupelekwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” (Mt. 10:18) Ni pendeleo kumwakilisha Yesu kwa njia hiyo. Jitihada zetu za kutetea habari njema zinaweza kutokeza ushindi wa kisheria. Ni kweli kwamba uamuzi wa wanadamu wasio wakamilifu hauwezi ‘kuthibitisha kisheria’ habari njema kwa ukamili. Ni Ufalme wa Mungu pekee utakaoleta kitulizo cha kudumu kutokana na ukandamizaji na ukosefu wa haki.—Mhu. 8:9; Yer. 10:23.

Hata hivyo, leo pia jina la Yehova linaweza kutukuzwa Wakristo wanapoitetea imani yao. Kama Paulo, sisi pia tunapaswa kujitahidi kuwa watulivu, wanyoofu, na wenye ushawishi. Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba hawangehitaji ‘kufanya mazoezi mapema ya jinsi watakavyojitetea, kwa maana angewapa kinywa na hekima, ambayo wapinzani wao wote wakiwa pamoja hawangeweza kushindana nayo wala kubisha.’—Luka 21:14, 15; 2 Tim. 3:12; 1 Pet. 3:15.

Wakristo wanapoitetea imani yao mbele ya wafalme, magavana, au maofisa wengine, wanaweza kuwatolea ushahidi watu ambao ingekuwa vigumu kuwafikia na ujumbe wa Kikristo. Baadhi ya maamuzi ya mahakama yanayotuunga mkono yameboresha mfumo wa kisheria na hivyo kulinda uhuru wa usemi na wa ibada. Lakini hata tupate matokeo gani mahakamani, ujasiri ambao watu wa Mungu wanaonyesha wanapojaribiwa unamfanya Mungu ashangilie.

Jina la Yehova linatukuzwa tunapoitetea imani yetu

^ fu. 8 Mwandishi James Parkes anasema hivi: “Wayahudi . . . walikuwa na haki ya kuadhimisha sherehe zao. Hilo halikuwa jambo la pekee kwa kuwa ilikuwa kawaida kwa Waroma kuwaruhusu watu wajitawale katika maeneo mbalimbali ya milki hiyo.”