Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mikono Yako Isilegee”

“Mikono Yako Isilegee”

“Mikono yako isilegee.”—SEF. 3:16.

NYIMBO: 81, 32

1, 2. (a) Watu wengi wanakabili matatizo gani leo, na hilo huwafanya wahisije? (b) Andiko la Isaya 41:10, 13 linatupatia tumaini gani hakika?

DADA mmoja ambaye ni painia wa kawaida na ameolewa na mzee wa kutaniko, anasema hivi: “Licha ya kuwa na ratiba nzuri ya mambo ya kiroho, nimepambana na tatizo la kuhangaika kwa miaka mingi. Tatizo hilo hunifanya nikose usingizi, linaathiri afya yangu na jinsi ninavyoshughulika na wengine, na nyakati nyingine hunifanya nihisi kukata tamaa na nijitenge na watu.”

2 Je, umewahi kuhisi kama dada huyo? Inasikitisha kwamba maisha katika ulimwengu huu mwovu wa Shetani, hutokeza mkazo mwingi unaoweza kusababisha mahangaiko na kumfanya mtu ahisi kulemewa. Mkazo huo unaweza kuwa wenye nguvu sana na hivyo ukatuzuia kusonga mbele. (Met. 12:25) Ni mambo gani yanayoweza kukufanya uhisi hivyo? Huenda unakabiliana na huzuni ya kifo cha mpendwa, ugonjwa mbaya, changamoto za kuandalia familia katika nyakati hizi zilizo ngumu kiuchumi, au upinzani. Baada ya muda, mkazo wa kihisia unaotokana na mambo hayo unaweza kufanya uishiwe na nguvu. Vilevile, mkazo huo unaweza kufanya upoteze shangwe yako. Hata hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu yuko tayari kukusaidia.—Soma Isaya 41:10, 13.

3, 4. (a) Biblia inatumiaje neno “mikono”? (b) Ni nini kinachoweza kufanya mikono yetu ilegee?

3 Mara nyingi Biblia hutumia viungo vya mwili wa mwanadamu kuelezea sifa au matendo mbalimbali. Kwa mfano, mkono umetajwa mara nyingi sana. Kutia nguvu mikono ya mtu kunaleta wazo la kumtia moyo, kumwimarisha, na kumwezesha kutenda. (1 Sam. 23:16; Ezra 1:6) Kunadokeza kumsaidia mtu awe na mtazamo mzuri na tumaini la wakati ujao.

4 Nyakati nyingine, kuacha mikono yetu ya mfano ilegee, kumetumiwa kuelezea mtu ambaye amevunjika moyo au kukosa tumaini. (2 Nya. 15:7; Ebr. 12:12) Ni kawaida kwa mtu kukata tamaa anapokuwa kwenye hali kama hiyo. Ikiwa unakabili hali zinazokusababishia mkazo au zinazofanya uhisi kulemewa kimwili, kihisia, au hata kiroho, unaweza kupataje ujasiri unaohitajika? Unaweza kupataje kitia moyo na nguvu ili uvumilie na uwe mwenye shangwe?

“MKONO WA YEHOVA HAUJAWA MFUPI MNO KWAMBA USIWEZE KUOKOA”

5. (a) Matatizo yanapotokea tunaweza kufanya nini, na tunapaswa kukumbuka nini? (b) Tutazungumzia nini?

5 Soma Sefania 3:16, 17. Badala ya kulemewa na woga na kukata tamaa, ambako ni kama kuruhusu mikono yetu ilegee, Baba yetu anayejali, Yehova, anatukaribisha ‘tutupe mahangaiko yetu yote juu yake.’ (1 Pet. 5:7) Tunaweza kuzingatia kile ambacho Mungu aliwaambia Waisraeli kwamba mkono wake wenye nguvu “haujawa mfupi mno kwamba usiweze [kuwaokoa]” watumishi wake washikamanifu. (Isa. 59:1) Tutazungumzia mifano mitatu yenye kutokeza kutoka kwenye Biblia inayoonyesha tamaa na uwezo wa Yehova wa kuwatia nguvu watu wake wafanye mapenzi yake licha ya hali ngumu na zenye kulemea. Fikiria jinsi mifano hiyo inavyoweza kukuimarisha.

6, 7. Tunajifunza mambo gani muhimu kutokana na ushindi wa Waisraeli dhidi ya Waamaleki?

6 Muda mfupi baada ya Waisraeli kukombolewa kimuujiza kutoka utumwani Misri, Waamaleki waliwashambulia. Kwa ujasiri, Yoshua aliwaongoza Waisraeli vitani akifuata mwongozo wa Musa. Wakati huohuo, Musa alienda pamoja na Haruni na Huru hadi kwenye kilima kilichokuwa karibu ambako wangeweza kuona vita hivyo. Je, wanaume hao watatu walikuwa wakivikimbia vita kwa sababu ya woga? La hasha!

7 Musa alitumia mbinu ambayo iliwasaidia washinde. Aliinua mikono yake kuelekea mbinguni, akiwa ameshika fimbo ya Mungu wa kweli. Maadamu Musa aliendelea kuinua mikono yake, Yehova aliitia nguvu mikono ya Waisraeli ili wawashinde Waamaleki. Hata hivyo, mikono ya Musa ilipokuwa mizito na kuanza kulegea, Waamaleki walianza kuwashinda Waisraeli. Mara moja, Haruni na Huru wakachukua “jiwe wakaliweka chini [ya Musa], naye akalikalia; naye Haruni na Huru wakaitegemeza mikono yake, mmoja upande huu na yule mwingine upande ule, hivi kwamba mikono yake ikawa imara mpaka jua lilipotua.” Naam, mkono wenye nguvu wa Mungu uliwasaidia Waisraeli washinde vita hivyo.—Kut. 17:8-13.

8. (a) Asa alitendaje Waethiopia walipotaka kushambulia Yuda? (b) Tunaweza kuigaje mfano wa Asa wa kumtegemea Mungu?

8 Katika siku za Mfalme Asa, Yehova alithibitisha tena kwamba mkono wake haukuwa mfupi. Kuna vita vingi ambavyo vimetajwa katika Biblia. Lakini jeshi kubwa zaidi ambalo limewahi kutajwa ni la Zera Mwethiopia. Alikuwa na wanajeshi 1,000,000 wenye uzoefu. Idadi ya wanajeshi Waethiopia ilikuwa karibu mara mbili ya wanajeshi Waisraeli. Unaweza kuwazia jinsi ambavyo ingekuwa rahisi kwa Asa kuhangaika, kuingiwa na hofu, na kukubali kushindwa kwa kuacha mikono yake ilegee. Badala ya kufanya hivyo, mara moja Asa alimwomba Yehova msaada. Katika hali ya kawaida, jeshi la Asa halingeweza kuwashinda Waethiopia, lakini “kwa Mungu mambo yote yanawezekana.” (Mt. 19:26) Mungu alionyesha nguvu zake nyingi na “akawashinda Waethiopia mbele ya Asa,” ambaye “moyo [wake] ulikuwa mkamilifu kwa Yehova siku zake zote.”—2 Nya. 14:8-13; 1 Fal. 15:14.

9. (a) Nehemia hakuruhusu nini kimzuie kujenga upya kuta za Yerusalemu? (b) Mungu alijibuje sala ya Nehemia?

9 Wazia jinsi Nehemia alivyohisi alipoenda Yerusalemu. Jiji hilo halikuwa na ulinzi wa kutosha, na Wayahudi wenzake walikuwa wamevunjika moyo sana. Wapinzani wa nchi jirani waliwatisha Wayahudi ili walegeze mikono yao na kuacha kujenga upya kuta za Yerusalemu. Je, Nehemia aliruhusu hali hiyo imfanye alegeze mikono yake na kuvunjika moyo kama Wayahudi wenzake? Hapana! Kama Musa, Asa, na watumishi wengine waaminifu wa Yehova, Nehemia alikuwa na kawaida ya kumtegemea Yehova katika sala. Na katika kisa hiki alifanya vivyo hivyo pia. Yehova alijibu ombi la unyoofu la Nehemia la kutaka msaada licha ya vikwazo ambavyo Wayahudi walihisi kuwa hawangeweza kukabiliana navyo. Mungu alitumia “uwezo [wake] mkubwa” na “mkono . . . wenye nguvu” kuitia nguvu mikono ya Wayahudi iliyokuwa imelegea. (Soma Nehemia 1:10; 2:17-20; 6:9.) Je, unaamini kwamba Yehova anatumia “uwezo [wake] mkubwa” na “mkono [wake] wenye nguvu” kuwaimarisha watumishi wake leo?

YEHOVA ATAITIA NGUVU MIKONO YAKO

10, 11. (a) Shetani anatumia njia gani kufanya mikono yetu ilegee? (b) Yehova anatumia nini kutuimarisha na kutupatia nguvu? (c) Umenufaikaje kutokana na elimu na mazoezi ya kitheokrasi?

10 Tunajua kwamba Ibilisi hatailegeza kamwe mikono yake anapojitahidi kuzuia utendaji wetu wa Kikristo. Anatumia uwongo na vitisho kutoka kwa serikali, viongozi wa kidini, na waasi imani. Akiwa na lengo gani? Anataka kufanya tulegeze mikono yetu katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Hata hivyo, Yehova anaweza, na yuko tayari kutupatia nguvu kupitia roho yake takatifu. (1 Nya. 29:12) Ni muhimu tutumie roho hiyo ili tufaulu kukabiliana na changamoto zozote kutoka kwa Shetani na mfumo wake mwovu. (Zab. 18:39; 1 Kor. 10:13) Tunathamini kwamba tuna Neno la Mungu ambalo limeongozwa na roho takatifu. Fikiria pia kuhusu chakula cha kiroho kinachotegemea Biblia tunachopata kila mwezi. Maneno yaliyo kwenye andiko la Zekaria 8:9, 13 (soma), yalisemwa hekalu la Yerusalemu lilipokuwa likijengwa upya, na maneno hayo yanatufaa sana.

11 Tunaimarishwa pia na elimu kutoka kwa Mungu ambayo tunapata kwenye mikutano ya Kikristo, makusanyiko, na katika shule mbalimbali za kitheokrasi. Mazoezi tunayopata yanaweza kutuchochea kuwa na mtazamo unaofaa, kuweka malengo ya kiroho, na kutimiza migawo yetu ya Kikristo. (Zab. 119:32) Je, una hamu ya kupata nguvu kupitia elimu hiyo?

12. Tunapaswa kufanya nini ili tuendelee kuwa imara kiroho?

12 Yehova aliwasaidia Waisraeli wawashinde Waamaleki na Waethiopia, na alimpa Nehemia na wenzake nguvu za kukamilisha kazi ya kujenga upya kuta za Yerusalemu. Vivyo hivyo, Mungu atatupatia nguvu za kusimama imara na kuendelea kuhubiri watu wanapotupinga, wasipopendezwa na habari njema, na tunapokuwa na mahangaiko. (1 Pet. 5:10) Hatutarajii Yehova atufanyie miujiza. Badala yake, tunapaswa kufanya sehemu yetu. Hilo linahusisha kusoma Neno la Mungu kila siku, kutayarisha na kuhudhuria mikutano kila juma, kulisha akili na moyo wetu kupitia funzo la kibinafsi na ibada ya familia, na kumtegemea Yehova katika sala nyakati zote. Kamwe tusiruhusu mambo mengine yatuzuie kunufaika na mpango wa Yehova wa kutuimarisha na kututia moyo. Ikiwa unahisi kwamba mikono yako imelegea kuhusiana na mambo hayo, mwombe Mungu msaada. Kisha utafurahi kuona jinsi roho yake ‘inavyotenda ndani yako ili uwe na nia na kutenda pia.’ (Flp. 2:13) Lakini unaweza kufanya nini ili kuitia nguvu mikono ya wengine?

INYOOSHENI MIKONO INAYOLEGEA

13, 14. (a) Ndugu mmoja alitiwaje nguvu mke wake alipokufa? (b) Tunaweza kuwatia wengine nguvu jinsi gani?

13 Yehova ametupatia undugu wa ulimwenguni pote ulio na waabudu wanaotujali ambao wanaweza kututia moyo. Kumbuka kwamba mtume Paulo aliandika hivi: “Inyoosheni mikono inayolegea na magoti yaliyo dhaifu, nanyi endeleeni kuifanyia miguu yenu mapito yaliyonyooka.” (Ebr. 12:12, 13) Wakristo wengi wa karne ya kwanza walitiwa nguvu kiroho kwa njia hiyo. Ndivyo ilivyo leo pia. Ndugu mmoja aliyefiwa na mke wake na kukabiliana na hali nyingine zenye kuumiza, alisema hivi: “Nilijifunza kwamba hatuwezi kuchagua ni majaribu gani yatakayotupata, yatatokea lini, au yatatupata mara ngapi. Sala na funzo la kibinafsi limekuwa kama boya linalonisaidia kuelea licha ya hali ngumu. Na nimefarijika sana kupitia msaada wa ndugu na dada zangu. Nimetambua umuhimu wa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kabla ya kupatwa na hali ngumu.”

Kila mmoja kutanikoni anaweza kuwatia moyo wengine (Tazama fungu la 14)

14 Haruni na Huru walitegemeza mikono ya Musa kihalisi wakati wa vita. Kwa upande wetu, tunaweza kutafuta fursa za kuwategemeza na kuwasaidia wengine. Ni nani wanaohitaji msaada huo? Wale wanaopambana na matatizo ya uzeeni, matatizo ya afya, upinzani kutoka katika familia, upweke, au kufiwa na wapendwa wao. Pia, tunaweza kuwatia nguvu vijana wanaokabiliana na mkazo wa kufanya dhambi au kutafuta “mafanikio” ya kielimu, kiuchumi, au katika taaluma fulani kwenye mfumo huu wa mambo. (1 The. 3:1-3; 5:11, 14) Tafuta nafasi za kuonyesha kwamba unapendezwa kikweli na wengine unapokuwa kwenye Jumba la Ufalme, katika huduma, mnapofurahia chakula pamoja, au mnapozungumza kupitia simu.

15. Maneno yenye kutia moyo yanaweza kuwa na matokeo gani kwa Wakristo wenzetu?

15 Baada ya Asa kupata ushindi mkubwa, nabii Azaria alitumia maneno haya kumtia moyo Asa pamoja na watu wake: “Nanyi iweni hodari na msiache mikono yenu ilegee, kwa sababu kuna thawabu kwa ajili ya kazi yenu.” (2 Nya. 15:7) Maneno hayo yalimchochea Asa kufanya mabadiliko mengi na kurudisha ibada safi. Kwa njia hiyohiyo, maneno yako yenye kutia moyo yanaweza kuwachochea sana wengine. Hivyo, unaweza kuwasaidia wamtumikie Yehova kikamili. (Met. 15:23) Pia, unapokuwa mikutanoni, kumbuka kwamba maelezo yako yenye kujenga yanaweza kuwachochea sana wengine.

16. Kama Nehemia, wazee wanaweza kuitiaje nguvu mikono ya wengine kutanikoni? Toa mifano ya jinsi ambavyo waamini wenzako wamekusaidia wewe binafsi.

16 Kwa msaada wa Yehova, Nehemia na wenzake waliitia nguvu mikono yao kwa ajili ya kazi. Hivyo, walifanikiwa kumaliza ujenzi wa kuta za Yerusalemu katika siku 52 tu! (Neh. 2:18; 6:15, 16) Nehemia hakuwa msimamizi wa kazi tu. Yeye mwenyewe alishiriki katika ujenzi huo. (Neh. 5:16) Vivyo hivyo, wazee wengi wenye upendo wamemwiga Nehemia kwa kushiriki katika miradi ya ujenzi ya kitheokrasi au katika kazi za kusafisha na kudumisha Jumba lao la Ufalme. Pia, wanapohubiri pamoja na wahubiri wenzao na kufanya ziara za uchungaji, wanaitia nguvu mikono dhaifu ya wale wanaohangaika moyoni.—Soma Isaya 35:3, 4.

“MIKONO YAKO ISILEGEE”

17, 18. Tunaweza kuwa na uhakika gani tunapokabili matatizo au kupata mahangaiko?

17 Kutumikia bega kwa bega na ndugu na dada zetu huchochea umoja. Vilevile kunatusaidia kuwa na urafiki wenye kudumu na kunaimarisha imani yetu sote kuelekea baraka za wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu. Tunapoitia nguvu mikono ya wengine, tunawasaidia wapambane na hali zinazowavunja moyo, na wadumishe mtazamo mzuri na tumaini la wakati ujao. Isitoshe, kuwatia nguvu wengine kunatusaidia tuendelee kukazia fikira mambo ya kiroho na kufanya ahadi za Mungu kuwa halisi zaidi. Naam, kufanya hivyo kunaitia nguvu mikono yetu pia.

18 Kuchunguza jinsi Yehova alivyowategemeza na kuwalinda watumishi wake waaminifu katika pindi mbalimbali nyakati za zamani, kunaimarisha imani yetu na kufanya tumtegemee leo. Hivyo, unapokabili mikazo na matatizo, usiruhusu “mikono yako [ilegee]”! Badala yake, mkaribie Yehova katika sala, na uruhusu mkono wake wenye nguvu ukuimarishe na kukuongoza kwenye baraka za Ufalme.—Zab. 73:23, 24.