Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nufaika na Mwongozo wa Yehova Leo

Nufaika na Mwongozo wa Yehova Leo

UAMUZI WA HEKIMA NCHINI POLAND

“NILIKUWA na umri wa miaka 15 nilipobatizwa, na miezi sita baadaye nikawa painia msaidizi. Baada ya mwaka mmoja, nikawa painia wa kawaida. Nilipohitimu shule ya sekondari, niliomba kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Nilitaka kuhama kutoka kwenye eneo letu na kwenda kuishi mbali na nyanya (bibi) yangu niliyekuwa nikiishi naye, ambaye hakuwa Shahidi wa Yehova. Nilisikitika sana mwangalizi wa mzunguko aliponiambia kwamba mgawo wangu ungekuwa hapohapo kwenye mji niliozaliwa. Sikutaka ajue jinsi nilivyohisi. Nikiwa nimevunjika moyo sana, niliondoka na kwenda kufikiria kile ambacho alikuwa amesema. Nilimwambia hivi dada tuliyeshirikiana naye: ‘Ninafikiri natenda kama Yona. Hata hivyo, mwishowe Yona alienda Ninawi. Kwa hiyo, mimi pia nitatumikia mahali nilipoagizwa.’”

“Sasa nimekuwa painia kwa miaka minne kwenye mji huu, na ninaona hekima ya kufuata mwongozo niliopewa. Tatizo kuu ni kwamba nilikuwa na mtazamo usiofaa. Sasa nina shangwe nyingi. Wakati fulani, nilifanikiwa kuongoza mafunzo ya Biblia 24 katika mwezi mmoja. Nimeanza kujifunza Biblia pamoja na nyanya yangu aliyekuwa akinipinga, na hiyo ni baraka kutoka kwa Yehova.”

MATOKEO MAZURI NCHINI FIJI

Mwanafunzi mmoja wa Biblia nchini Fiji alihitaji kuchagua kati ya kuhudhuria kusanyiko la Kikristo au kwenda na mume wake kwenye sherehe ya kuzaliwa ya mtu wao wa ukoo. Mume wake alimruhusu kuhudhuria kusanyiko. Mwanamke huyo alimwahidi mume wake kwamba angeungana naye kwenye sherehe hiyo baada ya kusanyiko. Hata hivyo, aliporudi nyumbani alihisi kwamba ingekuwa bora kuepuka mazingira ambayo yangehatarisha hali yake ya kiroho, hivyo hakwenda kwenye sherehe hiyo.

Wakati huohuo, mume wake alipowaambia watu wake wa ukoo kwamba amemwomba mke wake ajiunge naye baada ya kuhudhuria “mkutano wa Mashahidi,” walimwambia hivi: “Hatakuja; Mashahidi wa Yehova hawasherehekei siku za kuzaliwa!” *

Matokeo ni kwamba mwanamume huyo alifurahi sana kuona jinsi mke wake alivyochukua msimamo uliopatana na imani na dhamiri yake. Uaminifu wake ulimpa nafasi ya kumhubiria mume wake na kuwahubiria wengine. Matokeo yalikuwa nini? Mume huyo alianza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano pamoja na mke wake.

^ fu. 7 Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 2001.