Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana, Imarisheni Imani Yenu

Vijana, Imarisheni Imani Yenu

“Imani ni . . . uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.”—EBR. 11:1.

NYIMBO: 41, 69

1, 2. Leo, vijana wanashinikizwa kufanya nini, na wanaweza kuchukua hatua gani ili kukabiliana na hali hiyo?

DADA fulani kijana nchini Uingereza aliambiwa hivi na mwanafunzi mwenzake: “Watu wenye akili nyingi kama wewe hawamwamini Mungu.” Ndugu mmoja nchini Ujerumani aliandika hivi: “Walimu wangu wanaamini kwamba simulizi la Biblia kuhusu uumbaji ni nadharia. Na wanawatarajia wanafunzi waamini mageuzi.” Dada kijana nchini Ufaransa alisema hivi: “Walimu wa shule yetu wanashangaa kwamba kuna wanafunzi ambao bado wanaamini Biblia.”

2 Ukiwa kijana anayemtumikia Yehova au anayejifunza kumhusu, je, unashinikizwa kuamini mageuzi kama watu wengi wanavyofanya badala ya kumwamini Muumba? Ikiwa ndivyo, unaweza kuchukua hatua za kuimarisha imani yako na kuidumisha ikiwa imara. Hatua moja ni kutumia uwezo wako wa kufikiri uliopewa na Mungu, ambao “utakutunza.” Utakulinda kutokana na falsafa zinazoweza kuharibu imani yako.—Soma Methali 2:10-12.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Imani ya kweli inategemea ujuzi sahihi kumhusu Mungu. (1 Tim. 2:4) Kwa hiyo, unapojifunza Neno la Mungu au machapisho yetu ya Kikristo, usiyasome kijuujuu tu. Tumia uwezo wako wa kufikiri “kuelewa maana” ya kile unachosoma. (Mt. 13:23) Acheni tuone jinsi kufanya hivyo kunavyoweza kukusaidia kuimarisha imani yako kwa Mungu akiwa Muumba na katika Biblia. Kuna “uthibitisho ulio wazi” kuhusu habari hizo.—Ebr. 11:1.

JINSI YA KUIMARISHA IMANI YAKO

4. Kwa nini kwa njia fulani imani inahusika iwe tunamwamini Mungu au mageuzi, na tunapaswa kufanya nini ili tuwe na mtazamo unaofaa?

4 Je, watu wamewahi kukuambia wanaamini nadharia ya mageuzi kwa sababu inategemea sayansi ilhali kumwamini Mungu kunategemea imani? Watu wengi wana mtazamo kama huo. Lakini ni muhimu tukumbuke hivi: Kwa njia fulani imani inahusika, iwe mtu anamwamini Mungu au anaamini mageuzi. Jinsi gani? Hakuna mtu yeyote ambaye amewahi kumwona Mungu au kushuhudia kitu chochote kikiumbwa. (Yoh. 1:18) Na hakuna mwanadamu yeyote, hata kama yeye ni mwanasayansi, ambaye amewahi kushuhudia mageuzi ya mnyama wa aina yoyote. Kwa mfano, hakuna mtu aliyewahi kuona nyoka akigeuka kuwa simba. (Ayu. 38:1, 4) Hivyo, sisi sote tunapaswa kuchunguza uthibitisho na tutumie uwezo wetu wa kufikiri ili tufikie mkataa unaofaa. Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu uumbaji: “Sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.”—Rom. 1:20.

Unapojadiliana na watu, tumia vizuri vifaa vinavyopatikana katika lugha yako (Tazama fungu la 5)

5. Tukiwa watu wa Mungu tumeandaliwa vifaa gani vinavyotusaidia kutumia uwezo wetu wa kuelewa?

5 ‘Kuelewa’ kunamaanisha kutambua kitu ambacho hakionekani waziwazi. (Ebr. 11:3) Kwa hiyo, watu wenye uelewaji hutumia akili zao, si macho na masikio yao tu. Tengenezo la Yehova limeandaa vifaa vingi vilivyofanyiwa utafiti ili vitusaidie. Vifaa hivyo vinaweza kutusaidia ‘tumwone’ Muumba wetu kupitia macho yetu ya imani. (Ebr. 11:27) Vinatia ndani video yenye kichwa Maajabu ya Uumbaji Yanafunua Utukufu wa Mungu, broshua zenye kichwa Uhai—Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, na kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? Pia, tunapokea habari nzuri sana tunazopaswa kufikiria kwa uzito katika magazeti yetu. Mara nyingi gazeti la Amkeni! limechapisha maelezo ya wanasayansi na watu wengine wakieleza sababu zilizowafanya waanze kumwamini Mungu. Mfululizo wa makala zenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” zimezungumzia mifano ya vitu vya asili vilivyobuniwa kwa njia ya ajabu. Mara nyingi wanasayansi wanajitahidi kuiga ubuni huo wa ajabu.

6. Ni manufaa gani tunayopata kwa kutumia vifaa tulivyoandaliwa, nawe umenufaikaje?

6 Ndugu mwenye umri wa miaka 19 anayeishi Marekani, alisema hivi kuhusu broshua hizo mbili: “Broshua hizo zimenisaidia kwelikweli. Nimezisoma mara nyingi sana.” Dada kutoka Ufaransa aliandika hivi: “Makala zenye kichwa ‘Je, Ni Kazi ya Ubuni?’ zimenipendeza sana. Zimeonyesha kwamba wahandisi wenye ujuzi mwingi huiga ubuni wa vitu vya asili lakini kamwe hawafikii utata wa ubuni huo.” Wazazi wa msichana mwenye umri wa miaka 15 wanaoishi Afrika Kusini, walisema hivi: “Binti yetu husoma makala yenye kichwa, ‘Mahojiano’ mara tu anapopokea gazeti la Amkeni!” Namna gani wewe? Je, unatumia kikamili maandalizi hayo? Maandalizi hayo yanaweza kufanya imani yako iwe kama mti wenye mizizi yenye kina. Kwa njia hiyo, imani yako itakusaidia kukabiliana na mafundisho ya uwongo.—Yer. 17:5-8.

IMANI YAKO KATIKA BIBLIA

7. Kwa nini Mungu anataka utumie uwezo wako wa kufikiri?

7 Je, ni kosa kuuliza maswali ya unyoofu kuhusu Biblia? La, hasha! Yehova anataka utumie ‘nguvu zako za kufikiri’ ili ujithibitishie mwenyewe ukweli. Hataki uiamini Biblia kwa sababu tu wengine wanafanya hivyo. Kwa hiyo, tumia uwezo wako wa kufikiri kupata ujuzi sahihi. Ujuzi huo utakuwa msingi thabiti wa imani ya kweli. (Soma Waroma 12:1, 2; 1 Timotheo 2:4.) Unaweza kupata ujuzi huo kupitia miradi unayochagua ya kujifunza.

8, 9. (a) Unaweza kufurahia miradi gani ya kujifunza? (b) Wengine wamenufaikaje kwa kutafakari mambo wanayojifunza?

8 Watu fulani wamechagua miradi ya kujifunza unabii wa Biblia au kuchunguza usahihi wa Biblia kuhusu historia, akiolojia, na sayansi. Unabii mmoja wenye kusisimua ni ule ulio katika Mwanzo 3:15. Mstari huo unataja kwa mara ya kwanza kichwa kikuu cha Biblia, yaani, kutetewa kwa enzi kuu ya Mungu na kutakaswa kwa jina lake kupitia Ufalme wake. Kwa kutumia lugha ya mfano, mstari huo mmoja unaonyesha jinsi Yehova atakavyoondoa matatizo yote ambayo wanadamu wamepata tangu Edeni. Unaweza kutumia njia gani kuchunguza andiko la Mwanzo 3:15? Njia moja ni kuandika mfuatano wa matukio. Unaweza kuandika orodha ya maandiko makuu yanayoonyesha jinsi ambavyo Mungu alifunua hatua kwa hatua watu na mipango, ambayo inatajwa katika mstari huo na kuthibitisha kwamba unabii huo utatimia. Kadiri unavyoona maandiko yakipatana, bila shaka utakata shauri kwamba waandikaji wa Biblia na manabii lazima wawe ‘waliongozwa na roho takatifu.’—2 Pet. 1:21.

9 Ndugu mmoja nchini Ujerumani aligundua kwamba kila kitabu cha Biblia kina habari fulani kuhusu Ufalme. Alisema hivi: “Hilo ni kweli ingawa Biblia iliandikwa na wanaume 40. Wengi wao waliishi pindi tofauti na hawakujuana.” Dada kutoka Australia alichochewa na makala ya funzo kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 2013, iliyozungumzia maana ya Pasaka. Mwadhimisho huo wa pekee unahusiana kwa ukaribu na andiko la Mwanzo 3:15 na kuja kwa Masihi. Aliandika hivi: “Kujifunza mambo hayo kulinisaidia kuona jinsi Yehova alivyo na uwezo wa pekee. Nilipendezwa sana kugundua kwamba Yehova alifanya mpango ili Waisraeli waadhimishe tukio hilo, na baadaye Yesu atimize unabii uliofananishwa na tukio hilo. Nilihitaji kutua kihalisi na kutafakari jinsi unabii kuhusu mlo wa Pasaka ulivyo wa pekee!” Kwa nini dada huyo alihisi hivyo? Alitafakari kwa kina mambo aliyosoma na “kuelewa maana yake.” Hilo liliimarisha imani yake na kumsaidia amkaribie zaidi Yehova.—Mt. 13:23.

10. Unyoofu wa waandikaji wa Biblia unaimarishaje imani yetu katika Biblia?

10 Jambo lingine linaloweza kuimarisha imani yetu ni kuchunguza ujasiri na unyoofu wa wanaume walioandika Biblia. Waandishi wengi wa kale waliwarai viongozi wao na kutukuza falme zao. Hata hivyo, manabii wa Yehova walisema kweli nyakati zote. Walikuwa tayari kutaja makosa ya watu wa taifa lao, na hata yale ya wafalme wao. (2 Nya. 16:9, 10; 24:18-22) Pia, waliweka wazi makosa yao na ya watumishi wengine wa Mungu. (2 Sam. 12:1-14; Marko 14:50) Ndugu fulani kijana nchini Uingereza alisema hivi: “Si kawaida kuona unyoofu wa aina hiyo. Hilo linatuthibitishia hata zaidi kwamba kweli Biblia ni Neno la Yehova.”

11. Ni nini kinachoweza kuwasaidia vijana wathamini zaidi kanuni zenye thamani za Biblia?

11 Watu wengi wanasadiki kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu kwa sababu ya kanuni zake. (Soma Zaburi 19:7-11.) Dada mmoja kijana anayeishi Japani aliandika hivi: “Tulipotumia kanuni za Biblia katika familia yetu, tulipata furaha ya kweli. Tulikuwa na amani, umoja, na upendo.” Kanuni za Biblia hutulinda kutokana na ibada ya uwongo na ushirikina, mambo ambayo yamewafanya watu wengi kuwa watumwa. (Zab. 115:3-8) Je, falsafa zinazofundisha kwamba hakuna Mungu zinawaathiri watu? Mafundisho kama mageuzi huwafanya watu waabudu vitu vya asili, ibada ambayo inapaswa kuwa ya Yehova pekee. Wale wanaosema hakuna Mungu ni kana kwamba wanasema wanaweza kuamua wakati wao ujao utakuwaje. Hata hivyo, hawatoi tumaini lolote la wakati ujao.—Zab. 146:3, 4.

KUJADILIANA NA WENGINE

12, 13. Ni njia gani yenye matokeo tunayoweza kutumia tunapozungumzia uumbaji au Biblia pamoja na wanafunzi wenzetu, walimu, au watu wengine?

12 Unawezaje kuwa na matokeo unapojadiliana na wengine kuhusu uumbaji au Biblia? Kwanza, usiwe mwepesi kufikiri kwamba tayari unajua mambo ambayo wengine wanaamini. Baadhi ya watu wanaoamini mageuzi wanaamini pia kwamba Mungu yupo. Wanafikiri kwamba Mungu alitumia mageuzi kuumba vitu mbalimbali. Wengine wanaamini mageuzi kwa sababu wanahisi kwamba mambo yote yanayofundishwa shuleni ni hakika. Ilhali wengine wameacha kuamini kuwapo kwa Mungu kwa sababu wamevunjwa moyo na dini. Kwa hiyo, unapozungumza na mtu kuhusu chanzo cha uhai, ni jambo la hekima kumwuliza maswali kwanza. Jitahidi kujua kile ambacho mtu huyo anaamini. Ukiwa mwenye usawaziko na tayari kusikiliza, anaweza kuchochewa kukusikiliza pia.—Tito 3:2.

13 Ikiwa mtu anajaribu kushambulia imani yako kuhusu uumbaji, kwa busara unaweza kugeuzia mada upande wake. Unaweza kumwomba aeleze jinsi uhai ulivyoanza bila Muumba. Ili aina fulani ya uhai iendelee kuwapo, lazima uhai huo uwe na uwezo wa kutokeza uhai mwingine wa aina yake. Profesa mmoja wa kemia alisema kwamba baadhi ya vitu vinavyohitajika ili kutokeza uhai ni (1) utando wa kulinda chembe, (2) uwezo wa kupata na kutumia nishati, (3) habari ndani ya chembe za urithi, na (4) uwezo wa kutokeza nakala zaidi za habari hiyo. Aliongeza hivi: “Mtu anaweza kupendezwa na mambo tata kuhusu uhai hata ule unaonekana kuwa wa hali ya chini.”

14. Unaweza kufanya nini ikiwa hujajitayarisha kuzungumzia mageuzi au uumbaji?

14 Ikiwa unahisi hujajitayarisha kuzungumzia mageuzi au uumbaji, jaribu kutumia njia ya Paulo ya kujenga hoja. Aliandika hivi: “Kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Ebr. 3:4) Wazo hilo la msingi linaweza kukusaidia upate matokeo mazuri. Naam, ubuni tata hutokezwa na mtu mwenye akili nyingi. Njia nyingine nzuri ni kutumia chapisho fulani linalofaa. Dada mmoja alitumia broshua zilizotajwa awali kuzungumza na kijana fulani aliyeamini mageuzi na hakuamini kuwapo kwa Mungu. Baada ya juma moja hivi, kijana huyo alisema, “Sasa ninaamini kwamba Mungu yupo.” Kijana huyo alianza kujifunza Biblia na sasa yeye ni ndugu yetu.

15, 16. Unaweza kurekebishaje njia yako ya kuzungumzia Biblia, na unapaswa kuwa na lengo gani?

15 Unaweza kutumia kanuni hizohizo unapozungumza na mtu ambaye anatilia shaka Biblia. Jitahidi kufahamu anaamini nini hasa na ni habari gani zinazompendeza. (Met. 18:13) Ikiwa anapendezwa na mambo ya kisayansi, anaweza kuvutiwa ukimwonyesha kwamba Biblia ni sahihi kisayansi. Watu wengine wanaweza kuvutiwa ukiwaonyesha kwamba Biblia ina unabii uliotimia na ni sahihi kihistoria. Au, unaweza kutaja kanuni za Biblia kama zile zinazopatikana kwenye Mahubiri ya Mlimani.

16 Kumbuka, lengo lako linapaswa kuwa kufikia moyo, si kushinda mabishano. Kwa hiyo, uwe msikilizaji mzuri. Uliza maswali kwa unyoofu, na ujieleze kwa upole na heshima hasa unapozungumza na watu wenye umri mkubwa. Inaelekea wataheshimu maoni yako na pia wataona kwamba umetafakari kwa kina kuhusu imani yako. Hilo ni jambo ambalo vijana wengi hawafanyi. Ni vizuri kukumbuka kwamba si lazima ujibu maswali ya watu ambao hawako tayari kusikiliza au wale wanaotaka tu kudhihaki imani yako.—Met. 26:4.

FANYA KWELI IWE MALI YAKO

17, 18. (a) Ni nini kinachoweza kukusaidia ufanye kweli iwe mali yako? (b) Tutazungumzia swali gani katika makala inayofuata?

17 Imani yenye nguvu inategemea mengi zaidi ya kupata ujuzi wa msingi wa Biblia. Hivyo, chimba kwa kina ndani ya Neno la Mungu kana kwamba unatafuta hazina zilizofichika. (Met. 2:3-6) Tumia vizuri vifaa vinavyopatikana katika lugha yako, kama vile Watchtower Library katika DVD, Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO, na vilevile Fahirisi au Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Pia, weka lengo la kusoma Biblia nzima. Unaweza kujaribu kuisoma kwa muda wa mwaka mmoja. Ni vitu vichache sana vinavyoweza kuimarisha imani yako kama kusoma Neno la Mungu. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema hivi kuhusu wakati alipokuwa kijana: “Jambo moja lililonithibitishia kwamba Biblia ni Neno la Mungu ni kuisoma kuanzia mwanzo hadi mwisho. Mwishowe, nilielewa hadithi za Biblia nilizokuwa nimesoma tangu nilipokuwa mdogo sana. Kuanzia hapo hali yangu ya kiroho ilibadilika sana na nikaanza kufanya maendeleo ya kiroho.”

18 Wazazi mna fungu muhimu katika ukuzi wa kiroho wa watoto wenu. Mnaweza kuwasaidiaje wawe na imani yenye nguvu? Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.