Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Neno la Mungu liko hai”

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

“Neno la Mungu” linalotajwa katika Waebrania 4:12 ambalo “liko hai nalo lina nguvu,” ni nini?

Muktadha unaonyesha kwamba mtume Paulo alikuwa akizungumzia ujumbe unaopatikana katika Biblia, au kusudi la Mungu.

Mara nyingi machapisho yetu hunukuu andiko la Waebrania 4:12 kuonyesha kwamba Biblia ina nguvu za kubadili maisha ya watu, na ni sawa kabisa kutumia andiko hilo kwa njia hiyo. Hata hivyo, ni vema kuchunguza andiko la Waebrania 4:12 huku tukizingatia muktadha. Paulo alikuwa akiwahimiza Wakristo Waebrania waunge mkono makusudi ya Mungu. Tayari maandiko matakatifu yalikuwa yamefunua makusudi hayo. Paulo alitumia mfano wa Waisraeli ambao walikuwa wameokolewa kutoka Misri. Walikuwa na tumaini la kuingia kwenye nchi ya ahadi “inayotiririka maziwa na asali,” ambako wangefurahia pumziko la kweli.—Kut. 3:8; Kum. 12:9, 10.

Hilo ndilo lililokuwa kusudi la Mungu. Hata hivyo, baadaye Waisraeli walifanya mioyo yao kuwa migumu na wakakosa imani. Kwa hiyo, wengi wao hawakuingia katika pumziko hilo. (Hes. 14:30; Yos. 14:6-10) Lakini Paulo aliongeza kwamba bado kulikuwa na “ahadi . . . ya kuingia katika pumziko [la Mungu].” (Ebr. 3:16-19; 4:1) Ni wazi kwamba “ahadi” hiyo ni sehemu ya kusudi la Mungu. Kama Wakristo Waebrania walivyofanya, sisi pia tunaweza kusoma na kuunga mkono kusudi hilo. Ili kukazia kwamba ahadi hiyo inategemea Maandiko, Paulo alinukuu sehemu ya andiko la Mwanzo 2:2 na Zaburi 95:11.

Bila shaka, tunaguswa mioyo kujua kwamba “ahadi imebaki ya kuingia katika pumziko [la Mungu].” Tunaamini kwamba tumaini linalotegemea Biblia la kuingia katika pumziko la Mungu ni hakika, na tumechukua hatua za kuingia katika pumziko hilo. Hatujafanya hivyo kwa kujitahidi kushika Sheria ya Musa au kupata kibali cha Yehova kwa kufanya mambo mengine mazuri. Badala yake, kwa imani tumefurahia kuunga mkono kusudi la Mungu lililofunuliwa na tunaendelea kufanya hivyo. Kwa kuongezea, kama ilivyotajwa, maelfu ya watu ulimwenguni pote wameanza kujifunza Biblia na kujua kusudi la Mungu. Wengi wao wamechochewa kubadili mtindo wao wa maisha, wameonyesha imani, na kubatizwa. Jinsi maisha yao yalivyobadilika ni uthibitisho ulio wazi kwamba “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” Kusudi la Mungu, kama linavyoelezwa katika Biblia, tayari limebadili maisha yetu, na litaendelea kuwa na nguvu maishani mwetu.