Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi, Wasaidieni Watoto Wenu Wasitawishe Imani

Wazazi, Wasaidieni Watoto Wenu Wasitawishe Imani

“Enyi vijana, nanyi mabikira pia . . . na walisifu jina la Yehova.”—ZAB. 148:12, 13.

NYIMBO: 88, 115

1, 2. (a) Wazazi wanakabili changamoto gani, na wanaweza kushughulika nayo jinsi gani? (b) Tutachunguza mambo gani?

WENZI fulani wa ndoa nchini Ufaransa walisema hivi: “Tunamwamini Yehova, lakini hilo halimaanishi kwamba watoto wetu watamwamini pia.” Waliongeza hivi: “Imani si kitu unachoweza kurithi. Watoto wetu huisitawisha hatua kwa hatua.” Ndugu mmoja nchini Australia aliandika hivi: “Huenda kumsaidia mtoto wako asitawishe imani ndiyo changamoto kubwa zaidi utakayokabili unapomlea. Unahitaji kutumia maandalizi yote yanayopatikana. Unaweza kuhisi kwamba mtoto wako ameridhika na majibu unayompa. Kisha anakuuliza tena swali lilelile! Huenda majibu yanayomridhisha mtoto wako leo yasimridhishe kesho. Inaelekea kwamba kuna habari ambazo utahitaji kurudia mara kwa mara.”

2 Ikiwa wewe ni mzazi, je, nyakati nyingine unahisi kulemewa na daraka la kuwasaidia watoto wako wasitawishe na kudumisha imani yenye nguvu? Kwa kweli, hatuwezi kutimiza daraka hilo kwa kutumia hekima yetu wenyewe! (Yer. 10:23) Lakini tunaweza kufanikiwa tukimwomba Mungu atuongoze. Fikiria mambo manne unayoweza kufanya ili uwasaidie watoto wako wasitawishe imani: (1) Wafahamu watoto wako vizuri. (2) Wafundishe kutoka moyoni. (3) Tumia mifano inayofaa. (4) Uwe na subira na umtegemee Yehova katika sala.

WAFAHAMU WATOTO WAKO VIZURI

3. Wazazi wanaweza kuigaje mfano wa Yesu wanapofundisha?

3 Yesu hakuogopa kuwauliza wafuasi wake kile walichoamini. (Mt. 16:13-15) Iga mfano wake. Waombe watoto wako waeleze hisia zao hasa mnapokuwa mmestarehe. Hilo linahusisha kuzungumzia mambo ambayo huenda hawana uhakika nayo, au mambo wanayotilia shaka. Ndugu mmoja mwenye umri wa miaka 15 nchini Australia, aliandika hivi: “Mara nyingi Baba huzungumza nami kuhusu imani yangu na kunisaidia kutafakari. Yeye huniuliza hivi: ‘Biblia inasema nini?’ ‘Je, unaamini inachosema?’ ‘Kwa nini unaiamini?’ Anataka nimjibu kwa maneno yangu mwenyewe badala ya kurudia maneno yake au maneno ya Mama. Kadiri nilivyoendelea kukua ndivyo nilivyohitaji kuboresha majibu yangu.”

4. Kwa nini ni muhimu kuchukua kwa uzito maswali ambayo watoto wako wanauliza? Toa mfano.

4 Ikiwa mtoto wako anatilia shaka fundisho fulani, usiudhike na kuanza kutetea mambo unayoamini. Kwa subira, msaidie atafakari kuhusu jambo hilo. Baba mmoja alisema hivi: “Chukua kwa uzito maswali ambayo mtoto wako anauliza. Usiyapuuze au kuyaepuka kwa sababu hujihisi huru kuyazungumzia.” Kwa kweli, mara nyingi maswali ya unyoofu kutoka kwa mtoto huonyesha kwamba anajali na anataka kuelewa. Hata alipokuwa na umri wa miaka 12, Yesu aliuliza maswali mazito. (Soma Luka 2:46.) Kijana mwenye umri wa miaka 15 kutoka Denmark, anakumbuka hivi: “Niliposema kwamba nina shaka ikiwa dini yetu ni ya kweli, wazazi wangu walikuwa watulivu ingawa huenda walikuwa na wasiwasi kunihusu. Walijibu maswali yangu yote kwa kutumia Biblia.”

5. Wazazi wanaweza kuonyeshaje kwamba wanachukua kwa uzito imani ya watoto wao?

5 Jitahidi kufahamu vizuri mawazo, hisia, na mahangaiko ya watoto wako. Usifikiri kamwe kwamba wana imani eti kwa sababu wanahudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki utumishi wa shambani pamoja nawe. Muwe na mazungumzo ya kiroho katika shughuli zenu za kila siku. Sali pamoja na watoto wako na vilevile kwa ajili yao. Jaribu kutambua majaribu ya imani wanayokabili, na uwasaidie kukabiliana nayo.

FUNDISHA KUTOKA MOYONI

6. Kukazia kweli za Biblia moyoni mwa wazazi kunaweza kuwasaidiaje wawe walimu bora?

6 Akiwa mwalimu, Yesu alifikia mioyo kwa sababu alimpenda Yehova, Neno lake, na pia aliwapenda watu. (Luka 24:32; Yoh. 7:46) Wazazi wakiwa na upendo kama huo, wataifikia mioyo ya watoto wao. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:5-8; Luka 6:45.) Hivyo, wazazi iweni wanafunzi wazuri wa Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia. Pendezwa na uumbaji na makala katika machapisho yetu zinazozungumzia uumbaji. (Mt. 6:26, 28) Mkifanya hivyo mtaongeza ujuzi wenu, uthamini wenu kwa Yehova, na mtaboresha uwezo wenu wa kuwafundisha watoto wenu.—Luka 6:40.

7, 8. Moyo wa mzazi unapojaa kweli za Biblia, matokeo yatakuwa nini? Toa mfano.

7 Unapojaza moyo wako kweli za Biblia, utatamani kuzizungumzia pamoja na familia yako. Jitahidi kufanya hivyo kila wakati na si tu mnapotayarisha mikutano ya Kikristo au wakati wa ibada ya familia. Isitoshe, mazungumzo hayo hayapaswi kulazimishwa, bali yanapaswa kujitokeza kwa njia ya kawaida kama sehemu ya mazungumzo ya kila siku. Wenzi fulani wa ndoa nchini Marekani hutafakari kumhusu Yehova wanapofurahia uumbaji au aina fulani ya chakula wakiwa familia. Wazazi hao wanasema hivi: “Tunawakumbusha watoto wetu kuhusu upendo wa Yehova na jinsi alivyofikiria mapema kila kitu alichotuandalia.” Wenzi wa ndoa nchini Afrika Kusini huzungumzia maajabu ya jinsi mbegu huota na mimea inavyokua wanapotunza bustani yao. Wazazi hao wanasema hivi: “Sisi hujitahidi kuwasaidia binti zetu waheshimu uhai na waone jinsi ulivyo tata sana.”

8 Mwana wake alipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, baba mmoja nchini Australia alitumia fursa ya kutembelea jumba la makumbusho kumsaidia aimarishe imani yake kwa Mungu na uumbaji. Baba huyo alisema hivi: “Tuliona maonyesho ya viumbe wa zamani wa baharini jamii ya athropodi. Tulistaajabu kuona kwamba viumbe hao, ingawa tayari wametoweka, walikuwa wenye kuvutia, tata, na walikuwa na viungo vyote sawasawa kabisa na viumbe tunaowaona leo. Kwa hiyo, ikiwa mnyama mmoja aligeuka na kuwa mnyama tata zaidi, kwa nini viumbe hao wa zamani tayari walikuwa tata sana? Ni somo ambalo lilinivutia sana na nikazungumza na mwanangu kuhusu mambo niliyojifunza.”

TUMIA MIFANO YENYE MATOKEO

9. Kwa nini kutumia mifano huwa na matokeo mazuri, na mama mmoja alitumia mbinu hiyo jinsi gani?

9 Mara nyingi Yesu alitumia mifano iliyochochea kufikiri, iliyofikia mioyo, na kuwasaidia watu kukumbuka. (Mt. 13:34, 35) Kwa kawaida, watoto huwa na uwezo mzuri wa kuwazia. Hivyo, wazazi tumieni mifano kwa wingi mnapofundisha. Mama mmoja nchini Japani alifanya hivyo. Wavulana wake wawili walipokuwa na umri wa miaka minane na mwingine miaka kumi, aliwafundisha kuhusu anga-hewa la dunia na jinsi ambavyo Yehova alilitengeneza kwa makini. Ili afanye hivyo, aliwapa maziwa, sukari, na kahawa. Kisha akamwomba kila mmoja wao amtayarishie kahawa. Alieleza hivi: “Walikuwa makini sana walipokuwa wakiitayarisha. Nilipowauliza kwa nini walikuwa makini kiasi hicho, walisema kwamba walitaka iwe jinsi ambavyo mimi hupenda. Nilieleza kwamba Mungu alichanganya aina mbalimbali za hewa katika anga letu kwa njia hiyohiyo ili zitufae.” Mfano huo uliwafaa kwa sababu ya umri wao, na uliwachochea zaidi kuliko kuwafundisha kijuujuu tu. Hakuna shaka kwamba walikumbuka somo hilo kwa muda mrefu!

Unaweza kutumia vitu vya kawaida kuimarisha imani ya mtoto kuhusu Mungu na katika uumbaji (Tazama fungu la 10)

10, 11. (a) Unaweza kutumia mfano gani kumsaidia mtoto wako asitawishe imani kwa Mungu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Ni mifano gani ambayo umeona kuwa yenye matokeo?

10 Unaweza pia kutumia maagizo ya upishi ili kumsaidia mtoto wako asitawishe imani kwa Mungu. Jinsi gani? Baada ya kuoka keki au kupika maandazi, eleza umuhimu wa maagizo ya upishi. Halafu umpe mtoto wako tunda na umwulize hivi: “Je, ulijua kwamba ‘maagizo’ yalihitajika ili kutengeneza tunda hili?” Kisha kata tunda hilo na umpe mbegu yake. Unaweza kusema kwamba maagizo “yaliandikwa” kwenye mbegu hiyo, lakini kwa lugha tata kuliko iliyotumiwa kwenye maagizo ya upishi. Unaweza kumwuliza hivi: “Ikiwa mtu fulani aliandika maagizo ya upishi wa keki, ni nani aliyeandika maagizo ya kutengeneza tunda hili?” Kwa mtoto mwenye umri mkubwa zaidi, unaweza kueleza kwamba maagizo ya kutengeneza tunda na mti wenyewe yalikuwa sehemu ya habari iliyo ndani ya chembe za urithi. Mkiwa pamoja, mnaweza kuchunguza mifano na picha kwenye ukurasa wa 10 hadi 20 wa broshua yenye kichwa Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai.

11 Wazazi wengi hufurahia kuzungumza pamoja na watoto wao kuhusu mfululizo wa makala zenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?,” kwenye gazeti la Amkeni! Au wanatumia sehemu hiyo kama msingi wa kuwafundisha watoto wadogo mambo rahisi. Kwa mfano, wenzi wa ndoa nchini Denmark walilinganisha ndege za abiria na ndege wa angani. Walisema hivi: “Ndege za abiria zinafanana na ndege wa angani. Lakini, je, ndege za abiria hutaga mayai na kuangua ndege nyingine ndogo? Je, ndege wa angani wanahitaji uwanja wa kutua? Na je, kati ya sauti ya ndege za abiria na sauti za ndege wa angani, ni sauti ipi iliyo bora? Kwa hiyo, nani aliye na akili nyingi kati ya mtengenezaji wa ndege za abiria na Muumba wa ndege wa angani?” Maelezo kama hayo pamoja na maswali yanayofaa yanaweza kumsaidia mtoto asitawishe “uwezo wa kufikiri” na ajenge imani kwa Mungu.—Met. 2:10-12.

12. Mifano inaweza kuwasaidiaje watoto waiamini Biblia?

12 Mifano inayofaa inaweza kuimarisha imani ya mtoto kuhusu usahihi wa Biblia. Kwa mfano, fikiria andiko la Ayubu 26:7. (Soma.) Unaweza kuonyeshaje kwamba andiko hilo limeongozwa na roho ya Mungu? Huenda ukaamua tu kumwambia mambo hakika kuhusu andiko hilo. Lakini badala ya kufanya hivyo, kwa nini usichochee uwezo wa kuwazia wa mtoto wako? Mweleze kwamba Ayubu aliishi muda mrefu kabla ya darubini na vyombo vya angani kuvumbuliwa. Mwombe mtoto wako aonyeshe jinsi ilivyo vigumu kwa watu fulani kuamini kwamba kitu kizito, kama vile dunia, kingeweza kuning’inia bila kutegemezwa na chochote. Mtoto anaweza kutumia mpira au jiwe kuonyesha kwamba vitu vizito haviwezi kuning’inia pasipo na kitu. Somo kama hilo linaweza kukazia ndani ya akili ya mtoto kwamba Yehova alihakikisha mambo hakika yameandikwa katika Biblia muda mrefu kabla wanadamu hawajayathibitisha.—Neh. 9:6.

TOA MIFANO INAYOONYESHA THAMANI YA KANUNI ZA BIBLIA

13, 14. Wazazi wanaweza kukaziaje thamani ya kanuni za Biblia moyoni mwa watoto wao?

13 Ni muhimu sana ukazie thamani ya kanuni za Biblia moyoni mwa watoto wako. (Soma Zaburi 1:1-3.) Kuna njia nyingi za kufanya hivyo. Kwa mfano, unaweza kuwaomba watoto wawazie kwamba wanaenda kuishi kwenye kisiwa fulani kilicho mbali na wanahitaji kuchagua watu kadhaa wakaishi nao. Kisha waulize, “Ni sifa gani ambazo kila mmoja wao anahitaji kuwa nazo ili wote waishi kwa amani na umoja?” Pia, unaweza kuzungumza nao kuhusu mwongozo wenye hekima unaopatikana katika andiko la Wagalatia 5:19-23.

14 Zoezi hilo linaweza kuwafundisha mambo mawili muhimu. Kwanza, viwango vya Mungu huchochea amani na umoja. Pili, Yehova anapotuelimisha sasa anatutayarisha kuishi katika ulimwengu mpya. (Isa. 54:13; Yoh. 17:3) Unaweza kumsaidia aelewe mambo hayo kwa kutumia mambo yaliyoonwa katika machapisho yetu. Huenda ukatumia mfululizo wa makala zenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha,” zinazochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi. Au ikiwa kuna mtu kwenye kutaniko lenu ambaye amefanya mabadiliko makubwa maishani ili ampendeze Yehova, unaweza kumwalika awasimulie kisa chake. Mifano kama hiyo hufanya mtoto aelewe kwamba kanuni za Biblia zina manufaa maishani!—Ebr. 4:12.

15. Unapaswa kuwa na lengo gani kuu unapowafundisha watoto wako?

15 Jambo kuu ni hili: Unapowafundisha watoto usitumie mbinu ileile. Jitahidi kutumia uwezo wako wa kuwazia. Chochea nguvu zao za kufikiri ukizingatia umri wao. Wasaidie wafurahie kujifunza na waimarishe imani yao. Baba mmoja alisema hivi: “Usichoke kamwe kujaribu mbinu mpya za kufundisha mambo mliyojifunza zamani.”

UWE MWAMINIFU, MWENYE SUBIRA, NA UMTEGEMEE YEHOVA KATIKA SALA

16. Unapowafundisha watoto wako, kwa nini ni muhimu kuwa na subira? Toa mfano.

16 Tunahitaji roho ya Mungu ili tuwe na imani yenye nguvu. (Gal. 5:22, 23) Kama ilivyo kwa tunda halisi, muda unahitajiwa ili imani isitawi. Hivyo, utahitaji kuwa mwenye subira na ustahimilivu unapowafundisha watoto wako. Baba ya watoto wawili nchini Japani alisema hivi: “Mimi na mke wangu tulitumia muda mwingi pamoja na watoto wetu. Tangu walipokuwa wachanga, nilijifunza nao kwa dakika 15 kila siku, isipokuwa siku za mikutano ya Kikristo. Haikuwa vigumu kwetu na kwa watoto wetu kufanya hivyo kwa dakika kumi na tano.” Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliandika hivi: “Nilipokuwa kijana, nilikuwa na maswali na mashaka mengi ambayo sikuweza kuyaeleza. Kadiri muda ulivyopita, maswali mengi kati ya hayo yalijibiwa kwenye mikutano, funzo la familia, au funzo langu la kibinafsi. Hiyo ndiyo sababu ni muhimu wazazi waendelee kuwafundisha watoto wao bila kukata tamaa.”

Ili uwe mwalimu mwenye matokeo, lazima Neno la Mungu liwe moyoni mwako kwanza (Tazama fungu la 17)

17. Kwa nini mfano mzuri wa wazazi ni muhimu, na wenzi fulani wamewawekeaje binti zao mfano mzuri?

17 Bila shaka, jambo muhimu zaidi ni jinsi unavyowawekea watoto mfano kupitia imani yako. Watoto wako watatazama mambo unayofanya na hilo litawasaidia sana. Kwa hiyo, enyi wazazi endeleeni kujenga imani yenu. Acheni watoto wenu waone jinsi ambavyo Yehova ni halisi kwenu. Wenzi wa ndoa huko Bermuda wanapokuwa na mahangaiko, wao husali pamoja na watoto wao na kumwomba Yehova awaongoze, na wanawatia moyo watoto wasali kibinafsi. Wanasema hivi: “Huwa tunamwambia binti yetu mkubwa, ‘Mtegemee Yehova kabisa, uwe na mengi ya kufanya katika utumishi wa Ufalme, na usihangaike kupita kiasi.’ Anapoona matokeo, anatambua kwamba Yehova anatusaidia. Hilo limemsaidia awe na imani yenye nguvu kwa Mungu na katika Biblia.”

18. Wazazi wanapaswa kukumbuka jambo gani muhimu?

18 Ni kweli kwamba mwishowe watoto watahitaji kusitawisha imani yao wenyewe. Ukiwa mzazi, unaweza kupanda na kutia maji. Ni Mungu pekee anayeweza kuikuza. (1 Kor. 3:6) Hivyo, mwombe akupe roho yake na ujitahidi kuwafundisha watoto wako wapendwa. Kwa kufanya hivyo, Yehova atakubariki sana.—Efe. 6:4.