Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nimepata Baraka ya Kufanya Kazi na Ndugu Wakomavu Kiroho

Nimepata Baraka ya Kufanya Kazi na Ndugu Wakomavu Kiroho

KATIKATI ya miaka ya 1930, baba na mama yangu—James na Jessie Sinclair—walihamia eneo la Bronx, jijini New York City. Mmoja kati ya waliofahamiana nao mwanzoni ni Willie Sneddon, ambaye kama wao, alikuwa ametoka Scotland. Ndani ya dakika chache tu, wakaanza kuzungumza kuhusu familia zao. Hiyo ilikuwa miaka michache tu kabla sijazaliwa.

Mama alimweleza Willie kwamba muda mfupi kabla ya Vita Vikuu, baba na kaka yake walizama katika Bahari ya Kaskazini baada ya boti yao ya uvuvi kulipuliwa na bomu lililotegwa baharini. Willie akajibu hivi, “Baba yako yuko kuzimu!” Willie alikuwa Shahidi wa Yehova, na hivyo mama akasikia kweli ya Biblia kwa mara ya kwanza kwa njia hiyo yenye kushtua.

Willie na Liz Sneddon

Jambo ambalo Willie alisema lilimwudhi mama kwa kuwa alijua kwamba baba yake alikuwa mtu mzuri. Lakini Willie aliongeza hivi: “Je, itasaidia nikikuambia kwamba Yesu pia alienda kuzimu?” Mama alikumbuka fundisho la kanisa ambalo lilipoandikwa kwa mara ya kwanza, lilisema kwamba Yesu alishuka kwenda kuzimu na akafufuliwa siku ya tatu. Hivyo alijiuliza, ‘Ikiwa kuzimu ni mahali penye moto ambapo watu waovu huteswa, kwa nini Yesu alienda huko?’ Huo ulikuwa ndio mwanzo wa mama kupendezwa na kweli. Alianza kuhudhuria mikutano katika Kutaniko la Bronx na akabatizwa mwaka wa 1940.

Nikiwa na mama, na baadaye nikiwa na baba

Kipindi hicho, wazazi Wakristo hawakusisitiziwa wajifunze Biblia pamoja na watoto wao. Nilipokuwa mchanga, baba alibaki nami mama alipohudhuria mikutano na kushiriki katika kazi ya kuhubiri kwenye miisho juma. Baada ya miaka michache, mimi na baba tulianza kuhudhuria mikutano pamoja na mama. Mama alikuwa mwenye bidii sana katika kazi ya kuhubiri habari njema na aliongoza mafunzo mengi ya Biblia. Hata kuna wakati ambapo angewafundisha wakiwa kikundi kwa sababu baadhi yao waliishi katika eneo moja. Nilipofunga shule, nilihubiri pamoja naye. Kwa njia hiyo, nilijifunza mengi kuhusu Biblia na jinsi ya kufundisha wengine yale inayosema.

Ninasikitika kwamba nilipokuwa mdogo, sikuithamini kweli kikamili. Hata hivyo, nilipokuwa na umri wa miaka 12 hivi, nikawa mhubiri wa Ufalme, na tangu wakati huo nikaanza kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani. Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilijiweka wakfu kwa Yehova na nikabatizwa Julai 24, 1954, katika kusanyiko la wilaya lililofanywa jijini Toronto, Kanada.

UTUMISHI WA BETHELI

Katika kutaniko langu, baadhi ya ndugu walikuwa washiriki wa familia ya Betheli na wengine waliwahi kutumikia huko. Mfano wao ulinichochea sana. Nilipendezwa sana na uwezo wao wa kutoa hotuba na wa kufundisha kweli za Biblia. Ingawa walimu wangu shuleni walitaka niende chuo kikuu, mradi wangu ulikuwa kwenda Betheli. Hivyo, niliwasilisha fomu yangu ya Betheli nilipohudhuria kusanyiko hilo la Toronto. Niliwasilisha fomu nyingine mwaka wa 1955, nilipohudhuria kusanyiko lililofanywa katika uwanja wa Yankee Stadium, jijini New York City. Muda mfupi baadaye, Septemba 19, 1955, nikiwa na umri wa miaka 17, nilialikwa kutumikia katika Betheli ya Brooklyn. Siku ya pili baada ya kuwasili Betheli, nilianza kazi katika Idara ya Kujalidi Vitabu iliyokuwa kwenye jengo la 117 Adams Street. Muda si muda, nilianza kazi kwenye mashine iliyokusanya sehemu za vitabu zenye kurasa 32 na kuzitayarisha kwa ajili ya mashine nyingine iliyounganisha sehemu hizo kwa nyuzi na kutokeza vitabu.

Nilianza utumishi wangu katika Betheli ya Brooklyn nikiwa na umri wa miaka 17

Baada ya kufanya kazi kwa mwezi mmoja hivi katika idara hiyo, nilipangiwa kazi katika Idara ya Magazeti kwa kuwa nilijua kuchapa. Miaka hiyo, akina ndugu na dada walichapa anwani kwenye mabamba ya chuma kwa ajili ya watu wapya waliojiandikisha kupokea gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Miezi michache baadaye, nilianza kufanya kazi kwenye Idara ya Upakizi na Usafirishaji. Klaus Jensen, aliyekuwa mwangalizi wa idara, aliniomba ikiwa ningependa kuandamana na dereva aliyekuwa akisafirisha machapisho kwenda bandarini ili yasafirishwe ulimwenguni pote. Pia, kulikuwa na magazeti mengi yaliyohitaji kupelekwa posta ili yatumwe kwenye makutaniko kotekote Marekani. Ndugu Jensen alisema kwamba kazi hiyo ngumu ya kubeba machapisho ingenisaidia. Nilikuwa na uzito wa kilo 57 hivi, na nilikuwa mwembamba sana. Safari hizo za kwenda bandarini na posta ziliimarisha mwili wangu. Inaelekea Ndugu Jensen alijua kazi ambayo ingenifaa!

Idara ya Magazeti ilishughulikia pia maombi ya magazeti ya makutaniko. Hivyo, nikajua ni katika lugha zipi magazeti yetu yalichapishwa na kusambazwa kutoka Betheli ya Brooklyn kwenda sehemu nyinginezo za ulimwengu. Kabla ya hapo, sikuwahi kusikia kuhusu lugha nyingi kati ya hizo, lakini nilifurahi kujua kwamba maelfu ya magazeti yalikuwa yakitumwa kwenda nchi za mbali. Wakati huo, sikujua kwamba katika miaka ijayo ningepata pendeleo la kutembelea maeneo hayo.

Nikiwa pamoja na Robert Wallen, Charles Molohan, na Don Adams

Katika mwaka wa 1961, nilipewa mgawo wa kufanya kazi katika Ofisi ya Mweka Hazina chini ya uangalizi wa Grant Suiter. Baada ya kufanya kazi huko kwa miaka michache, niliitwa kwenye ofisi ya Nathan Knorr, ambaye alisimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote kipindi hicho. Ndugu Knorr alinieleza kwamba ndugu mmoja aliyefanya kazi katika ofisi yake angeenda kwenye Shule ya Huduma ya Ufalme kwa mwezi mmoja, na baada ya kurudi angefanya kazi kwenye Idara ya Utumishi. Nilipewa mgawo wa kufanya kazi yake nikishirikiana na Don Adams. Jambo la kupendeza ni kwamba Don ndiye aliyeipokea fomu yangu ya Betheli katika kusanyiko la wilaya la mwaka wa 1955. Tayari kulikuwa ndugu wawili waliokuwa wakifanya kazi katika ofisi hiyohiyo, yaani, Robert Wallen na Charles Molohan. Sote wanne tulifanya kazi pamoja kwa miaka zaidi ya 50. Nimepata shangwe kubwa kutumikia pamoja na wanaume waaminifu na wa kiroho kama hao!—Zab. 133:1.

Ziara yangu ya kwanza nchini Venezuela nikiwa mwangalizi wa eneo la dunia, mwaka wa 1970

Kuanzia mwaka wa 1970, nilipewa mgawo wa kusafiri kwa majuma machache kila mwaka au baada ya miaka miwili kwenda kwenye ofisi za tawi za Watch Tower Society nikiwa mwangalizi wa eneo la dunia, kama alivyojulikana zamani. Kazi hiyo ilihusisha kutembelea familia za Betheli na wamishonari ulimwenguni pote, kuwatia moyo, na kuchunguza rekodi za ofisi za tawi. Nilifurahi sana kukutana na baadhi ya ndugu na dada waliohitimu kwenye madarasa ya kwanza-kwanza ya Shule ya Gileadi na ambao bado walikuwa wakitumikia kwa uaminifu katika migawo yao katika nchi za kigeni! Nimefurahia pendeleo la kutembelea nchi zaidi ya 90 nikiwa katika kazi hiyo.

Nimefurahia sana kuwatembelea akina ndugu katika Nchi zaidi ya 90!

NINAMPATA MWENZI MWAMINIFU

Wanabetheli wote wa Brooklyn walitumwa kwenye makutaniko yaliyoko eneo la New York City. Mimi nilipangiwa kutaniko lililoko eneo la Bronx. Kutaniko la kwanza katika eneo hilo lilikua na kugawanywa. Kutaniko hilo la awali likaitwa Upper Bronx, nalo ndilo nililopangiwa.

Katikati ya miaka ya 1960, familia moja kutoka Latvia, iliyojifunza kweli katika eneo la kaskazini mwa Bronx, ilihamia katika eneo la kutaniko letu. Livija, binti yao wa kwanza, akawa painia mara tu baada ya kumaliza shule ya sekondari. Miezi michache baadaye, alihamia jimbo la Massachusetts ili atumikie katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Nikaanza kumwandikia barua kuhusu habari za kutaniko, naye angeniandikia kuhusu mafanikio yake ya utumishi kwenye eneo la Boston.

Mimi na Livija

Miaka michache baadaye, Livija aliwekwa kuwa painia wa pekee. Alitaka kufanya yote awezayo katika utumishi wa Yehova, hivyo akajaza fomu ya kuomba kutumikia Betheli na akaalikwa mwaka wa 1971. Niliiona kama ishara kutoka kwa Yehova! Hivyo, Oktoba 27, 1973, tulifunga ndoa na tukapata pendeleo la kutolewa hotuba ya ndoa na Ndugu Knorr. Methali 18:22 inasema: “Je, mtu amepata mke mwema? Amepata kitu chema, na mtu hupata nia njema kutoka kwa Yehova.” Kwa hiyo, mimi na Livija tumepata pendeleo la kutumikia Betheli tukiwa pamoja kwa miaka zaidi ya 40. Na tunaendelea kushirikiana na kutaniko lililo katika eneo hilohilo la Bronx.

KUTUMIKIA BEGA KWA BEGA NA NDUGU ZA KRISTO

Nilifurahia sana kufanya kazi na Ndugu Knorr. Alikuwa mwenye bidii kwa ajili ya kweli na aliwathamini sana wamishonari wote waliotumikia katika sehemu mbalimbali duniani. Wengi wao walikuwa ndio Mashahidi wa kwanza katika nchi ambazo walitumwa. Ilihuzunisha sana kumwona Ndugu Knorr akiugua kansa mwaka wa 1976. Pindi moja alipokuwa mgonjwa sana, aliniomba nimsomee habari fulani iliyokuwa ikitayarishwa ili ikachapishwe. Aliniomba nimwite Frederick Franz ili naye pia asikilize usomaji huo. Baadaye, nilikuja kugundua kwamba kwa sababu uwezo wa Ndugu Franz wa kuona ulikuwa umefifia, Ndugu Knorr alikuwa akitumia muda mwingi kumsomea habari kama hizo.

Nikiwa kwenye ziara ya mwangalizi wa eneo la dunia pamoja na Daniel na Marina Sydlik mwaka wa 1977

Ndugu Knorr alikufa mwaka wa 1977, lakini wale waliomjua na kumpenda walifarijika kwa sababu alimaliza mwendo wake wa kidunia akiwa mwaminifu. (Ufu. 2:10) Baadaye, Ndugu Franz alisimamia kazi yetu.

Kufikia wakati huo, nilikuwa nikifanya kazi ya ukarani kwa ajili ya Milton Henschel, ambaye alikuwa amefanya kazi pamoja na Ndugu Knorr kwa miaka mingi. Ndugu Henschel aliniambia kwamba wajibu wangu wa kwanza kabisa nikiwa Betheli ni kumsaidia Ndugu Franz kwa njia yoyote ambayo angehitaji msaada wangu. Hivyo, nilimsomea kwa ukawaida habari ambazo baadaye zingechapishwa. Ndugu Franz alikuwa na kumbukumbu ya pekee na alikuwa na uwezo wa ajabu sana wa kukazia fikira kilichokuwa kikisomwa. Nilifurahia sana kumsaidia katika njia hiyo hadi alipomaliza mwendo wake wa kidunia katika mwezi wa Desemba 1992!

Jengo la 124 Columbia Heights, ambapo nilifanya kazi kwa miaka mingi

Miaka 61 ambayo nimekuwa Betheli imepita haraka. Wazazi wangu walikufa wakiwa waaminifu kwa Yehova, na ninatazamia kwa hamu kuwakaribisha kwenye ulimwengu bora zaidi. (Yoh. 5:28, 29) Hakuna kitu katika mfumo huu kinachoweza kulinganishwa na pendeleo kubwa la kufanya kazi pamoja na wanaume na wanawake waaminifu kwa ajili ya watu wa Mungu ulimwenguni pote. Mimi na Livija tunaweza kusema kwa unyoofu kwamba katika kipindi chote cha utumishi wetu wa wakati wote, ‘shangwe ya Yehova imekuwa ndiyo ngome yetu.’—Neh. 8:10.

Tengenezo la Yehova halitegemei mtu mmoja, hivyo kazi ya kuhubiri Ufalme inaendelea. Kwa miaka mingi, nimefurahia sana pendeleo la kufanya kazi pamoja na ndugu na dada wengi washikamanifu na wenye imani yenye nguvu. Kwa sasa, wengi wa watiwa mafuta ambao nilifanya kazi nao, hawapo tena duniani. Lakini ninathamini sana kwamba nilishirikiana na watumishi hao waaminifu katika utumishi wa Yehova.