Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Yehova Katika Kuonyesha Huruma

Mwige Yehova Katika Kuonyesha Huruma

“Yehova, Yehova, Mungu mwenye rehema na neema.”​—KUT. 34:6.

NYIMBO: 57, 147

1. Yehova alijifunua kwa Musa katika njia gani ya pekee, na kwa nini hilo ni muhimu?

PINDI moja, Mungu alifunua utu wake kwa Musa kwa kutangaza jina na sifa Zake. Sifa alizotaja kwanza ni rehema na neema. (Soma Kutoka 34:5-7.) Yehova angeweza kukazia nguvu au hekima yake. Lakini alipozungumza na Musa, ambaye alitaka kuhakikishiwa kwamba Mungu angemsaidia, Yehova alikazia sifa zilizoonyesha utayari wake wa kuwasaidia watumishi wake. (Kut. 33:13) Je, huguswi moyo kwamba Mungu alitaja sifa hizo zenye kuvutia kwanza kabla ya kutaja sifa nyingine? Makala hii itakazia sifa ya neema au huruma, yaani, kutambua mateso au taabu ya mtu mwingine, kumsikitikia, na kutamani kumsaidia.

2, 3. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba wanadamu wameumbwa wakiwa na uwezo wa kuonyesha huruma? (b) Kwa nini unapaswa kupendezwa na kile ambacho Biblia inasema kuhusu sifa ya huruma?

2 Wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu. Hivyo, kwa sababu Yehova ni mwenye huruma, kiasili wanadamu hupendezwa na hali njema ya wengine. Mara nyingi, hata wale wasiomjua Mungu wa kweli huonyesha huruma. (Mwa. 1:27) Kuna masimulizi mengi katika Biblia yanayoonyesha sifa ya huruma. Kumbuka simulizi kuhusu makahaba wawili waliobishana mbele ya Sulemani kuhusu ni nani aliyekuwa mama halisi ya mtoto. Sulemani alipowajaribu kwa kuagiza mtoto huyo akatwe vipande viwili, hisia za huruma za mama halisi ziliamshwa. Zilimchochea achukue hatua, hata kama ilimaanisha kumpa mwanamke yule mwingine mtoto wake. (1 Fal. 3:23-27) Au mkumbuke binti ya Farao aliyemwokoa Musa akiwa mchanga. Ingawa alijua kuwa mtoto huyo alikuwa wa Mwebrania na alipaswa kuuawa, ‘alimwonea huruma’ na kuamua kumlea kama mtoto wake mwenyewe.—Kut. 2:5, 6.

3 Kwa nini unapaswa kupendezwa na sifa ya huruma? Kwa sababu Biblia inakuhimiza umwige Yehova. (Efe. 5:1) Ingawa wanadamu wameumbwa wakiwa na uwezo wa kuonyesha huruma, tukiwa wazao wa Adamu wasio wakamilifu tuna mwelekeo wa kuwa wabinafsi. Nyakati nyingine, huenda isiwe rahisi kuamua ikiwa tutawasaidia wengine au tutajifikiria wenyewe. Kwa baadhi ya watu, kufanya uamuzi huo ni changamoto ya kila siku. Ni nini kinachoweza kukusaidia usitawishe na kudumisha mtazamo wa kuwafikiria wengine? Kwanza, tumia muda kuchunguza jinsi ambavyo Yehova ameonyesha huruma na jinsi ambavyo wengine wamefanya hivyo pia. Pili, chunguza jinsi unavyoweza kuiga kielelezo cha Mungu na faida nyingi utakazopata kwa kufanya hivyo.

YEHOVA—KIELELEZO KIKAMILIFU CHA HURUMA

4. (a) Kwa nini Yehova aliwatuma malaika Sodoma? (b) Simulizi la Loti na binti zake linatufundisha nini?

4 Katika Biblia, kuna visa vingi ambavyo huruma ya Yehova ilihusika. Fikiria kile ambacho Mungu alimfanyia Loti. Mtu huyo mwadilifu ‘alitaabishwa sana’ na mwenendo mpotovu wa wakaaji wa Sodoma na Gomora. Kwa hakika, Mungu aliazimia kwamba watu hao wenye maadili mapotovu walistahili kufa. (2 Pet. 2:7, 8) Mungu alituma malaika wakamwokoe Loti. Walimhimiza yeye pamoja na familia yake wayakimbie majiji hayo ambayo yangeangamizwa. “Alipoendelea kukawia, ndipo kwa huruma za Yehova kwake, wale [malaika] wakaushika mkono wake na mkono wa mke wake na mikono ya binti zake wawili. Wakamtoa nje na kumweka nje ya jiji.” (Mwa. 19:16) Je, mfano huo hauonyeshi kwamba Mungu anaelewa kabisa hali ngumu ambazo huwapata watu wake waaminifu nyakati fulani?—Isa. 63:7-9; Yak. 5:11; 2 Pet. 2:9.

5. Maandiko, kama vile 1 Yohana 3:17, yanatusaidiaje kujifunza jinsi tunavyoweza kuonyesha huruma?

5 Yehova ameonyesha huruma na pia amewafundisha watu wake uhitaji wa kuonyesha sifa hiyo. Fikiria sheria waliyopewa Waisraeli kuhusu kuchukua vazi la mtu mwingine kuwa rehani. (Soma Kutoka 22:26, 27.) Mkopeshaji mwenye moyo mgumu angeweza kushawishiwa kuchukua vazi la mkopaji na kumwacha bila kitu cha kujifunika. Lakini Yehova aliwafundisha watu wake kuepuka mtazamo na mwenendo kama huo usioonyesha huruma. Watu wake walipaswa kuwa wenye huruma. Je, kanuni inayopatikana katika sheria hiyo haituchochei kutenda? Je, tungewaacha ndugu zetu bila kitu cha kujifunika, kwa njia ya mfano, ikiwa tunaweza kufanya jambo fulani ili kupunguza matatizo yao?—Kol. 3:12; Yak. 2:15, 16; soma 1 Yohana 3:17.

6. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyoendelea kuwasaidia Waisraeli watenda dhambi wabadilike?

6 Yehova aliwahurumia watu wake Israeli hata walipotenda dhambi. Tunasoma hivi: “Na Yehova Mungu wa mababu zao akaendelea kutuma juu yao kupitia kwa wajumbe wake, akatuma tena na tena, kwa sababu aliwahurumia watu wake na makao yake.” (2 Nya. 36:15) Je, hatupaswi kuwahurumia jinsi hiyo watu ambao wanaweza kuacha maisha yao ya dhambi na kupata kibali cha Mungu? Yehova hataki mtu yeyote aharibiwe katika hukumu ijayo. (2 Pet. 3:9) Kwa hiyo, mpaka Mungu atakapochukua hatua ya kuwaharibu waovu, acheni tuendelee kutangaza ujumbe wake wa huruma na unaoonya.

7, 8. Kwa nini familia moja iliamini kwamba Yehova aliwaonyesha huruma?

7 Mambo mengi yaliyoonwa yanaweza kutumiwa kuonyesha sifa ya Mungu ya huruma. Fikiria kilichopata familia ya mtoto tutakayemwita Milan, mwenye umri wa miaka 12. Kilikuwa kipindi cha vita vya kikabila katika miaka ya 1990. Milan, mdogo wake wa kiume, wazazi wake, na Mashahidi wengine kadhaa walikuwa kwenye basi wakisafiri kwenda Serbia kutoka Bosnia. Walikuwa wakielekea kwenye kusanyiko ambako wazazi wa Milan walitarajia kubatizwa. Lakini walipofika mpakani, wanajeshi waliamuru familia ya Milan ishuke kutoka kwenye basi hilo kwa sababu ya kabila lao; hata hivyo, wakawaruhusu ndugu wengine kuendelea na safari. Baada ya kuwazuia kwa siku mbili, ofisa aliyesimamia eneo hilo alimpigia simu msimamizi wake akiuliza hatua ambayo alipaswa kuwachukulia. Ofisa huyo alikuwa amesimama mbele ya familia hiyo, hivyo wote walimsikia msimamizi akisema, “Watoe nje na uwapige risasi!”

8 Ofisa huyo alipokuwa akizungumza na wanajeshi wake, watu wawili walikuja na kuzungumza na familia hiyo na kujitambulisha kuwa Mashahidi. Walikuwa wamepata habari hizo kutoka kwa wengine waliokuwa kwenye basi. Mashahidi hao walimwambia Milan na mdogo wake waingie kwenye gari lao ili wavuke mpaka kwa kuwa hati zao hazikuhitaji kukaguliwa. Kisha wakawaambia wazazi wa Milan wazunguke upande wa nyuma wa kituo hicho ili wakutane upande wa pili. Milan hakujua acheke au alie aliposikia pendekezo hilo. Wazazi wake wakauliza hivi: “Unafikiri wataturuhusu tu tuondoke?” Lakini walipoondoka, ni kana kwamba wanajeshi hao walikuwa wamepumbazika. Wazazi na watoto waliungana tena upande wa pili wa mpaka. Waliendelea na safari yao kwenda kusanyikoni, wakiwa wamesadiki kabisa kwamba Yehova alikuwa amejibu sala zao za bidii za kuomba msaada. Kupitia Biblia tumejifunza kwamba kuna nyakati nyingine ambazo Yehova hakuingilia kati ili kuwalinda watumishi wake. (Mdo. 7:58-60) Hata hivyo, Milan anaeleza jinsi alivyohisi. Anasema hivi: “Kwa maoni yangu ilikuwa kana kwamba malaika waliwapofusha wanajeshi hao na Yehova akatuokoa.”—Zab. 97:10.

9. Yesu alitendaje alipoona hali ya umati uliomfuata? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

9 Tunaweza pia kujifunza somo fulani kutoka kwa Yesu. Aliusikitikia umati aliokutana nao, kwa kuwa “walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” Alitendaje kuhusiana na hali yao yenye kusikitisha? “Akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Mt. 9:36; soma Marko 6:34.) Mtazamo wake ulikuwa tofauti kabisa na ule wa Mafarisayo, ambao hawakutaka hata kidogo kuwasaidia watu wa kawaida. (Mt. 12:9-14; 23:4; Yoh. 7:49) Je, una tamaa kama ya Yesu ya kuwalisha watu wenye njaa ya kiroho?

10, 11. Je, inafaa kuwaonyesha wengine huruma nyakati zote? Eleza.

10 Hilo halimaanishi kwamba tunapaswa kuonyesha huruma katika hali zote. Lilikuwa jambo linalofaa kwa Mungu kuonyesha huruma katika mifano inayotajwa hapo juu iliyo katika Biblia. Katika kisa fulani, Mfalme Sauli alifikiri kwamba anaonyesha huruma, lakini kihalisi alikuwa amekosa kutii. Alikosa kumwangamiza Agagi, adui wa watu wa Mungu, na vilevile mifugo bora zaidi. Kwa sababu hiyo, Yehova alimkataa Sauli kuwa mfalme wa Israeli. (1 Sam. 15:3, 9, 15) Bila shaka, Yehova ndiye Mwamuzi mwadilifu. Anaweza kusoma mioyo ya watu na anajua wakati ambapo hawapaswi kuonyeshwa huruma. (Omb. 2:17; Eze. 5:11) Hivi karibuni atatekeleza hukumu juu ya wote wanaokataa kumtii. (2 The. 1:6-10) Huo hautakuwa wakati wa kuwaonyesha huruma watu aliowahukumu kuwa waovu. Badala yake, kwa kuwaangamiza waovu, Mungu atakuwa akiwaonyesha waadilifu huruma inayofaa wale atakaowaokoa.

11 Ni wazi kwamba si jukumu letu kuamua watu wanaostahili kuangamizwa au kuokolewa. Kinyume chake, tunahitaji kufanya yote tunayoweza sasa ili kuwasaidia. Hivyo, ni katika njia zipi mbalimbali tunazoweza kuwaonyesha wanadamu wenzetu huruma inayofaa? Chunguza mapendekezo kadhaa.

KUSITAWISHA NA KUONYESHA HURUMA INAYOFAA

12. Mtazamo wako unaweza kuonyeshaje kwamba unawahurumia wengine unaposhughulika nao?

12 Uwe tayari kuwasaidia watu kila siku. Kumwonyesha huruma jirani na ndugu zetu Wakristo ni takwa la msingi kwa wale wanaojitahidi kumwiga Yesu. (Yoh. 13:34, 35; 1 Pet. 3:8) Maana moja ya neno huruma ni “kuteseka pamoja.” Mtu anayeonyesha huruma huchochewa kupunguza mateso ya wengine, labda kwa kuwasaidia wanapopata matatizo. Tafuta fursa za kufanya hivyo! Kwa mfano, je, unaweza kumsaidia mtu kwa kujitolea kumfanyia kazi fulani muhimu?—Mt. 7:12.

Waonyeshe wengine huruma kwa kuwasaidia (Tazama fungu la 12)

13. Ni sifa zipi za watu wa Mungu ambazo huonekana wazi baada ya misiba ya asili kutokea?

13 Shiriki katika kazi ya kutoa msaada. Kuteseka kwa wale waliokumbwa na misiba ya asili huwachochea wengi kuonyesha sifa ya huruma. Watu wa Yehova wanajulikana kwa kuchukua hatua ya kwanza kuwasaidia watu walio katika hali kama hizo. (1 Pet. 2:17) Dada mmoja kutoka Japani aliishi katika eneo ambalo liliharibiwa vibaya sana na tetemeko la ardhi na tsunami iliyotokea mwaka wa 2011. Anasema kwamba “alitiwa moyo sana na kufarijiwa” na jitihada za wajitoleaji wengi waliotoka sehemu mbalimbali nchini Japani na kutoka nchi nyingine ili kurekebisha majengo yaliyobomoka. Anaandika hivi: “Jambo hilo lilinisaidia kutambua kwamba Yehova ananijali. Na kwamba Mashahidi huwajali ndugu zao. Ndugu na dada wengi duniani kote wanasali kwa ajili yetu.”

14. Unaweza kuwasaidiaje wagonjwa na waliozeeka?

14 Wasaidie wagonjwa na waliozeeka. Tunapowaona wengine wakiathiriwa na madhara ya dhambi ya Adamu, hapana shaka kwamba tunachochewa kuwaonyesha huruma. Tunatamani kuona magonjwa na uzee ukikomeshwa. Kwa hiyo, tunasali Ufalme wa Mungu uje. Kwa sasa, tunafanya yote tuwezayo kuwasaidia wenye uhitaji. Fikiria kile ambacho mwandishi mmoja aliandika kumhusu mama yake aliyezeeka na ambaye alikuwa na ugonjwa wa Alzheimer unaoathiri akili. Siku moja, alijikojolea. Alipokuwa akijaribu kujisafisha, kengele ya mlangoni ikalia. Kumbe alikuwa ametembelewa na Mashahidi wawili ambao walizoea kuja kumwona. Dada hao walimwuliza ikiwa alihitaji msaada wowote. Mwanamke huyo akajibu hivi: “Ni jambo la aibu, lakini ni kweli ninahitaji msaada.” Dada hao walimsaidia kujisafisha. Kisha wakampikia chai na wakawa na mazungumzo. Mwanawe alishukuru sana. Aliandika hivi: “Ninawavulia kofia Mashahidi. Wao hutenda kulingana na mambo wanayofundisha.” Je, wewe huchochewa na huruma kufanya yote uwezayo kuwapunguzia mateso wagonjwa na waliozeeka?—Flp. 2:3, 4.

15. Kazi yetu ya kuhubiri inatupatia fursa zipi muhimu?

15 Wasaidie watu kiroho. Matatizo na mahangaiko ya watu hutusukuma tuwasaidie kiroho. Njia bora ya kufanya hivyo ni kuwafundisha kumhusu Mungu na kuhusu mambo ambayo Ufalme wake utawafanyia wanadamu. Njia nyingine ni kuwasaidia waone hekima ya kuishi kulingana na viwango vya Mungu. (Isa. 48:17, 18) Je, unaweza kuongeza huduma yako, kazi ambayo kwa kweli inamheshimu Yehova na inayoonyesha kwamba unawahurumia wengine?—1 Tim. 2:3, 4.

KUWAHURUMIA WENGINE HUKUNUFAISHA PIA!

16. Mtu mwenye huruma ananufaikaje?

16 Wataalamu wa magonjwa ya akili wanasema kwamba kuwahurumia wengine kunaweza kuboresha afya yako, maisha yako, na uhusiano wako na wengine. Unapowapunguzia wengine mateso yao, unakuwa mwenye furaha zaidi, mwenye mtazamo mzuri zaidi, unapunguza upweke, na kupunguza mwelekeo wa kuwa na mawazo yasiyofaa. Naam, kuwaonyesha wengine huruma kutakunufaisha. (Efe. 4:31, 32) Wakristo wanaosukumwa na upendo kuwasaidia wengine wanathawabishwa kwa kuwa na dhamiri njema kwa sababu wanajua kwamba wanatenda kulingana na kanuni za Mungu. Mtazamo huo humsaidia mtu kuwa mzazi bora, mwenzi bora, au rafiki bora. Na pia ni rahisi zaidi kwa wale wanaowaonyesha wengine huruma, kupokea msaada na utegemezo kutoka kwa wengine uhitaji unapotokea.—Soma Mathayo 5:7; Luka 6:38.

17. Kwa nini ungependa kusitawisha na kuonyesha sifa ya huruma?

17 Kujua kwamba utanufaika unapoonyesha sifa ya huruma hakupaswi kuwa ndio sababu ya msingi inayokuchochea kusitawisha sifa hiyo. Sababu ya msingi inapaswa kuwa tamaa yako ya kumwiga na kumtukuza Yehova Mungu, Chanzo cha upendo na huruma. (Met. 14:31) Anatuwekea mfano bora kabisa. Hivyo basi, acheni tumwige kwa kuchochea upendo wenye shauku kati ya ndugu zetu na kuwa na uhusiano mzuri na jirani zetu kwa kuwaonyesha huruma.—Gal. 6:10; 1 Yoh. 4:16.