Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Neno la Mungu Lina . . . Nguvu”

“Neno la Mungu Lina . . . Nguvu”

“Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—EBR. 4:12.

NYIMBO: 96, 94

1. Kwa nini hakuna shaka kwamba Neno la Mungu lina nguvu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

TUKIWA watu wa Yehova, hatuna shaka kwamba Neno la Mungu, yaani, ujumbe wake kwa wanadamu, ‘uko hai nao una nguvu.’ (Ebr. 4:12) Maisha ya wengi wetu yanathibitisha wazi jinsi Biblia ilivyo na nguvu ya kubadili maisha ya watu. Hapo awali, baadhi ya ndugu na dada zetu walikuwa wezi, waraibu wa dawa za kulevya, au wenye mwenendo mpotovu kingono. Wengine walikuwa na ufanisi katika mfumo huu wa mambo lakini wakahisi kwamba wanakosa kitu fulani maishani mwao. (Mhu. 2:3-11) Mara kwa mara, watu ambao walionekana kuwa wamekata tamaa waliipata njia ya uzima kupitia nguvu za Biblia za kubadili maisha. Inaelekea umesoma na kufurahia sana masimulizi hayo ya maisha yaliyochapishwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi kwenye mfululizo wenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha.” Na umejionea kwamba hata baada ya kukubali kweli, Wakristo huendelea kufanya maendeleo ya kiroho kwa msaada wa Maandiko.

2. Nguvu za Neno la Mungu zilikuwa na matokeo gani kwa watu katika karne ya kwanza?

2 Je, tunapaswa kushangaa kwamba watu wengi leo wamefanya mabadiliko makubwa kwa sababu ya kujifunza Neno la Mungu? La hasha! Watu hao wanatukumbusha ndugu na dada zetu wa karne ya kwanza waliokuwa na tumaini la kwenda mbinguni. (Soma 1 Wakorintho 6:9-11.) Baada ya kuorodhesha aina ya watu ambao hawastahili kuurithi Ufalme wa Mungu, mtume Paulo aliongeza hivi: “Wengine wenu mlikuwa hivyo.” Lakini walikuwa wamefanya mabadiliko kwa msaada wa Maandiko na roho takatifu ya Mungu. Hata baada ya kukubali kweli, baadhi yao bado walihitaji kupambana ili washinde matatizo makubwa ya kiroho. Biblia inamtaja Mkristo mmoja mtiwa mafuta wa karne ya kwanza ambaye ilibidi atengwe na ushirika; baadaye alirudishwa kutanikoni. (1 Kor. 5:1-5; 2 Kor. 2:5-8) Je, hatutiwi moyo kuona jinsi ambavyo waabudu wenzetu wamekabiliana na matatizo mbalimbali na jinsi walivyoyashinda kwa msaada wa Neno la Mungu?

3. Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Kwa kuwa Neno la Mungu lina nguvu nasi tunaweza kulipata kwa urahisi, bila shaka tungependa kulitumia kikamili. (2 Tim. 2:15) Hivyo, katika makala hii, tutachunguza jinsi tunavyoweza kutumia vizuri zaidi nguvu za Neno la Mungu (1) maishani mwetu, (2) tunaposhiriki katika huduma, na (3) tunapofundisha jukwaani. Vikumbusho hivyo vitatusaidia kuonyesha kwamba tunampenda na kumshukuru Baba yetu wa mbinguni, ambaye anatufundisha ili tujifaidi wenyewe.—Isa. 48:17.

MAISHANI MWETU

4. (a) Tunahitaji kufanya nini ili Neno la Mungu libadili maisha yetu? (b) Wewe hufanya nini ili upate wakati wa kusoma Biblia?

4 Ili Neno la Mungu libadili maisha yetu, tunahitaji kulisoma kwa ukawaida—ikiwezekana kila siku. (Yos. 1:8) Ni kweli kwamba wengi wetu tuna maisha yenye shughuli nyingi sana. Hata hivyo, hatupaswi kuruhusu jambo lolote, hata majukumu ya lazima, yavuruge ratiba yetu ya kusoma Biblia. (Soma Waefeso 5:15, 16.) Watumishi wengi wa Yehova wametafuta njia mbalimbali zitakazowawezesha kupata wakati wa kusoma Biblia kila siku, iwe ni mwanzoni mwa siku, mwishoni mwa siku, au mchana. Wanahisi kama mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.”—Zab. 119:97.

5, 6. (a) Kwa nini ni muhimu kutafakari? (b) Tunaweza kufanya nini ili kutafakari kwa njia inayofaa? (c) Wewe binafsi umenufaikaje kwa kusoma Neno la Mungu na kulitafakari?

5 Zaidi ya kusoma Biblia, ni muhimu pia kutafakari mambo tunayosoma. (Zab. 1:1-3) Ni kwa kufanya hivyo ndipo tu tutakapofanikiwa kutumia kikamili hekima isiyopitwa na wakati ya Biblia. Iwe tunasoma Neno la Mungu lililochapishwa au katika mfumo wa kielektroni, tunapaswa kuwa na lengo la kuingiza mawazo yaliyo kwenye kurasa zake ndani ya moyo wetu.

6 Tunaweza kufanya nini ili tutafakari kwa njia inayofaa? Wengi wamenufaika kwa kutua kidogo baada ya kusoma sehemu fulani ya Biblia na kujiuliza maswali kama haya: ‘Habari hii inanifundisha nini kumhusu Yehova? Kufikia sasa, ninatumiaje maishani mwangu kanuni zinazopatikana katika sehemu hii ya Neno la Mungu? Ni mambo gani ninayoweza kuboresha?’ Tunaposali na kutafakari kuhusu Neno la Mungu, ndivyo tutakavyochochewa kutumia ushauri wake kikamili zaidi. Kwa hakika, tukifanya hivyo nguvu za Neno la Mungu zitabadili maisha yetu kwa kiwango kikubwa sana.—2 Kor. 10:4, 5.

KATIKA HUDUMA

7. Tunaweza kulitumiaje Neno la Mungu vizuri zaidi tunapokuwa katika huduma?

7 Ni nini kinachoweza kutusaidia kutumia vizuri Neno la Mungu katika huduma yetu? Hatua ya kwanza ni kulitumia mara nyingi tunapohubiri na kufundisha. Ndugu mmoja alifafanua hivi jambo hilo: “Ikiwa ungehubiri nyumba kwa nyumba pamoja na Yehova, je, ungetawala mazungumzo au ungempa nafasi ya kuzungumza?” Alikuwa akimaanisha hivi: Tunaposoma moja kwa moja Neno la Mungu katika huduma yetu, tunamruhusu Yehova azungumze na mwenye-nyumba. Andiko lililochaguliwa kwa makini lina nguvu nyingi zaidi kuliko jambo lolote lile tunaloweza kusema. (1 The. 2:13) Jiulize hivi: ‘Je, mimi hutumia kila fursa kuwasomea watu Neno la Mungu ninapohubiri habari njema?’

8. Kwa nini haitoshi tu kusoma maandiko tunapohubiri?

8 Bila shaka, mengi zaidi yanahusika kuliko kuwasomea tu mistari ya Biblia wale tunaozungumza nao. Kwa nini? Kwa sababu watu wengi hawaielewi Biblia au hawaijui vizuri. Ilikuwa hivyo katika karne ya kwanza, na ndivyo ilivyo leo. (Rom. 10:2) Hivyo, hatupaswi kufikiri kwamba mtu ataelewa mstari fulani kwa sababu tu tumemsomea. Tunahitaji kukazia sehemu za mstari huo, labda kwa kurudia maneno tunayotaka kukazia, na kisha kufafanua maana ya maneno hayo. Tukifanya hivyo ujumbe wa Neno la Mungu utagusa akili na mioyo ya wasikilizaji wetu kwa njia kubwa sana.—Soma Luka 24:32.

9. Tunaweza kutoa utangulizi gani wa maandiko utakaowachochea watu waiheshimu Biblia? Toa mfano.

9 Kabla ya kusoma andiko fulani, ni vizuri pia kutoa utangulizi wa andiko hilo utakaowachochea wale unaowahubiria waiheshimu Biblia. Kwa mfano, unaweza kusema, “Acha tuone kile ambacho Muumba wetu anasema kuhusu jambo hili.” Unapozungumza na mtu ambaye si Mkristo, unaweza kusema, “Ona kile ambacho Maandiko Matakatifu yanatuambia.” Au ikiwa unamhubiria mtu ambaye hana imani yeyote ya kidini, unaweza kumwuliza hivi: “Umewahi kusikia methali hii ya kale?” Naam, tunamfikiria mtu mmoja-mmoja na kubadilikana kulingana na hali zake.—1 Kor. 9:22, 23.

10. (a) Simulia jambo moja lililoonwa na ndugu fulani. (b) Umeshuhudia jinsi gani nguvu za Neno la Mungu katika huduma yako?

10 Wengi wametambua kwamba kutumia Neno la Mungu katika huduma kunaweza kuwa na matokeo makubwa sana kwa wale wanaohubiriwa. Fikiria mfano huu. Ndugu mmoja alimrudia mwanamume fulani mwenye umri mkubwa ambaye amekuwa akisoma magazeti yetu kwa miaka kadhaa. Badala ya kumpa tu toleo la karibuni la Mnara wa Mlinzi, ndugu huyo aliamua kumsomea andiko lililokuwa katika toleo hilo. Alimsomea andiko la 2 Wakorintho 1:3, 4, linalosema, “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote . . . hutufariji katika dhiki yetu yote.” Andiko hilo lilimgusa moyo sana mwanamume huyo hivi kwamba akamwomba ndugu yetu alisome kwa mara nyingine. Alieleza kwamba yeye na mke wake wanahitaji sana faraja, na sasa mwanamume huyo akaanza kupendezwa na ujumbe wa Biblia. Je, hukubali kwamba Neno la Mungu lina nguvu tunapolitumia katika huduma yetu?—Mdo. 19:20.

UNAPOFUNDISHA JUKWAANI

11. Akina ndugu wanaofundisha jukwaani wana wajibu gani?

11 Sisi sote hufurahia kuhudhuria mikutano yetu ya Kikristo na vilevile makusanyiko. Sababu kuu ya kufanya hivyo ni ili tumwabudu Yehova. Pia, tunanufaika sana na miongozo ya kiroho tunayopata. Akina ndugu wanaofundisha jukwaani katika pindi hizo wana pendeleo kubwa. Na wakati huohuo, wanapaswa kutambua kwamba wana wajibu mzito. (Yak. 3:1) Sikuzote wanapaswa kuhakikisha kwamba wanachofundisha kinategemea kabisa Neno la Mungu. Ikiwa una mgawo wa kufundisha jukwaani, unaweza kutumiaje nguvu za Neno la Mungu katika ufundishaji wako?

12. Msemaji anaweza kuhakikishaje kwamba Maandiko ndiyo sehemu ya msingi ya hotuba yake?

12 Hakikisha kwamba Maandiko ndiyo sehemu ya msingi ya hotuba yako. (Yoh. 7:16) Hilo linahusisha nini? Kwanza, uwe makini kutoruhusu mambo yaliyoonwa, mifano, au njia yako ya ufundishaji, iwakengeushe wasikilizaji kutoka katika maandiko unayosoma. Pia, kumbuka kwamba kusoma tu maandiko kadhaa hakumaanishi kwamba unafundisha kutoka katika Biblia. Kwa kweli, kutumia maandiko mengi sana kunaweza kufanya wasikilizaji wasikumbuke andiko lolote. Kwa hiyo, chagua maandiko ya msingi kwa makini, na utumie wakati wa kutosha kuyasoma, kuyaeleza, kutoa mifano, na kuonyesha jinsi ya kuyatumia maishani. (Neh. 8:8) Ikiwa unatumia muhtasari ulioandaliwa na tengenezo, soma kwa makini muhtasari huo na uchunguze maandiko yaliyomo. Jitahidi kuelewa uhusiano uliopo kati ya habari iliyo kwenye muhtasari na maandiko yaliyotajwa. Kisha, tumia maandiko uliyochagua kufundisha habari iliyo kwenye muhtasari. (Unaweza kupata mapendekezo mazuri katika somo la 21 hadi 23 kwenye kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.) Zaidi ya yote, mwombe Yehova akusaidie kuwasilisha mawazo yake yenye thamani yaliyo katika Neno lake.—Soma Ezra 7:10; Methali 3:13, 14.

13. (a) Dada mmoja alichochewaje na maandiko yaliyosomwa katika Mikutano ya Kikristo? (b) Wewe umenufaikaje na ufundishaji wa Maandiko unaotolewa katika mikutano yetu?

13 Dada mmoja nchini Australia aliguswa moyo sana na maandiko yaliyosomwa alipokuwa kwenye Mkutano wa Kikristo. Licha ya kulelewa katika hali ngumu zenye kuhuzunisha, alikubali ujumbe wa Biblia na kujiweka wakfu kwa Yehova. Hata hivyo, ilikuwa vigumu sana kwake kukubali kwamba Yehova anampenda. Lakini baada ya muda, alisadiki kwamba Mungu anampenda. Ni nini kilichomsaidia kufikia mkataa huo? Mambo yalibadilika alipotafakari kuhusu andiko lililotumiwa katika moja ya mikutano yetu na akalihusianisha na mistari mingine ya Biblia. * Je, wewe pia umewahi kuguswa moyo kwa njia hiyo na Neno la Mungu liliposomwa katika mikutano na makusanyiko?—Neh. 8:12.

14. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini Neno la Yehova?

14 Je, hatumshukuru Yehova kwa Neno lake Biblia? Aliliandaa kwa ajili ya familia ya kibinadamu na vilevile akatimiza ahadi yake kwamba lingedumu licha ya upinzani. (1 Pet. 1:24, 25) Kwa hakika, inafaa sana kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida, kulitumia maishani mwetu, na kulitumia tunapowasaidia wengine. Hivyo, tutaonyesha kwamba tunaipenda na kuithamini hazina hii kutoka kwa Mungu. Lakini jambo la muhimu hata zaidi tutaonyesha kwamba tunampenda na kumthamini Mtungaji wake, Yehova Mungu.

^ fu. 13 Ona sanduku “ Mtazamo Wangu Ulibadilika.”