Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Neno la Mungu Wetu, Litadumu Milele’

‘Neno la Mungu Wetu, Litadumu Milele’

“Majani mabichi yamekauka, ua limenyauka; lakini kwa habari ya neno la Mungu wetu, litadumu mpaka wakati usio na kipimo.”ISA. 40:8.

NYIMBO: 95, 97

1, 2. (a  Maisha yangekuwaje bila Biblia? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kunufaika na Neno la Mungu?

JE, UNAWEZA kuwazia jinsi ambavyo maisha yako yangekuwa bila Biblia? Ungekosa mashauri yenye kutegemeka kuhusu maisha ya kila siku. Ungekosa majibu yenye kuridhisha ya maswali kuhusu Mungu, uhai, na wakati ujao. Na usingejua jinsi Yehova alivyoshughulika na wanadamu wakati uliopita.

2 Tunafurahi kujua kwamba hatukabili hali hiyo yenye kukatisha tamaa, kwa sababu Yehova ametupatia Neno lake Biblia. Naye ametoa uhakikisho kwamba ujumbe wa Neno lake utadumu milele. Mtume Petro alinukuu andiko la Isaya 40:8. Ingawa mstari huo haurejelei Biblia kihususa, maneno hayo yaliyoongozwa na roho yanahusu ujumbe unaopatikana katika Biblia. (Soma 1 Petro 1:24, 25.) Bila shaka, Biblia inaweza kutunufaisha hasa ikiwa inapatikana katika lugha tunayoelewa vizuri. Kwa muda mrefu, wale wanaolipenda Neno la Mungu wametambua ukweli huo. Ingawa hali haijawa rahisi nyakati zote, kwa karne nyingi watu wanyoofu wameendelea bila kukoma kutafsiri na kusambaza Maandiko. Tamaa yao ilipatana na mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Tim. 2:3, 4.

3. Tutachunguza nini katika makala hii? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Katika makala hii, tutachunguza mifano inayoonyesha jinsi ambavyo Neno la Mungu limedumu licha ya (1) mabadiliko katika lugha, (2) mabadiliko ya kisiasa yaliyoathiri lugha iliyotumiwa na watu wengi, na (3) vipingamizi vya kutafsiri Biblia. Tutanufaikaje kwa kuchunguza mambo hayo? Kufanya hivyo kutatusaidia kulithamini zaidi Neno la Mungu. Pia, tutachochewa kumpenda zaidi Mtungaji wa Biblia, ambaye alitupatia Neno lake ili litunufaishe.—Mika 4:2; Rom. 15:4.

MABADILIKO KATIKA LUGHA

4. (a) Lugha hubadilikaje baada ya muda? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Mungu wetu hana ubaguzi kuelekea watu wa lugha fulani, na hilo linakufanya uhisije?

4 Lugha hubadilika kadiri wakati unavyopita. Baada ya muda, maneno na misemo inaweza kuwa na maana tofauti kabisa na maana ya awali. Huenda unajua baadhi ya maneno na misemo katika lugha unayozungumza ambayo maana yake imebadilika. Na hilo ni kweli pia kuhusu Kiebrania na Kigiriki, lugha ambazo zilitumiwa kuandika sehemu kubwa ya Biblia. Kiebrania na Kigiriki cha sasa kinatofautiana na Kiebrania na Kigiriki cha nyakati za Biblia. Hivyo, karibu kila mtu anayetaka kuelewa Neno la Mungu lazima asome Biblia iliyotafsiriwa, hata wale wanaojua Kiebrania au Kigiriki cha sasa. Baadhi ya watu huhisi kwamba wanapaswa kujifunza Kiebrania na Kigiriki cha kale ili wasome Biblia katika lugha za awali. Hata hivyo, jambo hilo huenda lisiwasaidie kama walivyotazamia. * Tunafurahi kwamba sasa Biblia imetafsiriwa ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 3,000 hivi. Ni wazi kwamba Yehova anataka watu wa “kila taifa na kabila na lugha” wapate fursa ya kunufaika na Neno lake. (Soma Ufunuo 14:6.) Je, hilo halikuchochei umkaribie zaidi Mungu wetu mwenye upendo na asiye na ubaguzi?—Mdo. 10:34.

5. Ni nini kilichofanya tafsiri ya King James Version iwe ya pekee?

5 Ukweli wa kwamba lugha hubadilika baada ya muda unahusu pia lugha ambazo zimetumiwa kutafsiri Biblia. Tafsiri ya Biblia ambayo mwanzoni ilieleweka kwa urahisi huenda isieleweke vizuri baada ya muda. Fikiria mfano wa tafsiri ya Biblia katika lugha ya Kiingereza. Tafsiri ya Biblia ya King James Version ilitolewa kwa mara ya kwanza mwaka 1611. Biblia hiyo ni mojawapo ya tafsiri maarufu zaidi ya Biblia katika lugha ya Kiingereza, nayo ilichangia sana ukuzi wa lugha ya Kiingereza. * Hata hivyo, tafsiri ya King James Version haikukazia sana jina la Mungu. Ilitumia jina “Yehova” kwenye mistari michache, na neno “BWANA” kwa herufi kubwa katika mistari mingine kwenye Maandiko ya Kiebrania ambako jina la Mungu lilipatikana awali. Nakala zilizochapishwa baadaye za tafsiri hiyo zilikuwa na neno “BWANA” kwa herufi kubwa katika baadhi ya mistari ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa kufanya hivyo, tafsiri ya King James Version ilitambua kwamba jina la Mungu lilistahili kuwapo katika sehemu ya Biblia inayojulikana kuwa Agano Jipya.

6. Kwa nini tunafurahi kuwa na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya?

6 Hata hivyo, maneno mengi yaliyo katika tafsiri ya King James Version yamepitwa na wakati baada ya miaka mingi kupita. Imekuwa hivyo pia kuhusu tafsiri nyingine za awali za Biblia zinazopatikana katika lugha nyingine. Hivyo basi, je, hatufurahi kwamba tuna Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inayotumia lugha ya kisasa? Tafsiri hiyo inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha zaidi ya 150, na hivyo idadi kubwa ya watu leo wanaweza kuipata. Maneno yaliyotumiwa yanaeleweka wazi na hivyo ujumbe wa Neno la Mungu hugusa mioyo yetu. (Zab. 119:97) Jambo linalopendeza hata zaidi ni kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imerudisha jina la Mungu katika mahali pake panapofaa katika Maandiko.

LUGHA INAYOTUMIWA NA WATU WENGI

7, 8. (a) Kwa nini Wayahudi wengi katika karne ya tatu K.W.K. hawakuelewa Maandiko ya Kiebrania? (b) Septuajinti ya Kigiriki ni nini?

7 Nyakati nyingine, mabadiliko ya kisiasa yamechangia katika kuamua ni lugha gani itakayotumiwa na watu wengi katika kipindi fulani cha wakati. Mungu amehakikishaje kwamba mabadiliko hayo hayazuii Neno lake lisieleweke? Jambo fulani lililotendeka zamani litatusaidia kupata jibu. Vitabu 39 vya kwanza vya Biblia viliandikwa na Waisraeli, yaani, Wayahudi. Hao ndio watu ambao mwanzoni “walikabidhiwa maneno matakatifu ya Mungu.” (Rom. 3:1, 2) Hata hivyo, kufikia karne ya tatu K.W.K., Wayahudi wengi hawakuelewa Kiebrania. Kwa nini? Kwa sababu Aleksanda Mkuu alikuwa amepanua Milki ya Ugiriki aliposhinda maeneo mbalimbali vitani. (Dan. 8:5-7, 20, 21) Kadiri milki hiyo ilivyopanuka ndivyo Kigiriki kikawa lugha iliyotumiwa na raia wengi, kutia ndani Wayahudi waliokuwa wametawanyika kotekote katika milki hiyo. Lakini kadiri lugha ya Kigiriki ilivyoanza kutumiwa na Wayahudi wengi, ndivyo ilivyokuwa vigumu kwa wengi wao kuelewa Maandiko ya Kiebrania. Suluhisho lingekuwa nini?

8 Kufikia katikati ya karne ya tatu K.W.K., vitabu vitano vya kwanza vya Biblia vilikuwa vimetafsiriwa kutoka Kiebrania hadi Kigiriki. Kazi ya kutafsiri vitabu vingine vya Maandiko ya Kiebrania ilikamilika katika karne ya pili K.W.K. Mkusanyo wa vitabu hivyo vya Biblia ulikuja kujulikana kuwa Septuajinti ya Kigiriki. Tafsiri ya Septuajinti ndiyo tafsiri ya kwanza ya Maandiko yote ya Kiebrania.

9. (a) Septuajinti na tafsiri nyingine za mapema ziliwasaidiaje wasomaji wa Neno la Mungu? (b) Ni sehemu gani ya Maandiko ya Kiebrania unayopenda zaidi?

9 Septuajinti hiyo iliwasaidia sana Wayahudi na watu wengine waliozungumza Kigiriki kusoma na kuelewa Maandiko ya Kiebrania. Hebu wazia jinsi walivyosisimka kusikia au kusoma Neno la Mungu ambalo sasa lilipatikana katika lugha yao ya mama, lugha ya Kigiriki! Baada ya muda, baadhi ya sehemu za Biblia zilitafsiriwa katika lugha nyingine zilizotumiwa na watu wengi, kama vile Kisiria, Kigothi, na Kilatini. Kadiri watu wengi walivyochunguza Maandishi Matakatifu katika lugha waliyoelewa, ndivyo walivyozidi kuyafurahia. Hivyo, wakawa na mistari waliyoipenda zaidi, kama tu ilivyo kwetu leo. (Soma Zaburi 119:162-165.) Kwa hakika, Neno la Mungu limedumu licha ya mabadiliko katika lugha zilizotumiwa na watu wengi.

VIPINGAMIZI VYA KUTAFSIRI BIBLIA

10. Kwa nini ilikuwa vigumu sana kwa watu wengi walioishi katika kipindi cha John Wycliffe kuwa na Biblia?

10 Nyakati nyingine, watu wenye mamlaka wamejaribu kufanya Biblia isiwafikie watu wa kawaida. Hata hivyo, watu wanyoofu wamesimama imara licha ya vipingamizi hivyo. Kwa mfano, mfikirie mwanatheolojia wa karne ya 14 anayeitwa John Wycliffe. Aliamini kabisa kwamba kila mtu anapaswa kunufaika na Neno la Mungu. Lakini aliishi katika kipindi ambacho watu wa kawaida nchini Uingereza hawangeweza kupata Biblia. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba watu wengi hawangeweza kununua Biblia kwa kuwa nakala za Biblia ziliandikwa kwa mkono na ilikuwa ghali sana kuzitayarisha. Isitoshe, watu wengi hawakujua kusoma. Lakini huenda walisikia mistari ya Biblia ikisomwa walipoenda kanisani. Hata hivyo, inatiliwa shaka ikiwa walielewa walichosikia. Kwa nini? Kwa sababu Biblia iliyotumiwa kanisani (tafsiri ya Vulgate) ilikuwa ya Kilatini. Zaidi ya hilo, kufikia Enzi za Kati, lugha ya Kilatini haikuwa ikitumiwa na watu wa kawaida! Wangewezaje kuelewa hazina zenye thamani za Biblia?—Met. 2:1-5.

John Wycliffe na wengine walitamani Neno la Mungu lipatikane kwa watu wote. Je, wewe pia una tamaa kama yao? (Tazama fungu la 11)

11. Biblia ya Wycliffe ilikuwa na matokeo gani?

11 Katika 1382, tafsiri ya Kiingereza ambayo ilikuja kuitwa Biblia ya Wycliffe iliandikwa. Ndani ya kipindi kifupi, ilipendwa sana na wafuasi wa Wycliffe. Wakiwa na hamu kubwa ya kuhakikisha kwamba Neno la Mungu linafikia akili na mioyo ya watu wa kawaida, wahubiri waliojulikana kuwa Lollards, walisafiri kwa miguu kutoka kijiji hadi kijiji nchini Uingereza. Mara nyingi wahubiri hao waliwasomea watu waliokutana nao sehemu za Biblia ya Wycliffe na kuwaachia nakala zilizoandikwa kwa mkono. Jitihada zao zilikuwa sehemu ya msingi iliyochochea upya tamaa ya watu ya kulipenda Neno la Mungu.

12. Makasisi walimpingaje Wycliffe na jitihada zake?

12 Makasisi walitendaje? Walimchukia Wycliffe, tafsiri yake ya Biblia, na wafuasi wake. Viongozi wa kidini waliwatesa wahubiri hao waliojulikana kuwa Lollards, na walitafuta na kuharibu nakala zozote walizopata za Biblia ya Wycliffe. Hata baada ya Wycliffe kufa, bado alihukumiwa kuwa mwasi. Hata hivyo, haiwezekani kumwadhibu mtu aliyekufa. Lakini makasisi waliagiza mifupa ya Wycliffe itolewe kaburini na ichomwe, na majivu yatupwe kwenye Mto Swift. Ingawa hivyo, Kanisa halikuweza kuzuia nguvu za Neno la Mungu kuwachochea watu waliokuwa na tamaa ya kulisoma na kulielewa. Katika karne zilizofuata, wengi katika Bara la Ulaya na katika sehemu nyingine za dunia, walisaidia kutafsiri na kusambaza Biblia kwa faida ya watu wa kawaida.

“YEYE ANAYEKUFUNDISHA ILI UJIFAIDI MWENYEWE”

13. Tuna uhakika gani, na hilo linaimarishaje imani yetu?

13 Leo, Wakristo hawapaswi kufikiri kwamba kazi ya kutafsiri Septuajinti, Biblia ya Wycliffe, tafsiri ya King James Version, au tafsiri yoyote nyingine imeongozwa na roho ya Mungu. Hata hivyo, tunapochunguza historia ya tafsiri hizo na nyinginezo zilizochapishwa, tunapata uhakika wa jambo hili: Kama tu ambavyo Yehova aliahidi, Neno lake limedumu. Je, hilo haliimarishi imani yako kwamba ahadi nyingine zote ambazo Yehova ameahidi zitatimia?—Yos. 23:14.

14. Neno la Mungu linatusaidiaje kuongeza upendo wetu Kwake?

14 Zaidi ya kuimarisha imani yetu, kuchunguza jinsi ambavyo Biblia imedumu kwa karne nyingi kunaongeza upendo wetu kwa Yehova. * Kwa nini Yehova alitupatia Neno lake? Na kwa nini alitoa uhakikisho kwamba lingedumu licha ya upinzani? Kwa sababu anatupenda, na anataka kutufundisha jinsi tunavyoweza kujifaidi wenyewe. (Soma Isaya 48:17, 18.) Hivyo, kwa kuwa Yehova alionyesha kwamba anatupenda, inafaa tuonyeshe kwamba tunathamini upendo wake kwa kumpenda na kutii amri zake.—1 Yoh. 4:19; 5:3.

15. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

15 Ni jambo linaloeleweka kwamba kwa kuwa tunalithamini Neno la Mungu, tutajitahidi kunufaika nalo kikamili. Tunaweza kufanyaje ili tunufaike kikamili na usomaji wetu wa Biblia? Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia watu tunaokutana nao katika huduma waithamini zaidi Biblia? Wale wanaofundisha kutanikoni wanaweza kutumiaje Maandiko kuwa msingi wa mambo wanayofundisha? Tutachunguza majibu ya maswali hayo katika makala inayofuata.

^ fu. 4 Tazama makala yenye kichwa “Je, Unahitaji Kujifunza Kiebrania na Kigiriki?” katika toleo la Novemba 1, 2009, la Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 5 Misemo kadhaa ya Kiingereza ilitokana na tafsiri ya King James Version. Mifano ya misemo hiyo ni kama vile: “kuanguka chini kifudifudi,” “ngozi ya meno yangu,” na “mimineni moyo wenu.”—Hes. 22:31; Ayu. 19:20; Zab. 62:8.

^ fu. 14 Ona sanduku “ Jionee Mwenyewe!