Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sitawisha Sifa ya Kujizuia

Sitawisha Sifa ya Kujizuia

“Matunda ya roho ni . . . kujizuia.”GAL. 5:22, 23.

NYIMBO: 121, 36

1, 2. (a) Kukosa sifa ya kujizuia kunaweza kusababisha madhara gani? (b) Kwa nini ni muhimu kuchunguza sifa ya kujizuia leo?

KUJIZUIA ni sifa ambayo Yehova Mungu anaweza kutusaidia kusitawisha. (Gal. 5:22, 23) Yehova huonyesha sifa hiyo kikamilifu. Hata hivyo, wanadamu si wakamilifu, kwa hiyo wanahitaji kupambana sana ili kudumisha sifa ya kujizuia. Kwa kweli, matatizo mengi ambayo watu wanakabili leo yanatokana na kushindwa kuonyesha sifa ya kujizuia. Kukosa kuonyesha sifa hiyo huwafanya watu waahirishe mambo na wakose kutimiza majukumu yao shuleni au kazini. Pia, kunaweza kuwafanya watu wawatukane wengine, wawe walevi, wajeuri, watalikiane, wawe na madeni yasiyo ya lazima, wawe waraibu, wafungwe jela, wawe na matatizo ya kihisia, wapate magonjwa ya kuambukizwa kingono, na mimba zisizotakiwa. Hayo ni baadhi tu matokeo mabaya ya kukosa sifa ya kujizuia.—Zab. 34:11-14.

2 Ni wazi kwamba watu wanaokosa sifa ya kujizuia husababisha matatizo katika maisha yao na ya watu wengine. Na tatizo la kukosa sifa ya kujizuia linaendelea kuongezeka. Katika miaka ya 1940, wasomi walichunguza sifa ya kujizuia, lakini uchunguzi wa karibuni unaonyesha kwamba watu wanashindwa zaidi na zaidi kuonyesha sifa ya kujizuia. Hilo halitushangazi sisi tunaojifunza Neno la Mungu kwa sababu Biblia ilitabiri kwamba uthibitisho mmoja unaoonyesha kuwa tunaishi katika “siku za mwisho” ni kuwa watu watakuwa “wasiojizuia.”—2 Tim. 3:1-3.

3. Ni kwa nini Wakristo wanapaswa kusitawisha sifa ya kujizuia?

3 Kwa nini unapaswa kusitawisha sifa ya kujizuia? Fikiria sababu mbili muhimu. Kwanza, imeonekana kwamba kwa ujumla watu wanaojidhibiti hawapati matatizo mengi maishani. Wana utulivu zaidi wa kihisia, wana uwezo wa kuanzisha urafiki wenye kujenga, na si wenye hasira, mahangaiko, au kushuka moyo kama watu wasioweza kujidhibiti. Pili, uwezo wa kupinga vishawishi na wa kudhibiti tamaa zisizofaa ni jambo la msingi ili tudumishe kibali cha Mungu. Dhambi ambayo Adamu na Hawa walifanya inathibitisha ukweli huo. (Mwa. 3:6) Fikiria pia matokeo mabaya ambayo wengine wamepata tangu wakati huo kwa kushindwa kuonyesha sifa hiyo muhimu.

4. Ni nini kinachoweza kumtia moyo yeyote anayepambana kuonyesha sifa ya kujizuia?

4 Mwanadamu asiye mkamilifu hawezi kuonyesha sifa ya kujizuia kikamilifu. Yehova anajua jinsi watumishi wake wanavyojitahidi ili kuonyesha sifa hiyo na anataka kuwasaidia wadhibiti mielekeo yao ya dhambi. (1 Fal. 8:46-50) Kama Rafiki mwenye upendo, anawatia moyo kwa upendo watu wanyoofu wanaotamani kumtumikia lakini wanashindwa kuonyesha sifa ya kujizuia katika mambo fulani. Acheni tuchunguze mfano mkamilifu wa Yehova wa kuonyesha sifa hiyo. Kisha tutajifunza kutokana na mifano mizuri na mibaya iliyo katika Biblia. Na pia tutazungumzia mapendekezo yatakayotusaidia kuboresha sifa ya kujizuia.

YEHOVA ANATUWEKEA KIELELEZO

5, 6. Yehova ameweka kielelezo gani kuhusiana na sifa ya kujizuia?

5 Yehova huonyesha sifa ya kujizuia kikamilifu, kwa kuwa kila kitu anachofanya ni kikamilifu. (Kum. 32:4) Lakini sisi si wakamilifu. Hata hivyo, ili tuelewe vizuri sifa hiyo, tunahitaji kuchunguza kielelezo cha Yehova ili tuweze kumwiga vizuri zaidi. Ni katika pindi gani ambapo Yehova alionyesha sifa ya kujizuia?

6 Fikiria jinsi Yehova alivyoonyesha sifa ya kujizuia aliposhughulika na mwenendo wa uasi na wenye kukosa heshima wa Shetani. Suala hilo lilihitaji kutatuliwa. Hakuna shaka kwamba dai la Ibilisi liliwachukiza, kuwakasirisha, na kuwaudhi viumbe wa kiroho washikamanifu kwa Mungu. Huenda unahisi vivyo hivyo unapofikiria mateso yote ambayo Shetani amesababisha. Lakini Yehova hakuchukua hatua haraka-haraka. Alitenda kwa njia inayofaa kabisa. Ameonyesha kwamba yeye si mwepesi wa hasira na ametenda kwa haki katika kushughulika na uasi wa Shetani. (Kut. 34:6; Ayu. 2:2-6) Kwa nini Yehova ameruhusu muda upite? Kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali “hutaka wote wafikie toba.”—2 Pet. 3:9.

7. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo cha Yehova?

7 Kielelezo cha Yehova cha kuonyesha sifa ya kujizuia kinatufundisha kwamba tunapaswa kufikiria kwa uzito maneno na matendo yetu; hatupaswi kutenda haraka-haraka bila kufikiri. Unapofanya maamuzi muhimu, jipe muda wa kutosha ili utende kwa hekima. Sali ili upate hekima ya kusema au kufanya jambo linalofaa. (Zab. 141:3) Ni rahisi zaidi kuongozwa na hisia unapokasirika. Wengi wetu tumejutia maneno au matendo tuliyofanya bila kufikiri!—Met. 14:29; 15:28; 19:2.

MIFANO MIZURI NA MIBAYA YA WATUMISHI WA MUNGU

8. (a) Tunaweza kupata wapi mifano ya watu wenye sifa zinazompendeza Mungu? (b) Ni nini kilichomsaidia Yosefu kujizuia mke wa Potifa alipojaribu kumshawishi? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

8 Ni mifano gani katika Biblia inayokazia thamani ya kudhibiti matendo yetu? Bila shaka, unaweza kukumbuka watu kadhaa wanaotajwa katika Biblia walioonyesha sifa ya kujizuia walipojaribiwa. Mfano mmoja ni wa Yosefu mwana wa Yakobo. Alionyesha sifa ya kujizuia alipokuwa akitumikia katika nyumba ya Potifa, mkuu wa walinzi wa Farao. Mke wa Potifa alianza kumtamani Yosefu, ambaye alikuwa “mwenye umbo zuri na mwenye sura ya kupendeza,” naye akajaribu kumshawishi. Ni nini kilichomsaidia Yosefu asinaswe na ushawishi wake wa mara kwa mara? Hapana shaka kwamba alitumia muda kufikiria matokeo mabaya ya kulegeza msimamo wake. Na hali ilipokuwa mbaya zaidi, akakimbia. Alifikiri hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?”—Mwa. 39:6, 9; soma Methali 1:10.

9. Unaweza kujiandaa jinsi gani kupinga vishawishi?

9 Mfano wa Yosefu unatufundisha nini? Jambo moja tunalojifunza ni kwamba huenda tukahitaji kukimbia tunaposhawishiwa kuvunja mojawapo ya sheria za Mungu. Wakati uliopita, baadhi ya watu ambao sasa ni Mashahidi walipambana ili waache mazoea kama vile kula na kunywa kupita kiasi, kuvuta sigara, kutumia dawa za kulevya, upotovu wa maadili katika ngono, na mazoea mengine kama hayo. Hata baada ya kubatizwa, nyakati nyingine huenda wakashawishiwa kurudia mazoea yao ya zamani. Lakini ikiwa utashawishiwa kuvunja sheria ya Yehova, jiimarishe kwa kutumia muda kutafakari matokeo mabaya ya kiroho unayoweza kupata kwa kushindwa kudhibiti tamaa zenye dhambi. Unaweza kufikiria mapema hali ambazo zinaweza kutokeza kishawishi na kuamua jinsi utakavyoziepuka. (Zab. 26:4, 5; Met. 22:3) Na ikiwa utakabili kishawishi hicho, mwombe Yehova akupe hekima na akusaidie kuonyesha sifa ya kujizuia ili ukipinge.

10, 11. (a) Vijana wengi wanalazimika kukabili hali gani shuleni? (b) Ni nini kinachoweza kuwasaidia vijana Wakristo kupinga mikazo ya kujihusisha katika mwenendo usiofaa?

10 Vijana wengi Wakristo hukabili kishawishi kama cha Yosefu. Mfikirie Kim. Wengi kati ya wanafunzi wenzake walifanya ngono, na baada ya mwisho-juma walisimulia kwa majivuno habari kuhusu mahusiano yao ya kingono. Kim hakuwa na habari kama hizo za kuwasimulia. Anakiri kwamba nyakati nyingine kuwa tofauti kulifanya ahisi “mpweke na asiyependwa” na kwamba wanafunzi wenzake walimwona kuwa mjinga kwa sababu hakuwa na rafiki wa kiume. Hata hivyo, Kim alifahamu vizuri kwamba vijana wengi walikuwa na tamaa kubwa ya kufanya ngono. (2 Tim. 2:22) Mara nyingi, wanafunzi wenzake walimwuliza ikiwa bado yeye ni bikira. Na hilo lilimpa fursa ya kueleza kwa nini hangefanya ngono. Tunajivunia vijana Wakristo ambao wameazimia kupinga mkazo wa kujihusisha katika mwenendo mpotovu kingono, na Yehova pia anajivunia vijana hao!

11 Biblia ina mifano inayoonya ya watu waliokosa kujizuia kuhusiana na mwenendo mpotovu kingono. Inaonyesha pia matokeo yenye kuhuzunisha yanayoweza kutokana na mwenendo huo wa kukosa kujizuia. Yeyote anayekabili hali kama ya Kim anahitaji kutafakari kisa cha kijana asiye na hekima anayeelezewa katika Methali sura ya 7. Fikiria pia, mwenendo wa Amnoni na matokeo mabaya ya matendo yake. (2 Sam. 13:1, 2, 10-15, 28-32) Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao kuwa na hekima na kusitawisha sifa ya kujizuia inapohusu urafiki wa kimahaba kwa kuzungumzia habari hizo wakati wa ibada ya familia wakitumia Maandiko yaliyotajwa hapo juu.

12. (a) Yosefu alidhibiti hisia zake jinsi gani aliposhughulika na kaka zake? (b) Tunapaswa kudhibiti hisia zetu katika hali zipi?

12 Katika pindi nyingine, Yosefu aliweka tena mfano mzuri wa kujizuia. Ili aelewe kilichokuwa moyoni mwa kaka zake, Yosefu hakujitambulisha kwao walipokuja Misri kununua chakula. Na alipolemewa sana na hisia, alienda faraghani ili wasimwone akilia. (Mwa. 43:30, 31; 45:1) Mkristo mwenzako au mtu unayempenda anapofanya uamuzi mbaya, kujidhibiti kama alivyofanya Yosefu kunaweza kukusaidia kuepuka kutenda bila kufikiri. (Met. 16:32; 17:27) Ikiwa una watu wa familia waliotengwa, huenda ukahitaji kudhibiti hisia zako ili uepuke kushirikiana nao isivyo lazima. Kujidhibiti katika hali hizo hakujitokezi tu bila jitihada, hata hivyo, itakuwa rahisi zaidi kwetu ikiwa tutatambua kwamba tunaiga kielelezo cha Mungu na matendo yetu yanapatana na shauri lake.

13. Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi la Mfalme Daudi?

13 Biblia ina mfano wenye kutokeza wa Mfalme Daudi. Alikuwa na mamlaka kubwa lakini alijidhibiti asitumie mamlaka yake kwa hasira alipochokozwa na Sauli na Shimei. (1 Sam. 26:9-11; 2 Sam. 16:5-10) Hilo halimaanishi kwamba Daudi alijidhibiti sikuzote, kwa kuwa tunajua alifanya dhambi na Bath-sheba. Pia tunasoma kuhusu jinsi alivyotaka kumtendea Nabali mwenye pupa. (1 Sam. 25:10-13; 2 Sam. 11:2-4) Hata hivyo, tunaweza kujifunza mambo muhimu kutoka kwa Daudi. Kwanza, waangalizi miongoni mwa watu wa Mungu wanahitaji kujitahidi sana kuonyesha sifa ya kujizuia ili wasitumie mamlaka yao vibaya. Pili, kila mtu anapaswa kujihadhari, kwa kuwa hakuna asiyeweza kushawishiwa.—1 Kor. 10:12.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

14. Ndugu mmoja alipatwa na hali gani, na kwa nini ni muhimu tuzingatie tutakavyotenda katika hali kama hizo?

14 Unaweza kufanya nini ili uboreshe sifa ya kujizuia? Fikiria kisa hiki halisi. Gari la Luigi liligongwa upande wa nyuma na gari lingine. Licha ya kuwa dereva wa gari hilo ndiye aliyekuwa amekosea, alimtukana Luigi na kujaribu kuanzisha ugomvi. Luigi alisali, akimwomba Yehova amsaidie kuwa mtulivu, na akajaribu kumtuliza dereva huyo, lakini hakufanikiwa. Luigi aliandika taarifa za bima za dereva huyo na kuondoka huku mwanamume huyo akipiga kelele. Juma moja baadaye, Luigi alifanya ziara ya kurudia kwa mwanamke fulani na akagundua kwamba mume wake ndiye dereva aliyemtukana! Mwanamume huyo aliaibika na kuomba msamaha kwa jinsi alivyotenda. Alijitolea kuwasiliana na kampuni ya bima ya Luigi ili aharakishe malipo. Mwanamume huyo alishiriki katika mazungumzo hayo ya kiroho na alithamini sana mambo aliyosikia. Anapotafakari, Luigi anaona jinsi ilivyokuwa muhimu kuendelea kuwa mtulivu baada ya aksidenti hiyo na jinsi ambavyo hali ingekuwa mbaya ikiwa angekosa kujizuia.—Soma 2 Wakorintho 6:3, 4.

Huduma yetu ya Kikristo inaweza kuathiriwa ikitegemea kama tutakuwa watulivu au tutakasirika tunapochokozwa (Tazama fungu la 14)

15, 16. Kujifunza Biblia kunaweza kukusaidiaje wewe na familia yako kusitawisha sifa ya kujizuia?

15 Kujifunza Biblia kwa bidii na kwa makini kutawasaidia Wakristo kusitawisha sifa ya kujizuia. Kumbuka kwamba Mungu alimwambia Yoshua hivi: “Kitabu hiki cha sheria kisiondoke katika kinywa chako, nawe ukisome kwa sauti ya chini mchana na usiku, upate kuangalia kufanya kulingana na yote ambayo yameandikwa ndani yake; kwa maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.” (Yos. 1:8) Kujifunza Biblia kunaweza kukusaidiaje kusitawisha sifa ya kujizuia?

16 Kama ambavyo tumeona, Biblia ina masimulizi yanayoonyesha waziwazi manufaa na madhara ya matendo yetu. Yehova alihakikisha kwamba masimulizi hayo yameandikwa kwa kusudi fulani. (Rom. 15:4) Ni jambo la hekima sana kuyasoma, kuyatafakari, na kujifunza kuyahusu! Jaribu kuelewa jinsi unavyoweza kuyatumia maishani na katika familia yako. Mwombe Yehova akusaidie kutumia ushauri wa Neno lake. Ikiwa unatambua kwamba unashindwa kuonyesha sifa ya kujizuia katika jambo fulani maishani, usipuuze jambo hilo. Sali kulihusu, na ujitahidi kuona jinsi unavyoweza kuboresha sifa hiyo. (Yak. 1:5) Bila shaka, kufanya utafiti katika machapisho yetu ya Kikristo kunaweza kukusaidia kupata habari hususa zinazoweza kukunufaisha zaidi.

17. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wasitawishe sifa ya kujizuia?

17 Unaweza kuwasaidiaje watoto wako wasitawishe sifa ya kujizuia? Wazazi wanajua kwamba watoto hawazaliwi na sifa hiyo. Na kama ilivyo kwa sifa nyingine zote ambazo watoto wanahitaji kujifunza, wazazi wanapaswa kuwawekea kielelezo. (Efe. 6:4) Kwa hiyo, ukiona watoto wako wanashindwa kudhibiti hisia zao, jiulize ikiwa unawawekea kielelezo kizuri. Usipuuze umuhimu wa mfano wako wa kuwa wa kawaida katika utumishi wa shambani, kuhudhuria mikutano, na kuongoza ibada ya familia. Usiogope kusema hapana ikiwa watoto wako wanaomba jambo fulani unaloona halifai! Yehova aliwawekea Adamu na Hawa mipaka, ambayo ikiwa wangeifuata ingewachochea kuheshimu mamlaka. Vivyo hivyo, nidhamu na kielelezo cha wazazi kimekusudiwa kuwafundisha watoto kusitawisha sifa ya kujizuia. Miongoni mwa mambo muhimu zaidi unayoweza kufanya ni kuwasaidia watoto wako wapende mamlaka ya Mungu na kuheshimu viwango vyake.—Soma Methali 1:5, 7, 8.

18. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba rafiki wazuri ni baraka?

18 Bila shaka, iwe wewe ni mzazi au la, hupaswi kupuuza umuhimu wa kuchagua rafiki zako kwa hekima. Jitahidi kushirikiana na watu wanaokutia moyo kufikia malengo yanayofaa na kuepuka matatizo. (Met. 13:20) Rafiki wanaozingatia mambo ya kiroho maishani watakuchochea uige kielelezo chao cha kujizuia. Na hapana shaka kwamba mwenendo wako utawatia moyo rafiki zako. Sifa ya kujizuia uliyositawisha ni muhimu ili ufurahie kibali cha Mungu kila siku na ushiriki mambo mazuri pamoja na wapendwa wako.