Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Uwe Hodari . . . Nawe Utende”

“Uwe Hodari . . . Nawe Utende”

“Uwe hodari na mwenye nguvu nawe utende. Usiogope wala usiwe na hofu, kwa maana Yehova . . . yuko pamoja nawe.”—1 NYA. 28:20.

NYIMBO: 38, 34

1, 2. (a) Sulemani alipewa mgawo gani muhimu? (b) Kwa nini Daudi alikuwa na wasiwasi ikiwa Sulemani angeweza kutimiza mgawo huo?

SULEMANI alipewa kazi ya kusimamia mradi mkubwa na muhimu zaidi wa ujenzi, yaani, mradi wa ujenzi wa hekalu lililokuwa Yerusalemu. Jengo hilo lingekuwa lenye “utukufu zaidi kwa ajili ya uzuri wenye heshima kwa nchi zote.” La muhimu zaidi, hekalu hilo lingekuwa “nyumba ya Yehova, Mungu wa kweli.” Yehova aliagiza kwamba Sulemani asimamie mradi huo.—1 Nya. 22:1, 5, 9-11.

2 Mfalme Daudi alikuwa na uhakika kwamba Mungu angemtegemeza Sulemani, lakini Sulemani alikuwa “mchanga na mwororo.” Je, angekuwa na uhodari au ujasiri wa kufanya kazi hiyo ya kujenga hekalu? Je, kuwa mchanga na kutokuwa na uzoefu kungemzuia kutimiza kazi hiyo? Ili kufanikiwa, Sulemani angehitaji kuwa hodari au jasiri na kutenda.

3. Sulemani angeweza kujifunza nini kuhusu ujasiri kutoka kwa baba yake?

3 Inaelekea Sulemani alijifunza mengi kuhusu ujasiri kutoka kwa baba yake. Alipokuwa kijana, Daudi alipigana na wanyama wa mwituni waliochukua kondoo za baba yake. (1 Sam. 17:34, 35) Alionyesha ujasiri mwingi alipopambana na lile jitu shujaa la vita, Goliathi. Naam, kwa msaada wa Mungu, alitumia jiwe dogo na kulishinda jitu hilo.—1 Sam. 17:45, 49, 50.

4. Kwa nini Sulemani alihitaji kuwa mwenye ujasiri?

4 Wakati ulipofika, Daudi ndiye aliyestahili kabisa kumtia moyo Sulemani awe jasiri na kulijenga hekalu hilo! (Soma 1 Mambo ya Nyakati 28:20.) Ikiwa Sulemani hangekuwa hodari au jasiri, hofu ingeweza kufanya ashindwe hata kuianza kazi aliyopewa. Ingekuwa afadhali aanze kazi hiyo na kushindwa kuliko kutofanya lolote.

5. Kwa nini tunahitaji ujasiri?

5 Kama Sulemani, sisi pia tunahitaji msaada wa Yehova ili tuwe na ujasiri na kutimiza kazi. Ili tufanikiwe, tunahitaji kuchunguza baadhi ya mifano ya watu wa zamani walioonyesha ujasiri. Pia, tunaweza kutafakari kuhusu njia tunazoweza kuonyesha ujasiri ili kutimiza kazi yetu.

MIFANO YA WATU WALIOONYESHA UJASIRI

6. Ni nini kinachokupendeza kuhusu ujasiri wa Yosefu?

6 Fikiria ujasiri ambao Yosefu alionyesha mke wa Potifa alipomshawishi afanye ngono naye. Bila shaka alijua kwamba angepatwa na matokeo mabaya sana ikiwa angemkataa. Hata hivyo, badala ya kukubali kushawishiwa, alionyesha ujasiri na kukataa mara moja.—Mwa. 39:10, 12.

7. Eleza jinsi Rahabu alivyoonyesha ujasiri. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

7 Rahabu ni mfano mwingine wa ujasiri. Wapelelezi Waisraeli walipofika nyumbani kwake huko Yeriko, Rahabu angeweza kuingiwa na woga na kuwafukuza. Lakini akiwa na uhakika katika Yehova, kwa ujasiri aliwaficha wanaume hao wawili na baadaye kuwasaidia kutoroka. (Yos. 2:4, 5, 9, 12-16) Rahabu alijua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli, na aliamini kwamba kwa njia moja au nyingine, Yehova angewapa Waisraeli nchi hiyo. Rahabu hakuruhusu woga wa mwanadamu yeyote, kutia ndani mfalme wa Yeriko na wanaume wake, umzuie kutenda. Badala yake, alitenda kwa njia ambayo mwishowe iliokoa uhai wake na wa familia yake.—Yos. 6:22, 23.

8. Ujasiri wa Yesu uliwasaidiaje mitume?

8 Mitume waaminifu wa Yesu walituwekea mfano mzuri wa ujasiri. Walikuwa wameona ujasiri ambao Yesu alionyesha. (Mt. 8:28-32; Yoh. 2:13-17; 18:3-5) Mfano wa Yesu uliwasaidia kuwa na ujasiri. Walipopingwa na Masadukayo, mitume hawakuacha kufundisha kwa msingi wa jina la Yesu.—Mdo. 5:17, 18, 27-29.

9. Andiko la 2 Timotheo 1:7 linatusaidiaje kutambua mahali tunapoweza kupata ujasiri?

9 Yosefu, Rahabu, Yesu, na mitume walionyesha ujasiri uliowachochea kufanya mambo mengi mazuri. Ujasiri walioonyesha haukutokana na kujiamini kupita kiasi. Ulitokana na kumtegemea Yehova. Sisi pia hukabili hali zinazohitaji tuonyeshe ujasiri. Badala ya kujitegemea, tunapaswa kumtegemea Yehova. (Soma 2 Timotheo 1:7.) Tuchunguze maeneo mawili ambayo tunahitaji kuonyesha ujasiri, yaani, katika familia na kutanikoni.

HALI ZINAZOHITAJI UJASIRI

10. Kwa nini vijana Wakristo wanahitaji ujasiri?

10 Vijana Wakristo wanahitaji kuonyesha ujasiri katika hali mbalimbali ili wamtumikie Yehova. Wanaweza kujifunza na kuiga mfano wa Sulemani aliyeonyesha ujasiri alipofanya maamuzi ya hekima yaliyomsaidia kukamilisha ujenzi wa hekalu. Ingawa vijana Wakristo wanaweza na wanapaswa kupata mwongozo kutoka kwa wazazi wao, bado wao wenyewe wanahitaji kufanya maamuzi muhimu. (Met. 27:11) Wanahitaji kufanya maamuzi ya hekima kuhusu marafiki, burudani, usafi wa kiadili, na ubatizo, na yote hayo yanahitaji ujasiri. Hiyo ni kwa sababu vijana hao wanaenda kinyume na yale ambayo Shetani, anayemdhihaki Mungu, angependa wafanye.

11, 12. (a) Musa aliwekaje mfano mzuri wa ujasiri? (b) Vijana wanawezaje kumwiga Musa?

11 Uamuzi mmoja muhimu ambao vijana wanapaswa kufanya unahusu miradi yao. Katika nchi fulani, vijana hushinikizwa kuwa na miradi itakayowasaidia kupata elimu ya juu na kazi yenye mshahara mnono. Katika nchi nyingine, hali za kiuchumi huwafanya vijana wahisi kwamba wanapaswa kutanguliza miradi itakayowasaidia kutunza familia zao kimwili. Ikiwa utakabili moja kati ya hali hizo, fikiria mfano wa Musa. Kwa kuwa alilelewa na binti ya Farao, Musa angeweza kuwa na miradi ya kutafuta umashuhuri na hali nzuri ya kiuchumi. Bila shaka alikabili shinikizo kali kutoka kwa familia ya Farao iliyomlea, walimu, na washauri wake! Lakini badala ya kukubali kushinikizwa, kwa ujasiri Musa alichukua msimamo upande wa ibada safi. Baada ya kuacha mali za Misri, kwa ujasiri Musa alimtegemea Yehova. (Ebr. 11:24-26) Uamuzi huo ulimletea baraka za Yehova, na hapana shaka kwamba atapata baraka nyingi zaidi wakati ujao.

12 Vivyo hivyo, Yehova atawabariki vijana ambao kwa ujasiri wanajiwekea miradi ya kiroho na kutanguliza masilahi ya Ufalme maishani. Atawasaidia kutunza familia zao. Katika karne ya kwanza, kijana Timotheo alitanguliza miradi ya kiroho, nawe pia unaweza kufanya hivyo. *Soma Wafilipi 2:19-22.

Je, umeazimia kuonyesha ujasiri katika sehemu zote za maisha yako? (Tazama fungu la 13 hadi 17)

13. Ujasiri ulimsaidiaje dada fulani kijana kufikia miradi yake?

13 Dada mmoja Mkristo katika jimbo la Alabama, Marekani, alihitaji ujasiri ili ajiwekee miradi ya kiroho. Anaandika hivi: “Nilipokuwa nikikua, nilikuwa mwenye haya sana. Ilikuwa vigumu sana kwangu kuzungumza na watu katika Jumba la Ufalme, na vigumu hata zaidi kuzungumza na watu nisiowajua nilipokuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba.” Kwa msaada wa wazazi wake na wengine kutanikoni, dada huyo alifanikiwa kufikia mradi wake wa kuwa painia wa kawaida. Anaeleza hivi: “Ulimwengu wa Shetani unakazia kwamba miradi inayofaa ni elimu ya juu, umashuhuri, pesa, na kuwa na mali nyingi. Mara nyingi, ni vigumu kufikia miradi hiyo, na unapojaribu kuifikia unapata mkazo na unavunjika moyo. Hata hivyo, kumtumikia Yehova kumeniletea furaha nyingi na ninapata shangwe kwa sababu ya yale ninayotimiza.”

14. Wazazi Wakristo wanahitaji kuonyesha ujasiri katika hali zipi?

14 Wazazi Wakristo pia wanahitaji ujasiri. Kwa mfano, huenda mwajiri wako akakuomba mara kwa mara ufanye kazi saa za ziada au kwenye miisho juma, muda ambao umetenga kwa ajili ya ibada ya familia, utumishi wa shambani, na mikutano ya Kikristo. Unahitaji ujasiri ili kukataa maombi hayo ya mara kwa mara kutoka kwa mwajiri wako, na hivyo kuwawekea watoto wako mfano mzuri. Au huenda wazazi fulani kutanikoni wanawaruhusu watoto wao kufanya mambo ambayo hungependa mtoto wako afanye. Wazazi hao wanaweza kuuliza ni kwa nini mtoto wako hashiriki katika mambo hayo. Je, utaonyesha ujasiri kwa kuwaeleza kwa busara sababu za uamuzi wako?

15. Wazazi wanaweza kutumiaje andiko la Zaburi 37:25 na Waebrania 13:5?

15 Tunaonyesha ujasiri tunapowasaidia watoto wetu kujiwekea na kufikia miradi ya kiroho. Kwa mfano, wazazi fulani husita kuwatia moyo watoto wao kufanya upainia, kutumikia katika maeneo yenye uhitaji, kuwa Wanabetheli, au kujitolea kwenye miradi ya ujenzi. Huenda wazazi wakahofu kwamba watoto wao watashindwa kuwatunza watakapozeeka. Hata hivyo, wazazi wenye hekima huonyesha ujasiri na wanaamini kabisa ahadi za Yehova. (Soma Zaburi 37:25; Waebrania 13:5.) Hivyo, njia nyingine unayoweza kuonyesha ujasiri na kwamba unamtegemea Yehova ni kwa kumsaidia mtoto wako pia kumtegemea Yehova.—1 Sam. 1:27, 28; 2 Tim. 3:14, 15.

16. Baadhi ya wazazi wamewasaidiaje watoto wao kuweka miradi ya kiroho, na hilo limekuwa na faida gani?

16 Wenzi fulani nchini Marekani waliwasaidia watoto wao kujiwekea miradi ya kiroho. Mume anaeleza hivi: “Kabla watoto wetu hawajaanza kutembea na kuongea, tulikuwa tukiwaeleza kuhusu shangwe ya kuwa painia na ya kutumikia katika kutaniko. Na sasa huo ndio mradi wao. Kuwa na miradi ya kiroho na kuifikia huwasaidia watoto wetu kushinda mikazo ya mfumo wa Shetani na kukazia fikira jambo halisi, yaani, kumtumikia Yehova.” Ndugu mwenye watoto wawili aliandika hivi: “Wazazi wengi hutumia jitihada na pesa nyingi kuwasaidia watoto wao kufikia miradi katika nyanja za michezo, burudani, na elimu. Hata hivyo, ni jambo la hekima zaidi kutumia jitihada na pesa kuwasaidia watoto wetu wafikie miradi itakayowasaidia kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Kwa kweli, kuwaona watoto wetu wakifikia miradi ya kiroho na kuwa pamoja nao walipokuwa wakijitahidi kuifikia kumetuletea shangwe na uradhi mkubwa.” Uwe na hakika kwamba Mungu atawabariki wazazi wanaowasaidia watoto wao kuweka na kufikia miradi ya kiroho.

KUONYESHA UJASIRI KUTANIKONI

17. Toa mifano ya hali zinazohitaji ujasiri kutanikoni.

17 Tunahitaji kuonyesha ujasiri kutanikoni pia. Kwa mfano, wazee wanahitaji kuonyesha ujasiri wanaposhughulikia masuala ya kihukumu au wanapowasaidia wale wanaokabili dharura za kitiba zenye kuhatarisha uhai. Baadhi ya wazee hutembelea magereza ili kuwasaidia kiroho wafungwa. Vipi kuhusu dada waseja? Sasa wana fursa nyingi za kupanua utumishi wao kwa kuwa mapainia, kuhamia kwenye maeneo yenye uhitaji, kufanya kazi katika programu ya Usanifu-Majengo na Ujenzi, au kujaza ombi la kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Hata baadhi yao wanaweza kuhudhuria Shule ya Gileadi.

18. Dada wenye umri mkubwa wanaweza kuonyeshaje ujasiri?

18 Wanawake wenye umri mkubwa ni baraka kutanikoni. Tunawapenda sana dada hao wapendwa! Baadhi yao hawawezi kutimiza mengi katika utumishi wa Mungu kama walivyoweza zamani, lakini bado wanaweza kuonyesha ujasiri na kutenda. (Soma Tito 2:3-5.) Kwa mfano, dada mwenye umri mkubwa anahitaji ujasiri anapoombwa kuzungumza na dada kijana kuhusu mavazi. Hatamgombeza, ila atamtia moyo afikirie jinsi mavazi yake yanavyoweza kuwaathiri wengine. (1 Tim. 2:9, 10) Kuzungumza naye kwa njia hiyo ya upendo kunaweza kuwa na matokeo mazuri.

19. (a) Ndugu waliobatizwa wanaweza kuonyeshaje ujasiri? (b) Andiko la Wafilipi 2:13 na 4:13 linaweza kuwasaidiaje akina ndugu kusitawisha ujasiri?

19 Wengine wanaohitaji kuonyesha ujasiri na kutenda ni ndugu waliobatizwa. Wanaume wenye ujasiri walio tayari kubeba majukumu mengi zaidi ni baraka kutanikoni. (1 Tim. 3:1) Hata hivyo, wengine huenda wakasita kufikia mapendeleo. Labda ndugu ambaye alifanya makosa fulani wakati uliopita, anaweza kuhisi kwamba hastahili kuwa mtumishi wa huduma au mzee wa kutaniko. Na mwingine huenda akahisi hawezi kutimiza mgawo fulani. Ikiwa unahisi hivyo, Yehova anaweza kukusaidia kusitawisha ujasiri. (Soma Wafilipi 2:13; 4:13.) Kumbuka kwamba pindi moja Musa pia alihisi hawezi kutimiza mgawo fulani aliopewa. (Kut. 3:11) Hata hivyo, Yehova alimsaidia, na baada ya muda, Musa akapata ujasiri wa kutimiza kazi hiyo. Ndugu aliyebatizwa pia anaweza kusitawisha ujasiri kama huo kwa kusali kwa bidii Mungu amsaidie na kwa kusoma Biblia kila siku. Kutafakari kuhusu masimulizi ya watu walioonyesha ujasiri kutamsaidia pia. Kwa unyenyekevu, anaweza kuwaomba wazee wamzoeze na anaweza pia kuwa tayari kusaidia anapoombwa kufanya hivyo. Tunawasihi ndugu wote waliobatizwa wawe na ujasiri na wafanye kazi kwa bidii kwa ajili ya kutaniko!

“YEHOVA . . . YUKO PAMOJA NAWE”

20, 21. (a) Daudi alimpa Sulemani uhakika gani? (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani?

20 Mfalme Daudi alimkumbusha Sulemani kwamba Yehova angekuwa pamoja naye mpaka ujenzi wa hekalu ukamilike. (1 Nya. 28:20) Akiwa ameyaweka maneno ya baba yake akilini na moyoni, Sulemani hakuruhusu ujana na kutokuwa na uzoefu kumzuie kutimiza kazi hiyo. Alionyesha ujasiri mkubwa, akatenda, na kwa msaada wa Yehova akakamilisha ujenzi wa hekalu hilo lenye utukufu ndani ya miaka saba na nusu.

21 Kama ambavyo Yehova alimsaidia Sulemani, atatusaidia sisi pia tuwe na ujasiri na tutimize kazi yetu katika familia na kutanikoni. (Isa. 41:10, 13) Tunapoonyesha ujasiri katika ibada yetu kwa Yehova, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutapata baraka sasa na wakati ujao. Hivyo basi, “uwe hodari . . . nawe utende.”

^ fu. 12 Utapata madokezo mazuri ya jinsi ya kuweka miradi ya kiroho katika makala “Tumia Miradi ya Kiroho ili Kumtukuza Muumba Wako,” iliyochapishwa kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2004.