Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ikiwa Mnajua Mambo Haya, Mtakuwa Wenye Furaha Mkiyatenda”

“Ikiwa Mnajua Mambo Haya, Mtakuwa Wenye Furaha Mkiyatenda”

“Chakula changu ni kufanya mapenzi ya yule aliyenituma na kuimaliza kazi yake.”—YOH. 4:34.

NYIMBO: 80, 35

1. Roho yenye ubinafsi ya ulimwengu huu inaweza kuathirije unyenyekevu wetu?

KWA nini ni changamoto kwetu kutumia mambo tunayojifunza katika Neno la Mungu? Sababu moja ni kwamba ili tutende yaliyo sawa tunahitaji sifa ya unyenyekevu, lakini uwezo wetu wa kudumu tukiwa wanyenyekevu hujaribiwa kila siku. Katika ‘siku hizi za mwisho’ tumezungukwa na watu “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno,” na “wasiojizuia.” (2 Tim. 3:1-3) Mtumishi wa Mungu anaposikia habari kuhusu mwenendo fulani unaoonyesha roho ya ubinafsi, na unaopendwa na watu wengi, huenda akachukizwa nao lakini wakati uleule akawaonea wivu na kutamani mafanikio yaliyotokana na mwenendo wao wenye ubinafsi. (Zab. 37:1; 73:3) Huenda hata mtu akajiuliza: ‘Je, kweli kuna faida yoyote ya kuwatanguliza wengine? Nikijiendesha “kama mdogo zaidi,” je, kweli watu wataniheshimu?’ (Luka 9:48) Tukiruhusu roho yenye ubinafsi ya ulimwengu huu ituathiri, tunaweza kuhatarisha uhusiano wenye upendo tunaofurahia pamoja na wengine kutanikoni na kupoteza utambulisho wetu wa Kikristo. Lakini tunapojifunza na kuiga mifano mizuri ya watumishi wa Mungu inayopatikana katika Biblia, tunapata thawabu.

2. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya watumishi waaminifu wa Mungu?

2 Ikiwa tungependa kuiga mifano ya watumishi hao waaminifu, tunahitaji kuchunguza ni mambo gani waliyotenda ambayo yaliwafanya wafanikiwe. Ni nini kilichowasaidia wasitawishe urafiki pamoja na Mungu, wadumishe uhusiano mzuri pamoja naye, na kupata nguvu za kutimiza mapenzi Yake? Kujifunza na kutafakari kuhusu mifano hiyo ni sehemu muhimu ya ulishaji wetu wa kiroho.

CHAKULA CHA KIROHO KINAHUSISHA MENGI ZAIDI YA KUPATA UJUZI

3, 4. (a) Tunapokea mwongozo wa kiroho katika njia zipi? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba chakula cha kiroho kinahusisha mengi zaidi ya kupata ujuzi?

3 Sisi huzoezwa na kupata mashauri mengi kupitia Biblia, machapisho yetu ya Kikristo, Tovuti zetu, JW Broadcasting, na mikutano na makusanyiko yetu. Lakini kulingana na maneno ya Yesu kwenye Yohana 4:34, kujilisha chakula cha kiroho kunahusisha mengi zaidi ya kupata tu ujuzi. Ni jambo gani lingine linalohusika? Yesu alisema hivi: “Chakula changu ni kufanya mapenzi ya yule aliyenituma na kuimaliza kazi yake.”

4 Kwa maoni ya Yesu, kujilisha chakula cha kiroho kulitia ndani kutenda kulingana na mwongozo wa Mungu. Jinsi gani? Kama tu ambavyo miili yetu huridhika na kuimarishwa tunapokula chakula kizuri, ndivyo ambavyo mioyo yetu hutiwa nguvu na imani yetu kuimarishwa kwa ajili ya uzima wa milele, tunapofanya mapenzi ya Mungu. Ni mara ngapi umeenda kwenye mkutano wa utumishi wa shambani ukijihisi ukiwa umechoka—lakini baada ya utumishi siku hiyo ulijihisi ukiwa umeburudishwa na kutiwa nguvu?

5. Tunapata thawabu gani tunapotenda kwa hekima?

5 Kimsingi hekima inamaanisha kutumia mwongozo tunaopata kutoka kwa Mungu. (Yak. 3:13) Mtu anapokuwa na hekima anapata thawabu kubwa. Biblia inasema hivi kuhusu hekima: “Hakuna chochote unachotamani kinachoweza kulinganishwa nayo. . . . Ni mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika kwa nguvu wataitwa wenye furaha.” (Met. 3:13-18) Yesu alisema hivi: “Ikiwa mnajua mambo haya, mtakuwa wenye furaha mkiyatenda.” (Yoh. 13:17) Wanafunzi wa Yesu wangedumisha furaha yao ikiwa wangeendelea kufanya mambo ambayo Yesu aliwaamuru. Hawakusisimuliwa kwa muda mfupi tu na mafundisho yake au mfano aliowawekea, badala yake waliendelea kumfuata maisha yao yote.

6. Kwa nini tunapaswa kuendelea sikuzote kutenda kwa hekima?

6 Leo, sisi pia tunahitaji kuendelea kujitahidi kufanya mambo ambayo tunajua ni sahihi. Kwa mfano, huenda fundi wa magari akawa na vifaa vya kazi na ujuzi. Lakini vitu hivyo haviwezi kumnufaisha ikiwa hatavitumia. Ikiwa awali alifanya kazi ya kutengeneza magari na kupata uzoefu, ni lazima aendelee kutumia mambo aliyojifunza ili aendelee kuwa fundi stadi na kufanya kazi yake vizuri. Vivyo hivyo, huenda sisi pia mwanzoni tukafurahia matokeo mazuri ya kutumia yale tunayojifunza katika Biblia. Hata hivyo, tutapata furaha ya kudumu ikiwa tutaendelea kufuata mwongozo wa Yehova kwa unyenyekevu kila siku maishani mwetu.

7. Ili tuwe na hekima, tunapaswa kufanya nini tunaposoma kuhusu watumishi wa Mungu wanaotajwa katika Biblia?

7 Acheni tuchunguze baadhi ya mambo yanayoweza kujaribu unyenyekevu wetu, na tuone jinsi watumishi wa zamani wa Mungu walivyodumisha unyenyekevu chini ya hali hizo. Lakini ili tuimarishwe kiroho ni lazima tufanye mengi zaidi ya kujifunza tu mambo hayo. Ni lazima kila mmoja wetu atafakari jinsi anavyoweza kutumia mambo anayojifunza, na ayatumie bila kukawia.

WAONE WENGINE KUWA SAWA NAWE

8, 9. Simulizi lililo kwenye Matendo 14:8-15 linafunua nini kuhusu unyenyekevu wa Paulo? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

8 Mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Una maoni gani kuhusu watu wa jamii mbalimbali ambao bado hawajajifunza kweli? Ingawa mtume Paulo aliwatafuta kwenye masinagogi Wayahudi ambao tayari walijua mambo fulani kumhusu Mungu, aliwahubiria pia watu wengine. Watu hao walioabudu miungu mingine waliitikia katika njia iliyojaribu kina cha unyenyekevu wa mtume Paulo.

9 Kwa mfano, katika safari ya kwanza ya Paulo ya umishonari, Walikaonia walifikiri kimakosa kwamba Paulo na Barnaba ni watu wenye nguvu zisizo za kawaida, yaani, walikuwa miungu yao, Zeu na Herme, waliokuwa wameshuka kwao katika umbo la wanadamu. Je, Paulo na Barnaba wangetumia fursa hiyo kujipatia umashuhuri? Je, wangeliona tukio hilo kuwa badiliko lenye kufurahisha baada ya mateso waliyokuwa wamekabili hapo awali katika majiji mawili waliyotoka kutembelea? Je, waliwazia kwamba umashuhuri huo ungewasaidia kuendeleza habari njema? Sivyo hata kidogo! Mara moja walikataa katakata kwa kuyararua mavazi yao na kuruka ndani ya umati wakisema kwa sauti kubwa: “Kwa nini mnafanya mambo haya? Sisi pia ni wanadamu tulio na udhaifu kama wenu.”—Mdo. 14:8-15.

10. Paulo na Barnaba walijiona kuwa sawa na Walikaonia jinsi gani?

10 Paulo na Barnaba walipokiri kwamba wao pia si wakamilifu, hawakumaanisha kwamba njia yao ya ibada haikuwa na tofauti yoyote na ibada ya wapagani hao. Je, si kweli kwamba Paulo na Barnaba walikuwa wametumwa na Mungu kama wamishonari? (Mdo. 13:2) Je, si ni kweli kwamba walikuwa wametiwa mafuta kwa roho takatifu na kuvikwa tumaini tukufu? Ndiyo, lakini Paulo na Barnaba walielewa kwamba Walikaonia wangeweza kupokea mapendeleo hayohayo ikiwa wangekubali habari njema.

11. Tunapohubiri, tunaweza kuigaje mfano mzuri wa unyenyekevu wa Paulo?

11 Tunaweza kuigaje kielelezo kizuri cha unyenyekevu wa Paulo? Kwanza, ni lazima tupinge kabisa kishawishi chochote cha kutarajia au kukubali kukwezwa na watu wengine kwa sababu ya mambo tunayotimiza kwa uwezo wa Yehova. Ni vema kila mmoja wetu ajiulize hivi: ‘Nina maoni gani kuhusu watu ninaowahubiria? Je, inawezekana kwamba bila kujua mimi pia nina maoni yasiyofaa kuelekea watu wa jamii fulani, maoni ambayo yameenea katika jamii inayonizunguka?’ Jambo la kufurahisha ni kwamba Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wamekuwa wakiwatafuta watu wanaozungumza lugha mbalimbali, ambao wanaishi kwenye maeneo yao ili kuwasaidia wengi iwezekanavyo kusikia habari njema. Nyakati nyingine, hilo linatia ndani kujifunza lugha na utamaduni wa wale ambao jamii kwa ujumla inawabagua na kuwaona kuwa duni. Mashahidi wanaojitahidi kuwasaidia watu hao hawapaswi kwa njia yoyote ile kujiona kuwa bora kuliko wao. Badala ya kuwa na maoni ya ujumla kuhusu watu wa jamii fulani, wao hujitahidi kumfahamu mtu kibinafsi ili ujumbe wa Ufalme upenye moyoni mwake.

SALI KWA AJILI YA WENGINE UKIWATAJA KWA MAJINA

12. Epafra alionyeshaje kwamba aliwajali wengine bila ubinafsi?

12 Njia nyingine ya kuonyesha kwamba tunafuata kwa unyenyekevu mwongozo kutoka kwa Mungu ni kusali kwa ajili ya wale ambao tayari “wamepata imani, yenye thamani kama yetu.” (2 Pet. 1:1) Epafra alifanya hivyo. Anatajwa mara tatu tu kwenye Biblia, katika vitabu vilivyoandikwa na Paulo. Paulo alipokuwa katika kifungo cha nyumbani huko Roma, aliwaandikia Wakristo walioishi Kolosai kwamba Epafra “sikuzote [alikuwa akijikaza] kwa ajili [yao] katika sala zake.” (Kol. 4:12) Epafra aliwajua vizuri ndugu hao, na aliwajali sana. Hali yake alipokuwa na Paulo, ‘mfungwa mwenzake,’ haikumzuia kutambua mahitaji ya kiroho ya wengine. (Flm. 23) Naye alichukua hatua ili kuwasaidia. Je, jambo hilo halionyeshi kwamba aliwahangaikia wengine bila ubinafsi? Sala tunazotoa kwa ajili ya watumishi wenzetu wa Yehova huwa na nguvu nyingi sana, hasa tunapowakumbuka ndugu zetu kibinafsi, kama vile kwa kuwataja kwa majina.—2 Kor. 1:11; Yak. 5:16.

13. Unaweza kuigaje mfano wa Epafra unaposali?

13 Fikiria watu ambao unaweza kuwataja kwa majina katika sala zako. Kama Epafra, akina ndugu na dada wengi wanasali kwa ajili ya ndugu na dada zao kutanikoni na kwa ajili ya familia zilizo na majukumu mazito, au wale ambao wanahitaji kufanya maamuzi mazito au wanakabili vishawishi. Wengi husali kwa ajili ya ndugu zetu waliotajwa kwenye makala iliyo kwenye Tovuti ya jw.org yenye kichwa, “Mashahidi wa Yehova Walio Gerezani kwa Sababu ya Imani Yao.” (Tazama kwenye HABARI > MAMBO YA KISHERIA.) Pia, inafaa kuwakumbuka wale waliopoteza wapendwa wao katika kifo, waliokumbwa na misiba ya asili, vita, na wanaokabiliana na hali ngumu za kiuchumi. Ni wazi kwamba kuna ndugu na dada wengi wanaohitaji sala zetu na watakaofaidika nazo. Tunaposali kwa ajili yao, tunaonyesha kwamba tunaangalia si faida zetu wenyewe bali pia faida za wengine. (Flp. 2:4) Yehova husikiliza sala za aina hiyo.

UWE “MWEPESI WA KUSIKIA”

14. Yehova amewekaje kielelezo bora kabisa cha kuwasikiliza wengine?

14 Jambo lingine linaloonyesha kina cha unyenyekevu wetu ni utayari wetu wa kuwasikiliza wengine. Andiko la Yakobo 1:19 linasema kwamba tunapaswa kuwa ‘wepesi wa kusikia.’ Yehova mwenyewe ametuwekea kielelezo bora kabisa kuhusiana na hilo. (Mwa. 18:32; Yos. 10:14) Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mazungumzo yaliyo kwenye andiko la Kutoka 32:11-14. (Soma.) Ingawa Yehova hakuhitaji mchango wa mawazo kutoka kwa Musa, alimpa fursa ya kufunua hisia zake. Ni mwanadamu gani ambaye angekuwa tayari kusikiliza kwa kirefu mapendekezo ya mtu ambaye nyakati nyingine alikuwa na maoni yasiyo sahihi, na kisha kutenda kulingana na mapendekezo ya mtu huyo? Lakini Yehova huwasikiliza kwa subira wanadamu wote wanaosali kwake kwa imani.

15. Tunaweza kumwigaje Yehova katika kuwaonyesha wengine heshima?

15 Inafaa kila mmoja wetu ajiulize hivi: ‘Ikiwa Yehova anaweza kujishusha ili ashughulike na wanadamu na kuwasikiliza, kama alivyofanya katika kisa cha Abrahamu, Raheli, Musa, Yoshua, Manoa, Eliya, na Hezekia, je, mimi sipaswi kujitahidi hata zaidi kuwaonyesha heshima ndugu zangu wote, kuwaona kuwa wenye thamani, kusikiliza maoni yao, na hata kufuata maoni yao mazuri? Je, kwa sasa kuna yeyote kutanikoni au katika familia yangu ambaye ninahitaji kumwelekezea uangalifu? Ninapaswa kufanya nini? Nichukue hatua gani ili kumsaidia?’—Mwa. 30:6; Amu. 13:9; 1 Fal. 17:22; 2 Nya. 30:20.

“HUENDA YEHOVA ATAONA MATESO YANGU”

Daudi alisema: “Mwacheni!” Wewe ungefanya nini? (Tazama fungu la 16 na 17)

16. Mfalme Daudi alitendaje aliposhambuliwa na kutukanwa na Shimei?

16 Sifa ya unyenyekevu inatusaidia pia kuonyesha sifa ya kujizuia wengine wanapotukasirisha au kutuudhi. (Efe. 4:2) Mfano mzuri wa jambo hilo unapatikana katika andiko la 2 Samweli 16:5-13. (Soma.) Daudi na watumishi wake walishambuliwa na kutukanwa na Shimei aliyekuwa mtu wa ukoo wa Mfalme Sauli. Daudi alivumilia jambo hilo licha ya kwamba alikuwa na uwezo wa kulishughulikia. Daudi alipata wapi nguvu za kudhibiti hisia zake? Zaburi ya tatu inatusaidia kuelewa vizuri zaidi jambo hilo.

17. Ni nini kilichomsaidia Daudi kudhibiti hisia zake, na tunaweza kumwigaje?

17 Utangulizi wa Zaburi ya 3 unaonyesha kwamba Zaburi hiyo iliandikwa wakati Daudi “alipokuwa akimkimbia Absalomu mwanawe.” Mstari wa 1 na wa 2 wa Zaburi hiyo inataja matukio yanayofanana kabisa na yale yanayotajwa kwenye Kitabu cha Pili cha Samweli, sura ya 16. Kisha Zaburi 3:4 inaonyesha jambo lililomfanya Daudi awe na uhakika. Inasema hivi: “Nitamlilia Yehova kwa sauti kubwa, naye atanijibu kutoka kwenye mlima wake mtakatifu.” Sisi pia tunaweza kusali tunaposhambuliwa. Naye Yehova hujibu sala yetu kwa kutupatia roho yake takatifu inayotusaidia kuendelea kuvumilia. Je, unaweza kufikiria hali ambayo unahitaji kuonyesha sifa ya kujizuia au kuwasamehe wengine kwa hiari wanapokutendea kwa chuki bila sababu ya msingi? Je, una uhakika kwamba Yehova anaona mateso yako na kwamba atakubariki?

“HEKIMA NDILO JAMBO MUHIMU ZAIDI”

18. Tutanufaikaje ikiwa tutaendelea kutumia mwongozo tunaopata kutoka kwa Mungu?

18 Tunapofanya mambo ambayo tunajua ni sahihi tunapata baraka nyingi. Hivyo, haishangazi kwamba andiko la Methali 4:7 linasema kwamba “hekima ndilo jambo muhimu zaidi”! Ingawa ujuzi ndio msingi wa hekima, hekima hasa huonyeshwa kupitia mambo tunayoamua kufanya, wala si tu mambo tunayojua au kuelewa. Hata siafu pia huonyesha hekima. Siafu huongozwa na silika kuonyesha hekima kwa kujikusanyia chakula chao wakati wa kiangazi. (Met. 30:24, 25) Kristo, “hekima ya Mungu,” sikuzote hufanya mambo yanayompendeza Baba yake. (1 Kor. 1:24; Yoh. 8:29) Mungu anajua tofauti kati ya kufanya uamuzi ulio sahihi na kutenda kulingana na uamuzi huo. Naye huwathawabisha wale wanaoendelea kuonyesha sifa ya unyenyekevu na ambao hutenda kulingana na mambo wanayojua kuwa ni sahihi. (Soma Mathayo 7:21-23.) Hivyo, jitahidi kusitawisha unyenyekevu wa kweli. Unapofanya hivyo utaandaa mazingira mazuri ya kiroho kutanikoni ambapo wengine pia watatamani kumtumikia Yehova kwa unyenyekevu. Kutumia maishani mambo tunayojua kuwa ni sahihi huhitaji muda na subira. Lakini kufanya hivyo huonyesha kwamba tuna sifa ya unyenyekevu, sifa itakayotuletea furaha sasa na hata milele.