Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unajua Ni Saa Ngapi?

Unajua Ni Saa Ngapi?

UNAPOTAKA kujua ni saa ngapi, wewe hufanya nini? Huenda wewe hutazama saa yako ya mkononi au ya ukutani. Ikiwa rafiki yako angekuuliza ni saa ngapi, ungemjibuje? Kuna njia tofauti-tofauti za kusoma saa. Njia zipi?

Acha tuseme saa zima na nusu limepita baada ya saa sita mchana. Unaweza kusema ni 7:30. Ikitegemea mahali unapoishi na tamaduni, unaweza kusema ni 13:30. Njia hiyo ya kusoma saa inategemea mfumo wa saa 24. Kuna maeneo ambayo saa 7:30 inaweza kusemwa kuwa “nusu nane,” yaani, zimebaki dakika 30 kabla ya saa nane.

Ikiwa wewe ni msomaji wa Biblia, huenda ukajiuliza watu katika nyakati za Biblia walitumia njia gani kusoma saa. Hawakutumia njia moja tu. Maandiko ya Kiebrania yanataja maneno “asubuhi,” “mchana,” “adhuhuri,” na “jioni.” (Mwa. 8:11; 19:27; 43:16; Kum. 28:29; 1 Fal. 18:26) Hata hivyo, nyakati nyingine wakati hususa ulitajwa.

Katika nyakati za Biblia, ilikuwa kawaida kutumia walinzi, hasa wakati wa usiku. Karne nyingi kabla ya Yesu kuzaliwa, Waisraeli waligawanya wakati wa usiku katika sehemu tatu walizoziita makesha. (Zab. 63:6) Andiko la Waamuzi 7:19 linataja “kesha la katikati ya usiku.” Kufikia siku za Yesu, Wayahudi walikuwa wameiga mfumo wa Wagiriki na Waroma wa makesha manne ya usiku.

Vitabu vya Injili vinarejelea makesha hayo mara kadhaa. Kwa mfano, Yesu alitembea juu ya maji akielekea kwenye mashua iliyokuwa na wanafunzi wake “katika kesha la nne la usiku.” (Mt. 14:25) Katika mfano mmoja, Yesu alisema hivi: “Ikiwa mwenye nyumba angejua mwizi atakuja katika kesha gani, angekaa macho na hangeruhusu nyumba yake ivunjwe.”—Mt. 24:43.

Yesu alirejelea makesha yote manne alipowaambia hivi wanafunzi wake: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha, kwa maana hamjui bwana wa nyumba anakuja wakati gani, iwe ni jioni, usiku wa manane, kabla ya alfajiri, au asubuhi na mapema.” (Marko 13:35; maelezo ya chini) Kesha la kwanza, lile la “jioni,” lilianza jua lilipotua hadi saa tatu hivi usiku. La pili, lile la “usiku wa manane,” lilianza saa tatu hivi usiku hadi saa sita usiku. Kesha la tatu, linalotajwa kuwa “kabla ya alfajiri,” au kesha la “jogoo anapowika,” lilianza saa sita usiku hadi saa tisa hivi usiku. Huenda ni katika kesha hili ambapo jogoo aliwika katika usiku ambao Yesu alikamatwa. (Marko 14:72) Kesha la nne, linalotajwa kuwa la “asubuhi na mapema,” lilianza saa tisa hivi usiku hadi jua lilipochomoza.

Hivyo, ingawa vifaa vinavyotumiwa leo kutujulisha wakati havikuwapo katika nyakati za Biblia, watu walikuwa na mfumo uliowasaidia kujua saa, iwe ni usiku au mchana.