Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Kuonyeshana Upendo​—Unajenga

Endeleeni Kuonyeshana Upendo​—Unajenga

“Upendo hujenga.”—1 KOR. 8:1.

NYIMBO: 109, 121

1. Yesu alizungumzia jambo gani muhimu kwenye usiku wake wa mwisho pamoja na wanafunzi wake?

KATIKA usiku wa mwisho pamoja na wanafunzi wake, Yesu alitaja neno upendo karibu mara 30. Aliwaambia wanafunzi wake kihususa kwamba walipaswa ‘kupendana.’ (Yoh. 15:12, 17) Upendo huo ungekuwa wa pekee sana hivi kwamba ungewatambulisha waziwazi kuwa wafuasi wake wa kweli. (Yoh. 13:34, 35) Upendo huo si hisia tu. Yesu alikuwa akirejelea sifa yenye thamani sana, yaani, upendo usio na ubinafsi. Alisema hivi: “Hakuna mtu aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu atoe uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya mambo ninayowaamuru.”—Yoh. 15:13, 14.

2. (a) Tunajionea nini miongoni mwa watumishi wa Yehova? (b) Tutajibu maswali gani katika makala hii?

2 Upendo wa kweli usio na ubinafsi na umoja usioweza kuvunjika uliopo miongoni mwa watumishi wa Yehova leo, unawatambulisha kuwa watu wa Mungu. (1 Yoh. 3:10, 11) Ni jambo lenye kupendeza sana kwamba upendo wa Kikristo umesitawi kwelikweli miongoni mwa watumishi wa Yehova licha ya kwamba wanatoka katika taifa, kabila, lugha, na malezi mbalimbali! Hata hivyo, huenda tukajiuliza: ‘Kwa nini sifa ya upendo ni muhimu sana leo? Yehova na Yesu hutujenga katika upendo jinsi gani? Tukiwa mtu mmoja-mmoja tunaweza kuonyeshaje upendo wa Kikristo ambao “hujenga”?’—1 Kor. 8:1.

KWA NINI SIFA YA UPENDO NI MUHIMU SANA LEO

3. ‘Nyakati hizi za hatari’ zinawaathirije watu?

3 Kwa kuwa maisha “[yamejaa] taabu na huzuni,” watu wengi katika ‘nyakati hizi za hatari’ hupatwa na matatizo mbalimbali ya kihisia. (Zab. 90:10; 2 Tim. 3:1-5) Watu wengi wamepoteza tamaa ya kuendelea kuishi. Ripoti zinaonyesha kwamba zaidi ya watu 800,000 hujiua kila mwaka, yaani, mtu mmoja hujiua kila baada ya sekunde 40. Inasikitisha sana kwamba hata baadhi ya Wakristo wamelemewa na mikazo hiyo na kufikia hatua ya kujiua.

4. Ni watu gani katika Biblia waliotamani kufa?

4 Baadhi ya watumishi waaminifu wa Mungu katika nyakati za Biblia, walilemewa sana na hali walizokabili hivi kwamba walitamani kufa. Kwa mfano, Ayubu alihisi maumivu makali naye akalalamika hivi: “Ninachukia maisha yangu; sitaki kuendelea kuishi.” (Ayu. 7:16; 14:13) Yona alivunjika moyo sana katika mgawo wake wakati mambo yalipoenda kinyume na matarajio yake, naye akasema: “Sasa, Ee Yehova, nakusihi uniue, kwa maana afadhali nife badala ya kuishi.” (Yona 4:3) Pia, pindi fulani nabii mwaminifu Eliya alifadhaishwa sana na hali aliyokabili hivi kwamba akaomba afe. Alisema hivi: “Imetosha! Sasa, Ee Yehova, niue.” (1 Fal. 19:4) Hata hivyo, Yehova aliwathamini watumishi hao na alitaka waishi. Badala ya kuwashutumu kwa sababu ya jinsi walivyohisi, aliwasaidia kushinda hisia walizokuwa nazo za kutamani kufa naye akawajenga katika upendo ili waendelee kumtumikia kwa uaminifu.

5. Kwa nini leo hasa ndugu na dada zetu wanahitaji upendo wetu hata zaidi?

5 Hata ikiwa ndugu na dada zetu hawajapoteza tamaa yao ya kuendelea kuishi, wengi wao hukabili mikazo mingi na wanahitaji kujengwa katika upendo. Baadhi yao wanavumilia mateso na dhihaka. Wengine wanachambuliwa na kusengenywa wakiwa kazini. Au wengine wamechoka kwa sababu ya kufanya kazi saa za ziada au kwa sababu ya kung’ang’ana kukamilisha kazi kwa wakati mfupi. Ilhali wengine wanakabili matatizo ya nyumbani yanayowafyonza nguvu, huenda wanachambuliwa na mwenzi wao wa ndoa asiye mwamini. Kwa sababu ya mikazo hiyo na mingine mingi, ndugu na dada wengi kutanikoni huhisi wamechoka kabisa kimwili na kihisia. Ni nani anayeweza kuwasaidia watu waliovunjika moyo waendelee kusonga mbele?

JENGWA NA UPENDO WA YEHOVA

6. Yehova huwajengaje watumishi wake katika upendo?

6 Yehova huwajenga watumishi wake kwa kuwahakikishia kwamba anawapenda sasa na ataendelea kuwapenda milele na milele. Hapana shaka kwamba Waisraeli walitiwa moyo sana walipomsikia Yehova akisema maneno haya: “Ulikuwa mwenye thamani machoni pangu, uliheshimiwa, nami nimekupenda. . . . Usiogope, kwa maana nipo pamoja nawe”! (Isa. 43:4, 5) Ukiwa mtumishi wa Yehova, uwe na uhakika kwamba Yehova anakupenda kwa wororo sana. * Neno la Mungu linaahidi hivi kuwahusu wale wanaofuatia ibada safi: “Akiwa Mwenye nguvu, ataokoa. Atakushangilia kwa shangwe kubwa.”—Sef. 3:16, 17.

7. Ni katika njia gani upendo wa Yehova ni kama wa mama anayenyonyesha? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

7 Yehova anaahidi kuwategemeza na kuwafariji watu wake hata iwe watakabili jaribu gani. Biblia inasema hivi: “Mtanyonya na kubebwa kiunoni, nanyi mtachezeshwa kwenye magoti yake. Kama mama anavyomfariji mwanawe, ndivyo nitakavyoendelea kuwafariji.” (Isa. 66:12, 13) Huo ni ufananisho wenye kugusa moyo sana—mama mwenye upendo akimbeba mtoto wake kiunoni, au akimchezesha kwenye magoti yake! Kupitia ufananisho huo, Yehova anafunua kwa njia yenye kugusa moyo kina na wororo wa upendo alionao kuelekea waabudu wake wa kweli. Usiwe na shaka kamwe kwamba Yehova anakuona wewe binafsi kuwa mwenye thamani sana machoni pake.—Yer. 31:3.

8, 9. Upendo wa Yesu unaweza kutuimarishaje?

8 Wakristo wa kweli wana sababu nyingine inayowafanya wavutiwe na upendo wa Mungu: Yehova “aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Kwa kweli, Yesu pia alionyesha upendo mkubwa sana alipotoa uhai wake kwa ajili yetu! Na upendo huo hutuimarisha na kutuchochea sana! Neno la Mungu linaahidi kwamba hata “dhiki au taabu” haviwezi “[kututenga] na upendo wa Kristo.”—Rom. 8:35, 38, 39.

9 Tunapokabili matatizo yanayotuchosha kimwili, kihisia, au kiroho, upendo wa Kristo ambao una uwezo wa kutuchochea utatupatia nguvu za kuvumilia. (Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.) Upendo wa Yesu una uwezo wa kututegemeza na kutuchochea tusikate tamaa, hata tunapokabili matatizo kama vile misiba ya asili, mateso, tunapovunjika moyo, au tunapokuwa na wasiwasi unaotulemea.

NDUGU ZETU WANAHITAJI UPENDO WETU

Kujifunza kuhusu mfano wa Yesu kunaweza kukuchochea kuwatia moyo wengine (Tazama fungu la 10 na 11)

10, 11. Ni nani walio na jukumu la kuwajenga ndugu na dada waliovunjika moyo? Eleza.

10 Njia nyingine ambayo Yehova hutujenga katika upendo ni kupitia kutaniko la Kikristo. Tukiwa mtu mmoja-mmoja, tunaweza kuiga upendo wake kwa kuwapenda na kuwajenga ndugu na dada zetu si kwa njia ya kiroho tu, bali pia kihisia. (1 Yoh. 4:19-21) Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo hivi: “Endeleeni kutiana moyo na kujengana, kama vile kwa kweli mnavyofanya.” (1 The. 5:11) Naam, wote kutanikoni—si wazee tu—wanaweza kumwiga Yehova na Yesu kwa kuwafariji na kuwajenga ndugu na dada zao.—Soma Waroma 15:1, 2.

11 Baadhi ya ndugu na dada zetu wenye matatizo ya kihisia huenda wakahitaji dawa au kuwaona wataalamu wa afya. (Luka 5:31) Wazee na wengine kutanikoni huonyesha sifa ya kiasi kwa kutambua kwamba wao si wataalamu wa afya waliozoezwa. Hata hivyo, wazee na wengine kutanikoni wana jukumu muhimu la kutimiza, yaani, ‘kuwafariji wale walioshuka moyo, kuwasaidia walio dhaifu, na kuwa na subira kwa watu wote.’ (1 The. 5:14) Wakristo wote wanapaswa kuonyesha hisia mwenzi na subira, wakiwafariji waliovunjika moyo ili kuwajenga. Je, wewe ni chanzo cha faraja na kitia-moyo kwa wengine? Unapojua jinsi ya kuwafariji na kuwatia moyo wengine, utapata matokeo mazuri hata zaidi.

12. Toa mfano wa mtu aliyejengwa kwa sababu ya upendo alioonyeshwa kutanikoni.

12 Upendo wetu unaweza kuwajengaje wale wanaokabili maumivu ya kihisia? Dada mmoja kutoka Ulaya anasema hivi: “Nyakati nyingine mimi hupatwa na hisia za kujiua. Lakini nimezungukwa na watu wanaonitegemeza. Kutaniko ninaloshirikiana nalo limeokoa uhai wangu. Sikuzote ndugu na dada kutanikoni hunitia moyo sana na kunionyesha upendo. Ingawa ni wachache tu wanaojua kwamba nina ugonjwa wa kushuka moyo (sonona), sikuzote kutaniko huwa tayari kunisaidia. Wenzi fulani wa ndoa wamekuwa wazazi wangu wa kiroho. Wao hunitunza vizuri sana, na wako tayari kunisaidia saa zote 24 za siku.” Ni kweli kwamba si wote kutanikoni wanaoweza kutoa msaada kwa kiwango kilekile. Lakini msaada tunaochochewa kutoa kutoka moyoni unaweza kuwategemeza kwa njia kubwa sana wale wanaokabili maumivu ya kihisia. *

JINSI YA KUWAJENGA WENGINE KATIKA UPENDO

13. Ni jambo gani muhimu tunalopaswa kufanya ili kuwajenga wengine?

13 Uwe msikilizaji mzuri. (Yak. 1:19) Ni kitendo cha upendo kuwasikiliza wengine kwa hisia mwenzi. Kwa njia ya busara na huruma, unaweza kumuuliza maswali yule anayetaabika ukiwa na lengo la kuelewa hisia zake. Kwa kufanya hivyo utafanikiwa kumwonyesha hisia mwenzi na kumjenga mtumishi mwenzako. Ishara za uso wako zinapaswa kuonyesha kwamba unamhangaikia mtu huyo kwa upendo na kutoka moyoni. Ikiwa Mkristo mwenzako angependa kukueleza kwa undani zaidi habari zinazohusu hali yake, uwe mwenye subira na uepuke kumkatiza anapojieleza. Ukimsikiliza kwa makini, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba utaelewa hisia zinazomhangaisha. Jambo hilo litamfanya ndugu au dada yako akuamini, na hivyo atakuwa tayari kukusikiliza unapojitahidi kumjenga. Unapomwonyesha kwamba unamjali kikweli kwa kumhangaikia kwa upendo, jambo hilo linaweza kumfariji sana.

14. Kwa nini tungependa kuepuka roho ya kuwachambua wengine?

14 Epuka roho ya kuwachambua wengine. Kuwachambua wale walioshuka moyo kunaweza kuwaletea maumivu mengi hata zaidi na hata kuathiri jitihada zetu za kutoka moyoni za kuwajenga katika upendo. Biblia inasema hivi: “Maneno yanayosemwa bila kufikiri huchoma kama upanga, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Met. 12:18) Kwa kawaida, sisi ‘hatuwachomi’ kimakusudi kwa maneno yenye kuumiza wale walioshuka moyo. Hata hivyo, hata ikiwa mtu ‘anachomwa’ bila kukusudia, maumivu yanaweza kuwa makali sana. Ili tuwajenge wengine katika upendo kwa kuwatia moyo, tunapaswa kuwaonyesha hisia mwenzi, tukijitahidi kadiri tuwezavyo kujiweka katika hali zao.—Mt. 7:12.

15. Tunaweza kutumia kifaa gani chenye thamani kitakachotusaidia kuwajenga wengine katika upendo?

15 Tumia Neno la Mungu kuwafariji wengine. (Soma Waroma 15:4, 5.) Maandiko Matakatifu ni hazina iliyojaa mambo yanayotufariji na kutuliwaza. Biblia imetoka kwa “Mungu anayetoa uvumilivu na faraja.” Mbali na maandiko yenye kufariji, tuna vifaa vingine chungu nzima vya kutusaidia kujifunza Biblia. Tunaweza kutumia Fahirisi na Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Vifaa hivyo vinaweza kutusaidia kutafuta habari za Kimaandiko zinazojenga zitakazotusaidia kukabiliana na tatizo lolote lile. Hivyo, vifaa hivyo vinaweza kutusaidia tuwe na hazina ya maneno yaliyojaa hisia mwenzi yatakayotusaidia tuwe na matokeo mazuri zaidi tunapowafariji wengine kwa upendo.

16. Tunahitaji kuwa na sifa zipi tunapomfariji Mkristo aliyeshuka moyo?

16 Watendee wengine kwa wororo na upole. Sifa hizo zenye thamani ni sehemu ya upendo usio na ubinafsi tunaowaonyesha wengine tunapowatia moyo na kuwajenga. Yehova ni “Baba wa rehema nyororo na Mungu wa faraja yote,” naye ni mwenye “huruma nyororo” kuelekea watumishi wake. (Soma 2 Wakorintho 1:3-6; Luka 1:78; Rom. 15:13) Paulo alituwekea kielelezo kizuri kuhusu hilo, na aliandika hivi: “Tuliwatendea kwa upole, kama vile mama anayenyonyesha anavyowatunza watoto wake kwa wororo. Basi, kwa maana tulikuwa na upendo mwororo kwenu, tulijitahidi kuwapa habari njema ya Mungu na hata uhai wetu wenyewe, kwa sababu tuliwapenda sana.” (1 The. 2:7, 8) Tunapowaonyesha wengine sifa ya Mungu ya wororo, tunaweza kutumiwa kujibu sala ya mtu anayeteseka.

17. Ni mtazamo gani kuwahusu ndugu zetu utakaotusaidia tuwajenge katika upendo?

17 Usitarajie ukamilifu kutoka kwa ndugu na dada zako. Uwe na mtazamo uliosawazika kuwahusu ndugu na dada zako wa kiroho. Kutarajia kwamba ndugu na dada zako hawatakukosea ni jambo lisilo halisi na litakufanya uvunjike moyo. (Mhu. 7:21, 22) Kumbuka kwamba Yehova hatarajii tufanye mambo yanayopita uwezo wetu, Yeye huona mambo kihalisi. Tukiiga mfano wake, tutakuwa tayari kuvumilia kasoro za wengine. (Efe. 4:2, 32) Badala ya kuwafanya wengine wahisi ni kana kwamba hawafanyi yote wawezayo katika utumishi wa Yehova, azimia kuwapongeza kwa yale wanayotimiza. Kufanya hivyo kunaweza kuwatia moyo. Kuwapongeza wengine kunaweza kuwajenga katika upendo na kuwasaidia kupata “sababu ya kushangilia” kuhusiana na utumishi wao mtakatifu. Ni afadhali zaidi kufanya hivyo kuliko kuwalinganisha na wengine, jambo ambalo litawavunja moyo.—Gal. 6:4.

18. Ni jambo gani linalotuchochea tuwajenge wengine katika upendo?

18 Kila mmoja wa kondoo wa Yehova ni mwenye thamani sana machoni pake na machoni pa Yesu, ambaye alitoa dhabihu ya fidia. (Gal. 2:20) Tunawapenda sana ndugu na dada zetu wa kiroho. Nasi tungependa kuwahangaikia kwa wororo na upendo. Ili tuwaburudishe, acheni “tufuatilie mambo yanayoleta amani na mambo ya kujengana.” (Rom. 14:19) Tunasubiri kwa hamu Paradiso inayokuja ambapo hatutakuwa kamwe na sababu yoyote ya kuvunjika moyo! Hakutakuwa tena na magonjwa, vita, kifo, mateso, migogoro ya kifamilia, na mambo yanayotuvunja moyo. Utawala wa Miaka Elfu Moja utakapokwisha, wanadamu watakuwa wamefikia ukamilifu. Kisha wale watakaopita jaribu la mwisho watafanywa kuwa wana wa kidunia wa Yehova Mungu nao watapata “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Rom. 8:21) Hivyo, acheni sisi sote tuendelee kuonyeshana upendo unaojenga na tusaidiane kufikia mradi huo wenye kuthawabisha na unaoleta shangwe.

^ fu. 12 Ili kupata mapendekezo mazuri ya kukabiliana na fikira au hisia za kujiua, tazama makala zifuatazo katika gazeti la Amkeni!: Usikate Tamaa!—Sababu Tatu za Kuendelea Kuishi” (Aprili 2014); “Unapohisi Kwamba Hutaki Kuendelea Kuishi” (Januari 2012); na “Uhai Una Thamani” (Oktoba 22, 2001).