Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mweza Yote, Lakini Mwenye Ufikirio

Mweza Yote, Lakini Mwenye Ufikirio

“[Yehova] anajua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—ZAB. 103:14.

NYIMBO: 30, 10

1, 2. (a) Tofauti na wanadamu wenye mamlaka, Yehova huwatendeaje watu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

MARA nyingi watu wenye mamlaka na cheo “hupiga ubwana juu” ya wengine, au hata kuwakandamiza. (Mt. 20:25; Mhu. 8:9) Lakini Yehova hutenda kwa njia tofauti sana! Ingawa yeye ni Mweza Yote, Yehova huwaonyesha wanadamu wasio wakamilifu ufikirio mkubwa sana. Yeye ni mwenye fadhili na huzingatia hali zetu. Anajali hisia zetu na kuzingatia mahitaji yetu. Kwa kuwa “[anakumbuka] kwamba sisi ni mavumbi,” hadai kamwe tutimize mambo ambayo hatuwezi kutimiza.—Zab. 103:13, 14.

2 Biblia ina mifano mingi ya jinsi Yehova anavyoshughulika na watumishi wake kwa njia yenye ufikirio. Acheni tuzungumzie mifano mitatu. Kwanza, ufikirio ambao Mungu alimwonyesha mvulana Samweli alipokuwa akimsaidia kuwasilisha ujumbe wa hukumu kwa Kuhani Mkuu Eli; pili, jinsi Yehova alivyotenda kwa subira Musa alipokuwa akikataa kutumikia akiwa kiongozi wa Waisraeli; na tatu, ufikirio ambao Mungu aliwaonyesha Waisraeli alipokuwa akiwaongoza kutoka Misri. Tunapotafakari mifano hiyo, acheni tuzingatie mambo tunayojifunza kumhusu Yehova na tuone jinsi tunavyoweza kuyatumia maishani.

MVULANA AONYESHWA UFIKIRIO

3. Ni jambo gani lisilo la kawaida lililomtokea Samweli usiku mmoja, na hilo linatokeza swali lipi? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Samweli alianza ‘kumhudumia Yehova’ katika hema la ibada akiwa na umri mdogo sana. (1 Sam. 3:1) Usiku mmoja Samweli alipokuwa amelala, jambo lisilo la kawaida kabisa lilitendeka. * (Soma 1 Samweli 3:2-10.) Alisikia sauti ikimwita. Akifikiri kwamba ilikuwa sauti ya Kuhani Mkuu Eli aliyekuwa amezeeka, kwa utii Samweli alikimbia kwake na kumwambia hivi: “Nimekuja, kwa kuwa umeniita.” Eli akamwambia kwamba hakuwa amemwita. Jambo hilo lilipotokea mara mbili zaidi, Eli alitambua kwamba Mungu ndiye aliyekuwa akimwita Samweli. Hivyo alimwambia mvulana huyo jambo la kufanya, naye Samweli akatii. Kwa nini Yehova, kupitia malaika wake, hakujifunua kwa Samweli mara ya kwanza alipomwita? Biblia haisemi, lakini mfuatano wa matukio unadokeza kwamba Yehova alikuwa akimwonyesha Samweli ufikirio. Jinsi gani?

4, 5. (a) Samweli alihisije alipopewa mgawo na Mungu, na mambo yaliendaje asubuhi iliyofuata? (b)  Simulizi tulilozungumzia linatufundisha nini kumhusu Yehova?

4 Soma 1 Samweli 3:11-18. Sheria ya Yehova iliwaamuru watoto wawaheshimu watu wenye umri mkubwa, hasa waliokuwa viongozi. (Kut. 22:28; Law. 19:32) Je, unaweza kumwazia mvulana mdogo kama Samweli akimwendea Eli asubuhi na kumwambia kwa ujasiri ujumbe mkali wa hukumu kutoka kwa Mungu? Ni vigumu kuwazia jambo hilo! Isitoshe, simulizi hilo linatuambia kwamba Samweli “[aliogopa] kumwambia Eli maono hayo.” Hata hivyo, Mungu alimfunulia Eli kwamba Yeye ndiye aliyekuwa akimwita Samweli. Kwa sababu hiyo, Eli akachukua hatua ya kwanza na kumwambia Samweli amweleze mambo yote waziwazi. Eli alimwamuru hivi: “[Usinifiche] neno hata moja kati ya maneno yote ambayo alikwambia.” Samweli alitii na “akamwambia kila jambo.”

5 Ujumbe ambao Samweli alileta haukumshangaza sana Eli. Ulifanana na ujumbe wa “mtu wa Mungu” ambaye hatajwi kwa jina na ambaye hapo awali alikuwa amezungumza na kuhani mkuu Eli. (1 Sam. 2:27-36) Simulizi kuhusu Samweli na Eli linaonyesha jinsi Yehova alivyo mwenye ufikirio na hekima.

6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na njia ambayo Mungu alimsaidia Samweli?

6 Je, wewe ni kijana? Ikiwa ndivyo, simulizi la Samweli linaonyesha kwamba Yehova anaelewa changamoto unazokabili na jinsi unavyohisi. Huenda wewe ni mwenye haya na ni vigumu kwako kuwahubiria watu wazima ujumbe wa Ufalme, au unaogopa kuonekana kuwa tofauti na vijana wenzako. Uwe na hakika kwamba Yehova anataka kukusaidia. Hivyo, mmwagie moyo wako katika sala. (Zab. 62:8) Tafakari mifano ya Biblia ya vijana kama vile Samweli. Pia, zungumza na Wakristo wenzako, iwe ni vijana au watu wenye umri mkubwa, ambao wameshinda changamoto unazokabili. Kwa kweli, huenda wakakueleza kuhusu pindi ambazo Yehova aliwasaidia, labda hata kupitia njia ambazo hawakutarajia.

ALIMWONYESHA MUSA UFIKIRIO

7, 8. Yehova alimwonyeshaje Musa ufikirio wa pekee?

7 Musa alipokuwa na umri wa miaka 80, Yehova alimpa mgawo mzito. Musa alipewa mgawo wa kuwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri. (Kut. 3:10) Ni wazi kwamba Musa alishtuka alipopokea mgawo huo kwa sababu alikuwa mchungaji huko Midiani kwa miaka 40. Alisema hivi: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao na kuwatoa Waisraeli nchini Misri?” Mungu alimhakikishia Musa hivi: “Nitathibitika kuwa pamoja nawe.” (Kut. 3:11, 12) Pia, alimwahidi hivi: Wazee wa Israeli kwa “hakika wataisikiliza sauti yako.” Ingawa hivyo, Musa alimwambia Mungu hivi: ‘Tuseme kwamba hawasikilizi sauti yangu.’ (Kut. 3:18; 4:1) Kwa maneno mengine, Musa alikuwa akipinga maneno ya Yehova! Lakini Yehova alionyesha subira. Hata alifanya jambo lingine zaidi. Alimpa Musa nguvu za kufanya miujiza, na hivyo akawa mwanadamu wa kwanza anayetajwa katika Biblia kuwa na nguvu hizo.—Kut. 4:2-9, 21.

8 Musa aliendelea kutafuta visingizio zaidi, akidai kwamba hakuwa msemaji mwenye ufasaha. Mungu alimwambia hivi: “Nitakuwa pamoja nawe utakapokuwa ukizungumza, nami nitakufundisha unalopaswa kusema.” Je, sasa Musa alikuwa amesadikishwa? La, kwa sababu alimwomba Mungu kwa upole kwamba amtume mtu mwingine. Yehova akakasirika. Lakini hakukataa kumsikiliza. Badala yake, alimwonyesha Musa ufikirio kwa kujali hisia zake alipomchagua Haruni awe msemaji wake.—Kut. 4:10-16.

9. Subira na ufikirio wa Yehova ulimsaidiaje Musa katika mgawo wake?

9 Simulizi hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova? Kwa kuwa yeye ni Mungu Mweza Yote, alikuwa na uwezo wa kumtisha Musa ili ajitiishe kwake haraka. Badala yake, Yehova alikuwa mwenye subira na fadhili, na akafanya jitihada za kumhakikishia mtumishi wake mnyenyekevu na mwenye kiasi kwamba angekuwa pamoja naye. Je, njia hiyo yenye ufikirio ilikuwa na matokeo mazuri? Bila shaka! Musa akawa kiongozi mzuri sana ambaye alijitahidi kushughulika na wengine kwa njia ambayo Yehova alikuwa ameshughulika naye, yaani, kwa upole na ufikirio.—Hes. 12:3.

Je, unamwiga Yehova unaposhughulika na wengine? (Tazama fungu la 10)

10. Tunanufaikaje tunapomwiga Yehova kwa kuwaonyesha wengine ufikirio?

10 Tunajifunza nini? Je, wewe ni mume, mzazi, au mzee wa kutaniko? Ikiwa ndivyo, una mamlaka ya kadiri fulani. Basi, ni muhimu sana umwige Yehova kwa kuonyesha ufikirio, fadhili, na subira unaposhughulika na wale walio chini ya mamlaka yako. (Kol. 3:19-21; 1 Pet. 5:1-3) Unapojitahidi kumwiga Yehova na Musa Mkuu, Yesu Kristo, itakuwa rahisi zaidi kwa wengine kukufikia ili kuzungumza nawe na utawaburudisha. (Mt. 11:28, 29) Pia, utawawekea wengine mfano mzuri wa kuiga.—Ebr. 13:7.

MWOKOZI MWENYE KUOGOPESHA, LAKINI MWENYE UFIKIRIO

11, 12. Yehova alipokuwa akiwaongoza Waisraeli kutoka Misri, alifanya mambo gani ili wahisi wakiwa salama?

11 Huenda idadi ya Waisraeli ilikuwa zaidi ya watu milioni tatu walipoondoka Misri mwaka wa 1513 K.W.K. Umati huo ulikuwa na watu wa vizazi vitatu au vinne hivi, hivyo kulikuwa na watoto, wazee, na bila shaka wengine walikuwa wagonjwa au walemavu. Kwa hakika, ili kuongoza umati mkubwa hivyo kutoka Misri, Kiongozi mwenye ufikirio na anayeelewa hali za watu alihitajika. Yehova, akimtumia Musa, alithibitika kuwa Kiongozi wa namna hiyo. Na kwa sababu hiyo, Waisraeli walihisi wakiwa salama walipoondoka katika nchi pekee waliyoiona kuwa nyumbani.—Zab. 78:52, 53.

12 Yehova alifanya nini ili watu wake wajihisi wakiwa salama na wakiwa na ulinzi? Kwanza kabisa, aliwaongoza kutoka Misri wakiwa “wamejipanga kivita.” (Kut. 13:18) Kwa kweli, mpangilio huo uliwahakikishia Waisraeli kwamba Mungu ndiye aliyekuwa akiongoza mambo. Pia, Yehova alifanya uwepo wake uonekane waziwazi kupitia “wingu wakati wa mchana na . . . mwangaza wa moto” wakati wa usiku. (Zab. 78:14) Kwa njia nyingine, Yehova alikuwa akiwaambia: “Msiogope. Nipo pamoja nanyi ili kuwaongoza na kuwalinda.” Na muda si muda, uhakikisho huo ulihitajika!

Yehova aliwafanyia Waisraeli jambo gani lenye ufikirio katika Bahari Nyekundu? (Tazama fungu la 13)

13, 14. (a) Ni mambo gani yenye ufikirio ambayo Yehova aliwafanyia Waisraeli kwenye Bahari Nyekundu? (b) Yehova alionyeshaje kwamba ana nguvu nyingi kuliko Wamisri?

13 Soma Kutoka 14:19-22. Jiwazie ukiwa hapo, nyuma yako kuna majeshi ya Farao na mbele yako ni Bahari Nyekundu. Kisha Mungu anatenda. Nguzo ya wingu iliyokuwa mbele yenu inarudi upande wa nyuma wa kambi, na kuwawekea Wamisri kizuizi na sasa hawawezi kuona kwa sababu ya giza. Hata hivyo, kwa njia ya kimuujiza, kambi yenu ina mwangaza mkubwa! Kisha unamwona Musa akinyoosha mkono wake juu ya bahari, na upepo wenye nguvu wa mashariki unatengeneza njia pana baharini kutoka ng’ambo moja hadi nyingine. Kwa utaratibu mzuri, wewe, familia yako, wanyama wenu wa kufugwa, na umati wote wa watu mnatembea kwenye sakafu ya bahari. Mara moja, unagundua jambo fulani lisilo la kawaida. Sakafu ya bahari haina matope wala utelezi; ni kavu na ni rahisi kutembea juu yake. Hivyo, hata wale wanaotembea polepole wanavuka kwa usalama hadi upande wa pili.

14 Soma Kutoka 14:23, 26-30. Wakati huohuo, Farao mwenye kiburi na mpumbavu, anakimbia akiwafuata upesi katika sakafu ya bahari. Kwa mara nyingine, Musa ananyoosha mkono wake juu ya bahari. Pindi hii, zile kuta mbili za maji zinaporomoka. Maji ya bahari yanakutana kwa kishindo kikubwa, kama tsunami mbili ambazo zimekutana. Farao na majeshi yake hawawezi kuokoka!—Kut. 15:8-10.

15. Simulizi hili linakufundisha nini kumhusu Yehova?

15 Kutokana na simulizi hili, tunaona kwamba Yehova ni Mungu mwenye utaratibu—sifa inayotufanya tuhisi tukiwa salama salimini. (1 Kor. 14:33) Pia, Yehova anaonyesha kwamba yeye ni mchungaji mwenye upendo ambaye huwajali watu wake akizingatia mahitaji yao mbalimbali. Ni kana kwamba anawakumbatia kwa wororo, akiwalinda dhidi ya maadui wao. Hizo ni kweli zinazotupatia uhakika mwingi na faraja kadiri tunavyozidi kukaribia mwisho wa mfumo huu wa mambo!—Met. 1:33.

16. Tunaweza kunufaikaje kwa kuchunguza jinsi Yehova alivyowakomboa Waisraeli?

16 Leo pia, Yehova huwatunza na kuwalinda watu wake wakiwa kikundi—kiroho na kimwili. Naye ataendelea kufanya hivyo wakati wa dhiki kuu ambayo inakaribia kwa kasi sana. (Ufu. 7:9, 10) Hivyo, iwe sisi ni vijana au wazee, wazima au walemavu, tukiwa watu wa Mungu hatutaingiwa na wasiwasi wala kuogopa wakati wa dhiki kuu. * Badala ya kuogopa, tutatenda kwa njia tofauti kabisa! Tutakumbuka maneno haya ya Yesu Kristo: “Simameni wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.” (Luka 21:28) Watu wa Mungu watadumisha uhakika huo hata watakapokabili shambulizi la Gogu, yaani, muungano wa mataifa utakaokuwa na nguvu zaidi kuliko Farao wa kale. (Eze. 38:2, 14-16) Kwa nini watu wa Mungu watakuwa na uhakika kwamba Yehova atawalinda? Kwa sababu wanajua kwamba Yehova habadiliki. Atathibitika kuwa Mwokozi anayejali na mwenye ufikirio.—Isa. 26:3, 20.

17. (a) Tunaweza kunufaikaje kutokana na masimulizi ya Biblia ya jinsi Yehova anavyowajali watu wake? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

17 Mifano iliyotajwa kwenye makala hii ni baadhi tu ya mifano mingi inayoonyesha jinsi Yehova anavyowajali, anavyowaongoza, na kuwakomboa watu wake kwa njia yenye ufikirio na fadhili. Unapotafakari masimulizi hayo, zingatia hata mambo madogo-madogo yanayofunua sifa za Yehova ambazo huenda hungetambua kwa urahisi. Kufanya hivyo kutakusaidia ukazie kabisa akilini na moyoni sifa hizo nzuri, nawe utazidi kumpenda Mungu na imani yako kwake itaimarika. Katika makala inayofuata tutachunguza njia mbalimbali ambazo tunaweza kumwiga Yehova katika kuwaonyesha wengine ufikirio. Tutakazia fikira jinsi tunavyoweza kuonyesha ufikirio katika familia, kutanikoni, na katika huduma ya shambani.

^ fu. 3 Mwanahistoria Myahudi Yosefo anasema kwamba Samweli alikuwa na umri wa miaka 12 wakati huo.

^ fu. 16 Tunaweza kufikia mkataa kwamba baadhi ya watu watakaookoka Har–Magedoni watakuwa walemavu. Yesu alipokuwa duniani aliponya watu wenye “kila aina ya udhaifu,” na hivyo alitupatia picha ya mambo atakayowafanyia wale watakaookoka Har–Magedoni, si wale watakaofufuliwa. (Mt. 9:35) Bila shaka watu watakaofufuliwa tayari watakuwa wazima bila ulemavu wowote.