Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Yehova kwa Kuwaonyesha Wengine Ufikirio na Fadhili

Mwige Yehova kwa Kuwaonyesha Wengine Ufikirio na Fadhili

“Mwenye furaha ni mtu yeyote anayemjali [au, anayemfikiria] mtu wa hali ya chini.”​—ZAB. 41:1.

NYIMBO: 130, 107

1. Upendo huonyeshwaje miongoni mwa watu wa Mungu?

WATU wa Mungu ni familia ya kiroho, familia ambayo hutambuliwa kwa upendo walio nao. (1 Yoh. 4:16, 21) Upendo huo hauonyeshwi tu kupitia matendo machache makubwa ya kujidhabihu, bali kupitia matendo mengi madogo-madogo, kama vile, maneno na matendo yanayoonyesha ufikirio na fadhili. Tunapowatendea wengine kwa fadhili na ufikirio, tunakuwa “waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.”—Efe. 5:1.

2. Yesu alionyeshaje upendo kama wa Baba yake?

2 Yesu alimwiga Baba yake kikamilifu. Alisema hivi: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha . . . , kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni.” (Mt. 11:28, 29) Tunapoiga mfano wa Kristo kwa “[kumjali, au kumfikiria] mtu wa hali ya chini,” tunapokea kibali cha Baba yetu wa mbinguni na kupata furaha nyingi. (Zab. 41:1) Acheni tuone jinsi tunavyoweza kuwaonyesha wengine ufikirio katika familia, kutanikoni, na katika huduma ya shambani.

WAONYESHE UFIKIRIO WATU WA FAMILIA YAKO

3. Mume anaweza kuonyeshaje kwamba anamwelewa na kumfikiria mke wake? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Waume wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuwaonyesha ufikirio watu wa familia zao. (Efe. 5:25; 6:4) Kwa mfano, waume wanahimizwa wakae na wake zao “kulingana na ujuzi”—maneno yanayoweza kutafsiriwa kuwa “mkiwafikiria na kuwajali; kuwaelewa.” (1 Pet. 3:7; maelezo ya chini) Kumwelewa mtu na kumwonyesha ufikirio ni mambo mawili yanayoenda sambamba. Kwa mfano, mume anayemwelewa mke wake, ambaye ni kikamilisho chake, anajua kwamba yeye ni tofauti na mke wake katika njia nyingi, lakini hilo halimaanishi kwamba mke wake ni duni. (Mwa. 2:18) Hivyo yeye humwonyesha mke wake ufikirio kwa kuzingatia hisia zake, akimtendea kwa heshima na staha. Dada mmoja kutoka Kanada anasema hivi kumhusu mume wake: “Mume wangu hapuuzi kamwe hisia zangu au kusema, ‘Hupaswi kuhisi hivyo.’ Pia, yeye ni msikilizaji mzuri. Anaponisaidia kurekebisha maoni yangu kuhusu jambo fulani, yeye hufanya hivyo kwa fadhili.”

4. Anaposhughulika na wanawake wengine, mume anapaswa kumwonyesha ufikirio mke wake katika njia gani?

4 Pia, mume anayemwonyesha ufikirio mke wake huzingatia hisia zake anaposhughulika na wanawake wengine. Hawachezei kamwe wanawake wengine kimapenzi au kuwaonyesha upendezi kwa njia isiyofaa; wala hatumii mitandao ya kijamii kuwachezea kimapenzi wanawake wengine na hatembelei tovuti zisizofaa. (Ayu. 31:1) Naam, anabaki akiwa mshikamanifu kwa mke wake, si kwa sababu tu anampenda mke wake, bali pia kwa sababu anampenda Mungu na anachukia mambo maovu.—Soma Zaburi 19:14; 97:10.

5. Mke anaweza kumwonyeshaje ufikirio mume wake?

5 Mume anapomwiga Yesu Kristo ambaye ndiye kichwa chake, anafanya iwe rahisi zaidi kwa mke wake “kumheshimu sana.” (Efe. 5:22-25, 33) Heshima hiyo itamchochea mke kumwonyesha ufikirio mume wake, kwa mfano, wakati ambapo mume analazimika kutumia muda mwingi kushughulikia majukumu ya kitheokrasi au ikiwa ana tatizo fulani linalomhangaisha. Ndugu mmoja kutoka Uingereza anasema hivi kumhusu mke wake: “Nyakati nyingine mke wangu anaponitazama anaweza kugundua kwamba kuna jambo fulani linalonihangaisha. Kisha yeye hutumia kanuni iliyo katika andiko la Methali 20:5, hata ikiwa kufanya hivyo kunamaanisha kusubiri mpaka wakati unaofaa ili ‘ateke’ mawazo yangu ikiwa yanahusu jambo ambalo niko huru kuzungumzia pamoja naye.”

6. Sisi sote tunaweza kuwatiaje moyo watoto wawe wenye ufikirio, nao watanufaikaje?

6 Wazazi wanapoonyeshana ufikirio, wanawawekea watoto wao mfano mzuri wa kuiga. Bila shaka wazazi wana daraka la msingi la kuwafundisha watoto wao jinsi ya kuwaonyesha wengine ufikirio. Kwa mfano, wazazi wanaweza kuwafundisha watoto wao wasikimbie-kimbie kwenye Jumba la Ufalme. Kwenye tafrija, huenda wazazi wakawaambia watoto wao wawaruhusu watu wenye umri mkubwa watangulie kwanza kwenye foleni ya chakula. Bila shaka, wote kutanikoni wanaweza kuunga mkono jitihada za wazazi. Kwa mfano, mtoto anapotufanyia tendo fulani la fadhili, labda kutufungulia mlango, tunapaswa kumpongeza. Kufanya hivyo kunaweza kumtia moyo sana na kumsaidia ajifunze kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Mdo. 20:35.

“TUFIKIRIANE” KUTANIKONI

7. Yesu alimwonyeshaje ufikirio mtu aliyekuwa kiziwi na mwenye tatizo la kuzungumza, na tunaweza kujifunza mambo gani kutokana na mfano wa Yesu?

7 Pindi moja Yesu alipokuwa katika eneo la Dekapoli, watu “[walimletea] mtu aliye kiziwi na mwenye tatizo la kuzungumza.” (Marko 7:31-35) Badala ya kumponya hadharani, Yesu ‘alimpeleka faraghani’ na kumponya. Kwa nini? Huenda hali ambayo mwanamume huyo alikuwa nayo ilimfanya awe na wasiwasi akiwa katikati ya umati. Huenda Yesu alitambua hilo, hivyo akampeleka faraghani na kumponya. Ni kweli kwamba hatuwezi kuwaponya watu kimuujiza. Lakini tunaweza—na tunapaswa—kuwaonyesha waabudu wenzetu ufikirio kwa kuzingatia mahitaji na hisia zao. Mtume Paulo aliandika hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” (Ebr. 10:24) Yesu alielewa jinsi mtu huyo aliyekuwa kiziwi alivyohisi, naye akamtendea kwa ufikirio. Huo ni mfano mzuri sana kwetu!

8, 9. Tunaweza kuwaonyeshaje ufikirio wazee-wazee na wagonjwa? (Toa mifano.)

8 Waonyeshe ufikirio wazee-wazee na wagonjwa. Kutaniko la Kikristo hutambuliwa kwa sifa ya upendo, lakini si kwa sifa ya kutimiza mambo kwa njia bora zaidi au haraka. (Yoh. 13:34, 35) Upendo huo hutuchochea tujidhabihu ili kuwasaidia walio na umri mkubwa na wale walio na ulemavu fulani wahudhurie mikutano ya Kikristo na kuhubiri habari njema. Tunafanya hivyo hata ikiwa mambo wanayotimiza ni machache. (Mt. 13:23) Michael, ambaye hawezi kutembea na hutumia kiti cha magurudumu, anathamini sana msaada anaopata kutoka kwa familia yake na ndugu na dada katika kikundi chake cha utumishi wa shambani. Anasema hivi: “Kwa sababu ya msaada wanaonipa, ninafaulu kuhudhuria mikutano na kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani. Ninafurahia zaidi kushiriki katika mahubiri ya hadharani.”

9 Familia nyingi za Betheli zina ndugu na dada waliozeeka au wagonjwa. Waangalizi wenye upendo huwaonyesha ufikirio watumishi hao waaminifu kwa kufanya mipango ili wahubiri kwa njia ya barua au simu. Bill, ndugu mwenye umri wa miaka 86 na ambaye huwaandikia barua watu walio katika maeneo ya mashambani anasema hivi: “Tunathamini pendeleo la kuwaandikia watu barua.” Nancy, dada anayekaribia umri wa miaka 90, anasema hivi: “Kwangu mimi sioni kazi ya kuandika barua kuwa kujaza tu bahasha. Hii ni huduma ya shambani. Watu wanahitaji kujua kweli!” Ethel, dada ambaye alizaliwa mwaka wa 1921, anasema hivi: “Maumivu ni sehemu ya maisha yangu. Kuna siku ambazo ni vigumu kwangu hata kuvaa nguo zangu mwenyewe.” Ingawa hivyo, yeye hufurahia kuhubiri kupitia simu na ana watu kadhaa anaozungumza nao kuhusu Biblia kila juma. Barbara, dada mwenye umri wa miaka 85 anaeleza hivi: “Kwa sababu afya yangu ni mbaya, ni vigumu kwangu kwenda kwa ukawaida katika utumishi wa shambani. Lakini kuhubiri kwa njia ya simu hunisaidia kuzungumza na wengine. Asante Yehova!” Katika muda usiozidi mwaka mmoja, ndugu na dada fulani wapendwa wenye umri mkubwa walihubiri kwa saa 1,228, wakaandika barua 6,265, wakapiga simu zaidi ya 2,000, na kuwaachia watu machapisho 6,315! Bila shaka jitihada zao zilimletea Yehova shangwe nyingi!—Met. 27:11.

10. Tunaweza kuwasaidiaje ndugu zetu wanufaike kikamili na mikutano yetu ya Kikristo?

10 Onyesha ufikirio katika mikutano ya Kikristo. Tungependa ndugu zetu wanufaike kikamili na mikutano. Tunapowaonyesha ufikirio tunawasaidia kufanya hivyo. Jinsi gani? Njia moja ni kwa kufika kwa wakati ili tusiwakengeushe isivyo lazima. Bila shaka, pindi kwa pindi matukio yasiyotazamiwa yanaweza kutuchelewesha. Lakini ikiwa tuna kawaida ya kuchelewa, tunapaswa kujichunguza na kutambua mabadiliko tunayopaswa kufanya ili tuwaonyeshe wengine ufikirio zaidi. Kumbuka kwamba Yehova na Yesu ndio waliotualika. (Mt. 18:20) Hapana shaka kwamba tunapaswa kuwaonyesha heshima wanayostahili kwa kufika kwa wakati!

11. Kwa nini wale walio na sehemu mikutanoni wanapaswa kufuata mwongozo ulio kwenye andiko la 1 Wakorintho 14:40?

11 Kuwaonyesha ndugu zetu ufikirio kunamaanisha pia kutii agizo hili: “Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Akina ndugu wanaofundisha mikutanoni hutii mwongozo huo kwa kuzingatia muda waliopewa kushughulikia sehemu zao. Kwa kufanya hivyo hawamwonyeshi tu msemaji atakayefuata ufikirio, bali pia ndugu na dada kutanikoni. Huenda baadhi ya akina ndugu wanaishi mbali. Huenda wengine wanatumia usafiri wa umma. Na huenda wengine wana wenzi wa ndoa ambao si Mashahidi wa Yehova wanaowasubiri warudi nyumbani haraka.

12. Kwa nini wazee wa kutaniko wanaofanya kazi kwa bidii wanastahili ‘kufikiriwa kwa njia inayozidi ile ya kawaida katika upendo’? (Tazama sanduku lenye kichwa “ Wafikirie Wale Wanaoongoza.”)

12 Wazee wanaofanya kazi kwa bidii kwenye makutaniko na ambao huwa mstari wa mbele katika huduma ya shambani wanastahili kuonyeshwa ufikirio wa pekee. (Soma 1 Wathesalonike 5:12, 13.) Hapana shaka kwamba unathamini jitihada ambazo wazee wa kutaniko hufanya kwa ajili yako. Hivyo basi, fanya yote uwezayo kuonyesha kwamba unawathamini kwa kuwa tayari kushirikiana nao na kuwaunga mkono. Ukweli ni kwamba “wanaendelea [kukulinda] kama wale watakaotoa hesabu.”—Ebr. 13:7, 17.

WAONYESHE WENGINE UFIKIRIO KATIKA HUDUMA

13. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyowatendea watu?

13 Isaya alitabiri hivi kumhusu Yesu: “Hataponda tete lililovunjika, wala hatazima utambi unaofifia.” (Isa. 42:3) Yesu aliwaonyesha watu hisia mwenzi kwa sababu aliwapenda. Alielewa hisia za wale ambao walikuwa kama tete lililovunjika au utambi wa taa inayokaribia kuzima. Kwa sababu hiyo aliwaonyesha ufikirio, fadhili, na subira. Hata watoto wadogo walitaka kuwa karibu na Yesu. (Marko 10:14) Ni kweli kwamba hatuna utambuzi au uwezo wa kufundisha kama wa Yesu! Lakini tunaweza—na tunapaswa—kuwaonyesha ufikirio watu katika eneo letu. Hilo linahusisha jinsi tunavyozungumza nao, wakati tunaozungumza nao, na muda tunaotumia kuzungumza nao.

14. Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu jinsi tunavyozungumza na watu?

14 Tunapaswa kuzungumza na watu jinsi gani? Leo, mamilioni ya watu “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku” na wafanyabiashara, wanasiasa, na viongozi wa kidini waliopotoka na wasio na huruma. (Mt. 9:36) Hilo limewafanya watu wasimwamini yeyote na wasiwe na tumaini. Hivyo, ni muhimu sana kwamba maneno yetu na njia yetu ya kuzungumza ionyeshe kwamba tuna fadhili na huruma! Kwa hakika, watu wengi wanavutiwa na ujumbe wetu si kwa sababu tu ya ujuzi wetu wa Biblia au hoja zinazosadikisha, bali pia kwa sababu tunapendezwa nao kikweli na tunawaonyesha ufikirio.

15. Tunaweza kuwaonyeshaje ufikirio watu tunaowahubiria?

15 Kuna njia nyingi tunazoweza kuwaonyesha ufikirio watu tunaowahubiria. Kwa mfano, kutumia maswali ni mbinu nzuri ya kufundisha. Tunapaswa kuuliza maswali kwa njia yenye fadhili na heshima. Painia mmoja aliyehubiri katika eneo ambalo watu wengi ni wakimya na wenye haya alijifunza kuuliza maswali ambayo hayangewaaibisha wenye nyumba. Aliepuka maswali ambayo huenda mwenye nyumba angeshindwa kujibu au kutoa jibu lisilo sahihi. Kwa mfano, aliepuka maswali kama vile, ‘Je, unajua jina la Mungu?’ au ‘Je, unajua Ufalme wa Mungu ni nini?’ Badala yake, angesema hivi; “Nimejifunza katika Biblia kwamba Mungu ana jina lake binafsi. Ungependa nikuonyeshe jina hilo?” Bila shaka tamaduni na watu hutofautiana, hivyo hatuhitaji kuweka sheria kuhusu jambo hilo. Hata hivyo, sikuzote tunapaswa kuwaheshimu wengine na kuwaonyesha ufikirio, na jambo hilo linatia ndani kuwajua vizuri watu wa eneo letu.

16, 17. Tunaweza kuonyeshaje ufikirio (a) inapohusu muda tunaowatembelea watu katika nyumba zao? (b) inapohusu muda tunaotumia kuzungumza na watu katika huduma ya shambani?

16 Tunapaswa kuwatembelea watu wakati gani? Tunapohubiri nyumba kwa nyumba, sisi ni wageni wasiotazamiwa. Hivyo, ni muhimu sana tuwatembelee watu wakati ambapo ni rahisi zaidi kwao kuzungumza nasi! (Mt. 7:12) Kwa mfano, je, watu katika eneo lenu wanapenda kulala kwa muda mrefu zaidi wakati wa miisho-juma? Ikiwa ndivyo, huenda ukaanza huduma yako kwa kuhubiri barabarani, kufanya utumishi wa hadharani, au kuwarudia watu ambao unajua tayari wameamka.

17 Tunapaswa kutumia muda mrefu kadiri gani? Watu wengi wana shughuli nyingi, hivyo huenda ikafaa kuwa na mazungumzo mafupi nao, angalau siku za kwanza. Ni afadhali kuwa na mazungumzo mafupi kuliko marefu. (1 Kor. 9:20-23) Watu wanapoona kwamba tunatambua hali zao na tunatambua kwamba wana shughuli nyingi, huenda wakawa tayari zaidi kuturuhusu turudi tena. Kwa hakika, tunda la roho takatifu ya Mungu linapaswa kuonekana katika huduma yetu. Linapoonekana wazi, kwa kweli tunakuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu,” au hata tunaweza kutumiwa na Yehova kumvuta mtu kwenye kweli.—1 Kor. 3:6, 7, 9.

18. Tutapata baraka gani tunapowaonyesha wengine ufikirio?

18 Hivyo, acheni tufanye yote tuwezayo ili tuwaonyeshe wengine ufikirio, iwe ni katika familia, kutanikoni, au katika huduma ya shambani. Tunapofanya hivyo, tutapokea baraka nyingi sasa na wakati ujao. Andiko la Zaburi 41:1, 2 linasema hivi: “Mwenye furaha ni mtu yeyote anayemjali [au, anayemfikiria] mtu wa hali ya chini; Yehova atamwokoa siku ya msiba. . . . Atatangazwa kuwa mwenye furaha duniani.”