Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Enyi Wakristo Wenye Umri Mkubwa​—Yehova Anathamini Sana Ushikamanifu Wenu

Enyi Wakristo Wenye Umri Mkubwa​—Yehova Anathamini Sana Ushikamanifu Wenu

KOTEKOTE ulimwenguni, wazee wa makutaniko wanathamini sana mapendeleo ya utumishi waliyonayo miongoni mwa watu wa Mungu. Wazee hao ni baraka kwelikweli kwetu sote! Hata hivyo, hivi karibuni badiliko fulani lilifanyika. Wazee wa makutaniko wenye umri mkubwa waliombwa wawakabidhi wazee wenye umri mdogo zaidi baadhi ya majukumu mazito waliyonayo. Jinsi gani?

Chini ya mpango huo mpya, waangalizi wa mzunguko na walimu wa shule za kitheokrasi hawataendelea kutumikia katika mapendeleo hayo wanapofika umri wa miaka 70. Pia, wazee wanapofikisha umri wa miaka 80 watawakabidhi wazee wenye umri mdogo zaidi baadhi ya migawo waliyonayo, kama vile kuwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi au mratibu wa baraza la wazee kutanikoni. Ndugu hao wapendwa wenye umri mkubwa wameitikiaje mabadiliko hayo? Wameendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake!

Ken, ambaye ametumikia akiwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi kwa miaka 49 hivi anaeleza hivi: “Nilikubaliana kabisa na uamuzi huo. Kwa kweli, asubuhi ileile, kabla ya kupata habari kuhusu mabadiliko hayo, nilikuwa nimesali kwa Yehova nikimweleza kwamba tulihitaji ndugu mwenye umri mdogo zaidi atumikie akiwa mratibu.” Maelezo ya Ken yanafanana na maelezo ya ndugu wengi waaminifu wenye umri mkubwa ulimwenguni pote. Hata hivyo, kwa kuwa walipenda kuwatumikia ndugu zao kwa njia hizo, mwanzoni mabadiliko hayo yaliwahuzunisha kidogo.

Esperandio, ndugu ambaye alitumikia akiwa mratibu wa baraza la wazee kutanikoni anaeleza hivi: “Nilihuzunika kidogo.” Lakini anakiri hivi: “Nilihitaji muda mwingi zaidi wa kushughulikia matatizo yangu ya afya.” Hatushangai kwamba Esperandio anaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu na ni baraka kutanikoni.

Vipi kuhusu wale ambao wametumikia wakiwa waangalizi wasafirio kwa miaka mingi, lakini sasa wanatumikia katika aina tofauti za utumishi? Allan, ambaye alitumikia kwa miaka 38 akiwa mwangalizi anayesafiri, anakiri hivi: “Nilipopata habari hizo, nilishtuka sana.” Hata hivyo, alitambua faida za kuwazoeza kazi hiyo wanaume vijana, naye anaendelea kutumikia kwa uaminifu.

Russell, ambaye alitumikia kwa miaka 40 akiwa mwangalizi anayesafiri na pia mwalimu wa shule za kitheokrasi, anasema kwamba mwanzoni yeye na mke wake walivunjika moyo. Wanaeleza hivi: “Tulithamini sana pendeleo letu na tulihisi kwamba bado tuna nguvu za kuendelea na mgawo wetu.” Sasa Russell na mke wake wanatumia mazoezi na uzoefu waliopata kunufaisha kutaniko lao, na wahubiri wa kutaniko hilo wanafurahia sana kutumikia pamoja nao.

Hata ikiwa wewe binafsi hujapitia hali au hisia za ndugu waliotajwa mapema, simulizi fulani katika 2 Samweli linaweza kukusaidia kuelewa hisia za wale ambao wamepitia hali hizo.

MWANAMUME MWENYE KIASI, ALIYEONA MAMBO KIHALISI

Fikiria wakati Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi, alipoasi. Daudi alikimbia kutoka Yerusalemu hadi Mahanaimu, upande wa mashariki wa Mto Yordani. Akiwa huko, Daudi na watu aliokuwa nao walihitaji mahitaji muhimu. Je, unakumbuka kilichotukia?

Kwa ukarimu, wanaume watatu wa eneo hilo waliwaletea vitanda, vyakula mbalimbali, na vyombo walivyohitaji. Mmoja wao alikuwa Barzilai. (2 Sam. 17:27-29) Baada ya uasi wa Absalomu kukomeshwa, Daudi angeweza kurudi Yerusalemu, na Barzilai alimsindikiza hadi kwenye Mto Yordani. Daudi alimsihi Barzilai aende naye Yerusalemu. Mfalme alimwahidi kwamba angemwandalia chakula huko Yerusalemu, hata ingawa Barzilai alikuwa “tajiri sana” na hivyo hangehitaji chakula hicho. (2 Sam. 19:31-33) Inaonekana kwamba Daudi alithamini sana sifa nzuri za Barzilai na mapendekezo yoyote ambayo angeweza kumpa. Bila shaka lilikuwa pendeleo zuri sana kuishi na kufanya kazi kwenye makao ya mfalme!

Lakini kwa kuwa Barzilai aliona mambo kihalisi na alikuwa mwenye kiasi, alimtajia mfalme kwamba alikuwa na umri wa miaka 80. Kisha akasema hivi: “Je, ninaweza kutofautisha kati ya jema na baya?” Alimaanisha nini? Ni wazi kwamba Barzilai alikuwa amejipatia hekima kwa miaka mingi ambayo alikuwa ameishi. Na angeweza kumpa mfalme ushauri mzuri, kama walivyofanya wale “wanaume wazee” wakati wa Mfalme Rehoboamu. (1 Fal. 12:6, 7; Zab. 92:12-14; Met. 16:31) Hivyo, maneno ya Barzilai kuhusu kushindwa kutofautisha kati ya jema na baya huenda yalirejelea matatizo ya kimwili aliyokuwa nayo au matatizo yaliyotokana na umri wake mkubwa. Alikiri kwamba uzee ulikuwa umeathiri uwezo wake wa kuonja ladha ya chakula na uwezo wake wa kusikia. (Mhu. 12:4, 5) Hivyo, kwa hiari Barzilai alimsihi Daudi aende Yerusalemu pamoja na Kimhamu, mwanamume mwenye umri mdogo zaidi, ambaye inaelekea alikuwa mwana wake.—2 Sam. 19:35-40.

KUFANYA MIPANGO KWA AJILI YA WAKATI UJAO

Badiliko lililozungumziwa mwanzoni mwa makala hii, linaonyesha mtazamo kama ule aliokuwa nao Barzilai. Ni wazi kwamba mambo mengi zaidi yalihitaji kuzingatiwa katika kipindi chetu kuliko tu uwezo au hali ya mtu mmoja kama ilivyokuwa katika kisa cha Barzilai. Kulikuwa na uhitaji wa kufikiria kihalisi mpango bora zaidi ambao ungewafaa kabisa wazee waaminifu wa makutaniko wanaotumikia ulimwenguni pote.

Wanaume hao Wakristo wenye umri mkubwa na wenye kiasi, waliona waziwazi kwamba tengenezo la Yehova lingeimarishwa kwa ajili ya ukuzi wa wakati ujao ikiwa majukumu waliyoshughulikia kwa miaka mingi yangeshughulikiwa na akina ndugu wenye umri mdogo zaidi. Katika visa vingi, ndugu hao wenye umri mkubwa ndio waliowazoeza ndugu wenye umri mdogo zaidi, kama ambavyo huenda Barzilai alimzoeza mwana wake na mtume Paulo akamzoeza Timotheo. (1 Kor. 4:17; Flp. 2:20-22) Ndugu hao wenye umri mdogo zaidi wamejithibitisha wenyewe kuwa ‘wanaume waliotolewa kuwa zawadi,’ wanaosaidia “kuujenga mwili wa Kristo.”—Efe. 4:8-12; linganisha Hesabu 11:16, 17, 29.

KUSHIRIKI KATIKA FURSA NYINGINE ZA UTUMISHI

Katika kutaniko la ulimwenguni pote la watu wa Mungu, akina ndugu wengi ambao wamewakabidhi wengine mapendeleo yao wamefaulu kutumia vizuri fursa mpya za utumishi au kupanua utumishi wao katika kazi ya Yehova.

Marco, ambaye alitumikia kwa miaka 19 akiwa mwangalizi anayesafiri anaeleza hivi: “Sasa hali yangu inaniruhusu kuwasaidia kiroho waume wasioamini wa akina dada katika kutaniko langu.”

Geraldo, ambaye alitumikia kwa miaka 28 akiwa mwangalizi anayesafiri anaeleza hivi: “Malengo yetu mapya yanatia ndani kuwasaidia wale walioacha kutenda na pia kuwafundisha watu wengi zaidi Biblia.” Anaripoti kwamba kufikia sasa yeye na mke wake wana wanafunzi 15 wa Biblia na wengi wa wale waliokuwa wameacha kutenda sasa wanahudhuria mikutano.

Allan, ndugu aliyetajwa mapema, anaeleza hivi: “Sasa tuna fursa ya kutumia wakati mwingi zaidi katika aina mbalimbali za huduma yetu. Tunafurahia mahubiri ya hadharani, kuhubiri kwenye maeneo ya biashara, na kuwahubiria jirani zetu, na wawili kati yao wamefika kwenye Jumba la Ufalme.”

Ikiwa wewe ni ndugu mshikamanifu na mwenye uwezo, na umepokea mgawo mpya miongoni mwa watu wa Mungu, kuna njia nyingine ya pekee unayoweza kutumikia. Unaweza kutegemeza kazi ya Yehova kwa kutumia uzoefu wako wenye thamani kuwasaidia wanaume vijana kutanikoni. Russell, ndugu aliyetajwa mapema anasema hivi: “Yehova anawazoeza na kuwatumia wanaume wenye uwezo mkubwa ambao wana umri mdogo. Tengenezo linafaidika kutokana na ufundishaji na uchungaji wenye bidii wanaofanya!”—Tazama sanduku lenye kichwa, “ Wasaidie Wanaume Vijana Kufanya Yote Wawezayo.”

YEHOVA ANATHAMINI SANA USHIKAMANIFU WAKO

Ikiwa hivi karibuni ulianza utumishi wa aina tofauti, endelea kudumisha mtazamo mzuri. Tayari umewagusa moyo watu wengi sana kupitia kazi yako uliyotimiza kwa moyo wote, na bado unaweza kuendelea kufanya hivyo. Unapendwa sana na bila shaka wataendelea kukupenda.

Na jambo muhimu hata zaidi, una sehemu ya kudumu katika moyo wa Yehova. ‘Hatasahau kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuhudumu na kuendelea kuwahudumia watakatifu.’ (Ebr. 6:10) Maneno hayo yaliyoongozwa na roho yanatuhakikishia kwamba Yehova ataendelea kukumbuka hata kazi tulizofanya zamani. Wewe ni mwenye thamani sana machoni pa Yehova hivi kwamba hawezi kamwe kukusahau kwa jitihada ulizofanya zamani za kumpendeza na jitihada unazoendelea kufanya hata sasa ili kumpendeza!

Vipi ikiwa wewe binafsi hujabadilishiwa mgawo, kama ndugu waliotajwa mapema? Bado huenda habari hii inakuhusu moja kwa moja. Katika njia gani?

Ikiwa kwa sasa unashirikiana na ndugu mwaminifu mwenye umri mkubwa ambaye amebadilishiwa mgawo, unaweza kufaidika kutokana na ukomavu na uzoefu wake wa miaka mingi. Mwombe ushauri. Mwombe akupatie mapendekezo. Na ona jinsi anavyotumia kwa ushikamanifu uzoefu alionao katika mgawo wake mpya.

Iwe wewe ni ndugu mwenye umri mkubwa anayetumikia katika mgawo tofauti kwa sasa au ni ndugu au dada anayeweza kufaidika na uzoefu wa ndugu mwenye umri mkubwa, kumbuka kwamba Yehova anathamini sana ushikamanifu wa wale ambao wamemtumikia kwa muda mrefu na ambao wanaendelea kufanya hivyo.