Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wenye Furaha Ni Watu Wanaomtumikia “Mungu Mwenye Furaha”

Wenye Furaha Ni Watu Wanaomtumikia “Mungu Mwenye Furaha”

“Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—ZAB. 144:15.

NYIMBO: 44, 125

1. Kwa nini waabudu wa Yehova ni watu wenye furaha? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

HAPANA shaka kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wenye furaha. Mikutano, makusanyiko, na tafrija zao ni pindi zenye shangwe, furaha, na sauti za vicheko. Kwa nini wao ni watu wenye furaha sana? Sababu kuu ni kwamba wanamjua, wanamtumikia, na wanajitahidi kumwiga Yehova, “Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11; Zab. 16:11) Kwa kuwa Mungu ndiye Chanzo cha furaha, anataka tuwe na furaha, naye hutupatia sababu nyingi za kushangilia.—Kum. 12:7; Mhu. 3:12, 13.

2, 3. (a) Furaha ni nini? (b) Kwa nini inaweza kuwa vigumu kuwa na furaha?

2 Namna gani wewe binafsi? Je, una furaha? Je, unaweza kuongeza furaha yako? Furaha inaweza kufafanuliwa kuwa “hali nzuri yenye kuendelea ambayo mtu huwa nayo, inayohusisha hisia mbalimbali kuanzia hisia za kuridhika mpaka hisia zenye kina za shangwe ya kuishi, na inayohusisha tamaa ya asili ya kutaka kuendelea kuwa na hali hiyo.” Biblia inaonyesha kwamba furaha ya kweli inarejelea hali ambayo mtu ambaye amebarikiwa na Yehova huwa nayo. Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo, inaweza kuwa vigumu kuwa na furaha. Kwa nini?

3 Matukio yenye kufadhaisha kama vile kufiwa na mtu unayempenda au mpendwa wetu anapotengwa na ushirika, talaka, au kupoteza kazi yanaweza kufanya tupoteze furaha. Pia, tunaweza kukosa furaha ikiwa hakuna amani nyumbani kwa sababu ya ugomvi wa mara kwa mara. Kudhihakiwa na wafanyakazi au wanafunzi wenzetu, kuteswa au kufungwa gerezani kwa sababu ya imani yetu ni mambo yanayoweza kuathiri furaha yetu. Pia, tunaweza kukosa furaha ikiwa afya yetu inadhoofika, au tuna ugonjwa wa kudumu, au ikiwa tumeshuka moyo. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yesu Kristo, “Mtawala Mkuu wa pekee na mwenye furaha,” alifurahia kuwafariji watu na kuwatendea mambo ambayo yangewafurahisha. (1 Tim. 6:15; Mt. 11:28-30) Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitaja sifa kadhaa zinazoweza kutusaidia kuwa na furaha licha ya kwamba tunakabili hali zenye kufadhaisha katika ulimwengu wa Shetani.

HALI NZURI YA KIROHO —MSINGI WA KUWA NA FURAHA

4, 5. Tunaweza kupataje furaha na kuidumisha?

4 Jambo la kwanza ambalo Yesu alitaja katika Mahubiri yake ya Mlimani ni muhimu sana: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa Ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 5:3) Tunaonyeshaje kwamba tunatambua uhitaji wetu wa kiroho? Tunafanya hivyo kwa kujilisha chakula cha kiroho, kuthamini viwango vya kiroho, na kutanguliza ibada yetu kwa Mungu wetu mwenye furaha. Tukifanya hivyo, furaha yetu itaongezeka. Tutaimarisha imani yetu katika ahadi za Mungu zitakazotimia hivi karibuni. Nasi tutatiwa moyo na “tumaini lenye furaha” ambalo Neno la Mungu huwapa waabudu wa kweli.—Tito 2:13.

5 Kujenga uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova ni jambo muhimu linalotusaidia kuwa na furaha ya kudumu. Mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika hivi: “Shangilieni sikuzote katika Bwana [Yehova]. Nitasema tena, Shangilieni!” (Flp. 4:4) Ili tufurahie uhusiano huo wenye thamani, tunahitaji kujipatia hekima inayotoka kwa Mungu. Neno la Mungu linasema hivi: “Mwenye furaha ni mtu anayepata hekima, na mtu anayepata utambuzi. Ni mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika kwa nguvu wataitwa wenye furaha.”—Met. 3:13, 18.

6. Tunapaswa kufanya nini kingine ili tuendelee kuwa na furaha sikuzote?

6 Hata hivyo, ili tuendelee kuwa na furaha sikuzote, hatupaswi tu kusoma Neno la Mungu, bali pia ni muhimu tutumie mambo tunayosoma. Yesu alikazia umuhimu wa kutumia mambo tunayojifunza aliposema hivi: “Ikiwa mnajua mambo haya, mtakuwa wenye furaha mkiyatenda.” (Yoh. 13:17; soma Yakobo 1:25.) Hiyo ndiyo siri ya kutosheleza uhitaji wako wa kiroho na ya kuendelea kuwa na furaha sikuzote. Lakini tunawezaje kuwa na furaha ilhali kuna mambo mengi yanayoweza kufanya tukose furaha? Acheni tuchunguze jambo linalofuata lililotajwa na Yesu katika Mahubiri yake ya Mlimani.

SIFA ZINAZOONGEZA FURAHA

7. Wale wanaoomboleza wanawezaje kuwa wenye furaha?

7 “Wenye furaha ni wale wanaoomboleza, kwa kuwa watafarijiwa.” (Mt. 5:4) Huenda wengine wakajiuliza hivi: ‘Inawezekanaje kwa wale wanaoomboleza kuwa na furaha?’ Yesu hakuwa akizungumzia watu wanaoomboleza kwa sababu yoyote ile. Hata watu waovu huomboleza kwa sababu ya hali ngumu ambazo zimeenea katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Hata hivyo, wanaomboleza kwa sababu zao za kibinafsi na jambo hilo haliwafanyi wamkaribie Yehova; hivyo huzuni yao haiwaletei furaha. Yesu alikuwa akizungumza kuhusu watu wanaotambua uhitaji wao wa kiroho na kwa hiyo wanaomboleza kwa sababu ya hali mbaya ya kiroho iliyopo. Wanatambua kwamba wao ni wenye dhambi na wanatambua hali zenye kuvunja moyo zilizosababishwa na wanadamu wenye dhambi. Yehova anawaona watu hao wanaohuzunika kutoka moyoni; naye anawafariji na kuwabariki kwa kuwapa kitulizo cha kiroho, furaha, na tumaini la uzima wa milele.—Soma Ezekieli 5:11; 9:4.

8. Eleza jinsi kuwa wapole kunavyotusaidia kuwa wenye furaha.

8 “Wenye furaha ni wale walio wapole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mt. 5:5) Kuwa wapole kunaweza kutusaidiaje kuwa na furaha? Baada ya kupata ujuzi sahihi wa kweli, watu hubadilika. Huenda wakati uliopita walikuwa wakatili, wagomvi, na wakali. Lakini sasa wamejivika “utu mpya” na wanaonyesha sifa kama vile “upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu, upole, na subira.” (Kol. 3:9-12) Na matokeo ni kwamba sasa wanafurahia maisha yenye amani, upendo, na furaha. Zaidi ya hilo, Neno la Mungu linaahidi kwamba watu kama hao “watairithi dunia.”—Zab. 37:8-10, 29.

9. (a) Wapole “watairithi dunia” katika maana gani? (b) Kwa nini “wale walio na njaa na kiu ya uadilifu” wanaweza kuwa na furaha?

9 Wapole “watairithi dunia” katika maana gani? Wanafunzi wa Yesu waliotiwa mafuta watairithi dunia watakapotawala juu yake wakiwa wafalme na makuhani. (Ufu. 20:6) Hata hivyo, mamilioni ya watu ambao hawana mwito wa kwenda mbinguni watairithi dunia katika maana ya kwamba wataruhusiwa kuishi hapa duniani milele wakiwa wakamilifu, wenye amani, na furaha. Watiwa-mafuta na kondoo wengine ndio walewale wanaotajwa kuwa wenye furaha kwa sababu wana “njaa na kiu ya uadilifu.” (Mt. 5:6) Njaa yao ya kiroho na kiu yao ya uadilifu itatoshelezwa kikamili katika ulimwengu mpya. (2 Pet. 3:13) Mungu atakapoondoa uovu wote, furaha ya waadilifu itadumu kwa sababu hakutakuwa na uasi sheria wala ukosefu wa uadilifu.—Zab. 37:17.

10. Kuwa mwenye rehema kunamaanisha nini?

10 “Wenye furaha ni wale wenye rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mt. 5:7) Kitenzi cha Kiebrania kinachohusianishwa na rehema kinamaanisha “kuwaka, kuwa na joto la hisia nyororo; . . . kuwa mwenye huruma.” Vivyo hivyo, kitenzi cha Kigiriki kinatia ndani hisia ya kumhurumia mtu. Hata hivyo, rehema inahusisha mengi zaidi ya kuwa na hisia nyororo. Katika Biblia, kuwa na rehema kunatia ndani kuonyesha kwa matendo kwamba tunawasikitikia wengine, yaani, kwa kufanya tendo fulani la rehema.

11. Tunaweza kujifunza nini kuhusu kuwa wenye rehema kutokana na mfano wa Msamaria mwema?

11 Soma Luka 10:30-37. Mfano wa Yesu wa Msamaria mwema unaonyesha waziwazi kinachomaanishwa na kuonyesha rehema. Akichochewa na huruma na rehema ya kutoka moyoni, Msamaria huyo alichukua hatua inayofaa kwa kumpa kitulizo mwanamume aliyekuwa akiteseka. Baada ya kusimulia mfano huo, Yesu alisema hivi: “Nenda ukafanye vivyo hivyo.” Hivyo, tunaweza kujiuliza: ‘Je, mimi ninafanya hivyo? Je, mimi hutenda kama alivyotenda Msamaria huyo mwenye huruma? Je, ninaweza kuonyesha rehema hata zaidi na kuwatendea wale wanaoteseka matendo yenye fadhili? Kwa mfano, je, ninaweza kuwasaidia Wakristo wenzangu wenye umri mkubwa, wajane, na watoto ambao wazazi wao hawamtumikii Yehova? Je, ninaweza kuchukua hatua ya kwanza ili “[kuwafariji] wale walioshuka moyo”?’—1 The. 5:14; Yak. 1:27.

Chukua hatua ya kwanza kuonyesha rehema ujionee jinsi utakavyokuwa na furaha (Tazama fungu la 12)

12. Kuwa wenye rehema huchangiaje furaha yetu?

12 Hata hivyo, kuwa wenye rehema hutuleteaje furaha? Tunapowaonyesha wengine rehema, tunapata furaha inayotokana na kutoa. Isitoshe, tunajua kwamba tunampendeza Yehova. (Mdo. 20:35; soma Waebrania 13:16.) Mfalme Daudi alisema hivi kuhusu mtu anayeonyesha kwamba anawajali wengine: “Yehova atamlinda na kumhifadhi hai. Atatangazwa kuwa mwenye furaha duniani.” (Zab. 41:1, 2) Kuwatendea wengine kwa huruma kutatusaidia sisi pia kupokea rehema za Yehova, jambo ambalo litatuletea furaha milele.—Yak. 2:13.

KWA NINI “WALE WALIO SAFI MOYONI” NI WENYE FURAHA

13, 14. Kuna uhusiano gani kati ya kuwa safi moyoni na kuwa wenye furaha?

13 Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni, kwa kuwa watamwona Mungu.” (Mt. 5:8) Ili tuwe safi moyoni, ni lazima tuhakikishe kwamba mawazo yetu ni safi na tupende na kutamani mambo yaliyo safi. Lazima tudumishe mawazo yetu yakiwa safi ili ibada yetu kwa Yehova isiwe na dosari yoyote.—Soma 2 Wakorintho 4:2; 1 Tim. 1:5.

14 Wale walio safi moyoni wanaweza kufurahia msimamo safi mbele za Yehova, ambaye hutangaza hivi: “Wenye furaha ni wale wanaofua kanzu zao.” (Ufu. 22:14) ‘Wanafua kanzu zao’ katika maana gani? Wakristo watiwa-mafuta ‘wanafua kanzu zao’ katika maana ya kwamba wao ni safi machoni pa Yehova, nao watapewa uhai usioweza kufa na watakuwa na furaha milele huko mbinguni. Umati mkubwa wa watu walio na tumaini la kuishi duniani wanaweza pia kufurahia msimamo wa uadilifu wakiwa rafiki za Mungu. Hata sasa “[wanafua] kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwanakondoo.”—Ufu. 7:9, 13, 14.

15, 16. Ni katika njia gani wale walio safi moyoni “watamwona Mungu”?

15 Hivyo basi, ni katika njia gani wale walio safi moyoni “watamwona Mungu,” ilhali “hakuna mwanadamu anayeweza [kumwona Mungu] na aendelee kuishi”? (Kut. 33:20) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘ona’ linaweza kumaanisha “kuona kwa kutumia akili, kutambua, kujua.” Wale ambao humwona Mungu kupitia “macho ya moyo” wao ni wale ambao wamemjua Mungu kikweli, na kuthamini sifa zake. (Efe. 1:18) Yesu aliiga utu wa Mungu kikamilifu, hivyo angeweza kusema hivi: “Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yoh. 14:7-9.

16 Mbali na kujua sifa za Mungu, waabudu wa kweli ‘humwona Mungu’ wanapojionea jinsi anavyowasaidia maishani mwao. (Ayu. 42:5) Pia, wanamwona Mungu wanapokaza ‘macho ya moyo wao’ kwenye baraka nzuri ajabu ambazo Mungu anawaahidi wale wanaojitahidi kubaki wakiwa safi na kumtumikia kwa ushikamanifu. Bila shaka, watiwa-mafuta watamwona Yehova kihalisi watakapofufuliwa na kupokea thawabu yao mbinguni.—1 Yoh. 3:2.

WENYE FURAHA LICHA YA MATATIZO

17. Kufanya amani hutusaidiaje kuwa wenye furaha?

17 Yesu aliendelea kusema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani.” (Mt. 5:9) Wale wanaochukua hatua ya kwanza kufanya amani wana sababu nzuri ya kuwa wenye furaha. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Tunda la uadilifu hupandwa katika hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” (Yak. 3:18) Ikiwa uhusiano wetu pamoja na watu wa familia yetu au ndugu na dada kutanikoni si mzuri, tunaweza kumsihi Mungu atusaidie tuwe wenye kufanya amani. Kwa njia hiyo, roho takatifu ya Yehova itakusaidia kusitawisha sifa za Kikristo, nawe utakuwa na furaha zaidi. Yesu alikazia umuhimu wa kuchukua hatua ya kwanza kufanya amani aliposema hivi: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo unakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, iache zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, uende zako. Kwanza fanya amani na ndugu yako, kisha urudi na kutoa zawadi yako.”—Mt. 5:23, 24.

18, 19. Kwa nini Wakristo wanaweza kushangilia hata ikiwa wanateswa?

18 “Wenye furaha ni ninyi, watu wanapowashutumu na kuwatesa na kuwasingizia kila aina ya uovu kwa sababu yangu.” Yesu alimaanisha nini? Aliongeza hivi: “Furahini na kushangilia sana, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni, kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwapo kabla yenu.” (Mt. 5:11, 12) Mitume walipopigwa na kuamriwa waache kuhubiri, “[walitoka] mbele ya Sanhedrini, wakishangilia.” Ni kweli kwamba hawakuwa wakifurahia maumivu waliyopata kwa sababu ya kupigwa. Badala yake, walishangilia “kwa sababu walikuwa wamestahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina [la Yesu].”—Mdo. 5:41.

19 Katika nyakati zetu pia, watu wa Yehova wanavumilia kwa shangwe wanapoteseka kwa ajili ya jina la Yesu au wanapokabili majaribu makali. (Soma Yakobo 1:2-4.) Kama mitume, sisi pia hatufurahii aina yoyote ya mateso. Lakini ikiwa tutadumisha utimilifu wetu kwa Mungu wakati wa majaribu, Yehova atatusaidia tuendelee kuvumilia kwa ujasiri. Kwa mfano, katika mwezi wa Agosti mwaka wa 1944, wenye mamlaka katika nchi fulani iliyotawala kimabavu waliwapeleka Henryk Dornik na kaka yake kwenye kambi ya mateso. Hata hivyo, wapinzani hao walikiri hivi: “Huwezi kuwashawishi wafanye jambo lolote. Wanapata shangwe wanapokufa kwa ajili ya imani yao.” Ndugu Dornik alieleza hivi: “Ingawa si kwamba nilitaka kufa, kuteseka kwa ujasiri na kuheshimu ushikamanifu wangu kwa Yehova kuliniletea shangwe. . . . Sala za kutoka moyoni zilinisaidia kumkaribia Yehova zaidi, naye alithibitika kuwa Msaidizi mwenye kutegemeka.”

20. Kwa nini tunafurahia kumtumikia “Mungu mwenye furaha”?

20 Tunapokuwa na kibali cha “Mungu mwenye furaha,” tunaweza kuwa wenye furaha hata ikiwa tunateswa kwa sababu ya imani yetu, tunakabili upinzani nyumbani, sisi ni wagonjwa, au umri umesonga sana. (1 Tim. 1:11) Pia, tunakuwa wenye furaha kwa sababu ya ahadi zenye thamani ambazo Mungu wetu “asiyeweza kusema uwongo” ametuahidi. (Tito 1:2) Yehova atatimiza ahadi zake kwa njia yenye kustaajabisha sana hivi kwamba hatutakumbuka tena matatizo na majaribu tunayokabili kwa sasa. Katika Paradiso inayokuja, baraka tutakazopata kutoka kwa Yehova zitazidi jambo lolote tunaloweza kuwazia sasa. Na kwa hakika, tutakuwa na furaha isiyo na kifani. Naam, “[tutafurahia] kwelikweli wingi wa amani.”—Zab. 37:11.