Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 37

Jitiishe kwa Yehova kwa Hiari—Kwa Nini na Jinsi Gani?

Jitiishe kwa Yehova kwa Hiari—Kwa Nini na Jinsi Gani?

“Je, hatupaswi kujitiisha hata zaidi kwa Baba?”​—EBR. 12:9.

WIMBO 9 Yehova Ni Mfalme Wetu!

MUHTASARI *

1. Kwa nini tunapaswa kujitiisha kwa Yehova?

TUNAPASWA kujitiisha * kwa Yehova kwa sababu yeye ni Muumba wetu. Akiwa Muumba wetu, ana haki ya kuwawekea viumbe wake viwango wanavyopaswa kufuata. (Ufu. 4:11) Lakini tuna sababu nyingine kubwa ya kumtii yeye—njia yake ya kutawala ndiyo bora kabisa. Katika kipindi chote cha historia, watawala wengi wa kibinadamu wamekuwa wakiwatawala wanadamu wenzao. Lakini tofauti nao, Yehova ndiye Mtawala mwenye hekima nyingi zaidi, upendo, rehema, na huruma nyingi zaidi kupita watawala wote.—Kut. 34:6; Rom. 16:27; 1 Yoh. 4:8.

2. Andiko la Waebrania 12:9-11 linatupatia sababu gani za kujitiisha kwa Yehova?

2 Yehova anataka tumtii yeye, si kwa sababu tu tunamwogopa, bali kwa sababu tunampenda na tunamwona kuwa Baba yetu anayetupenda. Katika barua yake kwa Waebrania, Paulo anaeleza kwamba tunapaswa “kujitiisha [kwa hiari] hata zaidi kwa Baba” kwa sababu anatuzoeza “kwa faida yetu.”—Soma Waebrania 12:9-11.

3. (a) Tunaonyeshaje kwamba tunajitiisha kwa Yehova? (b) Tutajibu maswali gani?

3 Tunajitiisha kwa Yehova kwa kufanya yote tunayoweza ili kumtii katika mambo yote na kupinga mwelekeo wowote wa kutegemea uelewaji wetu wenyewe. (Met. 3:5) Kadiri tunavyojifunza na kuzijua sifa maridadi za Yehova ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwetu kujitiisha kwake. Kwa nini? Kwa sababu sifa hizo zinaonekana wazi katika mambo yote anayofanya. (Zab. 145:9) Kadiri tunavyojifunza mengi zaidi kumhusu Yehova, ndivyo tutakavyompenda zaidi. Na tunapompenda Yehova, hatutahitaji orodha ndefu ya sheria kuhusu mambo tunayopaswa kufanya na tusiyopaswa kufanya. Tutajitahidi kufanya hisia zetu na njia yetu ya kufikiri ipatane na mambo ambayo Yehova angependa tufanye au kuepuka. (Zab. 97:10) Hata hivyo, huenda nyakati nyingine ikawa vigumu kwetu kumtii Yehova. Kwa nini? Na ni mambo gani ambayo wazee wa kutaniko, akina baba, na akina mama wanaweza kujifunza kutokana na mfano wa Gavana Nehemia, Mfalme Daudi, na Maria, mama ya Yesu? Makala hii itajibu maswali hayo.

KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU KUJITIISHA KWA YEHOVA?

4-5. Kulingana na Waroma 7:21-23, kwa nini inaweza kuwa vigumu kwetu kujitiisha kwa Yehova?

4 Sababu moja inayoweza kufanya iwe vigumu kwetu kujitiisha kwa Yehova ni kwamba sisi sote tumerithi dhambi na hatujakamilika. Hivyo, tuna mwelekeo wa uasi ndani yetu. Adamu na Hawa walipomwasi Mungu na kula tunda walilokatazwa, walijiwekea viwango vyao wenyewe. (Mwa. 3:22) Leo pia, wanadamu wengi huchagua kumpuuza Yehova na hujiamulia wenyewe mambo yanayofaa na yasiyofaa.

5 Huenda ikawa vigumu hata kwa watu wanaomjua na kumpenda Yehova kujitiisha kikamili kwake. Mtume Paulo alipambana na hali hiyo. (Soma Waroma 7:21-23.) Kama Paulo, tunatamani kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova. Lakini ni lazima sikuzote tupambane na tamaa yoyote ya kufanya mambo yasiyofaa.

6-7. Taja sababu ya pili inayoweza kufanya iwe vigumu kwetu kujitiisha kwa Yehova. Toa mfano.

6 Sababu nyingine inayoweza kufanya iwe vigumu kwetu kujitiisha kwa Yehova ni kwamba tumeathiriwa na utamaduni wa mahali tulipolelewa. Njia ya kufikiri ya watu wengi hupingana na mapenzi ya Yehova, na huenda tukalazimika kupambana kufa na kupona ili kujiweka huru kutokana na njia yao ya kufikiri. Fikiria mfano mmoja.

7 Ni jambo la kawaida katika maeneo fulani kuwashinikiza vijana watumie maisha yao kujitafutia pesa nyingi. Dada anayeitwa Mary * alikabili changamoto hiyo. Kabla ya kujifunza kumhusu Yehova, alisoma katika mojawapo ya shule maarufu zaidi katika nchi yake. Mary alishinikizwa na watu wa familia yake atafute kazi yenye kuheshimika na yenye mshahara mnono. Yeye pia alitamani hivyo. Hata hivyo, baada ya kujifunza kumhusu Yehova na kuanza kumpenda, alibadili malengo yake. Lakini anasema hivi: “Nyakati nyingine mimi hupata fursa nzuri ya kufanya kazi itakayoniwezesha kupata pesa nyingi, lakini ambayo itanizuia kushikamana na ratiba yangu ya mambo ya kiroho. Kwa sababu ya malezi yangu, si rahisi kuikataa. Mimi humsihi Yehova anisaidie nipinge kishawishi cha kuikubali kazi hiyo ambayo inaweza kunizuia kumtumikia.”—Mt. 6:24.

8. Tutachunguza nini?

8 Tunajinufaisha sisi wenyewe tunapojitiisha kwa Yehova. Hata hivyo, wale ambao wamepewa mamlaka fulani na Yehova kama vile wazee wa kutaniko, akina baba, na akina mama wana sababu nyingine zaidi ya kufuata mwongozo wa Mungu; wana fursa ya kuwanufaisha wengine. Acheni tuchunguze mifano fulani ya Biblia itakayotufundisha jinsi tunavyoweza kutumia mamlaka tuliyo nayo kwa njia itakayomfurahisha Yehova.

WAZEE WANAJIFUNZA NINI KUTOKA KWA NEHEMIA?

Wazee hushiriki kufanya kazi kwenye Jumba la Ufalme, kama vile tu Nehemia alivyoshiriki moja kwa moja kazi ya kujenga upya Yerusalemu (Tazama fungu la 9 hadi 11) *

9. Nehemia alikabili changamoto gani?

9 Yehova amewapa wazee wa kutaniko jukumu zito la kuwachunga watu wake. (1 Pet. 5:2) Wazee wanaweza kujifunza mengi kwa kuchunguza jinsi Nehemia alivyoshughulika na watu wa Yehova. Akiwa gavana wa Yuda, Nehemia alikuwa na mamlaka kubwa. (Neh. 1:11; 2:7, 8; 5:14) Wazia baadhi ya changamoto ambazo Nehemia alikabili. Alipata habari kwamba watu walikuwa wamelitia unajisi hekalu na hawakuwategemeza kifedha Walawi kama Sheria ilivyoamuru. Wayahudi walikuwa wakivunja sheria ya Sabato, na baadhi ya wanaume walikuwa wameoa wanawake wa mataifa mengine. Ilibidi Gavana Nehemia ashughulikie hali hiyo ngumu.—Neh. 13:4-30.

10. Nehemia alishughulikiaje changamoto alizokabili?

10 Nehemia hakutumia vibaya mamlaka yake kwa kuwalazimisha watu wa Mungu wafuate mawazo yake. Badala yake, alitafuta mwongozo wa Yehova kwa kusali kwa bidii, na aliwafundisha watu Sheria za Yehova. (Neh. 1:4-10; 13:1-3) Pia kwa unyenyekevu, Nehemia alishirikiana bega kwa bega na ndugu zake, hata aliwasaidia kujenga upya kuta za Yerusalemu.—Neh. 4:15.

11. Kulingana na 1 Wathesalonike 2:7, 8, wazee wanapaswa kuwatendeaje wengine kutanikoni?

11 Huenda wazee wa kutaniko wasikabili changamoto ambazo Nehemia alikabili, lakini wanaweza kumwiga kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, wao hufanya kazi kwa bidii ili kuwanufaisha ndugu na dada zao. Na mamlaka waliyo nayo haiwafanyi wajione kuwa bora kuliko wengine. Badala yake, wanalitendea kutaniko kwa wororo. (Soma 1 Wathesalonike 2:7, 8.) Upendo wao wenye kina na unyenyekevu wao huwachochea wazungumze na wengine kwa fadhili. Andrew, ambaye ametumikia akiwa mzee wa kutaniko kwa miaka mingi anasema hivi: “Nimejionea kwamba kwa ujumla ndugu na dada huguswa moyo sana mzee anapowatendea kwa fadhili na wororo. Sifa hizo hulichochea kutaniko lishirikiane vizuri na wazee.” Tony, ambaye pia ametumikia kwa miaka mingi akiwa mzee wa kutaniko anaeleza hivi: “Mimi hujitahidi kutumia ushauri unaopatikana kwenye Wafilipi 2:3 na sikuzote ninajitahidi kuwaona wengine kuwa bora kuliko mimi. Jambo hilo hunisaidia nisitende kama dikteta.”

12. Kwa nini ni muhimu kwa wazee kuwa wanyenyekevu?

12 Wazee wanapaswa kuwa wanyenyekevu, kama Yehova alivyo mnyenyekevu. Ingawa Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote mzima, yeye “huinama chini” ili amwinue “mtu wa hali ya chini kutoka mavumbini.” (Zab. 18:35; 113:6, 7) Isitoshe, Yehova huchukizwa na watu wenye majivuno na wenye kiburi.—Met. 16:5.

13. Kwa nini mzee anapaswa ‘kuudhibiti kabisa ulimi wake’?

13 Mzee anayejitiisha kwa Yehova anapaswa ‘kuudhibiti kabisa ulimi wake.’ Asipofanya hivyo, anaweza kuzungumza kwa njia isiyo ya fadhili ndugu au dada anapokosa kumheshimu. (Yak. 1:26; Gal. 5:14, 15) Andrew, mzee aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Nyakati nyingine nilitamani kumjibu vibaya ndugu au dada aliyenikosea heshima. Hata hivyo, nimetafakari mifano ya wanaume waaminifu wanaotajwa katika Biblia, na jambo hilo limenisaidia kujifunza umuhimu wa kuwa mnyenyekevu na mpole.” Wazee huonyesha kwamba wanajitiisha kwa Yehova wanapozungumza na wengine kutanikoni na pia wazee wenzao kwa njia ya upendo na neema.—Kol. 4:6.

AKINA BABA WANAJIFUNZA NINI KUTOKA KWA DAUDI?

14. Yehova amewapa akina baba jukumu gani, naye anatarajia wafanye nini?

14 Yehova amewapa akina baba jukumu la kuwa vichwa vya familia, naye anatarajia wawazoeze na kuwatia nidhamu watoto wao. (1 Kor. 11:3; Efe. 6:4) Lakini mamlaka ya baba ina mipaka—anawajibika kwa Yehova, ambaye kila familia hupata jina kutoka kwake. (Efe. 3:14, 15) Akina baba huonyesha kwamba wanajitiisha kwa Yehova wanapotumia mamlaka yao kwa njia inayomfurahisha Mungu. Wanaweza kujifunza mengi kwa kuchunguza maisha ya Mfalme Daudi.

Sala ya baba Mkristo inapaswa kuonyesha unyenyekevu wake (Tazama fungu la 15 na 16) *

15. Kwa nini Mfalme Daudi ni mfano mzuri kwa akina baba?

15 Yehova hakumchagua Daudi kuwa kichwa cha familia yake tu bali pia kuwa kiongozi wa taifa lote la Israeli. Akiwa mfalme, Daudi alikuwa na mamlaka kubwa. Nyakati nyingine, alitumia mamlaka yake vibaya na kufanya makosa mazito. (2 Sam. 11:14, 15) Lakini alionyesha kwamba anajitiisha kwa Yehova kwa kukubali nidhamu. Aliumimina moyo wake kwa Yehova katika sala. Naye alijitahidi kadiri alivyoweza kutii shauri la Yehova. (Zab. 51:1-4) Zaidi ya hayo, alikuwa mnyenyekevu sana hivi kwamba hakupokea tu ushauri mzuri kutoka kwa wanaume, bali pia kutoka kwa wanawake. (1 Sam. 19:11, 12; 25:32, 33) Daudi alijifunza kutokana na makosa yake na jambo kuu maishani mwake lilikuwa kumtumikia Yehova.

16. Akina baba wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Daudi?

16 Fikiria baadhi ya mambo ambayo akina baba wanaweza kujifunza kutoka kwa Mfalme Daudi: Usitumie vibaya mamlaka uliyopewa na Yehova. Kubali makosa yako, na upokee mashauri yanayotegemea Biblia unayopewa na wengine. Ukifanya hivyo, familia yako itakuheshimu kwa sababu ya unyenyekevu wako. Unaposali pamoja na familia yako, mmiminie Yehova moyo wako—acha watu wa familia yako wasikie jinsi unavyomtegemea Yehova kabisa. Na zaidi ya yote, ufanye utumishi wako kwa Yehova kuwa jambo kuu maishani mwako. (Kum. 6:6-9) Mfano wako mzuri ni mojawapo ya zawadi zenye thamani sana unazoweza kuwapa watu wa familia yako.

AKINA MAMA WANAJIFUNZA NINI KUTOKA KWA MARIA?

17. Yehova amewapa akina mama jukumu gani?

17 Yehova amewapa akina mama jukumu lenye kuheshimika katika familia, na pia amewapa mamlaka ya kadiri fulani kuelekea watoto wao. (Met. 6:20) Isitoshe, mfano mzuri wa mama kwa watoto wake unaweza kuwachochea kwa njia kubwa kwa maisha yao yote. (Met. 22:6) Fikiria mambo ambayo akina mama wanaweza kujifunza kutoka kwa Maria, mama ya Yesu.

18-19. Akina mama wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Maria?

18 Maria aliyajua Maandiko vizuri sana. Alimheshimu sana Yehova na alikuwa amesitawisha urafiki wa karibu sana pamoja na Yehova. Alikuwa tayari kujitiisha kwa hiari chini ya mwongozo wa Yehova, ingawa kufanya hivyo kungefanya maisha yake yabadilike kabisa.—Luka 1:35-38, 46-55.

Ikiwa mama amechoka au amekasirika, huenda akahitaji kutia jitihada nyingi zaidi ili kuwaonyesha upendo watu wa familia yake (Tazama fungu la 19) *

19 Ukiwa mama, unaweza kumwiga Maria katika njia mbalimbali. Jinsi gani? Kwanza, kwa kudumisha urafiki wako pamoja na Yehova kupitia funzo la Biblia la kibinafsi na sala za kibinafsi. Pili, kwa kuwa tayari kufanya mabadiliko maishani ili kumpendeza Yehova. Kwa mfano, huenda ulilelewa na wazazi ambao walikuwa wepesi wa hasira na walizungumza kwa ukali na watoto wao. Hivyo, huenda unaamini kwamba hiyo ndiyo njia inayofaa ya kuwalea watoto. Hata baada ya kujifunza viwango vya Yehova, huenda ikawa vigumu kwako kuwa mtulivu na mwenye subira unaposhughulika na watoto wako, hasa wakati ambapo umechoka nao wanakosa kukutii. (Efe. 4:31) Wakati kama huo, unahitaji kumtegemea Yehova hata zaidi katika sala. Mama anayeitwa Lydia anasema hivi: “Nyakati nyingine, nilihitaji kusali sana ili nisizungumze kwa hasira mwanangu alipokosa kunitii. Hata ilibidi nikatishe maneno yangu kabla ya kumaliza nilichotaka kusema na kuanza kusali kimyakimya kwa Yehova ili anisaidie. Sala hunifanya niwe mtulivu.”—Zab. 37:5.

20. Akina mama wengine wanakabili changamoto gani, nao wanaweza kuishindaje?

20 Akina mama wengine wanakabili changamoto nyingine inayofanana na tuliyotoka kuzungumzia—ni vigumu kwao kuwaonyesha watoto wao kwamba wanawapenda. (Tito 2:3, 4) Wanawake fulani wamelelewa katika familia ambazo wazazi hawakuwa na uhusiano wa karibu pamoja na watoto wao. Ikiwa ulilelewa katika mazingira kama hayo, si lazima urudie makosa ya wazazi wako. Mama anayejitiisha kwa mapenzi ya Yehova atahitaji kujifunza jinsi ya kuwaonyesha upendo watoto wake. Huenda ikawa vigumu kwake kubadili njia yake ya kufikiri, kuhisi, na kutenda. Lakini inawezekana kufanya mabadiliko hayo, nayo yatamnufaisha yeye pamoja na familia yake.

ENDELEA KUJITIISHA KWA YEHOVA

21-22. Kulingana na Isaya 65:13, 14, tunanufaikaje tunapojitiisha kwa Yehova?

21 Mfalme Daudi alijua manufaa ya kujitiisha kwa Yehova. Aliandika hivi: “Maagizo kutoka kwa Yehova ni ya uadilifu, huufanya moyo ushangilie; amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae. Mtumishi wako ameonywa kupitia hizo; anapozishika anapata thawabu kubwa.” (Zab. 19:8, 11) Leo, tunajionea tofauti iliyopo kati ya watu wanaojitiisha kwa Yehova na wale wanaokataa kutii mashauri yake ya upendo. Wale wanaojitiisha kwa Yehova “[wanapiga] vigelegele kwa shangwe kwa sababu ya hali nzuri ya moyo.”—Soma Isaya 65:13, 14.

22 Wazee wa kutaniko, akina baba, na akina mama wanapojitiisha kwa hiari kwa Yehova, maisha yao huwa mazuri zaidi, familia zao huwa na furaha zaidi, na kutaniko lote linakuwa na umoja zaidi. Jambo muhimu zaidi ya yote, wanafanya moyo wa Yehova ushangilie. (Met. 27:11) Je, kuna thawabu kubwa zaidi ya hiyo?

WIMBO 123 Kutii Utaratibu wa Kitheokrasi kwa Ushikamanifu

^ fu. 5 Makala hii itazungumzia kwa nini tunapaswa kujitiisha kwa Yehova. Pia, itazungumzia jinsi wazee wa kutaniko, akina baba, na akina mama wanavyoweza kujifunza mengi kutoka kwa mfano wa Gavana Nehemia, Mfalme Daudi, na Maria, mama ya Yesu, kuhusu jinsi ya kutumia mamlaka ambayo wamepewa na Yehova.

^ fu. 1 UFAFANUZI WA MANENO: Maneno kujitiisha na ujitiisho huleta maana mbaya kwa watu ambao wamelazimishwa kumtii mtu fulani. Hata hivyo, watu wa Mungu wamechagua wenyewe kumtii yeye, hivyo hawalioni wazo la kujitiisha kuwa jambo baya.

^ fu. 7 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Mzee wa kutaniko akidumisha Jumba la Ufalme akiwa pamoja na mwanaye, kama vile tu Nehemia alivyoshiriki moja kwa moja kazi ya kujenga upya kuta za Yerusalemu.

^ fu. 64 MAELEZO YA PICHA: Baba akiiwakilisha familia yake katika sala inayotoka moyoni.

^ fu. 66 MAELEZO YA PICHA: Mvulana alitumia saa nyingi kucheza michezo ya kompyuta na hakumaliza kazi za nyumbani au za shule. Mama yake ametoka kazini na amechoka lakini anamtia nidhamu bila kukasirika au kuzungumza kwa ukali.