Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 38

“Njooni Kwangu, . . . Nami Nitawaburudisha”

“Njooni Kwangu, . . . Nami Nitawaburudisha”

Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha.”​—MT. 11:28.

WIMBO 17 “Nataka”

MUHTASARI *

1. Kama inavyoonyeshwa kwenye Mathayo 11:28-30, Yesu alitoa ahadi gani?

YESU alitoa ahadi hii nzuri sana kwa umati wa watu uliokuwa ukimsikiliza: “Njooni kwangu . . . nami nitawaburudisha.” (Soma Mathayo 11:28-30.) Hayo hayakuwa maneno matupu. Kwa mfano, fikiria mambo aliyomfanyia mwanamke aliyekuwa na ugonjwa mbaya sana.

2. Yesu alimtendeaje mwanamke fulani mgonjwa?

2 Mwanamke huyo alihitaji sana msaada. Alikuwa amewaona madaktari wengi akiwa na matumaini ya kupata tiba. Licha ya kuteseka kwa miaka 12, bado hakuwa amepona. Na kulingana na Sheria, hakuwa safi. (Law. 15:25) Kisha akapata habari kwamba Yesu alikuwa na uwezo wa kuwaponya watu wanaoteseka, basi akaenda kumtafuta. Alipompata, aligusa upindo wa vazi lake la nje, na mara moja akapona! Lakini Yesu alifanya mengi zaidi ya kumponya tu—alimrudishia heshima yake. Kwa mfano, alipozungumza naye, Yesu alimwita “binti” kuonyesha kwamba alimpenda na kumheshimu. Hapana shaka kwamba mwanamke huyo aliburudika sana na kutiwa nguvu!—Luka 8:43-48.

3. Tutajibu maswali gani?

3 Je, umetambua kwamba mwanamke huyo ‘alienda’ kwa Yesu? Alichukua hatua ya kwanza. Ndivyo ilivyo leo pia—ni lazima tufanye jitihada ya ‘kwenda’ kwa Yesu. Kwa sasa, Yesu hawaponyi kimuujiza wagonjwa ‘wanaoenda’ kwake. Lakini bado anatoa mwaliko huu: “Njooni kwangu, . . . nami nitawaburudisha.” Katika makala hii, tutajibu maswali matano: Tunaweza ‘kwenda’ kwa Yesu jinsi gani? Yesu alimaanisha nini aliposema: “Chukueni nira yangu”? Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Yesu? Kwa nini kazi ambayo ametupatia tufanye inaburudisha? Na tunaweza kuendelea kuburudika chini ya nira ya Yesu jinsi gani?

“NJOONI KWANGU”

4-5. Tunaweza ‘kwenda’ kwa Yesu jinsi gani?

4 Njia mojawapo ya ‘kwenda’ kwa Yesu ni kujifunza kadiri tuwezavyo kuhusu mambo aliyosema na kutenda. (Luka 1:1-4) Hakuna mtu mwingine yeyote anayeweza kufanya hivyo kwa niaba yetu—ni lazima tujifunze masimulizi hayo sisi wenyewe. Pia, ‘tunaenda’ kwa Yesu kwa kufanya uamuzi wa kubatizwa na kuwa wanafunzi wa Kristo.

5 Njia nyingine ya ‘kwenda’ kwa Yesu ni kuwaona wazee wa kutaniko tunapohitaji msaada. Yesu anawatumia ‘wanaume hao wakiwa zawadi’ kuwatunza kondoo wake. (Efe. 4:7, 8, 11; Yoh. 21:16; 1 Pet. 5:1-3) Ni lazima tuchukue hatua ya kwanza kutafuta msaada wao. Hatupaswi kutarajia kwamba wazee wanaweza kusoma akili zetu na kujua mambo tunayohitaji. Ndugu anayeitwa Julian anaeleza hivi: “Nililazimika kuacha mgawo wangu wa Betheli kwa sababu ya matatizo ya afya, na rafiki yangu mmoja akapendekeza niwaombe wazee wanifanyie ziara ya uchungaji. Mwanzoni, nilihisi kwamba sikuhitaji ziara hiyo. Lakini baadaye niliomba msaada, na ziara hiyo ya uchungaji ikawa mojawapo ya zawadi bora zaidi ambazo nimewahi kupata.” Wazee washikamanifu, kama hao waliomtembelea Julian, wanaweza kutusaidia kuijua “akili ya Kristo,” yaani, kuelewa na kuiga njia yake ya kufikiri na mtazamo wake. (1 Kor. 2:16; 1 Pet. 2:21) Kwa kweli, hiyo ni mojawapo ya zawadi bora zaidi wanazoweza kutupatia.

“CHUKUENI NIRA YANGU”

6. Yesu alimaanisha nini aliposema: “Chukueni nira yangu”?

6 Yesu aliposema: “Chukueni nira yangu,” huenda alimaanisha “Kubalini mamlaka yangu.” Huenda pia alimaanisha, “Njooni tuibebe nira pamoja, na kwa pamoja tufanye kazi ya Yehova.” Vyovyote vile, nira inamaanisha kwamba tunapaswa kufanya kazi.

7. Kulingana na Mathayo 28:18-20, tumepewa kazi gani, na tunaweza kuwa na uhakika gani?

7 Tunakubali mwaliko wa Yesu tunapoyaweka wakfu maisha yetu kwa Yehova na kubatizwa. Yesu anawaalika watu wote—naye hatamkataa kamwe mtu yeyote anayetamani kutoka moyoni kumtumikia Mungu. (Yoh. 6:37, 38) Wafuasi wote wa Kristo wamepewa pendeleo la kushiriki katika kazi ambayo Yehova amempa Yesu afanye. Tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yesu atatusaidia kufanya kazi hiyo.—Soma Mathayo 28:18-20.

“MJIFUNZE KUTOKA KWANGU”

Waburudishe wengine kama Yesu alivyofanya (Tazama fungu la 8 hadi 11) *

8-9. Kwa nini watu wanyenyekevu walijihisi huru kumkaribia Yesu, na tunapaswa kujiuliza maswali gani?

8 Watu wanyenyekevu walijihisi huru kumkaribia Yesu. (Mt. 19:13, 14; Luka 7:37, 38) Kwa nini? Fikiria tofauti kati ya Yesu na Mafarisayo. Viongozi hao wa kidini walikosa upendo na walikuwa na kiburi. (Mt. 12:9-14) Yesu alikuwa mwenye upendo na mnyenyekevu. Mafarisayo walipenda makuu na walijivunia cheo chao katika jamii. Yesu alishutumu mtazamo huo wa kujitafutia makuu, na aliwafundisha wanafunzi wake wajione kuwa watumishi wa hali ya chini. (Mt. 23:2, 6-11) Mafarisayo walitumia vitisho na woga kuwatawala wengine. (Yoh. 9:13, 22) Yesu aliwaburudisha watu kwa matendo yake ya upendo na maneno yake ya fadhili.

9 Je, umemwiga Yesu katika mambo hayo? Jiulize: ‘Je, ninajulikana kuwa mtu mpole na mnyenyekevu? Je, mimi hujitolea kwa hiari kufanya kazi za hali ya chini ili kuwatumikia wengine? Je, mimi huwatendea wengine kwa fadhili?’

10. Yesu aliwatengenezea wanafunzi wake mazingira gani ya kufanya kazi?

10 Yesu aliwatengenezea wafanyakazi wenzake mazingira mazuri yenye amani, na alifurahia kuwazoeza. (Luka 10:1, 19-21) Aliwatia moyo wanafunzi wake waulize maswali, na alitaka kujua maoni yao. (Mt. 16:13-16) Kama mimea katika bustani iliyonyweshwa maji vizuri, wanafunzi wa Yesu walisitawi. Walifyonza mambo ambayo Yesu aliwafundisha na kuzaa matunda kwa kufanya kazi njema.

Uwe mwenye kufikika na mwenye urafiki

Uwe mwenye bidii

Uwe mnyenyekevu na mchapakazi *

11. Tunapaswa kujiuliza maswali gani?

11 Je, umepewa mamlaka fulani juu ya wengine? Ikiwa ndivyo, jiulize hivi: ‘Ni mazingira ya aina gani ninayowatengenezea wengine kazini au nyumbani? Je, ninaendeleza amani? Je, ninawatia moyo wengine wajihisi huru kuuliza maswali? Na je, niko tayari kusikiliza maoni yao?’ Hatungependa kamwe kuwa kama Mafarisayo, ambao walichukizwa na watu ambao waliwauliza maswali na waliwatesa wale waliokuwa na maoni tofauti na yao.—Marko 3:1-6; Yoh. 9:29-34.

“NANYI MTAPATA BURUDISHO”

12-14. Kwa nini kazi ambayo Yesu ametupatia tufanye inaburudisha?

12 Kwa nini inaburudisha kufanya kazi ambayo Yesu ametupatia? Kuna sababu nyingi, lakini fikiria sababu hizi chache.

13 Tuna waangalizi bora kabisa. Yehova, Mwangalizi wetu Mkuu, si mwangalizi mkali au asiye na shukrani. Yeye huthamini kazi tunayofanya. (Ebr. 6:10) Naye hutupatia nguvu tunazohitaji ili tuweze kubeba mzigo wetu wa wajibu. (2 Kor. 4:7; Gal. 6:5, maelezo ya chini) Yesu, Mfalme wetu, ni kiongozi anayetuwekea mfano wa kuiga. (Yoh. 13:15) Na wazee wa kutaniko wanaotuchunga wanajitahidi kumwiga Yesu, “mchungaji mkuu.” (Ebr. 13:20; 1 Pet. 5:2) Wanafanya yote wawezayo kuwa wenye fadhili, wenye kutia moyo, na jasiri wanapotufundisha na kutulinda.

14 Tuna marafiki bora kabisa. Hakuna kikundi chochote kingine cha watu kilicho na marafiki wenye upendo au kilicho na kusudi maishani kama sisi. Hebu wazia: Tuna pendeleo la kufanya kazi pamoja na watu wenye viwango vya juu zaidi vya maadili lakini wasiojiona kuwa waadilifu kupita kiasi. Wana vipawa vingi lakini ni wenye kiasi, na hawajioni kuwa bora kuliko wengine. Hawatuoni tu kuwa wafanyakazi wenzi bali pia rafiki zao. Na kifungo hicho cha urafiki ni chenye nguvu sana hivi kwamba wako tayari kufa kwa ajili yetu!

15. Tunapaswa kuhisije kuhusu kazi tunayofanya?

15 Tunafanya kazi bora kabisa. Tunawafundisha watu kweli kumhusu Yehova na kufunua uwongo unaoenezwa na Ibilisi. (Yoh. 8:44) Shetani huwatwika watu mizigo inayowalemea. Kwa mfano, anataka tuamini kwamba Yehova hawezi kutusamehe dhambi zetu na kwamba hatupendeki. Huo ni mzigo mzito sana wenye kulemea na uwongo mbaya sana! ‘Tunapoenda’ kwa Kristo tunasamehewa dhambi zetu. Na ukweli wa mambo ni kwamba Yehova anatupenda sana sisi sote. (Rom. 8:32, 38, 39) Ni jambo lenye kuthawabisha sana kuwasaidia watu wajifunze kumhusu Yehova na kuwaona wakiboresha maisha yao!

ENDELEA KUPATA BURUDISHO CHINI YA NIRA YA YESU

16. Mzigo ambao Yesu anatuomba tubebe unatofautianaje na mizigo mingine ambayo lazima tubebe?

16 Mzigo ambao Yesu anatuomba tubebe ni tofauti na mizigo mingine ambayo ni lazima tubebe. Kwa mfano, baada ya kufanya kazi kwa siku nzima, watu wengi hawahisi tu wamechoka, bali pia wanahisi kwamba hawakutimiza chochote. Tofauti na hilo, baada ya kutumia wakati wetu kumtumikia Yehova na Kristo, sisi hujihisi tukiwa wenye furaha na tukiwa tumeridhika kabisa. Huenda tumechoka sana baada ya kufanya kazi kwa siku nzima, na lazima tujilazimishe ili tuhudhurie mikutano ya kutaniko jioni hiyo. Lakini mara nyingi tunarudi nyumbani baada ya mikutano tukiwa tumeburudika na tukiwa na nguvu mpya. Na ndivyo ilivyo pia tunapojitahidi kuhubiri na kufanya funzo letu la kibinafsi. Thawabu tunayopata ni kubwa zaidi kuliko nguvu tulizotumia!

17. Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu na kuona mambo kihalisi?

17 Ni lazima tuone mambo kihalisi. Kila mmoja wetu ana kiwango fulani cha nishati. Hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mambo tunayochagua kufanya. Kwa mfano, huenda tukapoteza nguvu zetu tukijaribu kujikusanyia vitu vya kimwili. Ona kile ambacho Yesu alimwambia mwanamume fulani kijana aliyekuwa tajiri ambaye alimuuliza hivi: “Ninapaswa kufanya nini ili niurithi uzima wa milele?” Tayari mwanamume huyo alikuwa akitii Sheria. Ni lazima awe alikuwa mtu mzuri kwa sababu simulizi la Injili ya Marko linataja kihususa kwamba Yesu ‘alimpenda.’ Yesu alimpa mtawala huyo kijana mwaliko. Alimwambia hivi: “Nenda ukauze vitu ulivyo navyo . . . kisha uje uwe mfuasi wangu.” Mwanamume huyo alitamani kumfuata Yesu, lakini inaonekana kwamba hakuwa tayari kuacha ‘mali zake nyingi.’ (Marko 10:17-22) Hivyo, alikataa mwaliko wa Yesu wa kuchukua nira yake, na badala yake akaendelea kuwa mtumwa wa “Utajiri.” (Mt. 6:24) Wewe ungechagua nini?

18. Tunapaswa kufanya nini mara kwa mara, na kwa nini?

18 Ni jambo linalofaa kutafakari mara kwa mara kuhusu mambo tunayotanguliza maishani mwetu. Kwa nini? Ili kuhakikisha kwamba tunatumia nguvu zetu kwa hekima. Mfikirie kijana anayeitwa Mark ambaye alisema hivi: “Kwa miaka mingi, nilifikiri kwamba nilikuwa nikiishi maisha rahisi. Nilikuwa painia, lakini sikuzote nilikuwa nikifikiria kuhusu pesa na jinsi ya kufanya maisha yangu yawe yenye kustarehesha zaidi. Sikuelewa kwa nini maisha yangu yalianza kuwa magumu. Kisha, nilitambua kwamba nilikuwa nikitanguliza masilahi yangu mwenyewe na kumpa Yehova masalio ya wakati na nguvu zangu.” Mark alibadili njia yake ya kufikiri na mtindo wake wa maisha na akajitoa hata zaidi katika utumishi wa Yehova. Anaeleza hivi: “Nyakati nyingine nina mahangaiko kuhusu pesa, lakini kwa msaada wa Yehova na utegemezo wa Yesu, nimeshinda matatizo yangu.”

19. Kwa nini ni muhimu kuwa na mtazamo unaofaa?

19 Tutaendelea kupata burudisho chini ya nira ya Yesu ikiwa tutafanya mambo matatu. Jambo la kwanza ni kudumisha mtazamo unaofaa. Tunafanya kazi ya Yehova, hivyo ni lazima ifanywe kwa njia ya Yehova. Sisi ni wafanyakazi, na Yehova ndiye Bwana wetu. (Luka 17:10) Ikiwa tutajaribu kufanya kazi yake kwa njia yetu, tutakuwa tukipingana na nira yake na tutafanya mambo yawe magumu kwetu. Hata ng’ombe dume mwenye nguvu anaweza kujiumiza na kujichosha ikiwa atang’ang’ania kwenda upande tofauti na kupingana na nira inayoongozwa na bwana wake. Kwa upande mwingine, tunaweza kufanya mambo makubwa sana na kushinda vizuizi vyovyote ikiwa tutafuata mwongozo wa Yehova. Kumbuka kwamba hakuna yeyote anayeweza kuzuia mapenzi ya Yehova kutimia!—Rom. 8:31; 1 Yoh. 4:4.

20. Nia yetu ya kubeba nira ya Yesu inapaswa kuchochewa na nini?

20 Jambo la pili ni kufanya kazi ukiwa na nia nzuri. Lengo letu ni kumletea utukufu Yehova, Baba yetu anayetupenda. Muda si muda, watu fulani katika karne ya kwanza waliochochewa na pupa au ubinafsi walipoteza shangwe yao na kuiacha nira ya Yesu. (Yoh. 6:25-27, 51, 60, 66; Flp. 3:18, 19) Tofauti na wao, watu ambao walichochewa na upendo wao kwa Mungu usio na ubinafsi, na upendo kwa jirani waliendelea kwa furaha kubeba nira hiyo katika kipindi chote cha maisha yao hapa duniani, wakiwa na tumaini la kutumikia pamoja na Kristo mbinguni. Kama wao, sisi pia tutaendelea kuwa na furaha ikiwa tutabeba nira ya Yesu huku tukichochewa na nia nzuri.

21. Kulingana na Mathayo 6:31-33, tunaweza kutarajia nini kutoka kwa Yehova?

21 Jambo la tatu ni kuwa na matarajio yaliyo sahihi. Tumechagua maisha ya kujidhabihu na yanayohusisha kazi ngumu. Yesu alituonya kwamba tungeteswa. Lakini tunatarajia kwamba Yehova atatupatia nguvu za kuvumilia changamoto zozote tutakazokabili. Kadiri tunavyoendelea kuvumilia, ndivyo tunavyozidi kuwa na nguvu. (Yak. 1:2-4) Pia, tunaweza kutarajia kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu, kwamba Yesu atatuchunga, na kwamba ndugu na dada zetu watatutia moyo. (Soma Mathayo 6:31-33; Yoh. 10:14; 1 The. 5:11) Kwa kweli, tuna kila kitu tunachohitaji ili kuvumilia changamoto yoyote!

22. Tuna sababu gani ya kushukuru?

22 Mwanamke aliyeponywa na Yesu, alipata burudisho siku ileile ambayo aliponywa. Hata hivyo, angepata burudisho la milele ikiwa tu angekuwa mwanafunzi mshikamanifu wa Kristo. Unafikiri alifanya nini? Ikiwa alikubali kubeba nira ya Yesu, wazia thawabu ambayo angepata—kutumikia pamoja na Yesu mbinguni! Mambo yoyote aliyodhabihu ili amfuate Kristo, yasingeweza kulinganishwa na baraka hiyo. Iwe tuna tumaini la kuishi milele mbinguni au duniani—sote tunashukuru sana kwamba tumekubali mwaliko huu wa Yesu: “Njooni kwangu!”

WIMBO 13 Kristo, Kielelezo Chetu

^ fu. 5 Yesu anatualika twende kwake. Kukubali mwaliko wa Yesu kunahusisha nini? Makala hii itajibu swali hilo, na itatukumbusha kuhusu jinsi tunavyoweza kuburudika kwa kufanya kazi pamoja na Kristo.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Yesu aliwaburudisha wengine kwa njia mbalimbali.

^ fu. 66 MAELEZO YA PICHA: Vivyo hivyo, ndugu huyu anawaburudisha wengine kwa njia mbalimbali.