Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 39

“Tazama! Umati Mkubwa”

“Tazama! Umati Mkubwa”

“Tazama! umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, . . . wakiwa wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwanakondoo.”​—UFU. 7:9.

WIMBO 60 Ni Uzima Kwao

MUHTASARI *

1. Mtume Yohana alikuwa akipitia hali gani mwishoni mwa karne ya kwanza W.K.?

MWISHONI mwa karne ya kwanza W.K., mtume Yohana alikuwa akipitia hali ngumu sana. Umri wake ulikuwa umesonga, na alikuwa amefungwa katika kisiwa cha Patmo, na huenda yeye pekee ndiye mtume aliyekuwa hai wakati huo. (Ufu. 1:9) Alijua kwamba wapinzani walikuwa wakiyapotosha makutaniko na kusababisha migawanyiko. Ilionekana kana kwamba kikundi hicho kidogo cha Wakristo kilikuwa karibu kutoweka.—Yuda 4; Ufu. 2:15, 20; 3:1, 17.

Mtume Yohana aliona “umati mkubwa” wa watu wakiwa wamevaa kanzu nyeupe na wakiwa na matawi ya mitende mikononi mwao (Tazama fungu la 2)

2. Kulingana na Ufunuo 7:9-14, Yohana alipokea maono gani ya kinabii yenye kusisimua? (Tazama picha kwenye jalada.)

2 Chini ya hali hizo ngumu, Yohana alipokea maono ya kinabii yenye kusisimua. Katika maono hayo, malaika wanaagizwa wazuie pepo za uharibifu za dhiki kuu mpaka kikundi cha watumwa kitiwe muhuri wa mwisho. (Ufu. 7:1-3) Kikundi hicho ni miongoni mwa wale 144,000 ambao watatawala na Yesu mbinguni. (Luka 12:32; Ufu. 7:4) Kisha, Yohana anataja kikundi kingine ambacho ni kikubwa sana hivi kwamba anasema hivi kwa mshangao: “Tazama!”—neno linaloonyesha kwamba anashangazwa na mambo anayoona. Yohana anaona nini? “Umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na jamii na lugha, wakiwa wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwanakondoo.” (Soma Ufunuo 7:9-14.) Wazia jinsi Yohana alivyofurahi kujua kwamba wakati ujao idadi kubwa ya watu wangejiunga na ibada ya kweli!

3. (a) Kwa nini maono ya Yohana yanapaswa kuimarisha imani yetu? (b) Tutajifunza nini katika makala hii?

3 Bila shaka maono hayo yalimwimarisha imani Yohana. Je, maono hayo hayapaswi kuimarisha imani yetu hata zaidi kwa kuwa tunaishi wakati ambapo yanatimizwa? Tumejionea kukusanywa kwa mamilioni ya watu walio na tumaini la kuokoka dhiki kuu na kuishi milele duniani. Katika makala hii, tutajifunza jinsi Yehova alivyowafunulia watu wake kuhusu umati huo mkubwa, zaidi ya miaka 80 iliyopita. Kisha, tutachunguza mambo mawili kuhusu umati huo: (1) ukubwa wake na (2) watu mbalimbali kutoka duniani kote wanaofanyiza umati huo. Mambo hayo yataimarisha imani ya wale wote walio na tumaini la kuwa sehemu ya kikundi hicho kilichobarikiwa.

UMATI MKUBWA UTAISHI WAPI?

4. Dini nyingi leo hazielewi kweli gani ya Maandiko, na Wanafunzi wa Biblia walitofautianaje na dini hizo kuhusu kweli hiyo?

4 Kwa ujumla, dini zinazodai kuwa za Kikristo hazifundishi kweli ya Maandiko kwamba siku moja wanadamu watiifu wataishi milele duniani. (2 Kor. 4:3, 4) Leo, dini nyingi hufundisha kwamba watu wote wema huenda mbinguni wanapokufa. Hata hivyo, kikundi cha Wanafunzi wa Biblia kilichokuwa kikichapisha Mnara wa Mlinzi mwishoni mwa miaka ya 1800 kilikuwa tofauti. Walielewa kwamba Mungu atairudisha Paradiso duniani na kwamba mamilioni ya wanadamu watiifu wataishi hapa duniani—na si mbinguni. Hata hivyo, iliwachukua muda mrefu kuelewa waziwazi kuhusu wanadamu hao watiifu ambao wangeishi duniani.—Mt. 6:10.

5. Wanafunzi wa Biblia waliamini nini kuhusu wale 144,000?

5 Bila shaka, kupitia Maandiko Wanafunzi wa Biblia walitambua pia kwamba baadhi ya watu ‘wangenunuliwa kutoka duniani’ ili wakatawale na Yesu mbinguni. (Ufu. 14:3) Kikundi hicho kingefanyizwa na Wakristo 144,000 wenye bidii na waliojiweka wakfu ambao walimtumikia Mungu kwa uaminifu walipokuwa duniani. Vipi kuhusu umati mkubwa?

6. Wanafunzi wa Biblia waliamini nini kuhusu umati mkubwa?

6 Katika maono yake, Yohana aliona umati mkubwa ‘ukiwa umesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwanakondoo.’ (Ufu. 7:9) Maneno hayo yaliwafanya Wanafunzi wa Biblia wafikie mkataa kwamba umati mkubwa, kama ilivyo kwa wale 144,000, utaishi mbinguni. Ikiwa wale 144,000 pamoja na umati mkubwa wataishi mbinguni, inawezekanaje kwamba kikundi kimoja kinatofautiana na kingine? Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba umati mkubwa ulifanyizwa na Wakristo ambao hawakumtii Mungu kikamili walipokuwa duniani. Ingawa waliishi maisha safi kiadili, huenda baadhi yao waliendelea kuwa washiriki wa makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Wanafunzi wa Biblia walifikia mkataa kwamba watu hao walikuwa na bidii kwa kiasi fulani lakini hawakutia bidii ya kutosha kiasi cha kuwafanya wastahili kutawala na Yesu. Kwa kuwa upendo wao kwa Mungu haukuwa na nguvu ya kutosha, umati huo mkubwa ungestahili kwenda mbinguni mbele ya kiti cha ufalme lakini haungestahili kuketi kwenye viti vya ufalme.

7. Kulingana na Wanafunzi wa Biblia, ni nani ambao wangeishi duniani wakati wa ile Miaka Elfu Moja, na Wanafunzi wa Biblia waliamini nini kuhusu watu waaminifu walioishi kabla ya Kristo?

7 Basi, ni nani ambao wangeishi duniani? Wanafunzi wa Biblia waliamini kwamba baada ya wale 144,000 na umati mkubwa kukusanywa mbinguni, mamilioni ya watu wengine wangeruhusiwa kuishi duniani ili wafurahie baraka za Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja. Wanafunzi wa Biblia hawakutarajia kwamba mamilioni hayo ya watu wangemtumikia Yehova kabla ya kuanza kwa Utawala wa Kristo. Badala yake, walifikiri kwamba kikundi hicho cha watu kitafundishwa njia za Yehova wakati wa ile Miaka Elfu Moja. Baada ya hapo, watu waliopatanisha maisha yao na viwango vya Yehova wangebarikiwa kwa kupata uzima wa milele duniani, ilhali wale walioasi wangeangamizwa. Pia, Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba huenda baadhi ya wale ambao wangetumikia wakiwa “wakuu” duniani wakati huo—kutia ndani “wakuu wa kale” waliofufuliwa, yaani, watu waaminifu waliokufa kabla ya Kristo—wangepata thawabu ya kwenda mbinguni mwishoni mwa ile Miaka Elfu Moja.—Zab. 45:16.

8. Taja vikundi vitatu ambavyo Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba vilikuwa sehemu ya kusudi la Mungu.

8 Hivyo, Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba kulikuwa na vikundi vitatu: (1) wale 144,000, ambao wangetawala pamoja na Yesu mbinguni; (2) umati mkubwa wa Wakristo ambao hawakuwa na bidii sana, utakaosimama mbele ya kiti cha ufalme cha Yesu mbinguni; na (3) mamilioni ya watu ambao wangefundishwa njia za Yehova duniani wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja. * Hata hivyo, kwa wakati uliowekwa na Yehova, nuru ya kweli ilianza kuangaza zaidi na zaidi kuhusu jambo hilo.—Met. 4:18.

NURU YA KWELI YAZIDI KUNG’AA

Katika kusanyiko la mwaka wa 1935, idadi kubwa ya watu waliokuwa na tumaini la kuishi duniani walibatizwa (Tazama fungu la 9)

9. (a) Umati mkubwa unasimamaje “mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwanakondoo”? (b) Kwa nini uelewaji huo wa Ufunuo 7:9 unapatana na akili?

9 Katika mwaka wa 1935, umati mkubwa ambao Yohana aliona katika maono yake ulieleweka vizuri. Mashahidi wa Yehova walitambua kwamba si lazima umati mkubwa usimame kihalisi mbinguni “mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwanakondoo.” Badala yake, wanafanya hivyo kwa njia ya mfano. Ingawa umati huo ungeishi duniani, ungesimama “mbele ya kiti cha ufalme” kwa kutambua mamlaka ya Yehova na kwa kujitiisha chini ya enzi yake kuu. (Isa. 66:1) Ungesimama “mbele ya Mwanakondoo” kwa kuonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Vilevile, kwenye Mathayo 25:31, 32, “mataifa yote”—kutia ndani watu waovuyanatajwa kwamba “yatakusanyika mbele” ya Yesu katika kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Ni wazi kwamba mataifa hayo yote hayako mbinguni, bali yako duniani. Uelewaji huo unapatana na akili. Unafunua wazi kwa nini Biblia haisemi kwamba umati mkubwa utafufuliwa ili ukaishi mbinguni. Ni kikundi kimoja tu kilichoahidiwa kupata uzima wa milele mbinguni, yaani, wale 144,000 ‘watakaotawala wakiwa wafalme juu ya dunia’ pamoja na Yesu.—Ufu. 5:10.

10. Kwa nini lingekuwa jambo la lazima kwa umati mkubwa kufundishwa njia za Yehova kabla ya ile Miaka Elfu Moja kuanza?

10 Hivyo, tangu mwaka wa 1935, Mashahidi wa Yehova wameelewa kwamba umati mkubwa ambao Yohana aliona katika maono yake unafanyizwa na kikundi cha Wakristo waaminifu walio na tumaini la kuishi milele duniani. Ili umati huo uokoke dhiki kuu, ungepaswa kufundishwa njia za Yehova kabla ya kuanza kwa ile Miaka Elfu Moja. Umati huo ungehitaji kuonyesha imani yenye nguvu ili ‘ufanikiwe kuponyoka mambo yote ambayo lazima yatukie’ kabla ya kuanza kwa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja.—Luka 21:34-36.

11. Kwa nini baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba baadhi ya watu wangeenda mbinguni baada ya ile Miaka Elfu Moja?

11 Vipi kuhusu lile wazo la kwamba watu fulani waaminifu duniani wangeenda mbinguni baada ya ile Miaka Elfu Moja? Wazo hilo ambalo lilitajwa miaka mingi iliyopita katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 1913 lilitegemea hoja ifuatayo, kwamba ‘Itawezekanaje watu waaminifu wa zamani wairithi dunia tu ilhali umati mkubwa wa Wakristo ambao hawakuonyesha uaminifu sana wapewe thawabu ya uzima mbinguni?’ Ni wazi kwamba Wanafunzi wa Biblia walifikiri hivyo kwa sababu ya mambo haya mawili yasiyo sahihi: (1) umati mkubwa ungeishi mbinguni na (2) umati mkubwa ungefanyizwa na Wakristo ambao hawakuwa na bidii sana.

12-13. Watiwa-mafuta pamoja na umati mkubwa wanatambua nini kuhusu thawabu yao?

12 Hata hivyo, kama tulivyoona, tangu mwaka wa 1935, Mashahidi wa Yehova wameelewa waziwazi kwamba waokokaji wa Har–Magedoni ndio umati mkubwa ambao Yohana aliuona kwenye maono. ‘Watatoka kwenye ile dhiki kuu’ hapa hapa duniani, nao ‘wataendelea kusema kwa sauti kubwa: “Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi kwenye kiti cha ufalme, na kwa Mwanakondoo.”’ (Ufu. 7:10, 14) Zaidi ya hayo, Maandiko yanafundisha kwamba wale wanaofufuliwa kwenda kuishi mbinguni wanapokea “kitu bora” kuliko watu waaminifu walioishi zamani. (Ebr. 11:40) Basi wakiwa na shauku, ndugu zetu walianza kuwaalika watu ili waje kumtumikia Yehova wakiwa na tumaini la kuishi duniani milele.

13 Watu walio katika umati huo mkubwa wanafurahia sana tumaini lao. Wanatambua kwamba Yehova ndiye anayeamua mahali ambapo waabudu wake waaminifu watamtumikia, iwe ni mbinguni ama duniani. Watiwa-mafuta pamoja na umati mkubwa wanatambua kwamba wanaweza kupata thawabu yao kwa sababu tu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova zinazoonyeshwa kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo.—Rom. 3:24.

NI UMATI MKUBWA

14. Baada ya mwaka wa 1935, kwa nini watu wengi walijiuliza kuhusu jinsi ambavyo unabii unaohusu umati mkubwa ungetimizwa?

14 Baada ya uelewaji wa watu wa Yehova kuhusu umati mkubwa kurekebishwa mwaka wa 1935, bado wengi walijiuliza, itawezekanaje kwa wale walio na tumaini la kuishi duniani kuongezeka na kuwa umati mkubwa? Kwa mfano, Ronald Parkin alikuwa na umri wa miaka 12, uelewaji kuhusu umati mkubwa ulipowekwa wazi. Anakumbuka hivi: “Wakati huo kulikuwa na wahubiri 56,000 ulimwenguni pote na wengi wao, na huenda karibu wote, walikuwa watiwa-mafuta. Hivyo, umati mkubwa haukuonekana kuwa mkubwa.”

15. Kazi ya kukusanya umati mkubwa imepiga hatua gani?

15 Hata hivyo, katika miaka iliyofuata, wamishonari walitumwa katika nchi nyingi, na idadi ya Mashahidi wa Yehova ikaendelea kuongezeka. Kisha, katika mwaka wa 1968, programu ya kujifunza Biblia ilianzishwa kwa kutumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Ufafanuzi wake rahisi wa kweli za Biblia uliwavuta watu wengi zaidi kuliko wakati mwingine wowote kabla ya hapo. Katika kipindi cha miaka minne tu, zaidi ya watu 500,000 walibatizwa na kuwa wanafunzi wa Kristo. Kadiri Kanisa Katoliki lilivyopoteza mamlaka yake huko Amerika ya Latini na nchi nyinginezo, na kadiri vizuizi vya kazi yetu vilivyozidi kuondolewa huko Ulaya Mashariki na sehemu fulani za Afrika, ndivyo mamilioni ya watu walivyozidi kubatizwa. (Isa. 60:22) Katika miaka ya karibuni, tengenezo la Yehova limeandaa vifaa vingine vingi vyenye matokeo mazuri ili kuwasaidia watu wajifunze mambo ambayo Biblia inafundisha. Hapana shaka lolote kwamba umati mkubwa—wenye zaidi ya watu milioni nane—umekusanywa.

UNAFANYIZWA NA WATU MBALIMBALI

16. Ni nani wanaofanyiza umati mkubwa?

16 Alipokuwa akiandika maono yake, Yohana alitaja kwamba umati mkubwa ungefanyizwa na watu kutoka “mataifa yote na makabila na jamii na lugha.” Miaka mingi mapema, nabii Zekaria alikuwa ametabiri kuhusu jambo linalofanana na hilo. Aliandika hivi: “Siku hizo watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, naam, watashika kwa nguvu joho la Myahudi, wakisema: ‘Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.’”—Zek. 8:23.

17. Ni kazi gani inayofanywa ili kuwasaidia watu wa mataifa yote na lugha mbalimbali?

17 Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba ili watu wa lugha zote wakusanywe, ni lazima habari njema ihubiriwe katika lugha nyingi. Kwa zaidi ya miaka 130, tumekuwa tukitafsiri vifaa vya kujifunzia Biblia, lakini sasa kuliko wakati mwingine wowote, tunatimiza kazi kubwa sana ya kutafsiri machapisho katika mamia ya lugha. Ni wazi kwamba katika siku zetu Yehova anafanya muujiza—muujiza wa kuukusanya umati mkubwa kutoka kwa watu wa mataifa yote. Kikundi hicho cha watu kutoka duniani pote kinamwabudu Yehova kwa umoja kwa sababu chakula cha kiroho kinazidi kupatikana katika lugha nyingi zaidi. Na Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa kazi yao ya kuhubiri kwa bidii na upendo wao wa kindugu. Jambo hilo linaimarisha imani kwelikweli!—Mt. 24:14; Yoh. 13:35.

MAONO YA YOHANA YANATUHUSUJE?

18. (a) Kulingana na Isaya 46:10, 11, kwa nini hatushangai kuona kwamba Yehova ametimiza unabii kuhusu umati mkubwa? (b) Kwa nini wale walio na tumaini la kuishi duniani hawahisi kwamba wamenyimwa jambo lolote?

18 Unabii kuhusu umati mkubwa unatupa kila sababu ya kuwa wenye shangwe na msisimko! Hatushangai kuona kwamba Yehova ametimiza unabii huo kwa njia yenye kustaajabisha sana. (Soma Isaya 46:10, 11.) Wale wa umati mkubwa wanamshukuru sana Yehova kwa tumaini alilowapa. Hawahisi kwamba wamenyimwa jambo fulani eti kwa sababu hawajatiwa mafuta kwa roho ya Mungu ili wakatumikie mbinguni pamoja na Yesu. Katika Maandiko, tunasoma kuhusu wanaume na wanawake wenye imani ambao waliongozwa na roho takatifu kwa njia kubwa; lakini wao si sehemu ya wale 144,000. Mfano mmoja ni Yohana Mbatizaji. (Mt. 11:11) Mfano mwingine ni Daudi. (Mdo. 2:34) Watu hao, pamoja na wengine wengi watafufuliwa ili waishi katika dunia itakayokuwa paradiso. Wote kwa pamoja—kutia ndani umati mkubwa—watapata fursa ya kuonyesha ushikamanifu wao kwa Yehova na enzi yake kuu.

19. Utimizo wa maono ya Yohana kuhusu umati mkubwa unaonyeshaje uharaka wa nyakati tunazoishi?

19 Leo, kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya wanadamu, Mungu amewaunganisha mamilioni ya watu kutoka katika mataifa yote. Iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani, tunahitaji kuwasaidia watu wengi kadiri iwezekanavyo ili wajiunge na umati mkubwa wa “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Hivi karibuni, Yehova ataleta dhiki kuu iliyotabiriwa ambayo itaangamiza serikali na dini ambazo zimewatesa wanadamu. Washiriki wote wa umati mkubwa wana pendeleo kubwa sana lililo mbele yao—pendeleo la kumtumikia Yehova duniani milele!—Ufu. 7:14.

WIMBO 139 Wazia Wakati Vitu Vyote Vitakuwa Vipya

^ fu. 5 Makala hii itazungumzia maono ya kinabii ya Yohana kuhusu kukusanywa kwa “umati mkubwa.” Bila shaka, itawaimarisha imani wale wote ambao ni sehemu ya kikundi hicho kilichobarikiwa.

^ fu. 8 Tazama kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, uku. 159-163.

Namba 1 hadi 8 zinawakilisha idadi ya wahubiri kuanzia milioni moja hadi milioni nane