Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 35

Yehova Anawathamini Watumishi Wake Wanyenyekevu

Yehova Anawathamini Watumishi Wake Wanyenyekevu

“Yehova . . . huwaona wanyenyekevu.”​—ZAB. 138:6.

WIMBO 48 Kutembea na Yehova Kila Siku

MUHTASARI *

1. Yehova anahisije kuhusu watu wanyenyekevu? Eleza.

YEHOVA anawapenda watu wanyenyekevu. Ni wale tu walio na unyenyekevu wa kweli wanaoweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Kwa upande mwingine, “anajitenga mbali na wenye kiburi.” (Zab. 138:6) Sote tungependa kumfurahisha Yehova na kuhisi upendo wake mwororo, hivyo tuna sababu nzuri za kujifunza jinsi ya kusitawisha sifa ya unyenyekevu.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Katika makala hii, tutachunguza maswali matatu: (1) Unyenyekevu ni nini? (2) Kwa nini tunapaswa kusitawisha sifa ya unyenyekevu? (3) Ni hali gani zinazoweza kujaribu unyenyekevu wetu? Kama tutakavyoona, tunapositawisha sifa ya unyenyekevu, tunaufurahisha moyo wa Yehova na tunajinufaisha sisi wenyewe.—Met. 27:11; Isa. 48:17.

UNYENYEKEVU NI NINI?

3. Unyenyekevu ni nini?

3 Unyenyekevu ni kutokuwa na kiburi au majivuno; ni kuwa na unyenyekevu wa akili. Biblia inaonyesha kwamba mtu mnyenyekevu ana mtazamo unaofaa kuhusu uhusiano wake pamoja na Yehova Mungu na wanadamu wenzake. Mtu mnyenyekevu anatambua kwamba kwa njia moja au nyingine watu wengine ni bora kuliko yeye.—Flp. 2:3, 4.

4-5. Kwa nini tunaweza kusema kwamba unyenyekevu wa kweli si jambo linaloonekana kwa nje tu?

4 Huenda kwa nje watu wengine wakaonekana kuwa wanyenyekevu. Huenda wao ni wakimya au wenye haya. Au huenda ni wenye heshima au adabu kwa sababu ya utamaduni au malezi yao. Lakini kihalisi moyoni mwao wanaweza kuwa ni wenye kiburi sana. Muda si muda, watafunua jinsi walivyo kikweli moyoni mwao.—Luka 6:45.

5 Kwa upande mwingine, watu wengine wanajiamini na ni wazungumzaji wazuri, lakini hilo halimaanishi kwamba wao wana kiburi. (Yoh. 1:46, 47) Hata hivyo, watu wenye utu wa aina hiyo wanapaswa kuwa waangalifu wasitegemee au kutumaini uwezo wao wa asili. Iwe sisi ni wazungumzaji wazuri au wenye haya, sote tunapaswa kujitahidi kusitawisha unyenyekevu wa moyoni.

Mtume Paulo alikuwa mnyenyekevu na hakujiona kuwa bora kuliko wengine (Tazama fungu la 6) *

6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 15:10?

6 Fikiria mfano wa mtume Paulo. Alitumiwa kwa njia kubwa na Yehova kuanzisha makutaniko mapya katika jiji moja baada ya lingine. Huenda alitimiza mengi zaidi katika huduma kuliko mitume wengine wote wa Yesu. Hata hivyo, Paulo hakujiona kuwa bora kuliko ndugu zake. Kwa unyenyekevu alikiri hivi: “Mimi ni mdogo zaidi kati ya mitume, nami sistahili kuitwa mtume, kwa sababu nililitesa kutaniko la Mungu.” (1 Kor. 15:9) Kisha, Paulo alionyesha wazi kwamba uhusiano wake mzuri pamoja na Yehova haukutokana na utu wake au jitihada zake mwenyewe, bali ni kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu. (Soma 1 Wakorintho 15:10.) Katika barua yake kwa Wakorintho, Paulo ni mfano mzuri sana wa mtu mnyenyekevu—hasa tunapokumbuka kwamba baadhi ya watu katika kutaniko hilo walikuwa wakijaribu kujionyesha kuwa bora kuliko yeye!—2 Kor. 10:10.

Karl F. Klein, ndugu mnyenyekevu aliyekuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza (Tazama fungu la 7)

7. Baadhi ya ndugu wanaojulikana katika siku zetu wameonyeshaje unyenyekevu? Toa mfano.

7 Watu wengi wa Yehova wametiwa moyo na simulizi la maisha la Ndugu Karl F. Klein, aliyekuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Katika simulizi lake la maisha, Ndugu Klein kwa unyenyekevu alitaja baadhi ya changamoto ambazo alikabili maishani mwake. Kwa mfano, katika miaka ya 1920, baada ya kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza, aliona kazi hiyo kuwa ngumu sana hivi kwamba hakuhubiri nyumba kwa nyumba kwa miaka miwili. Baadaye alipokuwa akitumikia Betheli, aliweka kinyongo kwa muda fulani baada ya kushauriwa. Pia, alipatwa na ugonjwa wa kihisia uliosababishwa na mikazo, lakini baadaye alipona. Hata hivyo, alifurahia pia mapendeleo mengi ya pekee. Hebu wazia unyenyekevu ambao ndugu huyo aliyejulikana sana alihitaji ili kukiri waziwazi udhaifu wake! Ndugu na dada wengi wanamkumbuka kwa upendo Ndugu Klein na simulizi lake la maisha lenye kuvutia na unyoofu wake. *

KWA NINI TUNAPASWA KUSITAWISHA SIFA YA UNYENYEKEVU?

8. Andiko la 1 Petro 5:6 linatusaidiaje kuona kwamba unyenyekevu ni sifa inayomfurahisha Yehova?

8 Sababu kuu zaidi inayotufanya tusitawishe unyenyekevu ni kwamba sifa hiyo inampendeza Yehova. Mtume Petro alionyesha jambo hilo waziwazi. (Soma 1 Petro 5:6.) Kikielezea maneno hayo ya Petro, kitabu “Njoo Uwe Mfuasi Wangu” kinasema: “Majivuno ni kama sumu. Matokeo yake yanaweza kuwa mabaya sana. Majivuno yanaweza kumfanya mtu mwenye vipawa vingi awe asiyefaa hata kidogo machoni pa Mungu. Kwa upande mwingine, unyenyekevu unaweza kumfanya hata mtu wa hali ya chini zaidi awe na thamani sana machoni pa Yehova. . . . [Yehova] atafurahia kukupa thawabu . . . kwa sababu ya unyenyekevu wako.” * Je, kweli kuna jambo bora zaidi kuliko kuufurahisha moyo wa Yehova?—Met. 23:15.

9. Sifa ya unyenyekevu huwavuta wengine kwetu jinsi gani?

9 Mbali na kumfurahisha Yehova, tunapositawisha sifa ya unyenyekevu tunapata faida nyingi. Unyenyekevu huwavuta wengine kwetu. Ili kuelewa ni kwa nini, jaribu kujiweka katika hali yao. (Mt. 7:12) Wengi wetu hatungependa kushughulika na watu ambao husisitiza maoni yao na wanakataa kukubali mapendekezo ya wengine. Kwa upande mwingine, tunafurahia kushirikiana na waamini wenzetu wanapotuonyesha “hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, huruma nyororo, na unyenyekevu.” (1 Pet. 3:8) Ikiwa tunavutiwa na watu wa aina hiyo, huenda wao pia wakavutiwa nasi—maadamu sisi ni wanyenyekevu.

10. Sifa ya unyenyekevu huturahisishia maisha jinsi gani?

10 Pia, sifa ya unyenyekevu huturahisishia maisha. Ukweli ni kwamba huenda mara nyingine tukajionea maishani mambo ambayo yanaonekana kuwa si sawa au si ya haki. Mfalme Sulemani, mwanamume mwenye hekima alikiri hivi: “Nimeona watumishi wakiwa wamepanda farasi lakini wakuu wakitembea kwa miguu kama watumishi tu.” (Mhu. 10:7) Nyakati nyingine, wale walio na uwezo mkubwa hawaheshimiwi au kutambuliwa kwa kazi yao. Na wale walio na uwezo mdogo hupewa sifa au heshima nyingi zaidi. Hata hivyo, Sulemani alisema kwamba ni jambo la hekima kwetu kukubali ukweli huo wa mambo, kuliko kuhangaishwa kupita kiasi na hali hizo. (Mhu. 6:9) Tukiwa wanyenyekevu, itakuwa rahisi zaidi kwetu kukubaliana na jinsi hali za maisha zilivyo, na si jinsi ambavyo tungependa ziwe.

NI HALI GANI ZINAZOWEZA KUJARIBU UNYENYEKEVU WETU?

Hali kama hii inaweza kujaribu unyenyekevu wetu jinsi gani? (Tazama fungu la 11 na 12) *

11. Tunapaswa kuitikiaje tunaposhauriwa?

11 Kila siku, tuna fursa nyingi sana za kuonyesha unyenyekevu. Fikiria hali zifuatazo. Tunaposhauriwa. Ni vizuri kukumbuka kwamba ikiwa mtu anachukua hatua ya kutushauri, kuna uwezekano mkubwa kwamba tumekosea kuliko tunavyodhani. Nyakati kama hizo, huenda mwelekeo wetu wa kwanza ukawa ni kukataa shauri hilo. Huenda tukamchambua aliyetushauri au jinsi alivyotoa shauri hilo. Lakini ikiwa sisi ni wanyenyekevu tutajitahidi kuwa na mtazamo mzuri.

12. Kulingana na Methali 27:5, 6, kwa nini tunapaswa kumthamini mtu anayetushauri? Toa mfano.

12 Mtu mnyenyekevu anathamini anapopewa shauri. Kwa mfano, wazia uko kwenye mkutano wa Kikristo. Baada ya kuzungumza na ndugu na dada kadhaa, mmoja anakuita pembeni na kwa busara anakuambia kwamba una mabaki ya chakula kwenye meno. Bila shaka, utaaibika. Lakini, je, hutathamini kwamba ndugu au dada huyo amekueleza jambo hilo? Ukweli ni kwamba ungetamani mtu mwingine angekuwa amekwambia jambo hilo mapema hata zaidi! Vivyo hivyo, kwa unyenyekevu tunapaswa kumthamini ndugu au dada aliye na ujasiri wa kutupatia shauri linapohitajika. Tunamwona kuwa rafiki yetu, na si adui yetu.—Soma Methali 27:5, 6; Gal. 4:16.

Kwa nini tunahitaji kuwa wanyenyekevu wengine wanapopata mapendeleo ya utumishi? (Tazama fungu la 13 na 14) *

13. Tunaweza kuonyeshaje unyenyekevu wengine wanapopata mapendeleo ya utumishi?

13 Wengine wanapopata mapendeleo ya utumishi. Mzee wa kutaniko anayeitwa Jason anakiri hivi: “Nyakati nyingine ninapoona wengine wakipewa mapendeleo, mimi hujiuliza kwa nini hawakunichagua mimi.” Je, umewahi kuhisi hivyo? Si kosa ‘kujitahidi’ kufikia mapendeleo makubwa zaidi ya utumishi. (1 Tim. 3:1) Hata hivyo, tunapaswa kulinda njia yetu ya kufikiri. Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kuruhusu kiburi kisitawi moyoni mwetu. Kwa mfano, mwanamume Mkristo anaweza kuanza kufikiri kwamba ni yeye ndiye anayestahili zaidi kupewa mgawo fulani. Au mke Mkristo anaweza kufikiri hivi: ‘Mume wangu anastahili zaidi mgawo huo kuliko ndugu fulani!’ Hata hivyo, ikiwa sisi ni wanyenyekevu kikweli, tutaepuka roho hiyo ya kiburi.

14. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Musa alivyotenda wengine walipopata mapendeleo?

14 Tunajifunza jambo fulani kutokana na jinsi Musa alivyotenda wengine walipopata mapendeleo. Musa alithamini mgawo wake wa kuliongoza taifa la Israeli. Lakini aliitikiaje Yehova alipowaruhusu wengine watumikie pamoja naye? Hakuwa na wivu. (Hes. 11:24-29) Ilipohusu kusikiliza kesi za watu, kwa unyenyekevu aliwaruhusu wengine wamsaidie kufanya kazi hiyo. (Kut. 18:13-24) Hilo lilimaanisha kwamba Waisraeli ambao Musa alikuwa amepewa mgawo wa kuwasikiliza, wangehudumiwa vizuri zaidi. Hivyo, Musa alihangaikia hali njema ya wengine badala ya kutanguliza mapendeleo yake. Huo ni mfano mzuri sana kwetu! Kumbuka kwamba ili Yehova atutumie vizuri, jambo muhimu zaidi kwake ni unyenyekevu wetu na si uwezo wetu. Ingawa “Yehova yuko juu, yeye huwaona wanyenyekevu.”—Zab. 138:6.

15. Ndugu na dada wengi wamekabili mabadiliko gani?

15 Tunapokabili hali mpya maishani. Katika miaka ya karibuni, ndugu na dada wengi ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi wamepata migawo mipya. Kwa mfano, mwaka wa 2014, waangalizi wa wilaya pamoja na wake zao walipewa migawo mingine ya utumishi wa wakati wote. Na tangu mwaka huo, waangalizi wa mzunguko hawaendelei na mgawo wao wanapofikisha umri wa miaka 70. Na ndugu wenye umri wa miaka 80 au zaidi hawaendelei kutumikia tena wakiwa waratibu wa baraza la wazee. Isitoshe, kwa miaka kadhaa iliyopita Wanabetheli wengi wamepewa migawo ya kwenda shambani. Wengine wameacha utumishi wa wakati wote wa pekee kwa sababu ya matatizo ya afya, majukumu ya familia, au hali nyingine za kibinafsi.

16. Ndugu na dada zetu wameonyeshaje unyenyekevu walipokabili hali mpya maishani?

16 Haikuwa rahisi kwa ndugu na dada hao kufanya mabadiliko hayo. Ni wazi kwamba waliupenda sana mgawo wao wa zamani, na wengi wao walikuwa wametumikia katika mgawo huo kwa miaka mingi. Baadhi yao walipitia “kipindi cha maombolezo” walipokuwa wakizoea hali yao mpya. Hata hivyo, baada ya muda walifaulu kuzoea hali yao mpya. Kwa nini? Sababu kuu ilikuwa upendo wao kwa Yehova. Walitambua kwamba walijiweka wakfu kwa Yehova—si kwa kazi, cheo, au mgawo fulani. (Kol. 3:23) Wanafurahia kuendelea kumtumikia Yehova kwa unyenyekevu katika mgawo wowote ule. ‘Wanatupa mahangaiko yao yote juu yake,’ wakijua kwamba anawajali.—1 Pet. 5:6, 7.

17. Kwa nini tunashukuru kwamba Neno la Mungu linatutia moyo tusitawishe sifa ya unyenyekevu?

17 Je, hatushukuru kwamba Neno la Mungu linatutia moyo tusitawishe sifa ya unyenyekevu? Tunapositawisha sifa hiyo nzuri, tunajinufaisha sisi wenyewe na wengine. Tunaweza kushughulikia kwa njia nzuri zaidi changamoto tunazokabili maishani. Zaidi ya yote, tunamkaribia Baba yetu wa mbinguni. Tunafurahi sana kujua kwamba ingawa yeye ni “Yule Aliye Juu na Aliyetukuka Sana,” anawapenda na kuwathamini watumishi wake wanyenyekevu!—Isa. 57:15.

WIMBO 45 Kutafakari kwa Moyo Wangu

^ fu. 5 Mojawapo ya sifa muhimu zaidi tunazopaswa kusitawisha ni unyenyekevu. Unyenyekevu ni nini? Kwa nini tunapaswa kusitawisha sifa hiyo? Na mabadiliko maishani yanaweza kujaribu unyenyekevu wetu jinsi gani? Makala hii itazungumzia maswali hayo muhimu.

^ fu. 7 Tazama makala yenye kichwa Jehovah Has Dealt Rewardingly With Mekatika toleo la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1984, la Kiingereza.

^ fu. 8 Tazama sura ya 3, fu. 23.

^ fu. 53 MAELEZO YA PICHA: Akiwa kwenye nyumba ya ndugu, kwa unyenyekevu mtume Paulo anafurahia ushirika pamoja na wengine, kutia ndani watoto.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Ndugu akikubali shauri la Kimaandiko kutoka kwa ndugu kijana.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Ndugu mwenye umri mkubwa zaidi hamwonei wivu yule ndugu kijana kwa sababu ya pendeleo alilo nalo kutanikoni.