Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 36

Je, Uko Tayari Kuwa Mvuvi wa Watu?

Je, Uko Tayari Kuwa Mvuvi wa Watu?

“Acha kuogopa. Kuanzia sasa utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.”​—LUKA 5:10.

WIMBO 73 Tupe Ujasiri

MUHTASARI *

1. Yesu aliwapa wavuvi wanne mwaliko gani, nao waliitikiaje?

WANAFUNZI Petro, Andrea, Yakobo na Yohana walikuwa wakifanya biashara ya uvuvi. Wazia jinsi walivyoshangazwa na mwaliko huu wa Yesu: “Nifuateni, nami nitawafanya muwe wavuvi wa watu.” * Waliitikiaje? Biblia inasema hivi: “Mara moja wakaziacha nyavu zao na kumfuata.” (Mt. 4:18-22) Uamuzi huo ulibadili kabisa maisha yao. Badala ya kuvua samaki halisi, wangekuwa ‘wakiwavua watu wakiwa hai.’ (Luka 5:10) Leo, Yesu anatoa mwaliko huohuo kwa watu wanyoofu wanaopenda kweli. (Mt. 28:19, 20) Je, umekubali mwaliko wa Yesu wa kuwa mvuvi wa watu?

2. Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uzito uamuzi wa kuwa wavuvi wa watu, na nini kitakachotusaidia kufikia uamuzi huo?

2 Huenda umekuwa ukijifunza Biblia kwa muda fulani, na umefanya mabadiliko maishani. Na sasa unahitaji kufanya uamuzi ikiwa utakuwa mhubiri wa habari njema. Ikiwa unasita kukubali mwaliko wa Yesu, usivunjike moyo. Huenda unasita kwa sababu unajua kwamba huo ni uamuzi mzito sana. Ni kweli kwamba Biblia inasema Petro na wenzake waliziacha nyavu zao “mara moja.” Hata hivyo, Petro na ndugu yake hawakufanya uamuzi huo bila kufikiri. Walikuwa wamemjua na kumkubali Yesu kuwa Masihi zaidi ya miezi sita kabla ya kukubali mwaliko huo. (Yoh. 1:35-42) Vivyo hivyo, huenda tayari umejifunza mambo mengi kumhusu Yehova na Yesu, na unataka kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho. Hata hivyo, hupaswi kufanya uamuzi huo bila kuhesabu gharama. Ni nini kilichowasaidia Petro, Andrea, na wengine kufikia uamuzi wao?

3. Ni sifa gani zitakazokusaidia uchochee tamaa yako ya kukubali mwaliko wa Yesu?

3 Wanafunzi wa Yesu wa kwanza walikuwa na tamaa ya kufanya kazi ya kuhubiri, walijua jinsi ya kufanya kazi yao vizuri, walikuwa jasiri, na walikuwa wakijitia nidhamu. Bila shaka, sifa hizo ziliwasaidia wawe na matokeo mazuri katika kuhubiri habari njema. Makala hii itazungumzia jinsi unavyoweza kuboresha sifa hizo ili uhubiri na kuwafundisha wengine habari njema kwa mafanikio.

CHOCHEA TAMAA YAKO YA KUHUBIRI

Petro na wengine walikuja kuwa wavuvi wa watu. Kazi hiyo muhimu inaendelea katika siku zetu (Tazama fungu la 4 na 5)

4. Ni nini kilichomchochea Petro awe mvuvi?

4 Petro hakuvua samaki ili tu kuitegemeza familia yake. Inaonekana kwamba Petro alipenda kazi yake ya kuvua samaki. (Yoh. 21:3, 9-15) Pia, alijifunza kupenda kazi ya kuvua watu. Na kwa msaada wa Yehova, Petro akaja kuwa mvuvi mwenye matokeo mazuri.​—Mdo. 2:14, 41.

5. Kulingana na Luka 5:8-11, kwa nini Petro aliogopa, na ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda hisia kama hizo?

5 Sababu kuu inayotuchochea kuhubiri ni upendo wetu kwa Yehova. Upendo wetu kwa Yehova unaweza kutusaidia tuwaambie wengine kumhusu hata ingawa tunahisi hatustahili. Yesu alipomwalika Petro awe mvuvi wa watu, alimwambia hivi: “Acha kuogopa.” (Soma Luka 5:8-11.) Petro hakuwa akiogopa kile ambacho kingetokea ikiwa angekubali kuwa mwanafunzi wa Yesu. Badala yake, alishtushwa na wingi wa samaki ambao Yesu aliwasaidia kuvua kimuujiza na alihisi kwamba hastahili kufanya kazi pamoja na Yesu. Huenda wewe pia ukaogopa unapotambua yale yanayohusika ili kuwa mwanafunzi wa Kristo. Ikiwa ndivyo, imarisha upendo wako kwa Yehova, Yesu, na jirani yako, nawe utachochewa kukubali mwaliko wa Yesu wa kuwa mvuvi wa watu.​—Mt. 22:37, 39; Yoh. 14:15.

6. Ni mambo gani mengine yanayotuchochea kuhubiri?

6 Fikiria baadhi ya sababu nyingine zinazotuchochea tuhubiri. Tunataka kutii amri hii ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi.” (Mt. 28:19, 20) Pia, tunahubiri kwa sababu watu “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji,” na wanahitaji sana kujifunza kweli kuhusu Ufalme. (Mt. 9:36) Yehova anataka watu wa namna zote wapate ujuzi sahihi wa kweli na waokolewe.​—1 Tim. 2:4.

7. Andiko la Waroma 10:13-15 linaonyeshaje umuhimu wa kazi ya kuhubiri?

7 Tutachochewa kuhubiri tunapofikiria jinsi kazi hiyo inavyoweza kuokoa uhai wa watu. Tofauti na mvuvi anayeuza au kula samaki anaowavua, sisi ‘tunavua’ watu ili kuokoa uhai wao.​—Soma Waroma 10:13-15; 1 Tim. 4:16.

ONGEZA UJUZI WAKO

8-9. Mvuvi anapaswa kujua nini, na kwa nini?

8 Katika siku za Yesu, mvuvi Mwisraeli alipaswa kujua aina ya samaki ambao angevua. (Law. 11:9-12) Pia, alipaswa kujua mahali ambapo samaki hao wanaweza kupatikana. Kwa kawaida, samaki wanaishi kwenye eneo lenye maji yanayowafaa na ambako kuna chakula cha kutosha. Je, mvuvi anaweza kwenda kuvua wakati wowote tu? Kuhusu wakati mzuri wa kwenda kuvua samaki halisi, ona kile ambacho Shahidi fulani kutoka visiwa vya Pasifiki, alimwambia mmishonari fulani alipomwalika kwenda kuvua. Mmishonari huyo aliposema, “Tukutane kesho saa tatu asubuhi.” Ndugu huyo alimwambia hivi: “Naona hujanielewa. Tunaenda kuvua wakati ambao tunaweza kupata samaki, na si wakati ambao sisi tunapenda kwenda kuvua.”

9 Vivyo hivyo, wavuvi wa watu katika karne ya kwanza, walienda kwenye maeneo ambayo wangewapata watu, na wakati ambao watu walipatikana. Kwa mfano, wafuasi wa Yesu walihubiri hekaluni na kwenye masinagogi, nyumba kwa nyumba, na sokoni. (Mdo. 5:42; 17:17; 18:4) Sisi pia tunahitaji kujua wakati ambao watu wanapatikana nyumbani au katika eneo tunalohubiri. Tunahitaji kubadilikana kulingana na hali na kuhubiri mahali na wakati ambao kuna uwezekano mkubwa zaidi wa kuwapata watu.​—1 Kor. 9:19-23.

WAVUVI WENYE USTADI . . . 1. huvua wakati na mahali ambapo kuna uwezekano mkubwa zaidi wa kupata samaki (Tazama fungu la 8 na 9)

10. Tengenezo la Yehova linatuandalia vifaa gani?

10 Mvuvi anahitaji kuwa na vifaa sahihi na anapaswa kujua jinsi ya kuvitumia. Sisi pia tunahitaji kuwa na vifaa sahihi kwa ajili ya kazi yetu. Na tunahitaji kujua jinsi ya kutumia vifaa hivyo. Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo ya jinsi wanavyoweza kuwa wavuvi wa watu. Aliwaambia vitu walivyopaswa kubeba, mahali ambapo wangehubiri, na mambo waliyopaswa kusema. (Mt. 10:5-7; Luka 10:1-11) Leo, tengenezo la Yehova limeandaa Sanduku la Vifaa vya Kufundishia lenye vifaa vinavyofanya kazi vizuri. * Na tunafundishwa jinsi ya kutumia vifaa hivyo. Mazoezi hayo yanatusaidia tupate uhakika na ustadi tunaohitaji ili kazi yetu iwe na matokeo mazuri.​—2 Tim. 2:15.

WAVUVI WENYE USTADI . . . 2. wamezoezwa kutumia vifaa sahihi (Tazama fungu la 10)

IMARISHA UJASIRI WAKO

11. Kwa nini ni lazima wavuvi wa watu wawe jasiri?

11 Wale wanaofanya kazi ya uvuvi wanahitaji kuwa jasiri. Nyakati nyingine wanakabili hali zisizotarajiwa wakiwa baharini. Mara nyingi wanafanya kazi usiku na kwenye maeneo ambayo dhoruba za ghafla zinaweza kutokea. Wavuvi wa watu pia wanahitaji ujasiri. Tunapoanza kuwahubiria wengine na kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova, tunaweza kukumbana na “dhoruba,” yaani, upinzani kutoka kwa watu wa familia, kudhihakiwa na marafiki, na watu kukataa kusikiliza ujumbe wetu. Lakini hilo halitushangazi. Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba angewatuma kwa watu ambao wangewapinga.​—Mt. 10:16.

12. Kulingana na Yoshua 1:7-9, ni nini kinachoweza kuimarisha ujasiri wetu?

12 Unaweza kuimarishaje ujasiri wako? Kwanza, uwe na hakika kwamba Yesu anaendelea kuongoza kazi ya kuhubiri akiwa mbinguni. (Yoh. 16:33; Ufu. 14:14-16) Kisha, imarisha imani yako katika ahadi ya Yehova ya kukutunza. (Mt. 6:32-34) Kadiri imani yako inavyokuwa yenye nguvu, ndivyo ujasiri wako utakavyoongezeka. Petro na wenzake walionyesha imani yenye nguvu walipoacha biashara yao ya uvuvi na kumfuata Yesu. Vivyo hivyo, wewe pia ulionyesha imani yenye nguvu ulipowaeleza marafiki na watu wa familia yako kwamba umeanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, na kwamba umeanza kuhudhuria mikutano yao! Bila shaka, umefanya mabadiliko makubwa katika mwenendo na mtindo wako wa maisha ili uishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Yehova. Hilo pia lilihitaji imani na ujasiri. Unapoendelea kuimarisha ujasiri wako, unaweza kuwa na uhakika kwamba ‘Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe mahali popote utakapoenda.’​—Soma Yoshua 1:7-9.

WAVUVI WENYE USTADI . . . 3. wanafanya kazi kwa ujasiri kwenye hali zinazobadilika-badilika (Tazama fungu la 11 na 12)

13. Kutafakari na kusali kunaweza kukusaidiaje kuimarisha ujasiri wako?

13 Unaweza kufanya jambo gani lingine ili kuimarisha ujasiri wako? Sali ili upate ujasiri na uhodari. (Mdo. 4:29, 31) Yehova atajibu sala zako, naye hatakuacha kamwe. Siku zote yupo ili kukusaidia. Pia, unaweza kutafakari kuhusu jinsi Yehova alivyowakomboa watu wengine wakati uliopita. Fikiria pia kuhusu jinsi ambavyo Yehova amekusaidia kushinda matatizo yako na kukupatia nguvu za kufanya mabadiliko maishani mwako. Kwa hakika, Yule aliyewaongoza watu wake wapite katikati ya Bahari Nyekundu, anaweza kukusaidia uwe mwanafunzi wa Kristo. (Kut. 14:13) Uwe na uhakika uleule kama wa mtunga zaburi aliyesema: “Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?”​—Zab. 118:6.

14. Umejifunza nini kutokana na mfano wa Masae na Tomoyo?

14 Njia nyingine ya kuimarisha ujasiri wetu ni kwa kujifunza jinsi ambavyo Yehova amewasaidia watu ambao kiasili ni wenye haya, lakini wamejifunza kuwa jasiri. Fikiria kisa cha dada anayeitwa Masae. Alikuwa mwenye haya na alihisi kwamba hangeweza kamwe kuhubiri hadharani. Aliona kwamba kuzungumza na watu asiowafahamu ni sawa na kujaribu kupanda ukuta mrefu, jambo ambalo aliamini hangefaulu kamwe kufanya. Hivyo, aliamua kufanya jitihada za pekee ili aimarishe upendo wake kwa Mungu na kwa jirani zake. Alitafakari kuhusu uharaka wa nyakati tunazoishi na alisali ili apate msaada wa kuchochea tamaa yake ya kuhubiri. Alifaulu kushinda woga wake na hata alitumikia akiwa painia wa kawaida. Yehova anaweza pia kuwasaidia wahubiri wapya ‘wawe jasiri.’ Fikiria kisa cha dada anayeitwa Tomoyo. Alipoanza kuhubiri nyumba kwa nyumba, mwenye nyumba wa kwanza aliyekutana naye alimwambia hivi kwa sauti kubwa: “Sitaki kuzungumza chochote na Mashahidi wa Yehova!” na kisha akafunga mlango kwa nguvu. Kwa ujasiri Tomoyo alimwambia hivi mwandamani wake: “Je, umesikia hilo? Sijasema neno lolote, lakini ametambua kuwa mimi ni Shahidi wa Yehova. Nimefurahi sana!” Sasa Tomoyo anatumikia akiwa painia wa kawaida.

SITAWISHA SIFA YA KUJITIA NIDHAMU

15. Sifa ya kujitia nidhamu ni nini, na kwa nini ni muhimu kwa Wakristo?

15 Wavuvi wenye mafanikio hujitia nidhamu. Kujitia nidhamu kunafafanuliwa kuwa ni “uwezo wa kujilazimisha kufanya mambo unayopaswa kufanya.” Ni lazima wavuvi wajitie nidhamu ili waamke mapema, wafanye kazi hadi itakapokamilika, na wavumilie hali mbaya ya hewa. Sisi pia tunahitaji kujitia nidhamu ili tuvumilie na kuikamilisha kazi yetu.​—Mt. 10:22.

16. Tunaweza kusitawishaje sifa ya kujitia nidhamu?

16 Hatuzaliwi tukiwa na uwezo wa kujitia nidhamu. Kinyume cha hilo, mwelekeo wetu wa kiasili ni kufanya jambo tunaloona kuwa rahisi kwetu. Tunahitaji sifa ya kujizuia ili tuweze kujitia nidhamu. Hivyo, tunahitaji msaada ili tujizoeze kufanya mambo ambayo huenda ni vigumu kwetu kuyafanya. Yehova anatupatia msaada huo kupitia roho yake takatifu.​—Gal. 5:22, 23.

17. Kulingana na 1 Wakorintho 9:25-27, Paulo alisema alihitaji kufanya nini ili kusitawisha sifa ya kujitia nidhamu?

17 Mtume Paulo alijitia nidhamu. Lakini alikiri kwamba alihitaji ‘kuupigapiga’ mwili wake ili kufanya yaliyo sawa. (Soma 1 Wakorintho 9:25-27.) Aliwahimiza wengine wajitie nidhamu na kufanya mambo yote “kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Ni lazima tujitie nidhamu ili tudumishe ratiba nzuri ya kiroho, inayotia ndani kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuvua watu.​—Mdo. 2:46.

USIKAWIE

18. Kwa maoni ya Yehova tutakuwa tumefanikiwa ikiwa tunafanya nini?

18 Mvuvi anapima mafanikio yake kwa kuhesabu idadi ya samaki aliowavua. Hata hivyo, sisi hatupimi mafanikio yetu kwa kuhesabu idadi ya watu tuliowasaidia wajiunge na tengenezo la Mungu. (Luka 8:11-15) Maadamu tunaendelea kuhubiri habari njema na kuwafundisha wengine, kwa maoni ya Yehova tutakuwa tumefanikiwa. Kwa nini? Kwa sababu tunamtii Yeye na Mwana wake.​—Marko 13:10; Mdo. 5:28, 29.

19-20. Ni sababu gani ya pekee inayotuchochea kuhubiri sasa?

19 Katika baadhi ya nchi, uvuvi unaruhusiwa katika miezi fulani tu. Katika nchi hizo, hisi ya uharaka ya mvuvi inaongezeka kadiri msimu wa uvuvi unavyokaribia kuisha. Tukiwa wavuvi wa watu, tuna sababu nyingine ya kuhubiri sasa: Mwisho wa mfumo huu unakaribia kwa kasi! Wakati uliobaki wa kushiriki katika kazi hii umepungua sana. Usikawie au kuhisi kwamba unahitaji kusubiri hadi hali ziwe bora ili ushiriki katika utendaji huu muhimu.​—Mhu. 11:4.

20 Jitahidi sasa kuchochea tamaa yako ya kuhubiri, kuongeza ujuzi wako wa Biblia, kuimarisha ujasiri wako, na kusitawisha sifa ya kujitia nidhamu. Jiunge na wavuvi zaidi ya milioni nane wa watu, nawe utajionea shangwe ya Yehova. (Neh. 8:10) Azimia kushiriki kikamili katika kazi hii hadi Yehova atakaposema imekamilika. Makala inayofuata itazungumzia njia tatu zitakazotusaidia kuimarisha azimio letu la kuendelea katika kazi ya kuhubiri Ufalme tukiwa wavuvi wa watu.

WIMBO 66 Tangaza Habari Njema

^ fu. 5 Yesu aliwaalika wavuvi wenye bidii na wanyenyekevu wawe wanafunzi wake. Leo, anaendelea kuwaalika watu wenye sifa kama hizo wawe wavuvi wa watu. Makala hii itazungumzia kile ambacho wanafunzi wa Biblia wanaosita kukubali mwaliko wa Yesu wanahitaji kufanya.

^ fu. 1 UFAFANUZI WA MANENO: Maneno “wavuvi wa watu,” yanarejelea wale wote wanaohubiri habari njema na kuwafundisha wengine ili wawe wanafunzi wa Kristo.

^ fu. 10 Tazama makala “Fundisha Kweli” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 2018, ukurasa wa 11-16.