Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 38

Tenda kwa Hekima Katika Kipindi Chenye Amani

Tenda kwa Hekima Katika Kipindi Chenye Amani

“Nchi haikuwa na usumbufu na hakuna yeyote aliyepigana vita naye katika miaka hiyo, kwa maana Yehova alimpumzisha.”—2 NYA. 14:6.

WIMBO 60 Ni Uzima Kwao

MUHTASARI *

1. Ni wakati gani ambapo inaweza kuwa vigumu kwetu kumtumikia Yehova?

UNA maoni gani? Ni wakati gani ulio mgumu zaidi kumtumikia Yehova—je, ni wakati unapokabiliana na matatizo makubwa maishani mwako au wakati maisha yako yanapokuwa na amani kwa kadiri fulani? Tunapokabili matatizo, ni rahisi kwetu kumtegemea Yehova. Lakini tunatendaje maisha yetu yanapokuwa na amani? Je, tunapunguza bidii yetu ya kumtumikia Yehova? Yehova aliwaonya Waisraeli kwamba jambo hilo linaweza kutokea.—Kum. 6:10-12.

Mfalme Asa alipinga kwa uthabiti ibada ya uwongo (Tazama fungu la 2) *

2. Mfalme Asa aliweka mfano gani?

2 Mfalme Asa ni mfano bora wa mtu aliyetenda kwa hekima kwa kumtegemea kikamili Yehova. Hakumtumikia Yehova katika nyakati mbaya tu, bali pia katika nyakati zenye amani. Tangu mapema, “moyo wa Asa ulimtumikia kikamili Yehova.” (1 Fal. 15:14, maelezo ya chini) Asa alithibitisha kwamba anamtumikia Yehova kwa moyo wake wote kwa kuondoa ibada ya uwongo katika Yuda. Biblia inasema kwamba “aliondoa madhabahu za kigeni na mahali pa juu, akazivunjavunja nguzo takatifu.” (2 Nya. 14:3, 5) Hata alimwondoa Maaka, nyanya yake kutoka katika cheo chake cha mama malkia. Kwa nini? Kwa sababu aliwachochea watu waabudu sanamu.—1 Fal. 15:11-13.

3. Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Asa alifanya mengi zaidi ya kuondoa ibada ya uwongo. Aliendeleza ibada safi kwa kuwasaidia watu wa Yuda wamrudie Yehova. Yehova alimbariki Asa na Waisraeli kwa kuwapa kipindi cha amani. * Katika kipindi cha miaka kumi wakati wa utawala wa Asa, “nchi ilikuwa na amani.” (2 Nya. 14:1, 4, 6) Katika makala hii, tutazungumzia jinsi Asa alivyotumia kipindi hicho cha amani. Kisha, tutachunguza mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza ambao kama Asa walitumia vizuri kipindi kilichokuwa na amani. Mwishowe, tutajibu swali hili: Ikiwa unaishi katika nchi ambayo inaruhusu uhuru wa ibada, unaweza kutumiaje kwa hekima kipindi hicho chenye amani?

MFALME ASA ALIUTUMIAJE WAKATI WENYE AMANI?

4. Kulingana na 2 Mambo ya Nyakati 14:2, 6, 7, Asa alitumiaje wakati wa amani?

4 Soma 2 Mambo ya Nyakati 14:2, 6, 7Asa aliwaambia watu kwamba Yehova ndiye ‘aliyewapumzisha pande zote.’ Asa hakuhisi kwamba kipindi hicho cha amani kilikuwa wakati wa kustarehe. Badala yake, alianza kujenga majiji, kuta, minara, na malango. Aliwaambia hivi watu wa Yuda: “Nchi bado imo mikononi mwetu.” Asa alimaanisha nini? Alimaanisha kwamba watu wangeweza kuzunguka kwa uhuru katika nchi waliyopewa na Mungu na kufanya ujenzi bila upinzani kutoka kwa maadui. Aliwahimiza watu wautumie vizuri wakati huo wa amani.

5. Kwa nini Asa aliimarisha jeshi lake?

5 Pia, Asa alitumia wakati huo wa amani kuimarisha jeshi lake. (2 Nya. 14:8) Je, hilo linamaanisha kwamba hakumtumaini Yehova? Hapana. Badala yake, Asa alijua kwamba akiwa mfalme alikuwa na wajibu wa kuwatayarisha watu kwa ajili ya matatizo ambayo huenda wangekabili wakati ujao. Asa alijua kwamba huenda kipindi cha amani ambacho Yuda ilifurahia kisingedumu milele, na hilo lilithibitika kuwa kweli.

WAKRISTO WA KARNE YA KWANZA WALIUTUMIAJE WAKATI WENYE AMANI?

6. Wakristo wa karne ya kwanza walitumiaje wakati wa amani?

6 Ingawa Wakristo wa karne ya kwanza walinyanyaswa mara kwa mara, walifurahia pia vipindi vyenye amani. Wanafunzi hao walitumiaje fursa hizo? Wanaume na wanawake hao waaminifu walihubiri habari njema bila kuacha. Kitabu cha Matendo kinasema kwamba ‘walitembea katika kumwogopa Yehova.’ Waliendelea kuhubiri habari njema, na matokeo yake ni kwamba ‘waliendelea kuongezeka.’ Ni wazi kwamba Yehova alibariki jitihada zao za kuhubiri kwa bidii katika nyakati za amani.—Mdo. 9:26-31.

7-8. Mtume Paulo na wengine walifanya nini fursa ilipojitokeza? Eleza.

7 Wanafunzi wa karne ya kwanza walitumia kila fursa kuhubiri habari njema. Kwa mfano, mtume Paulo alipokuwa Efeso alitambua kwamba amefunguliwa mlango mkubwa, hivyo akatumia fursa hiyo kuhubiri na kufanya wanafunzi katika jiji hilo.—1 Kor. 16:8, 9.

8 Fursa nyingine ya kuhubiri ilijitokeza kwa Paulo na Wakristo wengine wakati swala la tohara liliposuluhishwa mwaka wa 49 W.K. (Mdo. 15:23-29) Baada ya makutaniko kujulishwa uamuzi huo, wanafunzi waliongeza jitihada za kutangaza “habari njema ya neno la Yehova.” (Mdo. 15:30-35) Matokeo yalikuwaje? Biblia inasema kwamba “makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”—Mdo. 16:4, 5.

KUTUMIA NYAKATI ZENYE AMANI LEO

9. Hali ikoje katika nchi nyingi leo, na tunaweza kujiuliza swali gani?

9 Katika nchi nyingi leo, tunaweza kuhubiri kwa uhuru. Je, unaishi katika nchi ambayo ina uhuru wa ibada? Ikiwa ndivyo, jiulize, ‘Ninautumiaje uhuru huo?’ Katika siku hizi za mwisho zenye kusisimua, tengenezo la Yehova linafanya kampeni kubwa zaidi ya kuhubiri na kufundisha kuwahi kufanywa ulimwenguni pote. (Marko 13:10) Watu wa Yehova wana fursa nyingi za kushiriki katika kazi hiyo.

Wengi wamepata baraka nyingi kwa kushiriki katika huduma katika nchi nyingine au kwa kuwahubiria wale wanaozungumza lugha nyingine (Tazama fungu la 10 hadi 12) *

10. Andiko la 2 Timotheo 4:2 linatutia moyo tufanye nini?

10 Unaweza kutumiaje vizuri wakati wa amani? (Soma 2 Timotheo 4:2.) Kwa nini usichunguze hali zako na kuona ikiwa wewe au mtu wa familia yako anaweza kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri, labda hata kwa kutumikia akiwa painia? Huu si wakati wa kujikusanyia utajiri na vitu vya kimwili, kwa sababu hatutavuka na vitu hivyo kwenye dhiki kuu.—Met. 11:4; Mt. 6:31-33; 1 Yoh 2:15-17.

11. Baadhi ya wahubiri wamefanya nini ili kuwasaidia watu wengi kadiri iwezekanavyo wasikie habari njema?

11 Wahubiri wengi wamejifunza lugha mpya ili waweze kuwahubiria na kuwafundisha watu wengine. Tengenezo la Mungu linawaunga mkono kwa kuchapisha machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha nyingi zaidi. Kwa mfano, katika mwaka wa 2010 machapisho yetu yalikuwa yanapatikana katika lugha 500 hivi. Leo, idadi hiyo imeongezeka hadi kufikia lugha zaidi ya 1000!

12. Watu wananufaikaje kwa kusikia ujumbe wa Ufalme katika lugha yao ya mama? Toa mfano.

12 Watu wanahisije wanaposikia kweli za Neno la Mungu katika lugha yao ya mama? Fikiria kisa cha dada aliyenufaika kwa kuhudhuria kusanyiko la eneo huko Memphis, Tennessee, Marekani. Kusanyiko lilifanywa kwa Kinyarwanda, lugha ambayo kwa kawaida huzungumzwa nchini Rwanda, Kongo (Kinshasa), na Uganda. Baada ya kusanyiko, dada huyo anayezungumza Kinyarwanda alisema hivi: “Hii ni mara yangu ya kwanza kuelewa kikamili programu ya kiroho tangu nilipohamia Marekani miaka 17 iliyopita.” Ni wazi kwamba dada huyo aliguswa moyo sana aliposikia programu hiyo katika lugha yake ya mama. Ikiwa hali yako inaruhusu, je, unaweza kujifunza lugha nyingine ili kuwasaidia baadhi ya watu katika eneo lako? Huenda ukachochewa kufanya hivyo hasa ikiwa katika eneo la kutaniko lenu kuna watu ambao wanajihisi huru zaidi kuzungumza lugha nyingine. Jitihada zako zitathawabishwa.

13. Ndugu zetu nchini Urusi walitumiaje kipindi walichokuwa na amani?

13 Si ndugu na dada wote walio na uhuru wa kuhubiri waziwazi. Nyakati nyingine katika baadhi ya nchi, ndugu na dada zetu hawawezi kuhubiri kwa uhuru kwa sababu serikali zimeiwekea vizuizi kazi yetu ya kuhubiri. Kwa mfano, fikiria ndugu zetu nchini Urusi. Baada ya minyanyaso ya miaka mingi, walitambuliwa rasmi kisheria Machi 1991. Wakati huo, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme 16,000 hivi nchini Urusi. Miaka ishirini baadaye, idadi hiyo ilikuwa imeongezeka na kufikia wahubiri zaidi ya 160,000! Ni wazi kwamba ndugu zetu walitenda kwa hekima walipokuwa na fursa ya kuhubiri kwa uhuru. Kipindi hicho cha amani hakikudumu. Lakini hali hizo zilizobadilika hazijapunguza bidii yao ya kuendeleza ibada safi. Wanafanya yote wawezayo ili waendelee kumtumikia Yehova.

KIPINDI CHA AMANI HAKITADUMU

Baada ya Mfalme Asa kusali kwa bidii, Yehova aliwapa watu wa Yuda ushindi dhidi ya jeshi kubwa la maadui (Tazama fungu la 14 na 15)

14-15. Yehova alionyeshaje nguvu zake kwa niaba ya Asa?

14 Katika siku za Asa, hatimaye kipindi cha amani kilifikia mwisho. Jeshi kubwa kutoka Ethiopia lenye wanajeshi milioni moja liliwavamia. Zera, kamanda wa jeshi hilo alikuwa na uhakika kwamba jeshi lake lingewashinda watu wa Yuda. Hata hivyo, Mfalme Asa hakutegemea idadi ya jeshi lake, bali alimtegemea Yehova. Asa alisali hivi: “Tusaidie, Ee Yehova Mungu wetu, kwa maana tunakutegemea wewe, na katika jina lako tumekuja kupigana na umati huu.”—2 Nya. 14:11.

15 Ingawa jeshi la Waethiopia lilikuwa na idadi ya wanajeshi karibu mara mbili ya idadi ya jeshi lake, Asa alitambua kwamba Yehova alikuwa na nguvu na uwezo wa kutenda kwa niaba ya watu Wake. Na Yehova alimsaidia Asa; jeshi la Waethiopia lilishindwa vibaya sana.—2 Nya. 14:8-13.

16. Tunajuaje kwamba kipindi cha amani kitafikia mwisho wake?

16 Ingawa hatujui kihususa ni nini kitakachotokea kwa kila mmoja wetu wakati ujao, tunajua kwamba kipindi chochote cha amani ambacho watu wa Mungu wanafurahia sasa ni cha muda tu. Kumbuka kwamba Yesu alitabiri kuwa katika siku za mwisho, wanafunzi wake ‘wangechukiwa na mataifa yote.’ (Mt. 24:9) Vilevile, mtume Paulo alisema kwamba “wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Tim. 3:12) Shetani ana “hasira kali,” na tutakuwa tukijidanganya ikiwa tutafikiri kwamba kwa njia fulani tunaweza kuepuka ghadhabu yake.—Ufu. 12:12.

17. Huenda imani yetu ikajaribiwa katika njia zipi?

17 Hivi karibuni, utimilifu wa kila mmoja wetu utajaribiwa. Muda si mrefu, ulimwengu utakumbwa na “dhiki kuu ambayo haijawahi kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa.” (Mt. 24:21) Wakati huo, huenda watu wa familia wakatusaliti na kazi yetu ikapigwa marufuku. (Mt. 10:35, 36) Kama Asa, je, kila mmoja wetu atamtumaini Yehova ili kupata msaada na ulinzi?

18. Kulingana na Waebrania 10:38, 39, ni nini kitakachotusaidia kujitayarisha kwa ajili ya mwisho wa kipindi cha amani?

18 Yehova amekuwa akituandaa kiroho kwa ajili ya mambo yatakayotokea wakati ujao. Anamwongoza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anayetuandalia chakula cha kiroho chenye lishe kwa wakati unaofaa, kinachotusaidia kuendelea kuwa imara tunapomwabudu Mungu. (Mt. 24:45) Lakini ni lazima tufanye sehemu yetu ili tujenge imani thabiti katika Yehova.—Soma Waebrania 10:38, 39.

19-20. Baada ya kusoma 1 Mambo ya Nyakati 28:9, tunapaswa kujiuliza maswali gani, na kwa nini?

19 Kama Mfalme Asa, tunahitaji ‘kumtafuta Yehova.’ (2 Nya. 14:4; 15:1, 2) Tunaanza kumtafuta Yehova tunapojifunza kumhusu, na kubatizwa. Tunatumia kila fursa tunayopata kuimarisha upendo wetu kwa Yehova. Ili kupima maendeleo yetu katika jambo hilo, tunaweza kujiuliza hivi: Je, ninahudhuria kwa ukawaida mikutano ya kutaniko? Tunapohudhuria mikutano inayoandaliwa na tengenezo la Yehova, tunapata burudisho la kweli la kiroho pamoja na ushirika unaojenga. (Mt. 11:28) Pia, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninajifunza Biblia kwa ukawaida? ‘ Ikiwa una familia, je, umetenga wakati wa kufanya ibada ya familia kila juma? Au ikiwa unaishi peke yako, je, unatenga wakati wa kujifunza kibinafsi kama tu ambavyo ungefanya ikiwa ungekuwa unaishi na familia? Pia, je, unashiriki kikamili kadiri iwezekanavyo katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi?

20 Kwa nini tujiulize maswali hayo? Biblia inatuambia kwamba Yehova anachunguza mawazo na mambo yaliyo moyoni mwetu, sisi pia tunapaswa kufanya vivyohivyo. (Soma 1 Mambo ya Nyakati 28:9.) Ikiwa tunatambua kwamba tunahitaji kufanya mabadiliko fulani katika malengo yetu, mtazamo, au njia yetu ya kufikiri, tunapaswa kumwomba Yehova atusaidie kufanya mabadiliko hayo. Sasa ndiyo wakati wa kujitayarisha kwa ajili ya majaribu yaliyo mbele yetu. Usiruhusu chochote kikuzuie kutumia kwa hekima kipindi cha amani unachofurahia!

WIMBO 62 Wimbo Mpya

^ fu. 5 Je, unaishi katika nchi ambayo unaweza kumwabudu Mungu kwa uhuru? Ikiwa ndivyo, unatumiaje kipindi hicho chenye amani? Makala hii itakusaidia kuona jinsi unavyoweza kumwiga Mfalme Asa wa Yuda na Wakristo wa karne ya kwanza. Walitumia kwa hekima kipindi kilichokuwa na amani.

^ fu. 3 UFAFANUZI WA MANENO: Neno “amani” lina maana pana zaidi ya kutokuwa na vita. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa kuwa amani, pia linatokeza wazo la kuwa na afya njema, usalama, na hali njema.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Mfalme Asa alimnyang’anya nyanya yake cheo chake kwa sababu aliendeleza ibada ya uwongo. Watu washikamanifu waliomuunga mkono Asa walifuata mfano wake na kuziharibu sanamu.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Wenzi wa ndoa wenye bidii wanarahisisha maisha yao ili wakatumikie mahali palipo na uhitaji mkubwa wa wahubiri.