Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 37

“Usipumzishe Mkono Wako”

“Usipumzishe Mkono Wako”

“Panda mbegu zako asubuhi na usipumzishe mkono wako mpaka jioni.”—MHU. 11:6.

WIMBO 68 Kupanda Mbegu ya Ufalme

MUHTASARI *

1-2. Kuna uhusiano gani kati ya Mhubiri 11:6 na kuhubiri habari njema ya Ufalme?

KATIKA baadhi ya nchi, watu huitikia kwa njia nzuri wanaposikia habari njema. Wamekuwa wakisubiri kwa hamu habari hizo! Katika nchi nyingine, watu hawapendezwi na habari za Mungu au Biblia. Kwa kawaida watu huitikiaje katika eneo lako? Haidhuru watu wanaitikiaje, Yehova anatarajia tuendelee kuhubiri hadi atakaposema kazi hiyo imekamilika.

2 Tayari Yehova amepanga wakati ambapo kazi ya kuhubiri itakamilika, na ndipo “ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14, 36) Kabla ya wakati huo, tunaweza kutii jinsi gani maneno haya, “usipumzishe mkono wako”? *Soma Mhubiri 11:6.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Makala iliyotangulia ilizungumzia mambo manne tunayohitaji kufanya ili tuwe “wavuvi wa watu” wenye matokeo. (Mt. 4:19) Makala hii itazungumzia njia tatu zinazoweza kutusaidia kuimarisha azimio letu la kuendelea kuhubiri, haidhuru tunakabili hali gani. Tutajifunza kwa nini ni muhimu (1) tukazie fikira kazi yetu ya kuhubiri, (2) tuwe na subira, na (3) tudumishe imani yenye nguvu.

KAZIA FIKIRA KAZI YA KUHUBIRI

4. Kwa nini tunahitaji kukazia fikira kazi ambayo Yehova ametupatia?

4 Yesu alitabiri kuhusu matukio na hali ambazo zingekuwepo katika siku za mwisho na ambazo zingewakengeusha wafuasi wake na kuwafanya waache kukazia fikira kazi ya kuhubiri. Aliwahimiza wafuasi wake ‘waendelee kukesha.’ (Mt. 24:42) Leo, tunakabiliana na mambo yanayofanana na yale yaliyowazuia watu wa siku za Noa kukazia fikira onyo lililotolewa na Noa. (Mt. 24:37-39; 2 Pet. 2:5) Hivyo, tungependa kukazia fikira kazi ambayo Yehova ametupatia tufanye.

5. Andiko la Matendo 1:6-8 linafafanuaje jinsi ambavyo kazi ya kuhubiri ingeenea?

5 Leo, tunahitaji kukazia sana fikira kazi ya kuhubiri habari njema za Ufalme. Yesu alitabiri kwamba kazi hiyo ingefanywa kwa kiwango kikubwa zaidi na kuendelea kwa muda mrefu baada ya kifo chake. (Yoh. 14:12) Baada ya Yesu kufa, baadhi ya wanafunzi wake walirudia kazi yao ya uvuvi. Baada ya kufufuliwa, Yesu alifanya muujiza na kuwasaidia baadhi ya wanafunzi wake kuvua samaki wengi. Alitumia fursa hiyo kukazia kwamba mgawo wao wa kuwa wavuvi wa watu ulikuwa muhimu kuliko kazi nyingine yoyote. (Yoh. 21:15-17) Muda mfupi kabla ya kwenda mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba kazi ya kutoa ushahidi ingeenea hadi nje ya mipaka ya Israeli. (Soma Matendo 1:6-8.) Miaka mingi baadaye, Yesu alimpa mtume Yohana maono ili kumwonyesha mambo ambayo yangetukia katika “siku ya Bwana.” * Miongoni mwa mambo ambayo Yohana aliona ni tukio hili lenye kustaajabisha: Chini ya mwongozo wa malaika, “habari njema ya milele” ilikuwa ikihubiriwa “kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 1:10; 14:6) Ni wazi kuwa leo mapenzi ya Yehova ni kwamba anataka tushiriki katika kazi hii kubwa ya kutoa ushahidi mpaka itakapokamilika.

6. Tunaweza kuendelea kukazia fikira kazi ya kuhubiri jinsi gani?

6 Tunaweza kuendelea kukazia fikira kazi ya kuhubiri ikiwa tunatafakari kuhusu mambo yote ambayo Yehova anafanya ili kutusaidia. Kwa mfano, anatuandalia chakula kingi cha kiroho kupitia machapisho, kwa njia ya kielektroni, video, rekodi za sauti, na JW Broadcasting. Fikiria jambo hili: Katika tovuti yetu rasmi, habari zinapatikana katika lugha zaidi ya 1000! (Mt. 24:45-47) Katika ulimwengu huu uliogawanyika kisiasa, kidini, na kiuchumi, watumishi wa Mungu zaidi ya milioni nane wana umoja wa kweli katika undugu wao wa ulimwenguni pote. Kwa mfano, Ijumaa Aprili 19, 2019, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote waliungana pamoja kuzungumzia andiko la siku. Jioni hiyo umati wa watu 20,919,041 walikusanyika ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Tunachochewa kuendelea kukazia fikira kazi ya Ufalme tunapotafakari pendeleo letu la kujionea na kuwa sehemu ya muujiza huo wa siku zetu.

Yesu hakuruhusu chochote kimkengeushe kutoka kwenye kazi ya kutoa ushahidi kuhusu kweli (Tazama fungu la 7)

7. Mfano wa Yesu unatusaidiaje kuendelea kukazia fikira kazi yetu?

7 Njia nyingine tunayoweza kuendelea kukazia fikira kazi ya kuhubiri ni kwa kuiga mfano wa Yesu. Hakuruhusu chochote kimkengeushe kutoka kwenye kazi ya kutoa ushahidi kuhusu kweli. (Yoh. 18:37) Hakushawishiwa Shetani alipoahidi kumpa “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo”; wala hakushawishiwa watu walipomkamata na kutaka kumfanya awe mfalme. (Mt. 4:8, 9; Yoh. 6:15) Hakukengeushwa na tamaa ya kutaka utajiri; wala hakutishwa na upinzani mkali. (Luka 9:58; Yoh. 8:59) Imani yetu inapojaribiwa, tunaweza kuendelea kukazia fikira kazi yetu ikiwa tutakumbuka shauri la mtume Paulo. Aliwahimiza Wakristo waige mfano wa Yesu ili ‘wasichoke na kukata tamaa’!—Ebr. 12:3.

UWE NA SUBIRA

8. Subira ni nini, na kwa nini ni muhimu sana leo?

8 Subira ni uwezo wa kungojea kwa utulivu hadi hali zitakapobadilika. Tunahitaji kuwa na subira, iwe tunatarajia kwa hamu mwisho wa hali mbaya tunayokabili, au utimizo wa jambo fulani ambalo tumelitarajia kwa muda mrefu. Nabii Habakuki alingojea kwa muda mrefu mwisho wa ujeuri uliokuwa ukiendelea Yuda. (Hab. 1:2) Wanafunzi wa Yesu walitarajia kwamba Ufalme “ungetokea ghafla,” na ungewakomboa kutokana na ukandamizaji wa Waroma. (Luka 19:11) Tunasubiri kwa hamu siku ambayo Ufalme wa Mungu utaondoa uovu na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. (2 Pet. 3:13) Hata hivyo, tunahitaji kusubiri hadi wakati uliowekwa na Yehova ufike. Fikiria baadhi ya njia ambazo Yehova anatumia ili kutufundisha kuwa na subira.

9. Ni mifano gani inayoonyesha subira ya Yehova?

9 Yehova ametuwekea mfano mzuri inapohusu subira. Alimpa Noa wakati wa kutosha kujenga safina na kuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Pet. 2:5; 1 Pet. 3:20) Yehova alimsikiliza Abrahamu alipomuuliza tena na tena kuhusu uamuzi wake wa kuwaharibu wakaaji wa majiji yenye uovu ya Sodoma na Gomora. (Mwa. 18:20-33) Kwa karne nyingi, Yehova alilionyesha subira ya pekee taifa la Israeli lililokosa uaminifu. (Neh. 9:30, 31) Leo, tunaona uthibitisho wa subira ya Yehova anapowapa fursa ya ‘kufikia toba’ wale wote aliowavuta kwake. (2 Pet. 3:9; Yoh. 6:44; 1 Tim. 2:3, 4) Mfano wa Yehova unatupatia sababu nzuri ya kuonyesha subira tunapoendelea kuhubiri na kufundisha. Pia, anatufundisha kuonyesha subira kupitia mfano fulani unaopatikana katika Neno lake.

Kama mkulima mwenye bidii lakini mwenye subira, tunangojea matokeo ya jitihada zetu (Tazama fungu la 10 na 11)

10. Mfano wa mkulima kwenye andiko la Yakobo 5:7, 8, unatufundisha nini?

10 Soma Yakobo 5:7, 8Mfano wa mkulima anayepanda mazao unatufundisha jinsi ya kuwa na subira. Ni kweli kwamba baadhi ya mimea inakua haraka sana. Hata hivyo, mimea mingi, hasa ile inayozaa matunda, inachukua muda mrefu zaidi kukomaa. Msimu wa kilimo katika Israeli ulikuwa na urefu wa miezi sita hivi. Mkulima alipanda mbegu zake baada ya mvua za mapema katika majira ya majani kupukutika, na alivuna nafaka baada ya mvua za mwisho katika majira ya kuchipua. (Marko 4:28) Tutakuwa wenye hekima ikiwa tutaiga subira ya mkulima. Hata hivyo, huenda isiwe rahisi kufanya hivyo.

11. Sifa ya subira itatusaidiaje katika huduma yetu?

11 Kwa kawaida, wanadamu wasio wakamilifu wanataka kuona matokeo ya kazi yao papo hapo. Hata hivyo, ikiwa tunataka bustani yetu izae matunda ni lazima tuitunze kwa ukawaida—tuilime, tupande, tupalilie, na kuimwagilia maji. Pia, kazi ya kufanya wanafunzi inahitaji jitihada endelevu. Inachukua muda ili kuwasaidia wale tunaowafundisha wang’oe mielekeo yoyote ya ubaguzi na ya kutowajali wengine iliyo kama magugu. Subira itatusaidia tusivunjike moyo watu wasipotusikiliza. Hata ikiwa baadhi ya watu wanaitikia vizuri, bado ni lazima tuwe na subira. Hatuwezi kumlazimisha mwanafunzi wa Biblia asitawishe imani. Nyakati nyingine, hata wanafunzi wa Yesu walichukua muda mrefu kuelewa maana ya mambo aliyofundisha. (Yoh. 14:9) Acheni tukumbuke kwamba huenda sisi tukapanda na kutia maji, lakini Mungu ndiye anayeikuza.—1 Kor. 3:6.

12. Tunaweza kuonyeshaje subira tunapowahubiria watu wa ukoo wasio Mashahidi?

12 Huenda ikawa vigumu kuonyesha subira tunapowahubiria watu wa ukoo ambao si Mashahidi. Kanuni inayopatikana kwenye Mhubiri 3:1, 7 inaweza kutusaidia. Inasema hivi: “Kuna . . . wakati wa kunyamaza na wakati wa kuongea.” Tunaweza kuhubiri kupitia mwenendo wetu mzuri, hata hivyo sikuzote tuko macho kutumia fursa tunazopata kuzungumza na wengine kuhusu kweli. (1 Pet. 3:1, 2) Tunapohubiri na kufundisha kwa bidii tunawaonyesha subira watu wote, kutia ndani watu wa familia ambao si Mashahidi.

13-14. Tunaweza kuiga mifano gani ya wale walioonyesha subira?

13 Tunaweza kujifunza kuwa na subira kupitia mifano ya watu waaminifu wa nyakati za Biblia na wa siku zetu. Habakuki alitamani sana kuona mwisho wa uovu, lakini alisema hivi kwa uhakika: “Nitaendelea kusimama katika kituo changu cha ulinzi.” (Hab. 2:1) Mtume Paulo alieleza kuhusu hamu yake ya kutoka moyoni kwamba alitamani ‘kumaliza’ huduma yake na kupata thawabu yake ya mbinguni. Hata hivyo, aliendelea “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema” kwa subira.—Mdo. 20:24.

14 Fikiria mfano wa wenzi wa ndoa ambao walihitimu kutoka Shule ya Gileadi na kupewa mgawo katika nchi ambayo Mashahidi wa Yehova ni wachache, na ambako dini kuu ya nchi hiyo si Ukristo. Watu wengi hawakupenda kujifunza Biblia. Tofauti na wenzi hao, wanadarasa wenzao waliokuwa wakitumikia katika nchi nyingine, walikuwa wakiwatumia ripoti za mafunzo mengi ya Biblia waliyoongoza, yaliyokuwa yakifanya maendeleo. Lakini wenzi hao wa ndoa waliendelea kuhubiri kwa subira licha ya kwamba watu wengi katika eneo lao hawakusikiliza. Baada ya kuhubiri kwa miaka nane katika eneo lililoonekana kuwa halina matokeo, hatimaye walipata shangwe kwa kuona mmoja wa wanafunzi wao wa Biblia akibatizwa. Mifano hiyo ya zamani na ya sasa inatufundisha nini? Watu hao waaminifu hawakuwa goigoi, wala hawakuruhusu mkono wao upumzike, na Yehova aliwathawabisha kwa sababu ya subira yao. Walikuwa “waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Ebr. 6:10-12.

DUMISHA IMANI YENYE NGUVU

15. Imani inaimarishaje azimio letu la kuhubiri?

15 Tunaamini ujumbe tunaohubiri, hivyo tunatamani kushiriki ujumbe huo na watu wengi kadiri iwezekanavyo. Tunaamini ahadi zinazopatikana katika Neno la Mungu. (Zab. 119:42; Isa. 40:8) Tumeona unabii wa Biblia ukitimia katika siku zetu. Tumeshuhudia jinsi maisha ya watu yanavyobadilika na kuwa bora wanapoanza kutumia shauri la Biblia. Uthibitisho huo unaimarisha uhakika wetu kwamba kila mtu anahitaji kusikia habari njema za Ufalme.

16. Kulingana na Zaburi 46:1-3, imani katika Yehova na Yesu inaweza kuimarishaje azimio letu la kuhubiri?

16 Pia, tunamwamini Yehova, Chanzo cha ujumbe tunaohubiri, na tunamwamini yule aliyewekwa rasmi kuwa Mfalme wa Ufalme, Yesu. (Yoh. 14:1) Licha ya hali zozote tutakazokabili, sikuzote Yehova atakuwa kimbilio letu na nguvu zetu. (Soma Zaburi 46:1-3.) Pia, tuna hakika kwamba Yesu anaongoza kazi ya kuhubiri akiwa mbinguni, akitumia nguvu na mamlaka kutoka kwa Yehova.—Mt. 28:18-20.

17. Toa mfano unaoonyesha kwa nini tunapaswa kuendelea kuhubiri.

17 Imani huimarisha uhakika wetu kwamba Yehova atabariki jitihada zetu, na nyakati nyingine kwa njia tusiyoitarajia. (Mhu. 11:6) Kwa mfano, kila siku maelfu ya watu hupita na kuona machapisho yetu kwenye vigari na meza za machapisho. Je, njia hiyo ya kuhubiri ina matokeo? Bila shaka! Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba 2014 iliripoti kwamba msichana mmoja wa chuo kikuu alitaka kuandika insha kuhusu Mashahidi wa Yehova. Hakufanikiwa kupata Jumba la Ufalme, lakini aliona meza ya machapisho kwenye eneo la chuo, na pia alifanikiwa kupata habari alizokuwa akihitaji kwa ajili ya insha yake. Mwishowe, akawa Shahidi aliyebatizwa ambaye sasa anatumikia akiwa painia wa kawaida. Mambo kama hayo yaliyoonwa yanatuchochea tuendelee kuhubiri kwa sababu yanafunua kwamba bado kuna watu wanaohitaji kupata na kusikia ujumbe wa Ufalme.

AZIMIA KUTOPUMZISHA MKONO WAKO

18. Kwa nini tuna hakika kwamba kazi ya kuhubiri Ufalme itakamilika kama Yehova alivyokusudia?

18 Tunaweza kuwa na hakika kwamba kazi ya kuhubiri Ufalme itakamilika kwa wakati mwafaka. Fikiria kilichotokea katika siku za Noa. Yehova alionyesha kwamba Yeye ni Mtunza Wakati mkamilifu. Miaka 120 hivi mapema, Yehova aliweka wakati ambao Gharika ingeanza. Miaka mingi baadaye, Yehova alimwamuru Noa ajenge Safina. Miaka 40 au 50 hivi kabla ya Gharika kuanza, Noa aliendelea kufanya kazi kwa bidii. Licha ya kwamba watu hawakumsikiliza, aliendelea kuhubiri ujumbe wa onyo hadi Yehova aliposema kwamba wakati wa kuingiza wanyama kwenye safina umefika. Kisha, kwa wakati mwafaka “Yehova akaufunga mlango.”—Mwa. 6:3; 7:1, 2, 16.

19. Tunaweza kutazamia nini ikiwa hatutapumzisha mkono wetu?

19 Hivi karibuni Yehova atakamilisha kazi ya kuhubiri Ufalme; ‘ataufungia mlango’ mfumo wa mambo wa Shetani na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. Hadi wakati huo, acheni tumwige Noa, Habakuki, na wengine ambao hawakupumzisha mkono wao. Acheni tukazie fikira kazi ya kuhubiri, tuwe wenye subira na tudumishe imani yenye nguvu katika Yehova na ahadi zake.

WIMBO 75 “Mimi Hapa! Nitume Mimi!”

^ fu. 5 Makala iliyotangulia iliwatia moyo wanafunzi wa Biblia wanaofanya maendeleo wakubali mwaliko wa Yesu na kuwa wavuvi wa watu. Makala hii, itazungumzia njia tatu zitakazowasaidia wahubiri wote, iwe ni wapya au wenye uzoefu, kuimarisha azimio lao la kuendelea kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme hadi Yehova atakaposema imetosha.

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Katika makala hii, maneno “usipumzishe mkono wako” yanamaanisha kwamba tunahitaji kuazimia kuendelea kuhubiri habari njema hadi Yehova atakaposema kazi hiyo imekamilika.

^ fu. 5 “Siku ya Bwana” ilianza Yesu alipowekwa rasmi kuwa Mfalme mwaka 1914 na itaendelea hadi mwishoni mwa Utawala wake wa Miaka Elfu.