Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nimefurahia Kujifunza na Kuwafundisha Wengine Kumhusu Yehova

Nimefurahia Kujifunza na Kuwafundisha Wengine Kumhusu Yehova

NILIPOKUWA nikikua huko Easton, Pennsylvania, Marekani, nilikazia fikira kwenda chuo kikuu, nikiwa nimeazimia kufanikiwa maishani. Nilifurahia kujifunza na nilifanya vizuri kwenye somo la hesabu na sayansi. Mwaka wa 1956, shirika fulani la kutetea haki za kiraia lilinipa dola 25 kwa sababu nilipata alama za juu zaidi kati ya wanafunzi weusi. Baadaye, malengo yangu yalibadilika. Kwa nini?

JINSI NILIVYOJIFUNZA KUMHUSU YEHOVA

Mwanzoni mwa miaka ya 1940, wazazi wangu walijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ingawa waliacha kujifunza Biblia, mama yangu aliendelea kupokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Mwaka wa 1950, kusanyiko la kimataifa lilifanywa katika jiji la New York City, na familia yetu ilikubali mwaliko wa kuhudhuria.

Muda mfupi baada ya hapo, Ndugu Lawrence Jeffries alianza kututembelea. Alijitahidi kunisaidia nijifunze kweli. Mwanzoni, sikukubaliana naye kuhusu msimamo wa Mashahidi wa Yehova wa kutojihusisha na masuala ya kisiasa na kijeshi. Nilimwambia kwamba ikiwa kila mtu nchini Marekani angekataa kwenda vitani, maadui wangekuja na kuchukua nchi yote. Kwa subira, Ndugu Jeffries aliniuliza hivi: “Unafikiri Yehova Mungu angefanya nini ikiwa watu wote nchini Marekani wangekuwa wakimtumikia kisha maadui waje kuwashambulia? ” Maelezo yake kuhusu jambo hilo na mambo mengine yalinisaidia kuona kwamba maoni yangu hayakuwa sahihi. Hilo lilifanya nitamani kujifunza zaidi.

Siku niliyobatizwa

Nilitumia saa nyingi nikisoma matoleo ya zamani ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambayo mama yangu alikuwa amehifadhi. Baada ya muda, nilitambua kwamba nilikuwa nikijifunza kweli, basi nikakubali kujifunza Biblia pamoja na Ndugu Jeffries. Pia, nilianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Nilipenda mambo niliyojifunza, nami nikawa mhubiri wa habari njema. Nilibadili malengo yangu baada ya kuelewa kwamba ‘siku kuu ya Yehova ilikuwa karibu.’ (Sef. 1:14) Sikutamani tena kwenda chuo kikuu, badala yake, nilitaka kuwasaidia wengine wajifunze kweli za Biblia.

Nilimaliza masomo ya sekondari Juni 13, 1956, na siku tatu baadaye, nikabatizwa kwenye kusanyiko la mzunguko. Wakati huo, sikutambua kwamba ningepata baraka nyingi sana kwa kutumia maisha yangu kujifunza na kuwafundisha wengine kumhusu Yehova.

KUJIFUNZA NA KUFUNDISHA NIKIWA PAINIA

Miezi sita baada ya kubatizwa, niliwekwa rasmi kuwa painia wa kawaida. Huduma ya Ufalme ya Desemba 1956 ya Kiingereza ilikuwa na makala yenye kichwa, “Je, Unaweza Kutumikia Mahali Penye Uhitaji Mkubwa? ” Mwaliko huo ulinihusu mimi pia. Nilitaka kusaidia kwenye eneo lenye wahubiri wachache wa habari njema.​—Mt. 24:14.

Nilihamia huko Edgefield, South Carolina. Kutaniko la eneo hilo lilikuwa na wahubiri wanne tu. Nilipohamia idadi ikawa wahubiri watano. Tulifanya mikutano kwenye chumba cha mbele cha nyumba ya ndugu fulani. Kila mwezi, nilitumia saa 100 katika huduma ya shambani. Nilikuwa na shughuli nyingi kwa sababu niliongoza mikutano na kazi ya kuhubiri. Jambo la kupendeza ni kwamba kadiri nilivyofanya mengi, ndivyo nilivyojifunza mengi zaidi kumhusu Yehova.

Mwanamke fulani ambaye nilijifunza Biblia pamoja naye alimiliki sehemu ya kutunza maiti huko Johnston, mji uliokuwa umbali wa kilometa kadhaa. Kwa fadhili, alinipatia kazi ya muda ambayo nilihitaji sana na akaturuhusu tutumie jengo fulani dogo kama Jumba letu la Ufalme.

Ndugu Jolly Jeffries, mwana wa Ndugu ambaye alinifundisha Biblia, alihamia katika eneo hilo kutoka Brooklyn, New York, naye akawa painia mwenzangu. Tuliishi katika trela ndogo ambayo ndugu fulani alituazima.

Mishahara ilikuwa midogo katika maeneo ya kusini mwa Marekani. Tulilipwa dola mbili au tatu kwa kazi ya siku nzima. Siku moja, nilikuwa nimetumia kiasi cha mwisho cha pesa nilizokuwa nazo kununua chakula dukani. Nilipotoka dukani, mwanamume fulani alikuja na kuniuliza: “Unataka kazi? Nitakulipa dola moja kwa saa moja.” Alinipa kazi ya siku tatu ya kusafisha eneo fulani la ujenzi. Ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa akinisaidia ili niendelee kukaa huko Edgefield. Hata nilihudhuria kusanyiko la kimataifa la mwaka wa 1958 lililofanywa huko New York City.

Siku yetu ya harusi

Siku ya pili ya kusanyiko hilo, jambo la pekee lilitokea. Nilikutana na Ruby Wadlington, ambaye alikuwa akitumikia kama painia wa kawaida huko Gallatin, Tennessee. Kwa kuwa sote tulikuwa na tamaa ya kuwa wamishonari, tulihudhuria mkutano wa Gileadi kwenye kusanyiko hilo. Baadaye, tulianza kuandikiana barua. Kisha nikapewa mwaliko wa kutoa hotuba ya watu wote huko Gallatin. Nilitumia fursa hiyo kumwomba tufunge ndoa. Nilihamia kwenye kutaniko la akina Ruby, na tukafunga ndoa mwaka wa 1959.

KUJIFUNZA NA KUFUNDISHA KUTANIKONI

Nilipokuwa na umri wa miaka 23, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa kutaniko (sasa anaitwa mratibu wa baraza la wazee) huko Gallatin. Baada tu ya Ndugu Charles Thomspon kuwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko, alitembelea kutaniko letu. Alikuwa na uzoefu mwingi; ingawa hivyo, aliniuliza maoni yangu kuhusu mahitaji ya akina ndugu na jinsi waangalizi wengine wa mzunguko walivyoshughulikia mambo hayo. Nilijifunza kutoka kwake kwamba ni vizuri kuuliza maswali na kupata habari zote kabla ya kushughulikia jambo.

Mei 1964, nilialikwa kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme iliyofanywa kwa mwezi mmoja huko South Lansing, New York. Akina ndugu walioongoza shule hiyo walisitawisha ndani yangu tamaa kubwa ya kuendelea kujifunza mengi na kuwa Mkristo mkomavu.

KUJIFUNZA NA KUFUNDISHA NIKIWA MWANGALIZI WA MZUNGUKO NA WA WILAYA

Januari 1965, mimi na Ruby tulipokea mwaliko wa kufanya kazi ya kuzungukia makutaniko. Tulipewa mgawo wa mzunguko wenye eneo kubwa sana, kuanzia Knoxville, Tennessee, mpaka karibu na Richmond, Virginia. Ulitia ndani makutaniko ya huko North Carolina, Kentucky, na West Virginia. Nilitumikia katika makutaniko ya ndugu weusi kwa sababu wakati huo kulikuwa na ubaguzi wa rangi kusini mwa Marekani, basi watu weusi hawangeweza kukutana na weupe. Akina ndugu walikuwa maskini na tulijifunza kushiriki pamoja nao kile tulichokuwa nacho. Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliyekuwa ametumikia kwa muda mrefu alinifundisha somo hili muhimu: “Uwe ndugu. Unapofika kutanikoni usitende kama bosi, utafaulu kuwasaidia ikiwa watakuona kama ndugu yao.”

Tulipokuwa tukitembelea kutaniko moja dogo, Ruby alianzisha funzo na mwanamke kijana aliyekuwa na binti mwenye umri wa mwaka mmoja. Wakati ambapo hakukuwa na mtu wa kuongoza funzo hilo kutanikoni, Ruby aliongoza kupitia barua. Kwenye ziara yetu iliyofuata, mwanamke huyo alihudhuria kila mkutano. Dada wawili mapainia wa pekee walipohamia katika kutaniko hilo, waliendelea kujifunza naye na baada ya muda mfupi akabatizwa. Miaka 30 baadaye, mwaka wa 1995, kwenye Betheli ya Patterson, dada fulani kijana alikuja na kujitambulisha kwa Ruby. Alikuwa binti ya yule mwanamke ambaye Ruby alijifunza naye. Binti huyo na mume wake walikuwa wanafunzi wa darasa la 100 la Shule ya Gileadi.

Mgawo wetu wa pili wa kuzungukia makutaniko ulikuwa Florida ya kati. Wakati huo, tulihitaji gari, basi tukanunua gari fulani kwa bei nzuri sana. Hata hivyo, juma la kwanza, gari lilipata tatizo kwenye injini. Hatukuwa tumebaki na pesa zozote za kulirekebisha. Nilimpigia simu ndugu ambaye nilifikiri angeweza kutusaidia. Alimtuma mfanyakazi wake mmoja arekebishe gari na alikataa tumlipe kwa kazi hiyo. Alisema, “Siwadai chochote.” Hata alitupatia zawadi ya pesa! Huo ulikuwa mfano mzuri sana wa jinsi Yehova anavyowatunza watumishi wake. Ulitukumbusha kwamba tunapaswa kuwaonyesha wengine ukarimu.

Kila mara tulipotembelea kutaniko fulani, tulikaa nyumbani kwa akina ndugu. Matokeo ni kwamba, tulipata marafiki wengi wazuri. Siku moja, niliondoka na kuacha kwenye mashine ya kuchapa, ripoti niliyokuwa nikiandika kuhusu kutaniko. Niliporudi jioni hiyo, nilikuta kwamba mwana mwenye umri wa miaka mitatu wa familia hiyo alikuwa “amenisaidia” kukamilisha kuchapa ripoti hiyo. Nilimtania kuhusu jambo hilo kwa miaka mingi.

Mwaka wa 1971, nilipokea barua ya kuwekwa rasmi kutumikia kama mwangalizi wa wilaya huko New York City. Tulishtuka sana! Tulipohamia huko, nilikuwa na umri wa miaka 34 tu. Nilikuwa mwangalizi wao wa kwanza wa wilaya mweusi, na akina ndugu walinikaribisha kwa uchangamfu sana.

Nikiwa mwangalizi wa wilaya nilifurahia kuwafundisha watu kumhusu Yehova kila mwisho juma kwenye kusanyiko la mzunguko. Waangalizi wengi wa mzunguko walikuwa na uzoefu mwingi kuliko mimi. Mmoja wao alitoa hotuba yangu ya ubatizo. Ndugu mwingine, Theodore Jaracz, baadaye alikuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Pia, kulikuwa na ndugu wengine wengi wenye uzoefu waliotumikia katika Betheli ya Brooklyn. Nilifurahi sana kwamba waangalizi wa mzunguko na Wanabetheli walifanya nijihisi huru. Nilijionea mwenyewe kwamba walikuwa wachungaji wenye upendo, ambao walitegemea Neno la Mungu na kuunga mkono tengenezo kwa ushikamanifu. Unyenyekevu wao ulifanya iwe rahisi kwangu kutumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya.

KURUDI KWENYE KAZI YA MWANGALIZI WA MZUNGUKO

Mwaka wa 1974, Baraza Linaloongoza liliweka rasmi kikundi kingine cha waangalizi wa mzunguko wawe waangalizi wa wilaya, nami nikapewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko tena​—wakati huu huko South Carolina. Jambo la kufurahisha ni kwamba wakati huo, akina ndugu weusi na weupe waliruhusiwa kuchangamana katika makutaniko na mizunguko, akina ndugu walifurahi sana.

Mwishoni mwa mwaka wa 1976, nilipewa mgawo wa kutumikia kwenye mzunguko wa Georgia ulio kati ya Atlanta na Columbus. Ninakumbuka nilipotoa hotuba ya mazishi ya watoto watano weusi waliokufa baada ya mtu fulani kuchoma nyumba yao moto. Mama yao alilazwa hospitalini kwa sababu ya majeraha aliyopata. Mashahidi wa Yehova, weusi kwa weupe, walimiminika hospitalini ili kuwafariji wazazi hao. Nilijionea jinsi akina ndugu walivyoonyesha upendo kwa njia kubwa sana. Kuonyeshana huruma kwa njia hiyo kunaweza kuwasaidia watumishi wa Mungu wavumilie hali ngumu zaidi maishani.

KUJIFUNZA NA KUFUNDISHA BETHELI

Mwaka wa 1977, tulialikwa kwenye Betheli ya Brooklyn kwa miezi michache ili kusaidia kwenye mradi fulani. Tulipokuwa karibu kumaliza mradi huo, washiriki wawili wa Baraza Linaloongoza walikutana pamoja nami na kuniuliza ikiwa mimi na Ruby tungekuwa tayari kuwa Wanabetheli wa kudumu. Tulikubali mwaliko huo.

Kwa miaka 24, nilitumikia katika Idara ya Utumishi, ambako mara nyingi akina ndugu hushughulikia maswali magumu yenye utata. Kwa miaka mingi, Baraza Linaloongoza limeandaa mwongozo unaopatana na kanuni za Biblia. Mwongozo huo hutumiwa kama msingi wa kujibu maswali, na pia ndio msingi wa mazoezi ya waangalizi wa mzunguko, wazee, na mapainia. Mazoezi hayo, yamewasaidia wengi wawe wakomavu kiroho. Na jambo hilo limeimarisha tengenezo la Yehova.

Tangu mwaka wa 1995 hadi 2018, nilitembelea ofisi mbalimbali za tawi nikiwa mwakilishi wa makao mkuu, ambaye zamani aliitwa mwangalizi wa eneo la dunia. Nilikutana na washiriki wa Halmashauri za Tawi, Wanabetheli, na wamishonari ili kuwatia moyo na kushughulikia matatizo yoyote waliyokuwa nayo. Mimi na Ruby sikuzote tumetiwa moyo na mambo tuliyosimuliwa na akina ndugu. Kwa mfano, mwaka wa 2000 tulitembelea nchi ya Rwanda. Tuliguswa moyo kusikia jinsi akina ndugu na familia ya Betheli walivyookoka mauaji ya mwaka wa 1994. Wengi walipoteza wapendwa wao. Licha ya hali ngumu walizopitia, akina ndugu walionyesha imani, tumaini, na shangwe.

Kuadhimisha miaka 50 ya ndoa yetu

Sasa tuna umri wa miaka 80 na kitu. Kwa miaka 20 iliyopita, nimetumikia kwenye Halmashauri ya Tawi ya Marekani. Sikupata elimu ya chuo kikuu, ingawa hivyo, nimepata elimu bora zaidi kutoka kwa Yehova na tengenezo lake. Elimu hiyo imenisaidia kuwafundisha wengine kweli za Biblia ambazo zinaweza kuwanufaisha milele. (2 Kor. 3:5; 2 Tim. 2:2) Nimejionea jinsi ambavyo ujumbe wa Biblia umewasaidia watu waboreshe maisha yao na kusitawisha uhusiano mzuri pamoja na Muumba wao. (Yak. 4:8) Kila tunapopata fursa, mimi na Ruby tunaendelea kuwatia moyo wengine wathamini pendeleo la kujifunza kumhusu Yehova na kuwafundisha wengine kweli za Biblia, na hilo ndilo pendeleo kubwa zaidi ambalo mtumishi wa Yehova anaweza kupata!