Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni nani watakaofufuliwa duniani, na watapata ufufuo wa aina gani?

▪ Fikiria jinsi Biblia inavyojibu maswali hayo.

Andiko la Matendo 24:15 linasema kwamba “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Waadilifu ni wale ambao kabla ya kufa walimtii Mungu, basi majina yao yameandikwa katika kitabu cha uzima. (Mal. 3:16) Wasio waadilifu wanatia ndani wale ambao walikufa bila kupata nafasi ya kutosha kujifunza kumhusu Yehova, basi majina yao hayajaandikwa katika kitabu cha uzima.

Andiko la Yohana 5:28, 29 linarejelea vikundi viwili vinavyotajwa kwenye Matendo 24:15. Yesu alisema kwamba “wale waliotenda mema” watapata “ufufuo wa uzima, na wale waliozoea kutenda maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” Waadilifu walitenda mambo mazuri kabla ya kufa. Watapata ufufuo wa uzima kwa sababu majina yao bado yameandikwa katika kitabu cha uzima. Hata hivyo, wasio waadilifu walizoea kutenda maovu kabla ya kufa. Watapata ufufuo wa hukumu. Bado majina yao hayajaandikwa katika kitabu cha uzima, na watapitia kipindi cha hukumu ambapo matendo yao yatachunguzwa na kupimwa. Katika kipindi hicho, watapata nafasi ya kujifunza kumhusu Yehova na majina yao kuandikwa katika kitabu cha uzima.

Andiko la Ufunuo 20:12, 13 linaeleza kwamba wote watakaofufuliwa watahitaji kutii “mambo yaliyoandikwa katika vile vitabu” vya kukunjwa, yaani, sheria mpya ambazo zitaanza kutumiwa katika ulimwengu mpya. Wale ambao watakosa kutii wataondolewa.​—Isa. 65:20.

Andiko la Danieli 12:2 lilitabiri kwamba baadhi ya wale waliolala usingizi katika kifo wataamka na kupata “uzima wa milele na wengine watapata shutuma na chuki ya milele.” Mstari huo, unazungumzia matokeo ya mwisho kwa wale watakaofufuliwa, yaani, “uzima wa milele” au “chuki ya milele.” Basi, mwishoni mwa ile miaka 1,000, baadhi ya watu watapata uzima wa milele na wengine wataangamizwa milele.​—Ufu. 20:15; 21:3, 4.

Fikiria mfano ufuatao. Hali ya vikundi hivyo viwili vitakavyofufuliwa inaweza kulinganishwa na mhamiaji anayetaka kuishi katika nchi nyingine. Waadilifu ni kama wageni wanaopata vibali vya kufanya kazi au vya kuishi nchini ambavyo vinawasaidia kutambuliwa na kuwa na uhuru wa kadiri fulani. Kinyume chake, wasio waadilifu ni kama wageni wanaopata vibali vya muda au vibali vya kutembelea nchi. Wageni kama hao wanahitaji kuthibitisha kwamba wanastahili kabla ya kuruhusiwa kuendelea kuishi katika nchi hiyo mpya. Vivyo hivyo, wasio waadilifu watakaofufuliwa watahitaji kutii sheria za Yehova na kuthibitisha kwamba ni waadilifu ili waendelee kuishi katika Paradiso. Na hata iwe wageni wanapata vibali gani wanapoingia kwa mara ya kwanza katika nchi, mwishowe huenda baadhi yao wakapata uraia na wengine wakaondolewa nchini. Uamuzi wa mwisho utategemea mtazamo wao na mwenendo wao katika nchi waliyohamia. Vivyo hivyo, uamuzi wa mwisho kuhusu wale watakaofufuliwa utategemea uaminifu na mwenendo wao katika ulimwengu mpya.

Yehova ni Mungu mwenye huruma na pia Mungu wa haki ambaye hana upendeleo. (Kum. 32:4; Zab. 33:5) Ataonyesha upendo wake kwa kuwafufua waadilifu na wasio waadilifu pia. Wakati huohuo atadumisha viwango vyake vya juu vya maadili. Ni wale tu watakaojifunza kumpenda na kuishi kulingana na viwango vyake ndio watakaoruhusiwa kuendelea kuishi katika ulimwengu mpya.