Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 41

Masomo Tunayojifunza Katika Barua Mbili za Petro

Masomo Tunayojifunza Katika Barua Mbili za Petro

“Sikuzote ninakusudia kuwakumbusha mambo haya.”—2 PET. 1:12.

WIMBO 127 Napaswa Kuwa Mtu wa Namna Gani

MUHTASARI a

1. Muda mfupi kabla ya kifo chake, mtume Petro aliongozwa na roho kufanya nini?

 MTUME Petro alijua kwamba alikuwa anakaribia kufa. Katika kipindi cha miaka mingi ambacho alitumikia kwa uaminifu, alishirikiana na Yesu, alianza kuhubiri katika maeneo mapya, na akatumikia akiwa mshiriki wa baraza linaloongoza. Lakini bado alikuwa na kazi ya kufanya. Karibu mwaka wa 62-64 W.K., aliongozwa na roho kuandika barua mbili—kitabu cha 1 na cha 2 cha Petro katika Biblia. Petro alitumaini kwamba barua hizo zingewasaidia Wakristo baada ya kifo chake.—2 Pet. 1:​12-15.

2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba barua za Petro ziliandikwa kwa wakati unaofaa?

2 Petro aliandika barua zake zilizoongozwa na roho wakati ambao Wakristo wenzake walikuwa ‘wamehuzunishwa kwa majaribu mbalimbali.’ (1 Pet. 1:6) Watu waovu walikuwa wakijaribu kuingiza mafundisho ya uwongo na mwenendo usio safi kutanikoni. (2 Pet. 2:​1, 2, 14) Baada ya muda mfupi Wakristo waliokuwa wakiishi huko Yerusalemu, wangekabili “mwisho wa mambo yote,” yaani, jeshi la Waroma lingeharibu jiji hilo na mifumo ya mambo ya Wayahudi. (1 Pet. 4:7) Bila shaka, barua za Petro ziliwasaidia Wakristo watambue mambo ambayo wangeweza kufanya ili kuvumilia majaribu waliyokabili wakati huo na ya wakati ujao. b

3. Kwa nini tunapaswa kuchunguza barua za Petro zilizoongozwa na roho?

3 Ingawa Petro aliwaandikia barua Wakristo wa karne ya kwanza, Yehova alitia ndani barua hizo katika Neno Lake. Basi, leo tunaweza kunufaika na barua hizo. (Rom. 15:4) Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu unaoendeleza mwenendo usio safi, sisi pia tunakabili majaribu ambayo yanaweza kufanya iwe vigumu kwetu kumtumikia Yehova. Isitoshe, hivi karibuni tutakabili dhiki kubwa zaidi kuliko ile ambayo ilisababisha mwisho wa mifumo ya mambo ya Wayahudi. Tunapata vikumbusho muhimu katika barua mbili za Petro. Mambo hayo yatatusaidia kuendelea kutarajia siku ya Yehova, kushinda woga wa wanadamu, na kusitawisha upendo mwingi kati yetu. Pia, vikumbusho hivyo vinaweza kuwasaidia wazee wa kutaniko waone jinsi wanavyoweza kufanikiwa kushughulikia mahitaji ya ndugu na dada kutanikoni.

ENDELEA KUTARAJIA

4. Kama andiko la 2 Petro 3:​3, 4 linavyoonyesha, ni nini kinachoweza kutikisa imani yetu?

4 Tumezungukwa na watu ambao hawaamini unabii wa Biblia. Huenda wapinzani wakatudhihaki kwa sababu kwa miaka mingi tumekuwa tukisema kwamba mwisho unakaribia. Baadhi ya watu husema kwamba mwisho hautakuja kamwe. (Soma 2 Petro 3:​3, 4.) Tukisikia maneno kama hayo kutoka kwa mtu tunayemhubiria, mfanyakazi mwenzetu, au mtu wa familia yetu, imani yetu inaweza kutikiswa. Petro alieleza jambo linaloweza kutusaidia.

5. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo? (2 Petro 3:​8, 9)

5 Huenda baadhi ya watu wakahisi kwamba Yehova anakawia kuleta mwisho wa mfumo huu wa mambo. Maneno ya Petro yanaweza kutusaidia kudumisha mtazamo unaofaa, kwa sababu yanatukumbusha kwamba maoni ya Yehova kuhusu wakati yanatofautiana sana na maoni ya wanadamu. (Soma 2 Petro 3:​8, 9.) Kwa Yehova miaka elfu ni kama siku moja. Yehova ni mwenye subira kwa sababu hataki yeyote aangamizwe. Hata hivyo, mfumo huu utafikia mwisho, siku yake itakapofika. Tuna pendeleo la kutumia wakati uliobaki kuwahubiria watu wa mataifa yote.

6. Tunaendeleaje “kuweka karibu akilini” siku ya Yehova? (2 Petro 3:​11, 12)

6 Petro anatuhimiza tuweke “karibu akilini” siku ya Yehova. (Soma 2 Petro 3:​11, 12.) Tunawezaje kufanya hivyo? Ikiwezekana kila siku tunapaswa kutafakari kuhusu baraka tutakazofurahia katika ulimwengu mpya. Jiwazie ukipumua hewa safi kabisa, ukila chakula chenye lishe, ukiwakaribisha wapendwa wako baada ya kufufuliwa, na kuwafundisha watu walioishi karne nyingi zamani kuhusu utimizo wa unabii wa Biblia. Kutafakari kwa njia hiyo kutakusaidia kuendelea kutarajia wakati huo, na kuwa na uhakika kwamba hizi ni siku za mwisho. ‘Tukiwa na ujuzi huu wa mapema’ kuhusu wakati wetu ujao, ‘hatutapotoshwa’ na walimu wa uwongo.—2 Pet. 3:17.

SHINDA WOGA WA WANADAMU

7. Tunawezaje kuathiriwa na woga wa wanadamu?

7 Tunapoweka karibu akilini siku ya Yehova, tunachochewa kuwahubiria wengine habari njema. Hata hivyo, huenda wakati mwingine tukasita kufanya hivyo. Kwa nini? Huenda pindi fulani tukalemewa na woga wa wanadamu. Petro alipatwa na jambo hilo. Usiku ambao kesi ya Yesu ilifanywa, Petro aliogopa kujitambulisha kuwa mmoja wa wanafunzi wa Yesu na akakana mara kadhaa kwamba hamjui Yesu. (Mt. 26:​69-75) Hata hivyo, baadaye, mtume huyo alisema hivi kwa usadikisho: “Msiogope kile wanachokiogopa, wala msiwe na wasiwasi.” (1 Pet. 3:14) Maneno ya Petro yanatuhakikishia kwamba tunaweza kushinda woga wa wanadamu.

8. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda woga wa wanadamu? (1 Petro 3:15)

8 Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda woga wa wanadamu? Petro anatuambia hivi: “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu.” (Soma 1 Petro 3:15.) Hilo linatia ndani kutafakari cheo na mamlaka ya Bwana na Mfalme wetu, Kristo Yesu. Ikiwa unahisi wasiwasi au kuogopa unapopata nafasi ya kuwahubiria wengine habari njema, mkumbuke Mfalme wetu. Mwazie akitawala mbinguni akiwa amezungukwa na mamilioni ya malaika. Kumbuka kwamba ana “mamlaka yote mbinguni na duniani” na kwamba atakuwa ‘pamoja nawe sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.’ (Mt. 28:​18-20) Petro anatuhimiza ‘sikuzote tuwe tayari’ kutetea imani yetu. Je, ungependa kumhubiria mtu fulani kazini, shuleni, au mahali pengine? Fikiria mapema wakati ambao unaweza kufanya hivyo, kisha utayarishe mambo utakayosema. Sali ili upate ujasiri, na uwe na uhakika kwamba Yehova atakusaidia kushinda woga wa wanadamu.—Mdo. 4:29.

“PENDANENI SANA”

Petro alikubali kurekebishwa na Paulo. Barua mbili ambazo Petro aliandika zinatufundisha jinsi ya kuwapenda ndugu na dada zetu (Tazama fungu la 9)

9. Pindi moja Petro alikosaje kuonyesha upendo? (Tazama pia picha.)

9 Petro alijifunza jinsi ya kuonyesha upendo. Alikuwepo Yesu aliposema hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda, nanyi mpendane vivyo hivyo.” (Yoh. 13:34) Ingawa hivyo, baadaye Petro alilemewa na mkazo, na akakataa kula pamoja na ndugu na dada zake ambao walikuwa Watu wa Mataifa. Mtume Paulo alisema kwamba Petro alionyesha “unafiki.” (Gal. 2:​11-14) Petro alikubali aliporekebishwa na akajifunza kutokana na jambo hilo. Katika barua zake mbili anakazia kwamba hatupaswi tu kuhisi upendo kuwaelekea ndugu na dada zetu bali pia kuwaonyesha upendo.

10. “Upendo wa kindugu bila unafiki” unatokana na nini? Eleza. (1 Petro 1:22)

10 Petro anasema kwamba tunapaswa kuwaonyesha waabudu wenzetu “upendo wa kindugu bila unafiki.” (Soma 1 Petro 1:22.) Upendo huo unatokana na kuwa “watiifu kwa ile kweli.” Kweli hiyo inatia ndani fundisho la kwamba “Mungu hana ubaguzi.” (Mdo. 10:​34, 35) Hatuwezi kutii amri ya Yesu kuhusu kupendana ikiwa tunawaonyesha upendo baadhi ya watu kutanikoni na kuwabagua wengine. Ukweli ni kwamba huenda tukawa na uhusiano wa karibu zaidi na baadhi ya watu kama ilivyokuwa kwa Yesu. (Yoh. 13:23; 20:2) Lakini Petro anatuonyesha kwamba tunapaswa kujitahidi kuonyesha “upendo wa kindugu”—uhusiano mchangamfu kama wa familia—kuwaelekea ndugu na dada zetu wote.—1 Pet. 2:17.

11. Kuwapenda wengine “sana kutoka moyoni” kunahusisha nini?

11 Petro alituhimiza ‘tupendane sana kutoka moyoni.’ Katika muktadha huo, kupendana “sana” kunatia ndani kumpenda mtu hata kama ni vigumu kumwonyesha upendo. Namna gani ikiwa ndugu anatukasirisha au anatuumiza kwa njia fulani? Huenda tukashawishiwa kulipiza kisasi badala ya kuonyesha upendo. Ingawa hivyo, Petro alijifunza kutoka kwa Yesu kwamba Mungu hafurahishwi na watu wanaolipiza kisasi. (Yoh. 18:​10, 11) Petro aliandika hivi: “Msilipe ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano. Badala yake, lipeni kwa baraka.” (1 Pet. 3:9) Unapowaonyesha wengine upendo mwingi utachochewa kuwatendea kwa fadhili na ufikirio hata wale ambao huenda wamekuumiza.

12. (a) Kupendana sana kutatuchochea kufanya nini? (b) Ungependa kujitahidi kufanya nini kama inavyoonyeshwa kwenye video Dumisha Zawadi Yenye Thamani ya Umoja?

12 Katika barua yake ya kwanza, Petro alisema kwamba ‘kupendana sana,’ kutatusaidia kusamehe si makosa machache, bali “dhambi nyingi.” (1 Pet. 4:8) Huenda Petro alikumbuka somo kuhusu kusamehe ambalo Yesu alikuwa amemfundisha miaka mingi mapema. Wakati huo, Petro alifikiri kwamba angeonyesha fadhili nyingi, alipopendekeza kwamba angemsamehe ndugu yake “mpaka mara saba.” Lakini Yesu alimfundisha Petro—na sisi sote—kusamehe “mpaka mara 77,” yaani, bila kikomo. (Mt. 18:​21, 22) Ikiwa unahisi ni vigumu kutumia shauri hilo usife moyo! Kwa kuwa watumishi wote wa Yehova si wakamilifu, nyakati nyingine imekuwa vigumu kwao kusamehe. Jambo muhimu sasa ni kuchukua hatua yoyote inayohitajika ili kumsamehe ndugu yako na kufanya amani pamoja naye. c

WAZEE, LICHUNGENI KUNDI

13. Ni nini kinachoweza kufanya iwe vigumu kwa wazee kuwachunga ndugu na dada zao?

13 Bila shaka Petro hakusahau maneno haya ambayo Yesu alimwambia baada ya kufufuliwa: “Chunga kondoo wangu wadogo.” (Yoh. 21:16) Ikiwa wewe ni mzee wa kutaniko, unajua kwamba mwongozo huu unakuhusu. Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kwa mzee kupata wakati wa kutimiza mgawo huu muhimu. Wazee wanapaswa kutunza kwanza familia zao wenyewe kimwili, kihisia, na kiroho. Pia, wanaongoza katika kazi ya kuhubiri, vilevile wanatayarisha na kushughulikia migawo ya kufundisha kutanikoni, kwenye makusanyiko ya mzunguko, na makusanyiko ya eneo. Baadhi yao pia ni washiriki wa Halmashauri za Uhusiano na Hospitali au wana migawo katika Idara ya Usanifu Majengo na Ujenzi. Kwa kweli, wazee wana shughuli nyingi!

Ingawa wazee wenye upendo wana shughuli nyingi, wanafanya yote wanayoweza ili kulichunga kundi la Mungu (Tazama fungu la 14 na 15)

14. Ni nini kinachoweza kuwachochea wazee walichunge kundi? (1 Petro 5:​1-4)

14 Petro aliwahimiza hivi wazee wenzake: “Lichungeni kundi la Mungu.” (Soma 1 Petro 5:​1-4.) Ikiwa wewe ni mzee wa kutaniko, tunajua kwamba unawapenda ndugu na dada zako, na unataka kuwachunga kiroho. Hata hivyo, huenda nyakati nyingine ukahisi kwamba una shughuli nyingi sana au una uchovu mwingi sana hivi kwamba huwezi kutimiza mgawo huo. Unaweza kufanya nini? Mmiminie Yehova mahangaiko yako. Petro aliandika hivi: “Yeyote akihudumu, na afanye hivyo kama anayetegemea nguvu ambazo Mungu hutoa.” (1 Pet. 4:11) Huenda ndugu na dada zako wanakabili matatizo ambayo hayawezi kusuluhishwa kabisa katika mfumo huu wa mambo. Lakini kumbuka kwamba “mchungaji mkuu,” Yesu Kristo, anaweza kuwasaidia kwa njia nzuri zaidi kuliko unavyoweza. Anaweza kufanya hivyo leo na katika ulimwengu mpya. Mungu anataka wazee wawapende na kuwachunga ndugu zao na wawe “vielelezo kwa kundi.”

15. Mzee fulani analichungaje kundi? (Tazama pia picha.)

15 William, mzee wa kutaniko wa muda mrefu, anaelewa umuhimu wa kufanya uchungaji. Janga la COVID-19 lilipoanza, yeye pamoja na wazee wenzake, walihakikisha kwamba kila juma waliwasiliana na kila mtu, katika kikundi walichogawiwa. Anaeleza sababu: “Ndugu na dada wengi walikuwa peke yao nyumbani na ingekuwa rahisi kwao kulemewa na mawazo yasiyofaa.” Mkristo mwenzake anapokuwa na matatizo, William husikiliza kwa makini ili ajue mahitaji yake na mambo yanayomhangaisha. Kisha anatafuta habari hususa, mara nyingi video kwenye tovuti yetu, ili kumsaidia mwabudu mwenzake. Anasema hivi: “Tunahitaji kufanya uchungaji sasa kuliko wakati mwingine wowote. Tunatia jitihada nyingi ili kuwasaidia watu wajifunze kumhusu Yehova. Tunapaswa kufanya jitihada kama hizo ili kulichunga kundi na kuwasaidia kondoo wa Yehova wabaki katika kweli.”

MRUHUSU YEHOVA AMALIZE MAZOEZI YAKO

16. Tunaweza kutumia jinsi gani masomo tuliyojifunza katika barua za Petro?

16 Tumezungumzia masomo machache tu katika barua za Petro zilizoongozwa na roho. Labda umetambua jambo ambalo unahitaji kufanyia kazi. Kwa mfano, huenda ungependa kutafakari mara nyingi zaidi kuhusu baraka ambazo tutafurahia katika ulimwengu mpya. Je, umejiwekea lengo la kuhubiri kazini, shuleni, au katika sehemu nyingine? Je, umetambua njia ambazo unaweza kuonyesha kikamili zaidi kwamba unawapenda sana ndugu na dada zako? Je, wazee mmeazimia kuchunga kondoo wa Yehova kwa hiari na kwa hamu? Jichunguze kwa unyoofu ili kutambua udhaifu wowote ulio nao, lakini usivunjike moyo. “Bwana ni mwenye fadhili,” na atakusaidia kufanya maendeleo. (1 Pet. 2:3) Petro anatuhakikishia hivi: “Mungu . . . mwenyewe atamaliza mazoezi yenu. Atafanya muwe imara, atawatia nguvu, atawapa msingi imara.”—1 Pet. 5:10.

17. Ikiwa tutaendelea kuwa waaminifu na kumruhusu Yehova atuzoeze, matokeo yatakuwa nini?

17 Pindi moja, Petro alihisi kwamba hastahili kuwa pamoja na Mwana wa Mungu. (Luka 5:8) Lakini kwa msaada wa upendo kutoka kwa Yehova na Yesu, Petro aliendelea kuwa mwaminifu akiwa mfuasi wa Kristo. Hivyo, Petro alipata kibali cha “kuingia katika Ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:11) Hiyo ilikuwa baraka iliyoje! Ikiwa utaendelea kuwa mwaminifu kama Petro alivyofanya na kukubali kuzoezwa na Yehova, wewe pia utapata thawabu ya uzima wa milele. ‘Utafikia lengo la imani yako, wokovu wako.’—1 Pet. 1:9.

WIMBO 109 Pendaneni Sana Kutoka Moyoni

a Katika makala hii, tutaona jinsi masomo tunayopata katika barua za Petro yanavyoweza kutusaidia kuvumilia majaribu. Pia, wazee watasaidiwa kuona jinsi wanavyoweza kutimiza jukumu lao wakiwa wachungaji.

b Inawezekana kwamba Wakristo walioishi huko Palestina walipokea barua mbili za Petro kabla jiji la Yerusalemu halijashambuliwa kwa mara ya kwanza mwaka wa 66 W.K.

c Tazama video Dumisha Zawadi Yenye Thamani ya Umoja, kwenye jw.org.